Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 2

WIMBO 132 Sasa Tumekuwa Mwili Mmoja

Waume, Waheshimuni Wake Zenu

Waume, Waheshimuni Wake Zenu

“Enyi waume, . . . wapeni heshima.”1 PET. 3:7.

JAMBO KUU

Jinsi mume anavyoweza kumheshimu mke wake kwa maneno na matendo.

1. Ni sababu gani moja iliyomfanya Yehova aanzishe mpango wa ndoa?

 YEHOVA ni “Mungu mwenye furaha,” na anataka sisi pia tuwe na furaha. (1 Tim. 1:11) Ametupatia zawadi nyingi ili tufurahie maisha. (Yak. 1:17) Zawadi moja kati ya hizo ni ndoa. Mwanamume na mwanamke wanapofunga ndoa, wanaweka nadhiri ya kupendana na kuheshimiana. Kudumisha uhusiano wa karibu kunaweza kuwaletea shangwe ya kweli.—Met. 5:18.

2. Hali katika ndoa nyingi ikoje leo?

2 Kwa kusikitisha, wenzi wengi wa ndoa leo husahau ahadi ambazo waliweka katika siku yao ya ndoa. Matokeo ni kwamba wanakosa furaha. Ripoti ya karibuni kutoka katika Shirika la Afya Ulimwenguni inaonyesha kwamba waume wengi wanawapiga, wanawatukana, na kuwaumiza kihisia wake zao. Mume anayefanya hivyo huenda akamtendea mke wake kwa heshima mbele za watu, lakini akamtendea vibaya akiwa nyumbani. Pia, ndoa nyingi zinapata mkazo mume anapotazama ponografia.

3. Kwa nini baadhi ya waume wanawatendea wake zao kwa njia isiyofaa?

3 Kwa nini baadhi ya waume wanawatendea wake zao kwa njia isiyofaa? Huenda walilelewa na baba ambaye ni mkatili, hivyo wanafikiri kwamba kutenda kwa njia hiyo ni jambo la kawaida. Wengine wameathiriwa na utamaduni unaowazunguka, ambao huenda unaendeleza wazo lisilofaa la kwamba ni lazima “mwanamume wa kweli” atumie nguvu ili kumwonyesha mke wake kwamba yeye ndiye mwenye mamlaka. Wanaume wengine hawakufundishwa kudhibiti hisia zao, kutia ndani hasira. Baadhi ya wanaume wamesitawisha maoni yasiyofaa kuelekea wanawake na ngono kwa sababu ya kutazama ponografia kwa ukawaida. Kwa kuongezea, ripoti zinaonyesha kwamba janga la COVID-19 lilizidisha matatizo hayo. Bila shaka, sababu hizo zote hazipaswi kuwa kisingizio cha mume kumtendea mke wake kwa njia isiyofaa.

4. Waume Wakristo wanapaswa kujilinda dhidi ya nini, na kwa nini?

4 Waume Wakristo wanapaswa kujilinda ili wasiige maoni yasiyofaa kuelekea wanawake. a Kwa nini? Sababu moja ni kwamba mara nyingi mawazo ya mtu huongoza kwenye matendo. Mtume Paulo aliwaonya Wakristo watiwa-mafuta huko Roma “[waache] kufinyangwa na mfumo huu wa mambo.” (Rom. 12:​1, 2) Paulo alipowaandikia barua Wakristo huko Roma, inaelekea kwamba kutaniko hilo lilikuwa limeanzishwa miaka kadhaa iliyopita. Hata hivyo, maneno ya Paulo yalionyesha kwamba baadhi ya watu kutanikoni bado walikuwa wakiathiriwa na utamaduni na njia ya kufikiri ya ulimwengu. Hiyo ndiyo sababu aliwahimiza wabadili njia yao ya kufikiri na mwenendo wao. Kwa hakika, ushauri huo unawahusu waume Wakristo leo. Kwa kusikitisha, baadhi yao wameathiriwa na njia ya kufikiri ya ulimwengu huu na hata wamewatendea wake zao kwa njia isiyofaa. b Yehova anatarajia mume amtendeeje mke wake? Tutapata jibu la swali hilo katika andiko la msingi la makala hii.

5. Kulingana na 1 Petro 3:​7, mume anapaswa kumtendeaje mke wake?

5 Soma 1 Petro 3:7. Yehova anawaamuru waume wawaheshimu wake zao. Neno heshima linarejelea jinsi tunavyomtendea mtu tunayemstahi. Mume anayemheshimu mke wake atamtendea kwa njia ya fadhili na upendo. Katika makala hii, tutachunguza jinsi mume anavyoweza kumwonyesha heshima mke wake. Lakini kwanza, acheni tuzungumzie aina ya mwenendo unaomvunjia heshima mke.

KATAA MWENENDO UNAOMVUNJIA HESHIMA MKE WAKO

6. Yehova anahisije kuhusu wanaume wanaowapiga wake zao? (Wakolosai 3:19)

6 Kumpiga mke wako. Yehova humchukia mtu yeyote anayependa ukatili. (Zab. 11:5) Anawashutumu kihususa waume wanaowatendea wake zao kwa njia isiyofaa. (Mal. 2:16; soma Wakolosai 3:19.) Kulingana na andiko letu la msingi, 1 Petro 3:​7, ikiwa mume hamtendei mke wake kwa njia nzuri, uhusiano wake pamoja na Mungu utaathiriwa. Huenda hata Yehova asisikilize sala zake.

7. Kulingana na Waefeso 4:​31, 32, ni lazima waume waepuke kutumia maneno ya aina gani? (Tazama pia “Ufafanuzi wa Maneno.”)

7 Kumtukana mke wako. Baadhi ya waume wanazungumza kwa hasira na wake zao na kutumia maneno yanayoumiza. Lakini Yehova anachukia ‘hasira, ghadhabu, kufoka, na matusi.’ c (Soma Waefeso 4:​31, 32.) Anasikia kila kitu. Njia ambayo mume anazungumza na mke wake, hata wakiwa faraghani, ni jambo muhimu kwa Yehova. Mume anayezungumza na mke wake kwa ukali haharibu tu ndoa yake, bali pia urafiki wake pamoja na Mungu.—Yak. 1:26.

8. Yehova anahisije kuhusu ponografia, na kwa nini?

8 Kutazama ponografia. Yehova anahisije kuhusu ponografia? Anachukia ponografia. Hivyo, mume anayetazama picha chafu anaharibu uhusiano wake pamoja na Yehova na anamvunjia heshima mke wake. d Yehova anatarajia mume aendelee kuwa mshikamanifu kwa mke wake kupitia matendo yake, na pia mawazo yake. Yesu alisema kwamba mwanamume anayemtazama mwanamke mwingine kwa njia ya kimahaba tayari amefanya uzinzi pamoja naye “moyoni mwake.” eMt. 5:​28, 29.

9. Kwa nini Yehova anachukia mume anapomvunjia heshima mke wake wanapokuwa katika mahusiano ya kingono?

9 Kumvunjia heshima mke wake wanapokuwa katika mahusiano ya kingono. Baadhi ya waume huwashinikiza wake zao wafanye mambo fulani yanayowavunjia heshima na yanayowafanya wahisi wao si safi au hawapendwi, wanapokuwa katika mahusiano ya kingono. Yehova anachukia mwenendo huo wenye ubinafsi na usio na ufikirio. Anatarajia mume ampende mke wake, amtendee kwa fadhili, na kuheshimu hisia za mke wake. (Efe. 5:​28, 29) Namna gani ikiwa tayari mume Mkristo anamvunjia heshima au anamtendea kwa njia mbaya mke wake, au anatazama ponografia? Anawezaje kubadili matendo yake na njia yake ya kufikiri?

JINSI MUME ANAVYOWEZA KUACHA MWENENDO MBAYA

10. Waume wanaweza kunufaikaje kutokana na mfano wa Yesu?

10 Ni nini kinachoweza kumsaidia mume aache kumtendea mke wake kwa njia isiyofaa au inayomvunjia heshima? Anaweza kujitahidi kumwiga Yesu. Ingawa Yesu hakufunga ndoa, njia aliyowatendea wanafunzi wake ni kielelezo cha jinsi mume anavyopaswa kumtendea mke wake. (Efe. 5:25) Kwa mfano, fikiria mambo ambayo waume wanaweza kujifunza kutokana na njia ambayo Yesu aliwatendea mitume wake na jinsi alivyozungumza nao.

11. Yesu aliwatendeaje mitume wake?

11 Yesu aliwatendea mitume wake kwa fadhili na staha. Kamwe hakuwa mkali na hakuwakandamiza. Ingawa alikuwa Bwana wao, Yesu hakuhisi kwamba anahitaji kuthibitisha mamlaka yake juu yao kwa kuonyesha nguvu zake. Badala yake, aliwatumikia kwa unyenyekevu. (Yoh. 13:​12-17) Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu.” (Mt. 11:​28-30) Ona kwamba Yesu alikuwa mpole. Mtu mpole si dhaifu. Badala yake, ana nguvu za kujizuia. Anapochokozwa, anaendelea kuwa mtulivu na kudhibiti hisia zake.

12. Yesu alizungumza na wengine jinsi gani?

12 Yesu alitumia maneno yake kuwafariji na kuwaburudisha wengine. Hakuzungumza na wafuasi wake kwa ukali. (Luka 8:​47, 48) Hata wapinzani wake walipomtukana na kujaribu kumkasirisha, “hakujibu kwa kutukana.” (1 Pet. 2:​21-23) Nyakati nyingine, Yesu alichagua kukaa kimya badala ya kujibu kwa ukali. (Mt. 27:​12-14) Huo ni mfano mzuri sana kwa waume Wakristo!

13. Kama inavyoonyeshwa kwenye Mathayo 19:​4-6, mume anawezaje ‘kushikamana na mke wake’? (Tazama pia picha.)

13 Yesu aliwaagiza waume waendelee kuwa washikamanifu kwa wake zao. Alimnukuu Baba yake, ambaye alisema kwamba mume anapaswa ‘kushikamana na mke wake.’ (Soma Mathayo 19:​4-6.) Kitenzi cha Kigiriki kinachotumiwa katika andiko hilo na kutafsiriwa kuwa ‘kushikamana’ kihalisi kinamaanisha “kugundisha.” Hivyo, muungano kati ya mume na mke unapaswa kuwa imara sana kana kwamba wameunganishwa kwa gundi. Muungano wao ukivunjika, wote wawili wanapata madhara. Mume ambaye anasitawisha muungano kama huo pamoja na mke wake atakataa aina zote za ponografia. Mara moja atageuka na kuacha ‘kutazama mambo yasiyofaa.’ (Zab. 119:37) Kama Ayubu, yeye pia ameazimia kufanya agano na macho yake kwamba hatamtazama kwa kumtamani mwanamke mwingine yeyote isipokuwa mke wake.—Ayu. 31:1.

Mume mshikamanifu anakataa kutazama ponografia (Tazama fungu la 13) g


14. Mume anayemtendea mke wake kwa njia isiyofaa anapaswa kuchukua hatua gani ili kurekebisha uhusiano wake pamoja na Yehova na mke wake?

14 Mume ambaye anampiga au kumtukana mke wake anahitaji kuchukua hatua za ziada ili kurekebisha uhusiano wake pamoja na Yehova na mke wake. Anapaswa kuchukua hatua gani? Kwanza, anapaswa kutambua kwamba ana tatizo kubwa. Hakuna jambo linaloweza kufichwa machoni pa Yehova. (Zab. 44:21; Mhu. 12:14; Ebr. 4:13) Pili, anapaswa kuacha kumtendea mke wake kwa njia isiyofaa na kubadili tabia yake. (Met. 28:13) Tatu, anapaswa kukiri kwa Yehova na kwa mke wake maumivu yote aliyowasababishia, na kwa unyoofu aombe msamaha. (Mdo. 3:19) Pia, anapaswa amsihi Yehova ampatie hamu ya kubadilika na amsaidie kudhibiti mawazo, maneno, na matendo yake. (Zab. 51:​10-12; 2 Kor. 10:5; Flp. 2:13) Nne, anapaswa kutenda kulingana na sala zake kwa kujifunza kuchukia aina zote za ukatili na matusi. (Zab. 97:10) Tano, anapaswa kutafuta msaada mara moja kutoka kwa wachungaji wenye upendo kutanikoni. (Yak. 5:​14-16) Sita, anapaswa kuandaa mpango ambao utamsaidia kuepuka tabia zote hizo mbaya wakati ujao. Mume anayetazama ponografia anapaswa kufuata hatua hizohizo. Yehova atabariki jitihada zake za kubadili mwenendo wake. (Zab. 37:5) Lakini haitoshi tu kwa mume kuacha mwenendo usiofaa. Anahitaji pia kujifunza jinsi ya kumwonyesha heshima mke wake. Anawezaje kufanya hivyo?

JINSI YA KUMHESHIMU MKE WAKO

15. Mume anawezaje kumwonyesha upendo mke wake?

15 Mwonyeshe upendo. Baadhi ya akina ndugu ambao wana furaha kwenye ndoa wana zoea la kufanya jambo fulani kila siku ili kuwaonyesha wake zao jinsi wanavyowapenda. (1 Yoh. 3:18) Mume anaweza kumwonyesha mke wake upendo mwororo katika njia ndogo-ndogo, kama vile kumshika mkono au kumkumbatia kwa wororo. Anaweza kumtumia ujumbe mfupi wa simu na kumwambia “Nimekukosa” au kumuuliza “Siku yako inaendaje?” Pindi fulani, anaweza kumweleza mke wake kwamba anampenda kwa kumwandikia kadi yenye maneno machache yaliyochaguliwa vizuri. Mume anapofanya mambo hayo, anamheshimu mke wake, na anaimarisha ndoa yao.

16. Kwa nini mume anapaswa kumsifu mke wake?

16 Mweleze kwamba unamthamini. Mume ambaye anamheshimu mke wake anamjenga na kumtia moyo. Njia moja ambayo anafanya hivyo ni kwa kukumbuka kumshukuru kwa mambo yote ambayo anafanya ili kumuunga mkono. (Kol. 3:15) Mume anapomsifu kwa unyoofu mke wake, anamgusa moyo sana. Atahisi akiwa salama, anapendwa, na kuheshimiwa.—Met. 31:28.

17. Mume anawezaje kumwonyesha heshima mke wake?

17 Uwe mwenye fadhili na heshima. Mume anayempenda mke wake anamthamini na kumjali sana. Anamwona kuwa zawadi yenye thamani sana kutoka kwa Yehova. (Met. 18:22; 31:10) Matokeo ni kwamba anamtendea kwa fadhili na heshima, hata wakiwa katika mahusiano ya kingono. Hatamlazimisha ashiriki katika matendo ya kingono ambayo yanamfanya asijihisi huru, yanayomvunjia heshima, au yanayosumbua dhamiri yake. f Yeye pia atajitahidi kudumisha dhamiri safi mbele za Yehova.—Mdo. 24:16.

18. Waume wanapaswa kuazimia kufanya nini? (Tazama pia sanduku “ Njia Nne za Kuwa Mume Mwenye Heshima.”)

18 Waume, muwe na uhakika kwamba Yehova anaona na anathamini jitihada zenu za kuwaheshimu wake zenu katika sehemu zote za maisha yenu. Azimia kumwonyesha heshima mke wako kwa kuepuka mwenendo utakaomuumiza, na uwe mwenye fadhili na upendo. Ukifanya hivyo, utamwonyesha kwamba unampenda na kumthamini. Mheshimu mke wako, nawe utalinda uhusiano ulio muhimu zaidi kwako—urafiki wako pamoja na Yehova.—Zab. 25:14.

WIMBO 131 “Kile Ambacho Mungu Ameunganisha”

a Waume watanufaika kwa kusoma makala “Je, Unawatendea Wanawake Kama Yehova Anavyowatendea?” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 2024.

b Wale ambao wametendewa kwa ukatili nyumbani watanufaika kwa kusoma makala “Msaada kwa Wanaotendewa kwa Jeuri Nyumbani” katika mfululizo wa makala, “Habari Zaidi” kwenye jw.org na JW Library®.

c UFAFANUZI WA MANENO: “Matusi” yanatia ndani kumwita mtu majina yanayomvunjia heshima na kumchambua kwa njia ya ukali na mara kwa mara. Maneno yoyote ambayo ni yenye uhasama, yenye kudhalilisha, au ya dharau ni matusi.

d Tazama kwenye jw.org na JW Library makala “Ponografia Inaweza Kuiharibu Ndoa Yako.”

e Mke ambaye mume wake anatazama ponografia atanufaika kwa kusoma makala “Mwenzi wa Ndoa Anapotazama Ponografia” kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 2023.

f Biblia haisemi habari hususa kuhusu ni matendo gani ya kingono kati ya mume na mke yanayoonwa kuwa safi au si safi. Ni lazima wenzi wa ndoa Wakristo wafanye maamuzi ambayo yanaonyesha kwamba wameazimia kumheshimu Yehova, kuwapendeza wenzi wao, na kudumisha dhamiri safi. Kwa ujumla, wenzi wa ndoa hawatazungumza na wengine kuhusu suala hili la kibinafsi la ndoa yao.

g MAELEZO YA PICHA: Wafanyakazi wenzake ambao si Mashahidi wanajaribu kumshawishi ndugu atazame gazeti la ponografia.