Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kifo—Adui Asiyeepukika

Kifo—Adui Asiyeepukika

WAZIA unatazama filamu kuhusu maisha ya mtu fulani maarufu; huenda ni mwanamuziki ambaye unampenda. Inaanza kwa kuonyesha maisha yake ya utotoni, mafunzo yake ya muziki, na mazoezi mengi aliyokuwa akifanya. Kisha, unamwona akisafiri nchi mbalimbali na kutumbuiza kwenye majukwaa, na anajipatia umaarufu duniani pote. Punde si punde, anaanza kuzeeka, na filamu hiyo inapokaribia kwisha, anakufa.

Kihalisi, hivyo ndivyo maisha huwa. Iwe mtu huyo alikuwa mwanamuziki, mwanasayansi, mwanariadha, au mtu mwingine yeyote maarufu, mambo yangeenda vivyo hivyo. Huenda mtu huyo alitimiza mengi, lakini ni wazi kwamba angetimiza mengi zaidi ikiwa maisha yake hayangekatishwa na uzee na kifo, sivyo?

Kujua kwamba tutakufa kunahuzunisha, ila huo ndio ukweli. (Mhubiri 9:5) Licha ya jitihada zote ambazo tunafanya, bado tunazeeka na kufa. Na nyakati nyingine, maisha yetu yanaweza kukatishwa ghafla na aksidenti au ugonjwa. Biblia inatulinganisha na ukungu wa asubuhi “unaotokea kwa muda kidogo na kisha kutoweka.”—Yakobo 4:14.

Baadhi ya watu huhisi kwamba maisha hayatabiriki kabisa na hayana kusudi, kwa hiyo mtazamo wao ni: “Acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Lakini watu huishi maisha ya aina hiyo kwa sababu wanajua wanaweza kufa wakati wowote na hawana tumaini. Siku moja, hasa unapopitia hali ngumu, huenda wewe pia ukajiuliza, ‘Je, maisha yalikusudiwa kuwa hivi?’ Unaweza kupata wapi jibu la swali hilo?

Wengi huamua kutafuta suluhisho kwenye sayansi. Maendeleo katika sayansi na tiba yamesaidia kuongeza urefu wa maisha yetu. Na baadhi ya wanasayansi wanajaribu kufanya iwezekane kuishi muda mrefu hata zaidi. Iwe watafanikiwa au la, bado maswali yanabaki: Kwa nini tunazeeka na kufa? Je, kuna uwezekano wowote wa adui yetu kifo kuangamizwa? Tutachunguza majibu ya maswali haya katika makala zinazofuata na hivyo kupata jibu la swali, Je, maisha yalikusudiwa kuwa mafupi hivi?