Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Inawezekana Kufurahia Maisha Hata Sasa​—Jinsi Gani?

Inawezekana Kufurahia Maisha Hata Sasa​—Jinsi Gani?

KUISHI bila kuugua, kuzeeka, na kufa—hayo ni maisha ambayo wewe pia, unaweza kufurahia wakati ujao! Hata hivyo, leo maisha yamejaa changamoto na matatizo chungu nzima. Unaweza kuboreshaje hali zako sasa? Biblia ina ushauri unaoweza kukusaidia kuwa na maisha yenye furaha na yanayoridhisha hata sasa. Hebu tuchunguze baadhi ya matatizo na jinsi Biblia inavyoweza kutusaidia.

KURIDHIKA NA MAISHA YETU

Ushauri wa Biblia: “Njia yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu mlivyo navyo.”Waebrania 13:5.

Kila siku, bidhaa na huduma zinazosemekana kuwa za lazima zinazalishwa kwa wingi. Hata hivyo, Biblia inasema inawezekana ‘kuridhika na vitu tulivyo navyo.’ Jinsi gani?

Kwa kuepuka “kupenda pesa.” Watu wako tayari kufanya chochote hata kama kitaathiri afya yao, familia, na urafiki, au kushusha maadili na heshima waliyo nayo—yote kwa sababu ya “kupenda pesa.” (1 Timotheo 6:10) Wanachopoteza hakiwezi kulinganishwa hata kidogo na wanachotafuta! Na kwa vyovyote vile, mtu anayependa mali “hatatosheka.”—Mhubiri 5:10.

Kuwathamini watu, na si vitu. Ni kweli kwamba vitu vya kimwili ni muhimu. Lakini vitu haviwezi kuonyesha kwamba vinatupenda au kututhamini; wanadamu wenzetu tu ndio wenye uwezo huo. Kuwa na “rafiki wa kweli” hutusaidia kuridhika na maisha.—Methali 17:17.

TUNAWEZA KUFURAHIA MAISHA HATA SASA IKIWA TUTAFUATA MWONGOZO WA BIBLIA

KUKABILIANA NA MATATIZO YA AFYA

Ushauri wa Biblia: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.”Methali 17:22.

Kama “dawa nzuri,” kuwa na shangwe kunaweza kukusaidia kupambana na matatizo ya afya. Lakini unawezaje kuwa mwenye shangwe ilhali afya yako si nzuri?

Uwe mwenye shukrani. Tukikazia fikira matatizo yetu tu, “kila siku” itaonekana kuwa mbaya. (Methali 15:15, Biblia Habari Njema) Badala yake, Biblia inasema, ‘uwe mwenye shukrani.’ (Wakolosai 3:15) Jitahidi kuthamini mambo mazuri maishani, hata yawe madogo, kama kuangalia jua likitua, kupulizwa na upepo mwanana, au kumwona mtu unayempenda akitabasamu. Mambo haya hufanya tufurahie maisha.

Wasaidie wengine. Hata ikiwa tuna matatizo ya afya, “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Wengine wanapoonyesha wanathamini jitihada zetu, hisia nzuri hufurika kwenye moyo wetu, na hivyo kufanya tusahau matatizo tuliyo nayo. Tunaweza kufurahia maisha yetu kwa kuwasaidia wengine kupata furaha.

KUIMARISHA NDOA

Ushauri wa Biblia: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.”Wafilipi 1:10.

Wenzi wanapotumia muda mchache pamoja, ukaribu wao unaweza kuanza kufifia. Kwa hiyo, ni jambo la busara kwa mume na mke kuitanguliza ndoa yao, kwa kuwa ndoa ni kati ya mambo muhimu zaidi maishani.

Fanyeni mambo pamoja. Badala ya kufanya mambo yanayokupendeza kibinafsi, kwa nini msipange mambo hususa ambayo mtafanya pamoja? Biblia inasema: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja.” (Mhubiri 4:9) Mnaweza kupika pamoja, kufanya mazoezi, kwenda kutembea pamoja, kufurahia mlo na vinywaji pamoja, au kutazama mpira pamoja.

Mwonyeshe mwenzi wako kwamba unampenda. Biblia inawahimiza waume na wake wawe na heshima na wapendane. (Waefeso 5:28, 33) Kutabasamu kwa uchangamfu, kumkumbatia mwenzi wako kwa upendo, au kumpatia zawadi ndogondogo ni mambo yanayoweza kuimarisha sana ndoa yenu. Ni muhimu kuzingatia kwamba, wenzi hawapaswi kuonyesha upendo wa kimahaba kwa mtu mwingine tofauti na mwenzi wao.—Waebrania 13:4.