Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuelewa Maandiko Kimakosa, Je, Ni Tatizo Dogo?

Kuelewa Maandiko Kimakosa, Je, Ni Tatizo Dogo?

Msichana mdogo aliona moshi uliotoka kiwandani ukijikusanya na kutengeneza kitu kilichoonekana kama mawingu. Hivyo, akafikiri kimakosa kwamba hicho ni kiwanda cha kutengeneza mawingu. Kuelewa kimakosa mambo madogo kama hayo huchekesha. Hata hivyo, kuelewa kimakosa mambo ambayo ni muhimu, kunaweza kuhatarisha uhai wetu. Kwa mfano, ukikosea na kutumia dawa tofauti uliyopaswa kunywa, unaweza kupatwa na madhara makubwa sana.

Kuelewa Maandiko kimakosa kunaweza kuwa na matokeo mabaya hata zaidi. Kwa mfano, baadhi ya watu walielewa kimakosa mafundisho ya Yesu. (Yohana 6:48-68) Badala ya kujifunza mengi zaidi, walikataa mambo yote ambayo Yesu alifundisha. Jambo la kusikitisha kwelikweli!

Je, wewe husoma Biblia ili kupata mwongozo? Ni vizuri ikiwa unafanya hivyo. Lakini, je, unafikiri kuna uwezekano wa kuelewa kimakosa jambo fulani ulilosoma? Hali hiyo huwapata watu wengi. Fikiria mambo matatu ambayo wengi wameyaelewa kimakosa.

  • Baadhi ya watu wanaelewa kimakosa amri ya Biblia inayosema: “Mwogope Mungu wa kweli.” Wanafikiri amri hiyo inamaanisha kwamba Mungu anapaswa kuogopwa kama kitu kinachotisha. (Mhubiri 12:13) Lakini Mungu hataki watu wanaomwabudu wahisi hivyo. Mungu anasema hivi: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli.” (Isaya 41:10) Kumwogopa Mungu humaanisha kumheshimu kutoka moyoni.

  • Je, sayari yetu dunia itachomwa moto?

    Baadhi ya watu wanaelewa kimakosa maneno haya: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu, . . . wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa.” Wanafikiri maneno hayo yanamaanisha kwamba Mungu amepanga siku na saa ya kila mmoja wetu kufa. (Mhubiri 3:1, 2) Hata hivyo, andiko hilo linataja tu kuhusu mzunguko wa maisha ya wanadamu; tunazaliwa na hatimaye tutakufa. Neno la Mungu linatufundisha pia kwamba maamuzi tunayofanya yanaweza kuathiri urefu wa maisha yetu. Kwa mfano, Biblia inasema: “Kumwogopa Yehova kutaongeza siku.” (Methali 10:27; Zaburi 90:10; Isaya 55:3) Jinsi gani? Kwa mfano, ikiwa tunaliheshimu Neno la Mungu tutaepuka mazoea yanayoweza kuathiri afya yetu kama vile kunywa pombe kupita kiasi na ukosefu wa maadili.—1 Wakorintho 6:9, 10.

  • Wengine wanafikiri kwamba Biblia inaposema mbingu na dunia “zimewekwa akiba kwa ajili ya moto,” inamaanisha Mungu ataiharibu sayari yetu. (2 Petro 3:7) Lakini Mungu ameahidi kwamba kamwe hataruhusu sayari hii iangamizwe. “Ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5; Isaya 45:18) Ulimwengu huu uliopotoka ndio utakaoangamizwa usiwepo milele, kana kwamba umeharibiwa kwa moto, na si sayari yetu dunia. Namna gani kuhusu mbingu? Neno hilo linaweza kutumiwa kumaanisha anga la dunia, anga la juu lenye nyota, au makao ya Mungu. Vyote hivyo havitaangamizwa.

KWA NINI WAKATI MWINGINE BIBLIA INAELEWEKA KIMAKOSA?

Kama mifano hiyo inavyoonyesha, mara kwa mara watu huelewa Maandiko kimakosa. Lakini kwa nini Mungu anaruhusu jambo hilo litokee? Huenda wengine wakafikiri hivi: ‘Kwa kuwa Mungu ni mwenye hekima na ujuzi wote, alipaswa kutupatia kitabu kilichoandikwa kwa njia iliyo wazi, ambacho mtu yeyote angeweza kukielewa kwa urahisi. Kwa nini hakufanya hivyo?’ Fikiria sababu tatu zinazofanya watu waielewe Biblia kimakosa.

  1. Biblia imeandikwa kwa njia ambayo watu wanyenyekevu na walio tayari kujifunza ndio wanaoielewa. Yesu alimwambia hivi Baba yake: “Ninakusifu hadharani wewe, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha kwa uangalifu wenye hekima na walio na akili mambo hayo, nawe umeyafunua kwa watoto.” (Luka 10:21) Biblia imeandikwa kwa njia ambayo ni wale tu walio na mtazamo unaofaa wanaoweza kuelewa ujumbe wake. Watu wenye kiburi mara nyingi huielewa Biblia kimakosa. Kwa kawaida watu “wenye hekima na walio na akili” huwa na kiburi. Lakini wale wanaosoma Biblia wakiwa na mtazamo kama wa “watoto,” yaani, unyenyekevu na hamu ya kujifunza, wanauelewa ujumbe wa Biblia kwa usahihi. Kwa kweli Mungu aliongoza Biblia iandikwe kwa ustadi sana!

  2. Wanaofaidika na Biblia ni wale ambao hutafuta msaada wa Mungu ili waweze kuielewa. Yesu alionyesha kwamba watu wangehitaji msaada ili kuelewa kikamili mambo aliyofundisha. Wangepataje msaada huo? Yesu alieleza hivi: “Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba atatuma katika jina langu, hiyo itawafundisha ninyi mambo yote.” (Yohana 14:26) Kwa hiyo, Mungu huwapatia watu roho yake takatifu, yaani, nguvu ya utendaji, ili kuwasaidia waelewe mambo wanayosoma kwenye Biblia. Hata hivyo, Mungu huwanyima roho yake watu wasiomtegemea, kwa hiyo wanashindwa kuielewa Biblia. Pia, roho takatifu huwachochea Wakristo wenye ujuzi zaidi wa Biblia kuwasaidia wale wanaotaka kuielewa kwa kina.—Matendo 8:26-35.

  3. Baadhi ya Maandiko hayawezi kueleweka kwa wanadamu mpaka wakati unaofaa ufike. Kwa mfano, nabii Danieli aliambiwa aandike ujumbe kuhusu wakati ujao. Malaika alimwambia hivi: “Ee Danieli, yafanye siri maneno hayo na kukifunga kitabu kwa muhuri, mpaka wakati wa mwisho.” Kwa karne nyingi, watu wengi wamesoma kitabu cha Danieli lakini hawakukielewa. Kwa kweli, hata Danieli mwenyewe hakuelewa baadhi ya mambo aliyoandika. Kwa unyenyekevu alikiri hivi: “Nami nikasikia, lakini sikuweza kuelewa.” Hatimaye, watu wangeelewa kwa usahihi unabii wa Danieli, lakini hilo lingetokea katika wakati hususa uliowekwa na Mungu. Malaika alieleza hivi: “Nenda, Danieli, kwa sababu maneno hayo yamewekwa siri na kufungwa kwa muhuri mpaka wakati wa mwisho.” Ni nani ambao wangeelewa ujumbe wa Mungu? Malaika aliendelea kusema hivi: “Wala hakuna waovu wowote watakaoelewa; bali wale walio na ufahamu wataelewa.” (Danieli 12:4, 8-10) Kwa hiyo, Mungu hafunui maana ya baadhi ya Maandiko mpaka wakati unaofaa ufike.

Je, Mashahidi wa Yehova wamewahi kuelewa kimakosa Maandiko fulani kwa kuwa wakati wa Mungu kufunua maana yake haukuwa umefika? Ndiyo. Lakini wakati wa Mungu wa kufunua maana sahihi ulipofika, Mashahidi walibadili uelewaji wao. Wanaamini kwamba, kwa kufanya hivyo, wanawaiga mitume wa Kristo ambao walibadili maoni yao kila mara Yesu alipowarekebisha.—Matendo 1:6, 7.

Tatizo la msichana mdogo kuelewa kimakosa chanzo cha mawingu, si kubwa. Hata hivyo, mambo ambayo Biblia inafundisha ni muhimu sana kwako. Ujumbe wa Biblia ni muhimu sana, hivyo, hatupaswi kujitegemea wenyewe tunapoisoma. Kwa hiyo, tafuta msaada ili uelewe mambo unayosoma. Watafute wale ambao huisoma Biblia wakiwa na mtazamo wa unyenyekevu, watu wanaotegemea roho takatifu ya Mungu iwasaidie kuielewa Biblia, watu wanaoamini kwamba tunaishi katika kipindi ambacho Mungu anataka tuielewe Biblia zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Usisite kuzungumza na Mashahidi wa Yehova au kusoma habari walizofanyia utafiti kwa makini zinazopatikana kwenye tovuti ya jw.org/sw. Biblia inaahidi hivi: “Ikiwa utaita uelewaji . . . , utapata kumjua Mungu.”—Methali 2:3-5.