Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutii Onyo Kunaweza Kuokoa Uhai Wako!

Kutii Onyo Kunaweza Kuokoa Uhai Wako!

Desemba 26, 2004, tetemeko kubwa la kipimo cha 9.1 lilitikisa mji wa Simeulue, uliopo kaskazini-magharibi mwa pwani ya Sumatra, Indonesia. Watu wote waliokuwa pwani walitazama baharini. Maji yalirudi nyuma kuliko ilivyo kawaida. Punde si punde, watu walianza kukimbilia maeneo yenye miinuko huku wakipiga kelele na kusema “Smong! Smong!” neno la lugha ya kienyeji linalomaanisha tsunami. Kwa dakika 30, mawimbi makubwa yenye nguvu yalipiga pwani, yakaharibu nyumba nyingi na vijiji vingi.

Kisiwa cha Simeulue kilikuwa cha kwanza kukumbwa na tsunami. Kati ya wakazi 78,000 wa kisiwa hicho, ni saba tu waliokufa. Kwa nini walikufa wachache hivyo? * Watu wa kisiwa hicho husema hivi: ‘Kukiwa na tetemeko kubwa na maji ya bahari yanarudi nyuma, kimbilia kwenye eneo lenye mwinuko, kwa kuwa baada ya muda mfupi pwani itapigwa na mawimbi makubwa.’ Matukio yaliyopita yaliwafunza watu wa Simeulue kutambua dalili za tsunami kwa kuangalia mabadiliko ya bahari. Kutii onyo kuliokoa maisha yao.

Biblia inaeleza kuhusu janga baya litakalotukia hivi karibuni, “dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Kwa kuwa Mungu amekusudia dunia iwepo milele, dhiki hiyo haimaanishi uharibifu wa sayari yetu Dunia kupitia wanadamu au janga fulani la asili. (Mhubiri 1:4) Badala yake, dhiki hiyo itakuja ili Mungu ‘awaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ Huo utakuwa mwisho wa uovu na mateso. (Ufunuo 11:18; Methali 2:22) Itakuwa baraka iliyoje!

Tofauti na tsunami, matetemeko ya ardhi, au milipuko ya volkeno, uharibifu unaokuja hautaua watu wazuri. Biblia inasema “Mungu ni upendo,” na Mungu ambaye jina lake ni Yehova, ameahidi kwamba “waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (1 Yohana 4:8; Zaburi 37:29) Hata hivyo, unawezaje kuokoka dhiki kuu na kufurahia baraka zilizoahidiwa? Siri ni: Kutii maonyo!

TAMBUA HARAKA MABADILIKO

Hatuwezi kujua tarehe hususa ya kuondolewa kwa uovu na mateso, kwa kuwa Yesu alisema hivi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” Halafu akatutia moyo kwa maneno haya, “endeleeni kukesha.” (Mathayo 24:36; 25:13) Jinsi gani? Biblia inatueleza jinsi hali za ulimwengu zitakavyokuwa kabla Mungu hajaleta mwisho. Kama vile wakazi wa Simeulue walivyotambua kukaribia kwa tsunami kutokana na mabadiliko ya ghafula baharini, mabadiliko ya matukio ya ulimwengu huu yanatusaidia kutambua kwamba mwisho uko karibu. Sanduku linataja baadhi ya mabadiliko yanayozungumziwa katika Biblia.

Ni kweli kwamba baadhi ya matukio au hali hizo zilizoorodheshwa katika sanduku zilitokea kwa kiasi fulani wakati uliopita. Hata hivyo, Yesu anasema tunapoona “mambo yote hayo” tujue kwamba mwisho uko karibu sana. (Mathayo 24:33) Jiulize hivi, ‘Ni wakati gani mambo hayo yaliyotajwa (1) yalitukia ulimwenguni pote, (2) yalitukia kwa wakati mmoja, na (3) yalibadilika na kuwa mabaya zaidi?’ Kwa kweli, tunaishi wakati huo.

KUDHIHIRISHWA KWA UPENDO WA MUNGU

Rais wa zamani wa Marekani alisema, “kutoa onyo mapema . . . kunaokoa uhai.” Baada ya tsunami ya mwaka 2004, mfumo wa kutoa onyo uliwekwa katika eneo lote lililoathiriwa ili kuzuia vifo vya watu wengi wakati ujao. Vivyo hivyo Mungu ametoa onyo mapema. Biblia ilitabiri hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Mwaka uliopita, Mashahidi wa Yehova walitumia saa bilioni 1.9 kuhubiri habari njema kwenye nchi 240 kwa lugha zaidi ya 700. Maendeleo hayo ya kazi ya kuhubiri yanathibitisha kwamba mwisho upo karibu. Wakichochewa na upendo wao kwa jirani, Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kuwaonya kuhusu siku ya hukumu ambayo inakaribia sana. (Mathayo 22:39) Yehova anathibitisha kwamba anakupenda kwa kukupatia habari hizi zenye faida. Kumbuka, “[Mungu] hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Je, utathamini upendo wa Mungu na kutii onyo?

KIMBILIA MAHALI SALAMA!

Wakumbuke wakazi wa kijiji cha Simeulue, walipoona maji katika bahari yamerudi nyuma walikimbilia maeneo yaliyoinuka, hawakusubiri maji yarudi. Uamuzi mzuri waliofanya uliokoa uhai wao. Ili tuokoke dhiki inayokuja, tunapaswa kukimbilia maeneo yaliyoinuka kwa njia ya mfano kabla haijawa kuchelewa mno. Jinsi gani? Nabii Isaya aliandika kuhusu mwaliko wenye kuvutia ambao ungetolewa “katika siku za mwisho,” yaani, wakati huu tunaoishi. Mwaliko huo unasema hivi: “Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.”—Isaya 2:2, 3.

Ukiwa juu ya mlima unakuwa katika eneo lililoinuka na ambalo ni salama. Vivyo hivyo, kujua njia za Mungu kupitia kujifunza Biblia kumewasaidia watu wengi ulimwenguni wanufaike kwa kubadili maisha yao. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa kufanya hivyo, wanaanza ‘kutembea katika mapito ya [Mungu]’ na kufurahia baraka na ulinzi wake.

Je, utakubali mwaliko wa Mungu na kunufaika na upendo wake katika siku hizi za mwisho? Tunakusihi uchunguze kwa uangalifu uthibitisho wa Maandiko kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” unaoonyeshwa kwenye sanduku lililo katika makala hii. Mashahidi wa Yehova katika eneo unaloishi watafurahi kukusaidia uyaelewe vizuri maandiko na ujue jinsi ya kuyatumia. Au unaweza kupata majibu ya maswali yako kwa kutembelea tovuti yetu, www.pr418.com/sw. Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MAJIBU YA MASWALI YA BIBLIA.

^ fu. 3 Tsunami hiyo ya mwaka 2004 ilikuwa janga baya zaidi katika historia ambalo liliua watu zaidi ya 220,000.