Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dunia Itaharibiwa?

Je, Dunia Itaharibiwa?

Huenda unajua kwamba Biblia inazungumzia mwisho wa ulimwengu. (1 Yohana 2:17) Je, inamaanisha wanadamu wote wataangamizwa? Je, dunia itaangamizwa? Je, sayari yetu itabaki ukiwa bila kiumbe chochote?

JIBU LA BIBLIA KWA MASWALI HAYO YOTE NI HAPANA!

Ni Nini Ambacho Hakitaharibiwa?

WANADAMU

Biblia inasema nini? Mungu “hakuiumba tu [dunia] bila sababu, lakini aliiumba ili ikaliwe.”​—ISAYA 45:18.

SAYARI YETU, DUNIA

Biblia inasema nini? “Kizazi huenda, na kizazi huja, lakini dunia inadumu milele.”​—MHUBIRI 1:4.

HILO LINAMAANISHA NINI? Biblia inasema kwamba dunia itakaliwa sikuzote, haitaangamizwa kamwe. Kwa hiyo, mwisho wa dunia ni nini?

FIKIRIA HILI: Biblia inalinganisha mwisho wa ulimwengu unaokuja na mambo yaliyotukia katika siku za Noa. Wakati huo dunia ilijaa ukatili. (Mwanzo 6:13) Hata hivyo, Noa alikuwa mwadilifu. Kwa hiyo, Mungu alimwokoa Noa na familia yake lakini aliwaangamiza watu waovu kwa gharika. Ikielezea mambo yaliyotukia wakati huo, Biblia inasema hivi: “Ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji.” (2 Petro 3:6) Huo ulikuwa mwisho wa ulimwengu wa wakati huo. Hata hivyo, ni nini kilichoangamizwa? Ni watu waovu waliokuwepo duniani, na si sayari yetu dunia. Kwa hiyo, Biblia inapozungumzia mwisho wa ulimwengu haimaanishi kuangamizwa kwa sayari yetu. Badala yake, inamaanisha mwisho wa watu waovu duniani na mashirika yote waliyoanzisha.

Ni Nini Kitakachoondolewa?

MATATIZO NA UOVU

Biblia inasema nini? “Bado muda mfupi tu, na watu waovu hawatakuwepo tena; utapaangalia mahali walipokuwa, nao hawatakuwepo. Lakini wapole wataimiliki dunia, nao watafurahia kwelikweli wingi wa amani.”​—ZABURI 37:10, 11.

HILO LINAMAANISHA NINI? Gharika ya siku za Noa haikuondoa uovu milele. Baada ya gharika, watu waovu walifanya maisha yawe mabaya kwa kila mtu. Hata hivyo, hivi karibuni, Mungu atakomesha kabisa uovu. Kama mtunga-zaburi alivyosema, “watu waovu hawatakuwepo tena.” Mungu ataondoa uovu kupitia Ufalme wake, yaani, serikali kutoka mbinguni ambayo itawatawala wanadamu waadilifu duniani.

FIKIRIA HILI: Je, watawala wa serikali za wanadamu leo watakubali kutii Ufalme wa Mungu? Biblia inaonyesha kwamba hawatakubali. Kwa upumbavu, wataupinga Ufalme wa Mungu. (Zaburi 2:2) Matokeo yatakuwa nini? Ufalme wa Mungu utaondoa serikali zote za wanadamu, “nao pekee utasimama milele.” (Danieli 2:44) Hata hivyo, kwa nini serikali za wanadamu zinahitaji kuondolewa?

Utawala wa wanadamu UNAHITAJI kufika mwisho

Biblia inasema nini? “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”​—YEREMIA 10:23.

HILO LINAMAANISHA NINI? Wanadamu hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kujitawala wenyewe. Wameshindwa kuwatawala wanadamu wenzao na kutatua matatizo yao.

FIKIRIA HILI: Makala moja ya utafiti (The Britannica Academic) inasema kwamba inaonekana serikali za nchi mbalimbali zimeshindwa kuondoa “maadui wanaokumba ulimwengu mzima, yaani, umaskini, njaa, magonjwa, majanga ya asili, vita, na jeuri.” Makala hiyo inaendelea kusema: “Baadhi ya watu wanaamini kwamba matatizo hayo yote yanaweza kuisha ikiwa dunia nzima itatawaliwa na serikali moja.” Lakini, hata ikiwa serikali zote za wanadamu zitaungana, bado dunia itatawaliwa na wanadamu wasio wakamilifu ambao hawana uwezo wa kukabiliana na matatizo ya wanadamu. Ufalme wa Mungu ndio serikali pekee yenye uwezo wa kutatua milele matatizo yote duniani.

Hivyo, kulingana na Biblia, mwisho wa ulimwengu, yaani, mwisho wa wanadamu wote waovu na mashirika waliyoanzisha, si jambo litakalowaogopesha watu wazuri. Badala yake, ni jambo wanalotazamia kwa hamu kwa sababu ulimwengu huu ulioharibika utaondolewa, na ulimwengu mpya wa Mungu ambao ni mzuri utakuja!

Mambo hayo yatatokea lini? Makala inayofuata itaeleza jibu la Biblia.