Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 38

Vijana​​—⁠Maisha Yenu Yatakuwaje?

Vijana​​—⁠Maisha Yenu Yatakuwaje?

“Utambuzi utakulinda.”—MET. 2:11.

WIMBO 135 Mwaliko Wenye Upendo wa Yehova: “Uwe na Hekima, Mwanangu”

MUHTASARI a

1. Ni hali gani ngumu ambayo Yehoashi, Uzia, na Yosia walikabili?

 WAZIA kuwa mtawala wa watu wa Mungu ukiwa na umri mdogo sana! Ungetumiaje nguvu na mamlaka yako? Biblia inatuambia kuhusu baadhi ya vijana ambao walikuwa wafalme wa Yuda. Kwa mfano, Yehoashi alikuwa na umri wa miaka 7 tu, Uzia alikuwa na umri wa miaka 16, na Yosia alikuwa na umri wa miaka 8. Fikiria mkazo waliokabili! Ingawa walikabili hali ngumu, wote walipata msaada waliohitaji ili kushinda changamoto na kufanikiwa maishani.

2. Kwa nini ni vizuri kujifunza kuhusu mfano wa Yehoashi, Uzia, na Yosia?

2 Ingawa sisi si wafalme au malkia, tunaweza kujifunza masomo muhimu kutoka kwa watu hao watatu wanaotajwa katika Biblia. Walifanya maamuzi mazuri, lakini pia walifanya maamuzi mabaya. Kwa kutumia mifano yao, tutaona jinsi tunavyoweza kuchagua marafiki wanaofaa, kuendelea kuwa wanyenyekevu, na kuendelea kumtafuta Yehova.

CHAGUA MARAFIKI WAZURI

Leo, tunaweza kuiga mfano wa Yehoashi kwa kuwasikiliza marafiki wazuri (Tazama fungu la 3 na 7) c

3. Mfalme Yehoashi aliitikiaje mwongozo aliopewa na Kuhani Mkuu Yehoyada?

3 Iga maamuzi yenye hekima ya Yehoashi. Alipokuwa kijana, Mfalme Yehoashi alifanya uamuzi wenye hekima. Kwa kuwa hakuwa na baba, alifuata mwongozo kutoka kwa Kuhani Mkuu mwaminifu Yehoyada. Kuhani huyo alimshauri Yehoashi kana kwamba alikuwa mwana wake mwenyewe. Matokeo ni kwamba Yehoashi, kwa hekima, aliamua kuwaongoza watu katika ibada safi na kumtumikia Yehova. Yehoashi hata alifanya mpango ili hekalu la Yehova lifanyiwe marekebisho.—2 Nya. 24:​1, 2, 4, 13, 14.

4. Tunanufaikaje tunapotii amri za Yehova? (Methali 2:​1, 10-12)

4 Ikiwa unafundishwa kumpenda Yehova na kuishi kulingana na viwango vyake, unapewa zawadi yenye thamani sana. (Soma Methali 2:​1, 10-12.) Wazazi wako wanaweza kukuzoeza kwa njia nyingi. Fikiria jinsi baba ya dada anayeitwa Katya alivyomsaidia kufanya maamuzi mazuri. Kila siku baba yake alipokuwa akimpeleka shuleni, alizungumzia andiko la siku pamoja naye. Anasema hivi: “Mazungumzo hayo yalinisaidia kukabili hali ngumu ambazo zilijitokeza siku hiyo.” Namna gani ikiwa unahisi kwamba mwongozo unaotegemea Biblia ambao wazazi wako wanakupatia unakunyima uhuru? Ni nini kinachoweza kukusaidia kukubali mwongozo wao? Dada anayeitwa Anastasia anakumbuka kwamba wazazi wake walitumia muda kumweleza kwa nini waliweka sheria fulani. Anasema, “Hilo lilinisaidia kukubali sheria hizo na kuziona si kama vizuizi, bali kama ulinzi wenye upendo.”

5. Matendo yako yatawaathirije wazazi wako na Yehova? (Methali 22:6; 23:​15, 24, 25)

5 Unapofuata ushauri wa Maandiko unaopewa, utawafurahisha wazazi wako. Jambo muhimu zaidi, utamfurahisha Mungu na utajenga urafiki wa kudumu pamoja naye. (Soma Methali 22:6; 23:​15, 24, 25.) Je, hilo halikupatii sababu nzuri ya kuiga mfano wa Yehoashi alipokuwa kijana?

6. Yehoashi alianza kusikiliza ushauri wa nani, na matokeo yalikuwaje? (2 Mambo ya Nyakati 24:​17, 18)

6 Jifunze kutokana na maamuzi mabaya ya Yehoashi. Baada ya kifo cha Yehoyada, Yehoashi alichagua marafiki wabaya. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 24:​17, 18.) Alichagua kuwasikiliza wakuu wa Yuda ambao hawakumpenda Yehova. Huenda unakubali kwamba Yehoashi alipaswa kuepuka marafiki hao wasiofaa. (Met. 1:10) Badala yake, alisikiliza ushauri wao mbaya. Hata Zekaria, binamu ya Yehoashi alipojaribu kumrekebisha, Yehoashi aliamuru auawe. (2 Nya. 24:​20, 21; Mt. 23:35) Jambo hilo lilikuwa baya sana na la kipumbavu! Yehoashi alianza maisha yake vizuri, lakini kwa kusikitisha akawa mwasi-imani na muuaji. Hatimaye, watumishi wake mwenyewe walimuua. (2 Nya. 24:​22-25) Maisha yake yangekuwa tofauti kabisa ikiwa angeendelea kumsikiliza Yehova na wale waliompenda Yehova! Unajifunza somo gani kutokana na mfano huo?

7. Unapaswa kuchagua marafiki wa aina gani? (Tazama pia picha.)

7 Somo moja ambalo tunaweza kujifunza kutokana na uamuzi mbaya wa Yehoashi ni kwamba tunahitaji kuchagua marafiki ambao watatuchochea kufanya mambo mazuri—marafiki ambao wanampenda Yehova na wanaotaka kumfurahisha. Hatuhitaji kuchagua tu marafiki wenye umri kama wetu. Kumbuka kwamba Yehoashi alikuwa na umri mdogo sana kuliko rafiki yake, Yehoyada. Jiulize hivi kuhusu marafiki unaochagua: ‘Je, wananisaidia kuimarisha imani yangu kwa Yehova? Je, wananitia moyo kuishi kulingana na viwango vya Mungu? Je, wanazungumza kumhusu Yehova na kweli zake zenye thamani? Je, wanaheshimu viwango vya Mungu? Je, wananiambia tu mambo ambayo ninapenda kusikia au je, wana ujasiri wa kunirekebisha ninapokosea?’ (Met. 27:​5, 6, 17) Kwa kweli, ikiwa rafiki zako hawampendi Yehova, huwahitaji. Lakini ikiwa una marafiki ambao wanampenda Yehova, shikamana nao—watakusaidia kufanya mambo yanayofaa!—Met. 13:20.

8. Ikiwa tunatumia mitandao ya kijamii tunapaswa kuzingatia mambo gani?

8 Mitandao ya kijamii inaweza kukusaidia kudumisha mawasiliano kati yako na watu wa familia na rafiki zako. Hata hivyo, watu wengi hutumia njia hiyo ya mawasiliano kujionyesha kwa wengine, kwa kuweka picha na video za vitu ambavyo wamenunua au kufanya. Ikiwa unatumia mitandao ya kijamii jiulize hivi: ‘Je, nia yangu ni kujionyesha kwa wengine? Je, lengo langu ni kuwajenga wengine, au kujitafutia sifa? Je, ninawaruhusu watu wanaotumia mitandao ya kijamii waathiri mawazo, maneno, na matendo yangu kwa njia isiyofaa?’ Ndugu Nathan Knorr, ambaye alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa ushauri huu: “Usijaribu kuwapendeza wanadamu. Kwa kuwa mwishowe hutampendeza yeyote. Mpendeze Yehova, nawe utawapendeza wale wote wanaompenda.”

UNAHITAJI KUENDELEA KUWA MNYENYEKEVU

9. Yehova alimsaidia Uzia kufanya nini? (2 Mambo ya Nyakati 26:​1-5)

9 Iga maamuzi mazuri ya Uzia. Alipokuwa kijana Mfalme Uzia alikuwa mnyenyekevu. Alijifunza “kumwogopa Mungu wa kweli.” Aliishi kwa miaka 68, na kwa sehemu kubwa ya maisha yake Yehova alimbariki. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 26:​1-5.) Uzia aliwashinda maadui wengi na aliimarisha ulinzi wa jiji la Yerusalemu. (2 Nya. 26:​6-15) Bila shaka, Uzia alifurahia mambo yote ambayo Mungu alimsaidia kufanya.—Mhu. 3:​12, 13.

10. Uzia alipatwa na matokeo gani?

10 Jifunze kutokana na maamuzi mabaya ya Uzia. Mfalme Uzia alizoea kuwapa watu maagizo. Je, hilo lilimfanya afikiri kwamba angeweza kufanya chochote alichotaka? Siku moja, Uzia aliingia katika hekalu la Yehova na kwa kimbelembele alijaribu kufukiza uvumba kwenye madhabahu, jambo ambalo wafalme hawakuruhusiwa kufanya. (2 Nya. 26:​16-18) Kuhani Mkuu Azaria alijaribu kumrekebisha, lakini Uzia alikasirika sana. Kwa kusikitisha, Uzia aliharibu rekodi yake ya kutumikia kwa uaminifu na Yehova akampiga kwa ukoma. (2 Nya. 26:​19-21) Maisha yake yangekuwa tofauti sana ikiwa angeendelea kuwa mnyenyekevu!

Badala ya kujigamba kuhusu mambo ambayo tumetimiza, tunapaswa kumshukuru Yehova kwa mambo ambayo tunafanya (Tazama fungu la 11) d

11. Ni matendo gani yanayoweza kuonyesha kwamba sisi ni wanyenyekevu? (Tazama pia picha.)

11 Uzia alipokuwa na nguvu, alisahau kwamba Yehova ndiye aliyekuwa Chanzo cha nguvu zake na ufanisi wake. Tunajifunza somo gani? Tunapaswa kukumbuka kwamba baraka na mapendeleo yetu yanatoka kwa Yehova. Badala ya kujigamba kuhusu mambo ambayo tunatimiza, tunapaswa kumshukuru Yehova kwa mambo ambayo tunafanya. b (1 Kor. 4:7) Tunapaswa kutambua kwa unyenyekevu kwamba sisi sio wakamilifu na tunahitaji nidhamu. Ndugu fulani mwenye umri wa miaka 60 hivi, aliandika hivi: “Nimejifunza kutokasirika au kuvunjika moyo wengine wanapotambua makosa yangu. Ninapopokea nidhamu kwa sababu ya makosa ya kipumbavu ambayo wakati mwingine ninafanya, mimi hujitahidi kufanya marekebisho na kuendelea kumtumikia Yehova.” Ukweli ni kwamba ikiwa tutamwogopa Yehova na kuendelea kuwa wanyenyekevu, tutakuwa na maisha yenye kufurahisha sana.—Met. 22:4.

ENDELEA KUMTAFUTA YEHOVA

12. Alipokuwa kijana, Yosia alimtafutaje Yehova? (2 Mambo ya Nyakati 34:​1-3)

12 Iga maamuzi mazuri ya Yosia. Yosia alikuwa tineja alipoanza kumtafuta Yehova. Alitaka kujifunza kumhusu Yehova na kufanya mapenzi Yake. Hata hivyo, maisha hayakuwa rahisi kwa mfalme huyo kijana. Alihitaji kuchukua msimamo upande wa ibada safi wakati ambapo ibada ya uwongo ilikuwa imeenea. Na kwa kweli, alifanya hivyo! Kabla Yosia hajafikisha umri wa miaka 20, alianza kuondoa ibada ya uwongo katika taifa hilo.—Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:​1-3.

13. Maisha yako yatakuwaje ukijiweka wakfu kwa Yehova?

13 Hata ikiwa wewe ni kijana, unaweza kuamua kumwiga Yosia kwa kumtafuta Yehova na kujifunza kuthamini sifa Zake. Ukifanya hivyo, utachochewa kujiweka wakfu kwake. Kujiweka wakfu kutaathirije maisha yako ya kila siku? Luke, ambaye alibatizwa akiwa na umri wa miaka 14, anasema hivi: “Kuanzia sasa na kuendelea, nitatanguliza kumtumikia Yehova maishani mwangu na nitajitahidi kumfurahisha.” (Marko 12:30) Wewe pia utapata baraka ikiwa unatamani kufanya hivyo!

14. Toa mifano inayoonyesha jinsi baadhi ya vijana wanavyomwiga Mfalme Yosia.

14 Huenda ukakabili changamoto gani ukiwa kijana anayemtumikia Yehova? Johan, aliyebatizwa akiwa na umri wa miaka 12, anasema wanafunzi wenzake walimshinikiza avute sigara za kielektroni. Ili kupata nguvu za kupinga mkazo huo, Johan hujikumbusha jinsi kuvuta sigara za kielektroni kunavyoweza kuathiri afya yake na urafiki wake pamoja na Yehova. Rachel, aliyebatizwa akiwa na umri wa miaka 14, anaeleza jambo linalomsaidia kukabiliana na changamoto anazopata shuleni. Anasema hivi: “Ninajaribu kuona uhusiano kati ya mambo ninayoona shuleni na mambo ya kiroho. Kwa mfano, huenda somo la historia likanikumbusha kuhusu simulizi au unabii fulani katika Biblia. Au mazungumzo fulani yanaweza kunikumbusha kuhusu andiko muhimu ninaloweza kushiriki na mtu fulani.” Huenda changamoto unazokabili zikawa tofauti na changamoto ambazo Mfalme Yosia alikabili, lakini unaweza kuwa mwenye hekima na mshikamanifu kama alivyokuwa. Kukabiliana na majaribu ukiwa kijana kutakutayarisha kukabiliana na changamoto nyingine wakati ujao.

15. Ni nini kilichomsaidia Yosia amtumikie Yehova kwa uaminifu? (2 Mambo ya Nyakati 34:​14, 18-21)

15 Alipokuwa na umri wa miaka 26, Mfalme Yosia alianza kazi ya kurekebisha hekalu. Kazi hiyo ilipokuwa ikiendelea, “kitabu cha Sheria ya Yehova kilichotolewa kupitia Musa” kilipatikana. Mfalme aliposikia kikisomwa, alichochewa kuchukua hatua na kutenda kulingana na mambo yaliyoandikwa humo. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:​14, 18-21.) Je, ungependa kusoma Biblia kwa ukawaida? Ikiwa tayari unafanya hivyo je, unafurahia? Je, unaweka kumbukumbu ya mistari ambayo inaweza kukusaidia kibinafsi? Luke, aliyetajwa awali, huandika katika daftari mambo yenye kupendeza anayopata. Je, wewe pia unaweza kufanya hivyo ili kukumbuka mistari au mambo yenye kupendeza uliyojifunza? Kadiri unavyozidi kuijua na kuipenda Biblia, ndivyo utakavyozidi kutamani kumtumikia Yehova. Na kama Mfalme Yosia, utachochewa kutenda kulingana na Neno la Mungu.

16. Kwa nini Yosia alifanya kosa zito, na tunapata somo gani?

16 Jifunze kutokana na uamuzi mbaya wa Yosia. Yosia alipokuwa na umri wa miaka 39, alifanya uamuzi mbaya uliomsababishia kifo. Alijitegemea mwenyewe badala ya kumwomba Yehova mwongozo. (2 Nya. 35:​20-25) Tunapata somo fulani hapa. Hata iwe tuna umri gani au tumekuwa tukijifunza Biblia kwa muda mrefu kadiri gani, tunapaswa kuendelea kumtafuta Yehova. Hilo linatia ndani kusali kwake kwa ukawaida ili kupata mwongozo, kujifunza Neno lake, na kusikiliza ushauri wa Wakristo wakomavu. Tukifanya hivyo, tutapunguza uwezekano wa kufanya makosa mazito na tutakuwa wenye furaha zaidi.—Yak. 1:25.

VIJANA—MNAWEZA KUWA NA MAISHA MAZURI

17. Tunapata masomo gani kutokana na wafalme watatu wa Yuda?

17 Kipindi cha ujana kina fursa nyingi nzuri. Masimulizi ya Yehoashi, Uzia, na Yosia yanaonyesha kwamba vijana wanaweza kufanya maamuzi yenye hekima na kuishi maisha yanayomfurahisha Yehova. Ukweli ni kwamba jitihada zinahitajika ili kupata matokeo mazuri. Ingawa hivyo, tunaweza kuiga mambo mazuri ambayo wafalme hao walifanya na kuepuka makosa waliyofanya. Kisha tunaweza kutarajia kuwa na matokeo mazuri.

Kijana Daudi alimkaribia Yehova. Alipata kibali cha Mungu, na maisha yake yalikuwa mazuri (Tazama fungu la 18)

18. Ni mifano gani katika Maandiko inayoonyesha kwamba unaweza kuwa na maisha yenye furaha? (Tazama pia picha.)

18 Maandiko yana masimulizi ya vijana wengine ambao walimkaribia Yehova, wakapata kibali chake, na kuwa na maisha yenye kuridhisha. Daudi alikuwa mmoja wao. Alipokuwa na umri mdogo, aliamua kumwabudu Mungu na baadaye akawa mfalme mshikamanifu. Ni kweli kwamba pindi fulani alifanya makosa, lakini kwa ujumla alipata kibali cha Mungu. (1 Fal. 3:6; 9:​4, 5; 14:8) Unaweza kutiwa moyo na kuchochewa kwa kujifunza kuhusu maisha ya Daudi na jinsi alivyomtumikia Yehova kwa uaminifu. Au unaweza kuwa na mradi wa kujifunza kumhusu Marko au Timotheo. Utaona kwamba walianza kumtumikia Yehova walipokuwa na umri mdogo nao wakaendelea kumtumikia kwa uaminifu; na walikuwa na maisha mazuri sana.

19. Unaweza kuwa na maisha ya aina gani?

19 Maisha yako ya wakati ujao yanategemea jinsi unavyotumia maisha yako sasa. Ikiwa utamtegemea Yehova badala ya uelewaji wako mwenyewe, atakusaidia kufanya maamuzi yenye hekima. (Met. 20:24) Unaweza kuwa na maisha yenye furaha na yenye kuthawabisha. Kumbuka, Yehova anathamini mambo ambayo unafanya kwa ajili yake. Bila shaka, njia bora ya kutumia maisha yako ni kumtumikia Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo.

WIMBO 144 Kaza Macho Kwenye Zawadi!

a Vijana, Yehova anajua mnakabili changamoto ambazo zinaweza kuathiri urafiki wenu pamoja naye. Mnawezaje kufanya maamuzi yenye hekima ambayo yatamfurahisha Baba yenu wa mbinguni? Tutachunguza mifano ya wavulana watatu ambao walikuwa wafalme wa Yuda. Ona mambo ambayo unaweza kujifunza kutokana na maamuzi yao.

b Tazama sanduku “Jihadhari na ‘Unyenyekevu wa Kinafiki’” katika makala “Umaarufu Mtandaoni ni Muhimu Kadiri Gani?” kwenye jw.org.

c MAELEZO YA PICHA: Dada mkomavu anampa ushauri wenye hekima dada kijana.

d MAELEZO YA PICHA: Dada aliye na sehemu katika kusanyiko anamtegemea Yehova na kumwelekezea sifa.