Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Dunia itatoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, atatubariki.”​—ZABURI 67:6

Furahia Baraka za Muumba Wetu Milele

Furahia Baraka za Muumba Wetu Milele

Mungu alimwahidi nabii Abrahamu kwamba mmoja kati ya wazao wake atayaletea “mataifa yote ya dunia” baraka. (Mwanzo 22:18) Mzao huyo ni nani?

Karibu miaka 2,000 iliyopita, Mungu alimpa Yesu, mzao wa Abrahamu, uwezo wa kufanya miujiza. Miujiza hiyo ilithibitisha kwamba ahadi ambayo Abrahamu alipewa, kwamba mataifa yote yangebarikiwa, ingetimizwa na Yesu.​—Wagalatia 3:14.

Miujiza ambayo Yesu alifanya ilithibitisha kwamba amechaguliwa na Mungu kuwabariki wanadamu, na pia ilionyesha jinsi Mungu atakavyomtumia kuwabariki wanadamu milele. Miujiza ambayo alifanya ilifunua sifa zake nzuri. Kwa mfano:

Aliwajali watu—Yesu aliwaponya wagonjwa.

Siku moja mtu fulani mwenye ukoma alimwomba Yesu amponye. Yesu akamgusa na kumwambia: “Ninataka!” Mara moja ule ukoma ukaisha.​—Marko 1:40-42.

Ukarimu—Yesu aliwalisha wenye njaa.

Yesu hakutaka watu wawe na njaa. Katika nyakati tofauti, Yesu alifanya miujiza ya kuwalisha maelfu ya watu kupitia vipande vichache vya mikate na samaki. (Mathayo 14:17-21; 15:32-38) Watu walikula na kushiba, na chakula kingi kilibaki.

Huruma​—Yesu aliwafufua watu waliokufa.

Mjane fulani alifiwa na mwana wake na hakuwa na mtu mwingine wa kumtunza. Yesu alipomwona mjane huyo akiomboleza, ‘akamsikitikia’ na kumfufua mwana wake.​—Luka 7:12-15.