Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wana Maoni Gani Kuhusu Kusali?

Watu Wana Maoni Gani Kuhusu Kusali?

“Ninaposali, ninahisi Mungu yupo pamoja nami, amenishika mkono na ananiongoza ninapohisi nimepotea.” —MARÍA

“Mke wangu alikufa baada ya kuugua kansa kwa miaka 13. Ninakumbuka nilisali kwa Mungu kila siku na nilihisi alikuwa akinisikiliza na alielewa uchungu niliokuwa nao. Kisha, nilipata amani na utulivu.”—RAÚL

“Sala ni zawadi bora kutoka kwa Mungu.”—ARNE

María, Raúl, Arne na wengine wengi, wamejionea kwamba sala ni zawadi ya pekee. Wanahisi kwamba kupitia sala, wanaweza kuzungumza na Mungu, kumshukuru, na kumwomba awasaidie. Wanaamini kabisa kwamba mambo ambayo Biblia inasema kuhusu sala ni ya kweli. Biblia inasema hivi: “Huu ndio uhakika tulio nao kwake, kwamba tukiomba chochote kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”​—1 Yohana 5:14.

Kwa upande mwingine, watu wengi hawaamini kile ambacho Biblia inasema kuhusu sala. Steve anaeleza maoni yake, “Nilipokuwa na umri wa miaka 17, rafiki zangu watatu walikufa katika aksidenti mbili tofauti. Mmoja alikufa kwenye aksidenti ya gari, na wengine wawili walizama baharini.” Steve alifanya nini? Anasema hivi: “Nilimwomba Mungu anisaidie kujua kwa nini mambo hayo yalitokea lakini sikupata jibu lolote. Kwa hiyo nikajiuliza, ‘Kuna umuhimu gani wa kusali ikiwa sipati majibu yoyote?’” Watu wengi wanahisi kwamba sala zao hazijibiwi, kwa hiyo hawaoni umuhimu wa kuendelea kusali.

Kuna sababu nyingine zinazowafanya watu wahisi kwamba sala haziwasaidii. Wengine wanafikiri kwamba kwa kuwa Mungu anajua mambo yote, tayari anajua mahitaji yetu na matatizo yetu, kwa hiyo hakuna umuhimu wa kumwambia mambo hayo.

Wengine wanaamini kwamba Mungu hataki kusikiliza sala zao kwa sababu ya makosa waliyofanya zamani. Jenny anasema hivi: “Tatizo kubwa nililo nalo, ni kuhisi kwamba sifai kitu. Zamani nilifanya mambo ambayo sasa ninajutia, hivyo ninajiambia kwamba sistahili kumwomba Mungu jambo lolote.”

Wewe una maoni gani kuhusu kusali kwa Mungu? Ikiwa una maoni kama ya watu waliotajwa katika makala hii, uwe na uhakika kwamba unaweza kupata majibu yenye kuridhisha kwenye Biblia. Tunaweza kuamini kabisa kile ambacho Biblia inasema kuhusu sala, * na inaweza kutusaidia kupata majibu ya maswali kama vile:

  • Je, kweli Mungu husikiliza sala zetu?

  • Kwa nini baadhi ya sala hazijibiwi?

  • Unapaswa kusali kwa njia gani ili Mungu asikilize sala zako?

  • Kuna faida gani za kusali?

^ fu. 9 Sala za watumishi wengi wa Mungu zimeandikwa kwenye Biblia, kutia ndani sala za Yesu Kristo. Kuna sala zaidi ya 150 ambazo zimeandikwa katika Maandiko ya Kiebrania, ambayo pia yanaitwa Agano la Kale.