Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 47

WIMBO 103 Wachungaji—Zawadi Katika Wanadamu

Akina Ndugu—Je, Mnajitahidi Kustahili Kutumikia Mkiwa Wazee wa Kutaniko?

Akina Ndugu—Je, Mnajitahidi Kustahili Kutumikia Mkiwa Wazee wa Kutaniko?

“Ikiwa mwanamume anajitahidi kuwa mwangalizi, anatamani kazi njema.”1 TIM. 3:1.

JAMBO KUU

Baadhi ya sifa za kustahili za Kimaandiko ambazo ni lazima ndugu afikie ili atumikie akiwa mzee wa kutaniko.

1-2. “Kazi njema” ambayo mzee wa kutaniko hufanya inahusisha nini?

 IKIWA umetumikia kwa muda fulani ukiwa mtumishi wa huduma, inaelekea kwamba umekuwa ukijitahidi kusitawisha sifa nyingi zinazohitajika ili kustahili kuwa mzee wa kutaniko. Je, unaweza kujitahidi kufikia ‘kazi hiyo njema’?—1 Tim. 3:1.

2 Kazi ya mzee wa kutaniko inahusisha nini? Anaongoza katika kazi ya kuhubiri, anajitahidi kufanya ziara za uchungaji na kufundisha, na kulijenga kutaniko kwa maneno na mfano wake. Hiyo ndiyo sababu Biblia inawaita wazee wanaofanya kazi bidii ‘wanaume walio zawadi.’—Efe. 4:8.

3. Ndugu anawezaje kustahili kuwa mzee wa kutaniko? (1 Timotheo 3:​1-7; Tito 1:​5-9)

3 Unawezaje kustahili kutumikia ukiwa mzee wa kutaniko? Kustahili kuwa mzee si sawa na kustahili kupata kazi fulani ya kimwili. Mara nyingi ili kupata kazi ya kimwili, unahitaji tu kuwa na ujuzi au ustadi wa msingi ambao mwajiri anatafuta. Tofauti na hilo, ikiwa unatamani kuwekwa rasmi kuwa mzee wa kutaniko, unahitaji mengi zaidi ya kuwa mhubiri au mwalimu mwenye ustadi. Unahitaji kufikia sifa za Kimaandiko za kustahili kuwa mzee wa kutaniko zinazotajwa kwenye 1 Timotheo 3:​1-7 na Tito 1:​5-9. (Soma.) Katika makala hii, tutazungumzia mambo haya matatu ambayo wazee wanahitaji kuzingatia: kujifanyia jina zuri ndani na nje ya kutaniko, kuweka mfano mzuri wakiwa vichwa vya familia, na kuwa tayari kulitumikia kutaniko.

KUJIFANYIA JINA ZURI

4. Inamaanisha nini “kuwa mtu asiyelaumika”?

4 Ili ustahili kuwa mzee, ni lazima uwe “mtu asiyelaumika,” yaani, uwe na jina zuri kutanikoni kwa sababu mwenendo wako mzuri hauwezi kutiliwa shaka. Kwa kuongezea, unapaswa “kushuhudiwa vema na watu walio nje.” Watu wasioamini wanaweza kuchambua imani yako ya Kikristo, lakini hawapaswi kuwa na sababu yoyote ya kutilia shaka unyoofu au mwenendo wako. (Dan. 6:​4, 5) Jiulize hivi: ‘Je, ninajulikana kuwa mtu mwenye jina zuri ndani na nje ya kutaniko?’

5. Unawezaje kuonyesha kwamba wewe ni mtu “anayependa mema”?

5 Ikiwa wewe ni mtu “anayependa mema,” utaona sifa nzuri za wengine na kuwapongeza. Pia, unafurahia kuwatendea wengine mambo mema, na hata kufanya mengi zaidi ya yale unayotarajiwa kufanya. (1 The. 2:8) Kwa nini sifa hiyo ni muhimu sana kwa wazee? Kwa sababu wanatumia muda mwingi kulichunga kutaniko na kushughulikia migawo yao. (1 Pet. 5:​1-3) Ingawa wanatumia muda mwingi kufanya hivyo, shangwe inayotokana na kuwatumikia wengine inazidi kwa mbali jambo lolote wanalojidhabihu.—Mdo. 20:35.

6. Inamaanisha nini kuwa “mkaribishaji wageni”? (Waebrania 13:​2, 16; tazama pia picha.)

6 Unaonyesha kwamba wewe ni “mkaribishaji wageni” unapowatendea wengine mema, kutia ndani wale ambao si rafiki zako wa karibu. (1 Pet. 4:9) Kitabu kimoja cha marejeo kinamfafanua hivi mtu aliye na sifa ya ukaribishaji wageni: “Mlango wa nyumba yake, na moyo wake, ni lazima uwe wazi kwa ajili ya wageni.” Jiulize hivi: ‘Je, ninajulikana kuwa mtu mwenye sifa ya ukaribishaji wageni?’ (Soma Waebrania 13:​2, 16.) Mtu aliye na sifa ya ukaribishaji wageni anashiriki chochote anachoweza pamoja na wageni wake, kutia ndani wale walio na kipato cha chini na watumishi wa Yehova wanaofanya kazi kwa bidii, kama vile waangalizi wa mzunguko na wasemaji wanaotembelea kutaniko.—Mwa. 18:​2-8; Met. 3:27; Luka 14:​13, 14; Mdo. 16:15; Rom. 12:13.

Wenzi wa ndoa Wakristo wakimkaribisha nyumbani mwangalizi wa mzunguko na mke wake (Tazama fungu la 6)


7. Mzee wa kutaniko anaonyeshaje kwamba yeye “si mtu anayependa pesa”?

7 “Si mtu anayependa pesa.” Hilo linamaanisha kwamba hukazii fikira maishani vitu vya kimwili. Iwe wewe ni tajiri au maskini, unatanguliza masilahi ya Ufalme katika kila sehemu ya maisha yako. (Mt. 6:33) Unatumia muda, nguvu, na mali zozote ulizo nazo ili kumwabudu Yehova, kuitunza familia yako, na kulitumikia kutaniko. (Mt. 6:24; 1 Yoh. 2:​15-17) Jiulize hivi: ‘Nina maoni gani kuhusu pesa? Je, ninaridhika na mambo muhimu maishani? Au je, ninakazia fikira kupata pesa nyingi na kujikusanyia vitu vingi vya kimwili?’—1 Tim. 6:​6, 17-19.

8. Ni katika njia zipi unaweza kuonyesha kwamba wewe ni “mwenye kiasi katika mazoea” na ni mtu “anayejidhibiti”?

8 Ikiwa wewe ni “mwenye kiasi katika mazoea” na ni mtu “anayejidhibiti,” una usawaziko katika kila sehemu ya maisha yako. Hilo linamaanisha kwamba utaepuka kula na kunywa kupita kiasi, mavazi na mapambo yako yatakuwa yenye kiasi, na utafanya maamuzi mazuri inapohusu burudani. Hutakuwa mtumwa wa mitindo ya ulimwengu. (Luka 21:34; Yak. 4:4) Unaendelea kuwa mtulivu, hata unapochokozwa. Wewe ‘si mlevi’; na hujulikani kuwa mtu anayekunywa kileo kupita kiasi. Jiulize hivi: ‘Je, mtindo wangu wa maisha unaonyesha kwamba mimi ni mwenye kiasi katika mazoea yangu na ninajidhibiti?’

9. Kuwa “mwenye utimamu wa akili” na “mwenye utaratibu” kunahusisha nini?

9 Ikiwa wewe ni “mwenye utimamu wa akili,” unachanganua mambo kwa makini kwa kutegemea kanuni za Biblia. Umetafakari kwa kina kuhusu kanuni hizo, na hilo limekusaidia kuwa na ufahamu na uelewaji. Hufanyi maamuzi ya haraka-haraka bila kuwa na habari kamili. Badala yake, unahakikisha kwamba una habari zote zinazohitajika. (Met. 18:13) Matokeo ni kwamba unafanya maamuzi yenye usawaziko yanayoonyesha unafuata njia ya Yehova ya kufikiri. Ikiwa wewe ni “mwenye utaratibu,” unapanga mambo vizuri na unatimiza mambo kwa wakati. Unajulikana kuwa mtu anayetegemeka na anayefuata mwongozo. Ikiwa utasitawisha sifa hizo tulizozungumzia, utajifanyia jina zuri. Sasa, acheni tuzungumzie jinsi ya kufikia sifa za Kimaandiko ambazo mzee anapaswa kuwa nazo ili aweke mfano mzuri akiwa kichwa cha familia.

KUWEKA MFANO MZURI UKIWA KICHWA CHA FAMILIA

10. Mwanamume ‘anaisimamiaje nyumba yake vizuri’?

10 Ikiwa wewe ni mume na unatamani kustahili kuwa mzee wa kutaniko, familia yako inahitaji kuwa na sifa nzuri ili ustahili. Hivyo, unahitaji kuwa mtu “anayeisimamia nyumba yake vizuri.” Unahitaji kujulikana kuwa kichwa cha familia mwenye upendo na anayewajibika. Hilo linatia ndani kuongoza katika mambo yote yanayohusu ibada yetu. Kwa nini jambo hilo ni muhimu sana? Mtume Paulo alitoa sababu hii: “Ikiwa mtu hajui jinsi ya kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje kutaniko la Mungu?”—1 Tim. 3:5.

11-12. Kwa nini mwenendo wa watoto wa ndugu anayetamani kustahili kuwa mzee wa kutaniko ni muhimu? (Tazama pia picha.)

11 Ikiwa wewe ni baba, ni lazima watoto wako walio chini ya umri wa miaka 18 wawe “wanaojitiisha na kuchukua mambo kwa uzito.” Unahitaji kuwafundisha na kuwazoeza kwa upendo. Bila shaka, kama watoto wengine, watafurahia kucheka na kucheza. Lakini kwa sababu umewazoeza vizuri, watakuwa watiifu, wenye heshima, na wenye adabu. Pia, ni lazima ufanye yote uwezayo ili kuwasaidia watoto wako wasitawishe uhusiano mzuri na Yehova, waishi kulingana na kanuni za Biblia, na wafanye maendeleo ili kufikia hatua ya ubatizo.

12 “Mwenye watoto wanaoamini ambao hawana mashtaka ya kuwa wapotovu au waasi.” Ikiwa mtoto anayefanya maendeleo au ambaye amebatizwa anatenda dhambi nzito, hilo linawezaje kumwathiri baba yake? Ikiwa baba huyo alipuuza daraka lake la kumzoeza na kumtia nidhamu, inaelekea hatastahili kutumikia akiwa mzee wa kutaniko.—Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1996, ukurasa wa 21, fungu la 6-7.

Vichwa vya familia wanawazoeza watoto wao kwa kuwahusisha katika shughuli mbalimbali zinazohusiana na utumishi mtakatifu (Tazama fungu la 11)


KULITUMIKIA KUTANIKO

13. Unawezaje kuonyesha kwamba wewe ni “mwenye usawaziko,” na ‘si mshupavu’?

13 Akina ndugu wanaoonyesha sifa nzuri za Kikristo ni wenye thamani kutanikoni. Mtu “mwenye usawaziko” anaendeleza amani. Ikiwa unapenda kujulikana kuwa mtu mwenye usawaziko, wasikilize wengine na uwe tayari kukubali maoni yao. Kwa mfano, mnapokuwa katika kikao cha wazee, je, utakuwa tayari kukubali uamuzi unaoungwa mkono na wengi ikiwa hakuna sheria au kanuni ya Biblia inayovunjwa? ‘Si mshupavu’ inamaanisha kwamba husisitizi mambo yafanywe kwa njia yako. Unajua kwamba ni muhimu kusikiliza na kuthamini maoni ya wengine. (Mwa. 13:​8, 9; Met. 15:22) Wewe “si mgomvi” au mwenye “kukasirika upesi.” Badala ya kuwa mkali au mtu asiyetaka makubaliano, wewe ni mpole na mwenye busara. Kwa kuwa wewe ni mtu mwenye kufanya amani, unachukua hatua ya kwanza ili kufanya amani hata katika hali ngumu. (Yak. 3:​17, 18) Maneno yako yenye fadhili yanaweza kubadili mtazamo wa wengine, kutia ndani wapinzani.—Amu. 8:​1-3; Met. 20:3; 25:15; Mt. 5:​23, 24.

14. Maneno “si mtu aliyegeuka hivi karibuni” na “mshikamanifu” yanamaanisha nini?

14 Ndugu anayestahili kuwa mzee “si mtu aliyegeuka hivi karibuni.” Ingawa huhitaji kuwa umebatizwa kwa miaka mingi, unahitaji muda ili kuwa Mkristo mkomavu. Kabla ya kuwekwa rasmi kuwa mzee, lazima uonyeshe kwamba kama Yesu, wewe ni mnyenyekevu na umeridhika kumngojea Yehova akupatie mgawo wowote. (Mt. 20:23; Flp. 2:​5-8) Unaweza kuthibitisha kwamba wewe ni “mshikamanifu” kwa kushikamana na Yehova na viwango vyake vya uadilifu na kwa kufuata miongozo inayotolewa na tengenezo lake.—1 Tim. 4:15.

15. Je, ni lazima mzee awe msemaji mwenye uwezo wa pekee? Eleza.

15 Maandiko yanaonyesha wazi kwamba ni lazima mwangalizi awe “mwenye uwezo wa kufundisha.” Je, hilo linamaanisha kwamba ni lazima uwe msemaji mwenye uwezo wa pekee? Hapana. Ingawa wazee wengi wenye kustahili si wasemaji wenye uwezo wa pekee, wanafundisha kwa njia yenye matokeo katika huduma na kwenye ziara za uchungaji. (Linganisha 1 Wakorintho 12:​28, 29 na Waefeso 4:11.) Hata hivyo, unahitaji kuendelea kuboresha ustadi wako wa kufundisha. Unawezaje kufundisha kwa njia yenye matokeo mazuri zaidi?

16. Unawezaje kuwa mwalimu mwenye matokeo mazuri zaidi? (Tazama pia picha.)

16 “Anayefuata kikamili neno la uaminifu.” Ili upate matokeo zaidi, tegemea Neno la Mungu unapofundisha hadharani na unapotoa shauri faraghani. Uwe mwanafunzi mzuri wa Biblia na wa machapisho yetu. (Met. 15:28; 16:23) Unapojifunza, kazia uangalifu jinsi machapisho yetu yanavyoonyesha matumizi yanayofaa ya Maandiko. Na unapofundisha, jitahidi kugusa mioyo ya wasikilizaji wako. Unaweza kuboresha ufundishaji wako ikiwa utaomba mapendekezo kutoka kwa wazee wenye uzoefu na kuyatumia. (1 Tim. 5:17) Wazee wanahitaji kuwa na ‘uwezo wa kuwatia moyo’ ndugu na dada zao; hata hivyo, nyakati nyingine ni lazima wawape shauri au hata “kuwakaripia.” Iwe wazee wanatia moyo au wanatoa shauri, ni lazima sikuzote wawe wenye fadhili. Ikiwa wewe ni mpole na mwenye upendo, na mafundisho yako yanategemea Neno la Mungu, utakuwa mwalimu mwenye matokeo mazuri kwa sababu utakuwa ukimwiga Mwalimu Mkuu, Yesu.—Mt. 11:​28-30; 2 Tim. 2:24.

Mtumishi wa huduma akitumia vizuri nafasi ya kushirikiana na mzee mwenye uzoefu kujifunza jinsi ya kufundisha kupitia Biblia. Pia, mtumishi wa huduma huyo anafanya mazoezi ya hotuba mbele ya kioo (Tazama fungu la 16)


ENDELEA KUJITAHIDI ILI USTAHILI

17. (a) Ni mambo gani yanayoweza kuwasaidia watumishi wa huduma waendelee kujitahidi ili wastahili kuwa wazee wa kutaniko? (b) Wazee wanapaswa kukumbuka nini wanapochunguza ikiwa ndugu ana sifa za kustahili kuwa mzee? (Tazama sanduku “Uwe Mwenye Kiasi Unapochanganua Sifa za Kustahili za Wengine.”)

17 Baada ya kuchunguza sifa za kustahili kuwa mzee, huenda baadhi ya watumishi wa huduma wakahisi kwamba hawawezi kamwe kustahili. Lakini kumbuka kwamba Yehova na tengenezo lake halitarajii uonyeshe sifa hizo kwa ukamilifu. (1 Pet. 2:21) Na roho yenye nguvu ya Yehova ndiyo inayokusaidia kusitawisha sifa hizo. (Flp. 2:13) Je, kuna sifa hususa ambayo ungependa kuiboresha? Sali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. Fanya utafiti kuhusu sifa hiyo, na umwombe mmoja wa wazee akupe mapendekezo ya jinsi ya kuiboresha.

18. Watumishi wote wa huduma wanatiwa moyo kufanya nini?

18 Acheni sisi sote, kutia ndani wale ambao tayari wanatumikia wakiwa wazee wa kutaniko, tuendelee kusitawisha sifa zilizozungumziwa katika makala hii. (Flp. 3:16) Je, wewe ni mtumishi wa huduma? Jitahidi kustahili kuwa mzee! Mwombe Yehova akuzoeze na akufinyange ili akutumie hata zaidi na ulitumikie kutaniko. (Isa. 64:8) Yehova na abariki jitihada zako za kustahili kutumikia ukiwa mzee wa kutaniko.

WIMBO 101 Kufanya Kazi Pamoja kwa Umoja