Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Mwongozo Unaotegemeka wa Kuwa na Maisha Bora ya Wakati Ujao?

Je, Kuna Mwongozo Unaotegemeka wa Kuwa na Maisha Bora ya Wakati Ujao?

Kama tulivyozungumzia kwenye makala zilizopita, watu wamejaribu kutafuta maisha bora ya wakati ujao kupitia mambo kama vile majaliwa, elimu, utajiri, na kuwa watu wema. Hata hivyo, kutumia njia hizo ni sawa na kutumia ramani isiyo sahihi ukitumaini utafika mahali unapotaka kwenda. Je, hilo linamaanisha hakuna mwongozo unaotegemeka wa wakati ujao? Hapana!

MWONGOZO KUTOKA KATIKA CHANZO KIKUU

Mara nyingi tunapotaka kufanya uamuzi tunaomba ushauri kutoka kwa mtu mwenye umri mkubwa na mwenye hekima zaidi kuliko sisi. Vilevile, tunaweza kupata mwongozo unaofaa wa wakati ujao kutoka kwa Mtu aliyeishi kwa muda mrefu zaidi na mwenye hekima nyingi zaidi kuliko sisi. Tunapata ushauri Wake kutoka katika maandishi matakatifu yaliyoanza kuandikwa karibu miaka 3,500 hivi iliyopita. Maandishi hayo matakatifu ni Biblia.

Kwa nini uitumaini Biblia? Kwa sababu Mtungaji wake ameishi muda mrefu zaidi na ana hekima nyingi kuliko mtu yeyote ulimwenguni. Anaitwa “Mzee wa Siku” ambaye ni wa “tangu milele hadi milele.” (Danieli 7:9; Zaburi 90:2) Yeye ni “Muumba wa mbingu, Mungu wa kweli, Yule aliyeiumba dunia.” (Isaya 45:18) Anajitambulisha kwa jina lake la kibinafsi, Yehova.—Zaburi 83:18.

Kwa sababu Biblia ni kitabu kutoka kwa Muumba wa wanadamu wote, hakisemi kwamba utamaduni fulani au watu fulani ni bora kuliko wengine. Ushauri wake haupitwi na wakati na unawanufaisha watu wote ulimwenguni. Biblia inapatikana katika lugha nyingi na imesambazwa kwa wingi kuliko kitabu kingine chochote. * Inamaanisha watu ulimwenguni pote wanaweza kusoma, kuelewa, na kuongozwa na ushauri wa Biblia. Mambo hayo yanathibitishwa na ukweli huu tunaosoma kwenye Biblia:

“Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.”​—MATENDO 10:34, 35.

Kama mzazi mwenye upendo anavyowaongoza watoto wake, Yehova Mungu ni Baba mwenye upendo anayetusaidia kupitia Neno lake, Biblia. (2 Timotheo 3:16) Tunaweza kulitumaini Neno lake; isitoshe, yeye ndiye aliyetuumba na anajua njia tunayopaswa kuifuata maishani ili tufanikiwe.

Unapaswa kufanya nini ili upate maisha hayo? Chunguza makala inayofuata.

^ fu. 6 Kwa maelezo zaidi kuhusu kutafsiriwa na kusambazwa kwa Biblia, tembelea tovuti ya www.pr418.com/sw na utazame chini ya MAFUNDISHO YA BIBLIA > HISTORIA NA BIBLIA.

^ fu. 16 Kwa maelezo zaidi, ona sura ya 9 ya kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia, kinapatikana mtandaoni kupitia www.pr418.com/sw. Tazama chini ya MAKTABA > VITABU NA BROSHUA.