Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 37

Mtegemee Yehova Kama Samsoni Alivyofanya

Mtegemee Yehova Kama Samsoni Alivyofanya

“Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, nikumbuke, tafadhali, na kunitia nguvu.”—AMU. 16:28.

WIMBO 30 Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu

MUHTASARI a

1-2. Kwa nini tunapaswa kupendezwa na simulizi la Samsoni?

 UNAFIKIRIA kuhusu nini unaposikia jina Samsoni? Inawezekana kwamba unamfikiria mwanamume aliyekuwa na nguvu sana. Hilo ni kweli. Lakini Samsoni alifanya uamuzi mbaya uliomsababishia mateso mengi. Hata hivyo, Yehova alikazia fikira mambo yote ambayo Samsoni alikuwa amefanya ili kumtumikia kwa uaminifu, na alitia ndani mfano wa Samsoni katika Biblia ili kutunufaisha.

2 Yehova alimtumia Samsoni kutimiza mambo yenye kustaajabisha ili kuwasaidia watu aliowachagua, Waisraeli. Karne nyingi baada ya kifo cha Samsoni, Yehova alimwongoza mtume Paulo kutia ndani jina la Samsoni kwenye orodha ya wanaume waliokuwa na imani ya pekee. (Ebr. 11:​32-34) Mfano wa Samsoni unaweza kututia moyo. Alimtegemea Yehova, hata alipokabili hali ngumu. Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kutiwa moyo na pia kujifunza masomo fulani kutokana na mfano wake.

SAMSONI ALIMTUMAINI YEHOVA

3. Samsoni alipewa mgawo gani?

3 Samsoni alipozaliwa, Wafilisti walikuwa wakitawala taifa la Israeli na kuwanyanyasa. (Amu. 13:1) Utawala wao wa kikatili uliwasababishia Waisraeli mateso mengi. Yehova alimchagua Samsoni “[kuwaokoa] Waisraeli kutoka mikononi mwa Wafilisti.” (Amu. 13:5) Hilo lilikuwa jukumu zito sana! Ili kutimiza jukumu hilo gumu, Samsoni alihitaji kumtegemea Yehova.

Samsoni alimtegemea Yehova na alikuwa tayari kufanya mabadiliko. Alitumia silaha iliyopatikana ili kutimiza mapenzi ya Mungu (Tazama fungu la 4 na 5)

4. Yehova alimsaidiaje Samsoni kujiweka huru kutoka kwa Wafilisti? (Waamuzi 15:​14-16)

4 Fikiria mfano unaoonyesha kwamba Samsoni alimtumaini Yehova na alimtegemea ili kupata msaada. Pindi moja, wanajeshi Wafilisti walikuja kumkamata Samsoni huko Lehi, inawezekana kwamba ni huko Yuda. Wanaume wa Yuda waliogopa, basi wakaamua kumkabidhi Samsoni kwa maadui wao. Waisraeli wenzake, walimfunga Samsoni kwa kamba mbili mpya na kumpeleka kwa Wafilisti. (Amu. 15:​9-13) Hata hivyo, ‘roho ya Yehova ilimtia nguvu’ Samsoni na akajifungua kutoka katika zile kamba. Kisha “akaona utaya mbichi wa punda dume,” akauchukua, na kuutumia kuwaua wanaume 1,000 Wafilisti!—Soma Waamuzi 15:​14-16.

5. Samsoni alipotumia utaya wa punda alionyeshaje kwamba anamtegemea Yehova?

5 Kwa nini Samsoni alitumia utaya wa punda? Hiyo ilikuwa silaha isiyo ya kawaida! Bila shaka Samsoni alijua kwamba mafanikio yake yalimtegemea Yehova, bali si silaha aliyotumia. Naam, mwanamume huyo mwaminifu alitumia silaha iliyopatikana ili kutimiza mapenzi ya Yehova. Ni wazi kwamba kwa sababu ya kumtegemea Yehova, Samsoni alibarikiwa kwa kupata mafanikio makubwa.

6. Tunaweza kujifunza jambo gani kutoka kwa Samsoni tunapotimiza migawo yetu ya kitheokrasi?

6 Sisi pia tunaweza kuimarishwa na Yehova ili kutimiza migawo yetu, hata migawo inayoonekana kuwa migumu. Mungu anaweza kutusaidia kufanya hivyo kwa njia ambayo inaweza kutushangaza. Uwe na hakika kwamba Yehova, ambaye alimtia nguvu Samsoni, atakusaidia ufanye mapenzi Yake ikiwa utamtegemea ili akusaidie.—Met. 16:3.

7. Ni mfano gani unaoonyesha umuhimu wa kutafuta mwongozo kutoka kwa Yehova?

7 Ndugu na dada wengi ambao wanashiriki katika miradi ya ujenzi ya kitheokrasi wameonyesha kwamba wanamtumaini Yehova. Zamani, kwa kawaida akina ndugu walibuni muundo na kujenga Majumba mapya ya Ufalme na majengo mengine. Hata hivyo, hatimaye, mabadiliko yalihitaji kufanywa kwa sababu ya uhitaji wa tengenezo la Yehova linalozidi kukua. Akina ndugu wanaoongoza walisali ili kupata mwongozo wa Yehova na wakajaribu mbinu mpya, kama vile kununua majengo kisha kuyakarabati. Robert, ambaye kwa miaka ya hivi karibuni ameshiriki katika miradi mingi ya ujenzi sehemu mbalimbali ulimwenguni, anasema hivi: “Mwanzoni, haikuwa rahisi kwa baadhi ya akina ndugu kufanya mambo kwa njia hiyo mpya.” Anaongezea hivi: “Ilikuwa tofauti kabisa na njia ambayo tulikuwa tunatumia kwa miaka mingi. Lakini akina ndugu walikuwa tayari kufanya mabadiliko na imethibitika kwamba Yehova anabariki mabadiliko haya.” Huo ni mfano mmoja unaoonyesha jinsi Yehova anavyowaongoza watu wake kutimiza mapenzi yake. Pindi kwa pindi, sisi sote tunapaswa kujiuliza hivi, ‘Je, ninatafuta mwongozo wa Yehova na kuwa tayari kufanya mabadiliko katika utumishi wangu kwake?’

SAMSONI ALITUMIA MAANDALIZI YA YEHOVA

8. Pindi moja Samsoni alipohisi kiu sana, alifanya nini?

8 Huenda umesoma kuhusu pindi nyingine ambazo Samsoni alifanya matendo ya kustaajabisha. Akiwa peke yake, alimuua simba na baadaye akawaua wanaume 30 Wafilisti katika jiji la Ashkeloni. (Amu. 14:​5, 6, 19) Samsoni alijua kwamba hangeweza kamwe kufanya jambo kama hilo bila msaada wa Yehova. Hilo lilionekana wazi pindi moja alipohisi kiu sana baada ya kuwaua Wafilisti 1,000. Alifanya nini? Badala ya kujitegemea ili kupata maji ya kunywa, alimlilia Yehova ili kupata msaada.—Amu. 15:18.

9. Yehova alifanya nini Samsoni alipomwomba msaada? (Waamuzi 15:19 na maelezo ya chini)

9 Yehova alijibu kilio cha Samsoni cha kuomba msaada kwa kumwandalia maji kimuujiza. Samsoni alipokunywa maji hayo, “nguvu zake zikamrudia akapata nguvu tena.” (Soma Waamuzi 15:19 na maelezo ya chini.) Inaonekana kwamba chemchemi hiyo ya maji ilikuwepo miaka mingi baadaye nabii Samweli alipoongozwa na roho kuandika kitabu cha Waamuzi. Waisraeli waliojionea maji hayo yakitiririka huenda walikumbuka kwamba ikiwa watamtegemea, Yehova atawasaidia waabudu wake waaminifu wakati wa uhitaji.

Samsoni alipata nguvu baada ya kunywa maji ambayo Yehova alimwandalia. Tunahitaji kutumia vizuri maandalizi ambayo Yehova anatuandalia ili tuendelee kuwa na nguvu kiroho (Tazama fungu la 10)

10. Tunapaswa kufanya nini ili tupate msaada wa Yehova? (Tazama pia picha.)

10 Sisi pia tunahitaji kumtegemea Yehova ili kupata msaada hata iwe tuna vipawa au uwezo gani, au licha ya mambo ambayo tumetimiza katika utumishi wake. Tunapaswa kuwa wenye kiasi na kukubali kwamba tunaweza kupata mafanikio ya kweli ikiwa tu tutamtegemea Yehova. Kama vile Samsoni alivyotiwa nguvu alipokunywa maji ambayo Yehova alimwandalia, sisi pia tutatiwa nguvu kiroho ikiwa tutatumia maandalizi yote ambayo Yehova anatuandalia.—Mt. 11:28.

11. Tunawezaje kutegemea kabisa msaada wa Yehova? Toa mfano.

11 Fikiria mfano wa Aleksey, mmoja wa ndugu zetu nchini Urusi ambaye anavumilia mateso makali. Ni nini ambacho kimemsaidia kuvumilia hali ngumu sana? Yeye na mke wake wana ratiba nzuri ya kiroho. Anasema hivi: “Ninajitahidi kudumisha ratiba yangu ya kiroho kwa kujifunza kibinafsi na kusoma Biblia kila siku. Kila asubuhi, mimi na mke wangu tunazungumzia andiko la siku na kusali kwa Yehova pamoja.” Tunajifunza nini? Badala ya kujitegemea tunapaswa kumtegemea Yehova. Jinsi gani? Tunajenga imani yetu kwa kuwa na ratiba nzuri ya kujifunza Biblia kibinafsi na kushiriki katika shughuli nyingine za kitheokrasi. Kisha, Yehova atabariki sana jitihada zetu za kumtumikia. Alimwimarisha Samsoni, na kwa hakika anaweza kutuimarisha sisi pia.

SAMSONI HAKUKATA TAMAA

12. Samsoni alifanya uamuzi gani mbaya na kisa hicho kilikuwaje tofauti na visa vilivyotangulia?

12 Samsoni alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu kama sisi, basi wakati mwingine alifanya maamuzi mabaya. Uamuzi mmoja aliofanya hasa ulisababisha matokeo mabaya sana. Baada ya Samsoni kutumikia akiwa mwamuzi kwa muda fulani, “akampenda mwanamke fulani katika Bonde la Soreki, aliyeitwa Delila.” (Amu. 16:4) Hapo awali, Samsoni alikuwa amemchumbia mwanamke Mfilisti, lakini Yehova ndiye ‘aliyeongoza jambo hilo’ kwa sababu “alikuwa akitafuta nafasi ya kuwapiga Wafilisti.” Baadaye, Samsoni alikaa katika nyumba ya kahaba katika jiji la Wafilisti lililoitwa Gaza. Katika pindi hiyo, Mungu alimwezesha Samsoni kung’oa na kubeba malango ya jiji hilo, na kuliacha bila ulinzi. (Amu. 14:​1-4; 16:​1-3) Hata hivyo, kisa cha Delila kilikuwa tofauti kwa sababu inaelekea kwamba alikuwa Mwisraeli.

13. Delila alimshawishi Samsoni jinsi gani aingie katika hali mbaya?

13 Delila alikubali kiasi kikubwa cha pesa kutoka kwa Wafilisti ili amsaliti Samsoni. Je, Samsoni alimwamini sana na kupofushwa na upendo kumwelekea hivi kwamba akakosa kutambua njama ya Delila? Vyovyote vile, Delila alimshinikiza Samsoni tena na tena amfunulie chanzo cha nguvu zake, na mwishowe Samsoni akamwambia. Kwa kusikitisha, Samsoni alijiruhusu kuingia katika hali ambayo ilimfanya apoteze nguvu zake na pia kukosa kibali cha Yehova kwa muda fulani.—Amu. 16:​16-20.

14. Samsoni alipatwa na matokeo gani kwa sababu ya kumwamini Delila?

14 Samsoni alipatwa na matokeo mabaya kwa sababu ya kumwamini Delila badala ya kumtegemea Yehova. Wafilisti walimkamata Samsoni na kumpofusha. Alifungwa gerezani katika jiji la Gaza, ambako hapo awali alikuwa amewapiga watu wa jiji hilo, lakini sasa walimfanya kuwa mtumwa aliyesaga nafaka. Kisha Wafilisti wakamfedhehesha kwa kumleta katika sherehe yao. Walimtolea dhabihu kubwa mungu wao wa uwongo Dagoni, kwa sababu waliamini kwamba yeye ndiye aliyewasaidia kumkamata Samsoni. Walimtoa Samsoni gerezani na kumleta kwenye sherehe hiyo ili “awatumbuize”—na ili wamdhihaki.—Amu. 16:​21-25.

Yehova alimwimarisha Samsoni ili atekeleze hukumu Yake dhidi ya Wafilisti (Tazama fungu la 15)

15. Samsoni alionyeshaje kwamba alimtegemea tena Yehova? (Waamuzi 16:​28-30) (Tazama picha kwenye jalada.)

15 Samsoni alikuwa amefanya kosa zito lakini hakufa moyo. Alitafuta fursa ya kutimiza mgawo aliopewa na Mungu wa kupigana dhidi ya Wafilisti. (Soma Waamuzi 16:​28-30.) Samsoni alimsihi hivi Yehova: “Acha niwalipize kisasi Wafilisti.” Mungu wa kweli alijibu ombi la Samsoni na kumrudishia nguvu zake za kipekee. Matokeo ni kwamba Samsoni aliwaua Wafilisti wengi zaidi pindi hiyo kuliko alivyofanya hapo awali.

16. Tunajifunza nini kutokana na kosa la Samsoni?

16 Ingawa Samsoni alipatwa na matokeo mabaya kwa sababu ya kosa lake, aliendelea kujitahidi kufanya mapenzi ya Yehova. Hata ikiwa tutafanya kosa na kuhitaji kukaripiwa au kupoteza pendeleo fulani, hatupaswi kufa moyo. Kumbuka kwamba Yehova yuko tayari kutusamehe. (Zab. 103:​8-10) Licha ya makosa yetu, Yehova anaweza kutupatia nguvu za kufanya mapenzi yake kama alivyomsaidia Samsoni.

Inaelekea kwamba Samsoni alihisi vibaya kwa sababu ya kosa lake, lakini hakufa moyo—sisi pia hatupaswi kufa moyo (Tazama fungu la 17 na 18)

17-18. Ni jambo gani linalokutia moyo kuhusu kisa cha Michael? (Tazama pia picha.)

17 Fikiria mfano wa ndugu kijana anayeitwa Michael. Alikuwa na bidii katika utumishi wa Yehova, akitumikia kama mtumishi wa huduma na painia wa kawaida. Kwa kusikitisha, alifanya kosa na hivyo akapoteza mapendeleo yake kutanikoni. Anasema hivi: “Kufikia wakati huo, nilikuwa na shughuli nyingi sana katika utumishi wa Yehova. Kisha ghafla, nikahisi kana kwamba nimegonga ukuta. Sikuwaza kamwe kwamba Yehova angeniacha, lakini nilijiuliza ikiwa uhusiano wangu pamoja naye ungekuwa tena kama ulivyokuwa zamani, au ikiwa ningeweza tena kumtumikia kikamili kutanikoni kama nilivyofanya zamani.”  

18 Jambo lenye kupendeza ni kwamba Michael hakufa moyo. Anaongezea hivi: “Nilikazia fikira kurekebisha uhusiano wangu pamoja na Yehova kwa kumfungulia moyo wangu na kusali kwake kwa ukawaida, kujifunza, na kutafakari.” Baada ya muda, Michael alipewa tena mapendeleo kutanikoni. Sasa anatumikia akiwa mzee wa kutaniko na painia wa kawaida. Anasema hivi: “Kwa kuwa wazee walinisaidia na kunitia moyo, hilo lilinisaidia kutambua kwamba bado Yehova ananipenda. Sasa ninaweza kutumikia tena kutanikoni nikiwa na dhamiri safi. Kisa hiki kimenifundisha kwamba Yehova anaweza kumsamehe mtu yeyote anayetubu kikweli.” Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ataturuhusu sisi pia tumtumikie na atatubariki, hata iwe tulifanya makosa, ikiwa tu tumefanya yote tunayoweza kurekebisha mwenendo wetu na kuendelea kumtegemea.—Zab. 86:5; Met. 28:13.

19. Mfano wa Samsoni umekuimarishaje?

19 Katika makala hii, tumechunguza matukio machache yenye kusisimua katika maisha ya Samsoni. Alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu; ingawa hivyo, hakuacha kujitahidi kumtumikia Yehova hata alipofanya kosa kuhusiana na Delila. Na Yehova aliendelea kumtumia Samsoni. Mungu alimtumia tena Samsoni kwa njia kubwa sana. Bado Yehova alimwona kuwa mwanamume mwenye imani ya pekee, na kumtaja kwenye orodha ya watumishi waaminifu inayopatikana kwenye Waebrania sura ya 11. Inatia moyo kujua kwamba tunamtumikia Baba wa mbinguni mwenye upendo ambaye anatamani kutuimarisha hasa tunapokuwa dhaifu! Basi kama Samsoni, acheni tumsihi hivi Yehova: “Nikumbuke, tafadhali, na kunitia nguvu.”—Amu. 16:28.

WIMBO 3 Tumaini, Nguvu, na Uhakika Wetu

a Samsoni—watu wengi wanafahamu jina la mtu huyu anayetajwa katika Biblia, hata wale ambao hawana ujuzi mwingi wa Maandiko. Simulizi lake limeonyeshwa katika michezo ya kuigiza, limeandikwa katika nyimbo na kuigizwa kwenye sinema. Lakini simulizi lake si hadithi ya kufurahisha tu. Tunaweza kujifunza mengi kutoka kwa mwanamume huyo aliyekuwa na imani kubwa.