Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 4

WIMBO 18 Tunathamini Fidia

Fidia Inatufundisha Nini?

Fidia Inatufundisha Nini?

“Hivi ndivyo upendo wa Mungu ulivyofunuliwa kwetu.”1 YOH. 4:9.

JAMBO KUU

Mambo ambayo fidia inafunua kuhusu sifa zenye kuvutia za Yehova Mungu na Yesu Kristo.

1. Tunanufaikaje kwa kuhudhuria Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo?

 BILA shaka unakubali kwamba fidia ni zawadi yenye thamani sana! (2 Kor. 9:15) Kwa kuwa Yesu alidhabihu uhai wake wa kibinadamu, tunaweza kuwa na urafiki wa karibu pamoja na Yehova Mungu. Pia, unaweza kuwa na tumaini la kuishi milele. Hivyo, inafaa tuonyeshe shukrani kwa fidia na kwa Yehova, ambaye alichochewa na upendo kuiandaa! (Rom. 5:8) Ili kutusaidia kuendelea kuonyesha shukrani na kutosahau kamwe kile ambacho Yehova na Yesu walitufanyia, Yesu alianzisha Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo chake.—Luka 22:​19, 20.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Mwaka huu, tutaadhimisha Ukumbusho Jumamosi, Aprili 12, 2025. Bila shaka sisi sote tunapanga kuhudhuria. Tutanufaika sana ikiwa tutatumia muda wakati wa majira ya Ukumbusho kutafakari a mambo ambayo Yehova na Mwana wake wametufanyia. Katika makala hii, tutazungumzia kile ambacho fidia inatufundisha kumhusu Yehova na Mwana wake. Katika makala inayofuata, tutasaidiwa kuelewa jinsi tunavyoweza kunufaika kutokana na fidia hiyo na jinsi tunavyoweza kuonyesha shukrani.

MAMBO AMBAYO FIDIA INATUFUNDISHA KUMHUSU YEHOVA

3. Kifo cha mtu mmoja kingewezaje kuwakomboa mamilioni ya watu? (Tazama pia picha.)

3 Fidia inatufundisha kuhusu haki ya Yehova. (Kum. 32:4) Jinsi gani? Fikiria jambo hili: Tulirithi dhambi inayoongoza kwenye kifo kutoka kwa Adamu ambaye hakutii. (Rom. 5:12) Ili kutuweka huru kutokana na dhambi na kifo, Yehova alipanga Yesu atoe fidia. Lakini dhabihu ya mtu mmoja mkamilifu ingewezaje kuwakomboa mamilioni ya watu? Mtume Paulo anaeleza hivi: “Kama vile kupitia kutotii kwa mtu mmoja [Adamu] wengi walifanywa kuwa watenda dhambi, vivyo hivyo pia kupitia kutii kwa mtu mmoja [Yesu] wengi watafanywa kuwa waadilifu.” (Rom. 5:19; 1 Tim. 2:6) Kwa maneno mengine, mtu mmoja mkamilifu ambaye hakutii alisababisha tuwe watumwa wa dhambi na kifo. Hivyo, alihitajika mtu mmoja mkamilifu ambaye angetii ili kutuweka huru.

Mtu mmoja alisababisha tuwe watumwa wa dhambi na kifo. Vivyo hivyo, mtu mmoja alituweka huru (Tazama fungu la 3)


4. Kwa nini Yehova hangeweza kuwaruhusu tu wazao wa Adamu wenye mioyo minyoofu waishi milele?

4 Je, kweli Yesu alihitaji kufa ili kutuokoa? Je, Yehova hangeweza kuamua tu kuwaruhusu wazao wa Adamu wenye mioyo minyoofu waishi milele? Kwa wanadamu wasio wakamilifu, jambo hilo lingeonekana kuwa lenye fadhili na njia nzuri ya kutatua tatizo. Lakini kufanya hivyo hakungezingatia haki kamilifu ya Yehova. Kwa kuwa Yehova ni mwenye haki, hangeweza kamwe kupuuza dhambi nzito ya Adamu ya kutotii.

5. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote Yehova atafanya lililo sawa?

5 Hata hivyo, namna gani ikiwa Yehova hangeandaa fidia na hangefuata viwango vyake vya haki kwa kuwaruhusu wana na mabinti wasio wakamilifu wa Adamu waishi milele? Huenda watu wangefikiri kwamba Mungu angepuuza viwango vyake vya haki katika masuala mengine pia. Kwa mfano, je, atashindwa kutimiza ahadi zake? Hatuhitaji kuwa na wasiwasi kuhusu uwezekano wa jambo hilo kutokea. Kwa nini? Kwa sababu Yehova alitenda kwa haki hata ingawa jambo hilo lilimgharimu sana—kumtoa Mwana wake mpendwa kuwa dhabihu. Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote atafanya jambo lililo sawa.

6. Ni sifa gani nyingine iliyomchochea Yehova kumtuma Mwana wake? (1 Yoh. 4:​9, 10)

6 Ingawa fidia inatusaidia kuelewa kwamba Yehova ni mwenye haki, inatusaidia hasa kuelewa kina cha upendo wake. (Yoh. 3:16; soma 1 Yohana 4:​9, 10.) Fundisho la fidia linafunua kwamba Yehova angependa tupate uzima wa milele na pia tuwe sehemu ya familia yake. Fikiria jambo hili: Adamu alipotenda dhambi, Yehova alimfukuza na hivyo hangeendelea kuwa sehemu ya familia ya waabudu Wake. Matokeo ni kwamba sisi sote tumezaliwa nje ya familia ya Mungu. Lakini kwa msingi wa fidia, Yehova anatusamehe dhambi zetu na hatimaye atawakaribisha watu wote ambao wanaonyesha imani na wale ambao ni watiifu katika familia yake. Hata sasa tunaweza kufurahia uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na waabudu wenzetu. Kwa kweli, Yehova ametuonyesha upendo wake mwororo!—Rom. 5:​10, 11.

7. Kuteseka kwa Yesu kunatusaidiaje kuelewa jinsi Yehova anavyotupenda?

7 Tunaweza kuelewa vizuri zaidi jinsi Yehova anavyotupenda ikiwa tutachunguza jinsi fidia ilivyomgharimu. Shetani anadai kwamba hakuna mtumishi wa Mungu ambaye ataendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova inapokuwa vigumu kufanya hivyo. Ili kujibu shtaka hilo, Yehova alimruhusu Yesu ateseke kabla ya kufa. (Ayu. 2:​1-5; 1 Pet. 2:21) Yehova aliona wapinzani wa kidini wakimdhihaki Yesu, askari wakimpiga mijeledi na kuchana ngozi yake, na akitundikwa mtini. Kisha, Yehova alitazama Mwana wake mpendwa akifa kifo chenye maumivu makali. (Mt. 27:​28-31, 39) Yehova alikuwa na nguvu za kuingilia kati na kuzuia mambo hayo wakati wowote. Kwa mfano, wapinzani waliposema: “Acheni Mungu amwokoe ikiwa anamtaka,” Yehova angeweza kufanya hivyo. (Mt. 27:​42, 43) Hata hivyo, ikiwa Mungu angeingilia kati, hakuna fidia ambayo ingelipwa na tungeachwa bila tumaini. Hivyo, Yehova alimruhusu Mwana wake avumilie kuteseka hadi alipovuta pumzi yake ya mwisho.

8. Je, Yehova alihisi uchungu alipomwona Mwana wake akiteseka? Eleza. (Tazama pia picha.)

8 Hatupaswi kufikiri kwamba kwa sababu Mungu ni Mweza-Yote, basi yeye hana hisia! Tumeumbwa kwa mfano wake, tukiwa na uwezo wa kuwa na hisia, hivyo inapatana na akili kwamba Yehova pia ana hisia. Biblia inamtaja kuwa anahisi “uchungu” na ‘huzuni.’ (Zab. 78:​40, 41) Fikiria pia mfano wa Abrahamu na Isaka. Utakumbuka kwamba Abrahamu aliagizwa amtoe mwana wake wa pekee kuwa dhabihu. (Mwa. 22:​9-12; Ebr. 11:​17-19) Fikiria jinsi Abrahamu alivyohuzunika na kuhangaika alipokuwa akijitayarisha kumuua Isaka haraka kwa kutumia kisu. Ni lazima Yehova alihuzunika hata zaidi alipomtazama Mwana wake akitendewa kwa ukatili na kuuawa na watu wasiomwogopa Mungu!—Tazama video Igeni Imani Yao—Abrahamu, Sehemu ya 2 kwenye jw.org.

Yehova aliumia alipomwona Mwana wake akiteseka (Tazama fungu la 8)


9. Waroma 8:​32, 38, 39 inakusaidiaje kuelewa kina cha upendo wa Yehova kwako na kwa waabudu wenzako?

9 Fidia inatufundisha kwamba hakuna anayetupenda zaidi kuliko Yehova—hata watu wetu wa ukoo wa karibu au rafiki yetu wa karibu zaidi. (Soma Waroma 8:​32, 38, 39.) Bila shaka, Yehova anatupenda kuliko tunavyojipenda wenyewe. Je, ungependa kuishi milele? Yehova angependa hata zaidi uishi milele. Je, ungependa kusamehewa dhambi zako? Yehova angependa hata zaidi dhambi zako zisamehewe. Jambo pekee analotarajia tufanye ni kukubali zawadi hiyo yenye thamani kwa kuonyesha imani na kuwa watiifu. Kwa kweli, fidia ni wonyesho mkubwa wa upendo wa Mungu. Na katika ulimwengu mpya, tutajifunza hata zaidi kuhusu upendo wa Yehova.—Mhu. 3:11.

FIDIA INATUFUNDISHA NINI KUMHUSU YESU?

10. (a) Ni jambo gani hasa lililomhuzunisha Yesu kuhusu kifo chake? (b) Yesu aliliteteaje jina la Yehova? (Tazama pia sanduku “ Utimilifu wa Yesu Ulilitetea Jina la Yehova.”)

10 Yesu anajali sana kuhusu sifa ya Baba yake. (Yoh. 14:31) Yesu alihuzunika kwa sababu alishtakiwa kuwa mkufuru na mchochezi na jambo hilo lingeliletea suto jina la Baba yake. Hiyo ndiyo sababu alisali hivi: “Baba yangu, ikiwa inawezekana, niondolee kikombe hiki.” (Mt. 26:39) Kwa kudumisha utimilifu wake kwa Yehova hadi kifo, Yesu alilitetea kabisa jina la Baba yake.

11. Yesu alionyeshaje kwamba anawapenda sana watu? (Yoh. 13:1)

11 Pia, fidia inatufundisha kwamba Yesu anawajali sana watu, hasa wanafunzi wake. (Met. 8:31; soma Yohana 13:1.) Kwa mfano, Yesu alijua kwamba baadhi ya mambo ambayo angefanya katika huduma yake duniani yangekuwa magumu sana, hasa kifo chake chenye maumivu makali. Hata hivyo, alipokuwa akitimiza mgawo wake duniani, hakuufanya tu kwa sababu ameagizwa na Yehova. Badala yake, Yesu alihubiri, alifundisha, na kuwahudumia wengine kwa moyo wake wote. Hata siku ya kifo chake, Yesu alitumia wakati wake kuosha miguu ya mitume wake na kuwapatia faraja na maagizo katika maneno yake ya mwisho kwao. (Yoh. 13:​12-15) Kisha, alipokuwa ametundikwa mtini, Yesu alitumia dakika chache kumpa tumaini mhalifu ambaye alikuwa karibu kufa na alifanya mipango ili Yohana amtunze mama yake. (Luka 23:​42, 43; Yoh. 19:​26, 27) Hivyo, upendo wenye kina wa Yesu haukuonyeshwa tu kupitia kifo chake, bali pia kupitia maisha yake yote duniani.

12. Ni katika maana gani Yesu anaendelea kujidhabihu kwa ajili yetu?

12 Ingawa Kristo alikufa “mara moja kwa wakati wote,” bado anajidhabihu kwa ajili yetu. (Rom. 6:10) Jinsi gani? Anaendelea kutumia wakati na jitihada ili kutupatia mambo mengi mazuri ambayo yanawezekana kwa sababu ya fidia. Fikiria mambo ambayo kwa sasa anafanya kwa bidii. Yeye ni Mfalme wetu, Kuhani Mkuu, na kichwa cha kutaniko. (1 Kor. 15:25; Efe. 5:23; Ebr. 2:17) Anasimamia kazi ya kuwakusanya watiwa-mafuta na umati mkubwa, kazi ambayo itakamilika kabla ya dhiki kuu kuisha. b (Mt. 25:32; Marko 13:27) Pia, anahakikisha kwamba watumishi wake waaminifu wanalishwa vizuri kiroho katika siku hizi za mwisho. (Mt. 24:45) Na katika Utawala wa Miaka Elfu Moja, ataendelea kutufanyia mambo mazuri. Kwa kweli, Yehova alimtoa Mwana wake kwa ajili yetu!

USIACHE KAMWE KUJIFUNZA

13. Kutafakari kunawezaje kukusaidia kuendelea kujifunza kuhusu upendo ambao Mungu na Kristo wametuonyesha?

13 Unaweza kuendelea kujifunza kuhusu upendo ambao Yehova Mungu na Kristo Yesu wanatuonyesha ikiwa utaendelea kutafakari kuuhusu. Huenda katika ya majira ya Ukumbusho ya mwaka huu, unaweza kusoma kwa makini kitabu kimoja au zaidi cha Injili. Usijaribu kusoma habari nyingi sana kwa wakati mmoja. Badala yake, soma kwa mwendo wa taratibu na utafute sababu nyingine zinazotuchochea kumpenda Yehova na Yesu. Na kwa kadiri uwezavyo, shiriki na wengine mambo ambayo umejifunza.

14. Kulingana na Zaburi 119:97 na maelezo ya chini, kufanya utafiti kunawezaje kutusaidia kuendelea kujifunza kuhusu fidia na mafundisho mengine? (Tazama pia picha.)

14 Ikiwa umekuwa katika kweli kwa miaka mingi, huenda ukajiuliza ikiwa inawezekana kujifunza mambo mapya kuhusu mambo tunayoyajua vizuri kama vile haki ya Mungu, upendo wake, na fidia. Ukweli ni kwamba hakuna mwisho wa kujifunza inapohusu mambo hayo na habari nyingine. Hivyo, unaweza kufanya nini? Tumia kikamili habari nyingi zinazopatikana kwenye machapisho yetu. Unaposoma andiko ambalo hulielewi vizuri, fanya utafiti. Kisha, siku hiyo yote, tafakari kuhusu mambo mapya ambayo umejifunza na yale uliyojifunza kumhusu Yehova, Mwana wake, na upendo wao kukuelekea.—Soma Zaburi 119:97 na maelezo ya chini.

Hata ikiwa tumekuwa katika kweli kwa miaka mingi, tunaweza kuongeza uthamini wetu kwa zawadi ya fidia (Tazama fungu la 14)


15. Kwa nini tunapaswa kuendelea kutafuta hazina katika Biblia?

15 Usivunjike moyo ikiwa hutapata jambo jipya au lenye kusisimua kila mara unapojifunza au kufanya utafiti. Kwa njia ya mfano, wewe ni kama mtu anayetafuta dhahabu. Kwa subira, wale wanaotafuta dhahabu hutumia saa au siku nyingi kabla ya kupata hata kipande kidogo sana cha dhahabu. Hata hivyo, wanaendelea kutafuta kwa sababu kila kipande cha dhahabu ni chenye thamani kwao. Kwa kweli, kila hazina ya kweli ya Biblia ni yenye thamani kubwa hata zaidi! (Zab. 119:127; Met. 8:10) Hivyo, uwe na subira na ushikamane na ratiba yako ya usomaji wa Biblia.—Zab. 1:2.

16. Tunawezaje kumwiga Yehova na Yesu?

16 Unapojifunza, tafuta njia za kutumia mambo unayojifunza. Kwa mfano, iga haki ya Yehova kwa kuwatendea wengine bila ubaguzi. Iga upendo wa Yesu kwa Baba yake na wengine kwa kuwa tayari kuteseka kwa ajili ya jina la Yehova na kujitoa kwa ajili ya Wakristo wenzako. Pia, mwige Yesu kwa kuwahubiria wengine ili wao pia wapate fursa ya kukubali zawadi hiyo ya Yehova yenye thamani kubwa sana.

17. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

17 Kadiri tunavyoielewa na kuithamini fidia, ndivyo tutakavyompenda zaidi Yehova na Mwana wake. Nao pia watatupenda hata zaidi. (Yoh. 14:21; Yak. 4:8) Hivyo, acheni tutumie maandalizi ya Yehova ili tuendelee kujifunza kuhusu fidia. Makala inayofuata itazungumzia baadhi ya njia tunazoweza kunufaika kutokana na fidia na jinsi tunavyoweza kuonyesha tunathamini upendo huo wa Yehova.

WIMBO 107 Mungu—Kielelezo cha Upendo

a UFAFANUZI WA MANENO: “Kutafakari” kunamaanisha kukazia fikira habari fulani na kuichunguza kwa kina zaidi.

b Kukusanywa kwa “vitu vilivyo mbinguni” ambako Paulo anataja kwenye Waefeso 1:​10, ni tofauti na kukusanywa kwa “watu wake waliochaguliwa” ambako Yesu anataja kwenye Mathayo 24:31 na Marko 13:27. Paulo anarejelea wakati ambao Yehova anawachagua wale watakaotawala mbinguni pamoja na Yesu kwa kuwatia mafuta kwa roho takatifu. Yesu anarejelea wakati ambao watiwa-mafuta waliobaki duniani watakusanywa na kwenda mbinguni wakati wa dhiki kuu.