Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 46

WIMBO 49 Kufurahisha Moyo wa Yehova

Akina Ndugu—Je, Mnajitahidi Kustahili Kuwa Watumishi wa Huduma?

Akina Ndugu—Je, Mnajitahidi Kustahili Kuwa Watumishi wa Huduma?

“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”MDO. 20:35.

JAMBO KUU

Kuwatia moyo akina ndugu waliobatizwa wajitahidi kustahili kuwa watumishi wa huduma.

1. Mtume Paulo aliwaonaje watumishi wa huduma?

 WATUMISHI wa huduma wanatimiza kazi muhimu kwenye makutaniko. Ni wazi kwamba mtume Paulo aliwathamini wanaume hao washikamanifu. Kwa mfano, alipowaandikia barua Wakristo jijini Filipi, aliwasalimu kihususa watumishi wa huduma pamoja na wazee wa kutaniko.—Flp. 1:1.

2. Ndugu anayeitwa Luis anahisije kuhusu mgawo wake akiwa mtumishi wa huduma?

2 Ndugu wengi waliobatizwa, iwe ni vijana au wazee, wanapata shangwe kubwa wanapotumikia wakiwa watumishi wa huduma. Kwa mfano, Devan alikuwa na umri wa miaka 18 alipowekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma. Kwa upande mwingine, ndugu anayeitwa Luis, aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma akiwa na umri wa miaka 50 na kitu. Luis anafafanua hisia za watumishi wengi wa huduma anaposema hivi: “Ninahisi likiwa pendeleo kubwa kutumikia nikiwa mtumishi wa huduma, hasa ninapofikiria upendo mwingi ninaoonyeshwa na kutaniko!”

3. Tutajibu maswali gani?

3 Ikiwa wewe ni ndugu aliyebatizwa na bado hujawekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma, je, unaweza kujiwekea lengo hilo? Ni nini kinachoweza kukuchochea kufanya hivyo? Na ni sifa gani za Kimaandiko unazohitaji kufikia? Katika makala hii, tutachunguza majibu ya maswali hayo. Lakini kwanza, acheni tuchunguze majukumu ya watumishi wa huduma.

WATUMISHI WA HUDUMA WANA MAJUKUMU GANI?

4. Watumishi wa huduma wana majukumu gani? (Tazama pia picha.)

4 Mtumishi wa huduma ni ndugu aliyebatizwa ambaye amewekwa rasmi na roho takatifu ili kuwasaidia wazee kutimiza kazi nyingi muhimu kutanikoni. Baadhi ya watumishi wa huduma huhakikisha kwamba wahubiri wana maeneo ya kutosha ya kuhubiri na machapisho kwa ajili ya huduma. Wengine wanasaidia katika usafi na udumishaji wa Jumba la Ufalme. Pia, watumishi wa huduma wanatumikia wakiwa wakaribishaji na kushughulikia mfumo wa sauti na video wakati wa mikutano ya kutaniko. Kazi nyingi zinazofanywa na watumishi wa huduma ni kazi za mikono. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ni kwamba watumishi wa huduma ni wanaume wa kiroho; wanaompenda Yehova na kuishi kulingana na viwango vyake vya uadilifu. Na wanawapenda sana ndugu na dada zao Wakristo. (Mt. 22:​37-39) Ndugu aliyebatizwa anawezaje kujitahidi kustahili kuwa mtumishi wa huduma?

Watumishi wa huduma wanamwiga Yesu kwa kujitoa ili kuwatumikia wengine (Tazama fungu la 4)


5. Ndugu anawezaje kujitahidi kufikia pendeleo la kuwa mtumishi wa huduma?

5 Biblia inataja sifa za kustahili ambazo ndugu anahitaji kuwa nazo ili kuwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma. (1 Tim. 3:​8-10, 12, 13) Unaweza kujitahidi kufikia pendeleo hilo kwa kujifunza sifa hizo za Kimaandiko na kisha kufanya yote unayoweza ili kuzionyesha. Lakini kwanza, unahitaji kuchunguza kwa uangalifu nia yako ya kujitahidi kufikia pendeleo hilo.

NI NINI KINACHOKUCHOCHEA KUWA MTUMISHI WA HUDUMA?

6. Ni nini kinachopaswa kukuchochea kuwatumikia ndugu na dada zako? (Mathayo 20:28; tazama pia picha.)

6 Fikiria kumhusu Yesu Kristo ambaye ndiye kielelezo chetu kikuu. Kila kitu alichofanya kilichochewa na upendo kwa Baba yake na kwa wanadamu. Upendo huo ulimchochea kufanya kazi kwa bidii, kuwahudumia wengine, na hata kufanya kazi zilizoonwa na wengine kuwa za hali ya chini. (Soma Mathayo 20:28; Yoh. 13:​5, 14, 15) Ikiwa unachochewa na upendo, Yehova atakubariki na kukusaidia kufikia lengo lako la kuwa mtumishi wa huduma.—1 Kor. 16:14; 1 Pet. 5:5.

Kupitia mfano wake, Yesu anawafundisha mitume wake wawatumikie wengine kwa unyenyekevu badala ya kujitafutia umashuhuri (Tazama fungu la 6)


7. Kwa nini ndugu anapaswa kuepuka mtazamo wa kujitakia makuu?

7 Leo, watu ulimwenguni wanavutiwa na watu wanaojiona kuwa muhimu. Lakini watu wa Yehova ni tofauti. Kama Yesu, ndugu anayechochewa na upendo, hatamani kuwatawala wengine, au kutaka aonekane na wengine kuwa mtu muhimu. Ikiwa mtu anayejitafutia makuu atawekwa rasmi kutanikoni, huenda akakataa kufanya kazi zinazoonwa kuwa za hali ya chini ambazo zinahitaji kufanywa ili kuwatunza kondoo wa Yehova wenye thamani. Huenda akajiona kuwa mtu wa maana sana hivi kwamba asiweze kufanya kazi hizo. (Yoh. 10:12) Yehova hatabariki jitihada za mtu yeyote anayechochewa na kiburi au mtazamo wa kujitakia makuu.—1 Kor. 10:​24, 33; 13:​4, 5.

8. Yesu aliwapatia mitume wake ushauri gani?

8 Nyakati nyingine, hata wanafunzi wa Yesu walitaka kufikia mapendeleo wakiwa na nia mbaya. Fikiria jambo walilofanya Yakobo na Yohana, wanafunzi wawili wa Yesu. Walimwomba Yesu awapatie migawo ya pekee katika Ufalme wake. Yesu hakuwapongeza kwa mtazamo wao wa kujitakia makuu. Badala yake, aliwaambia mitume wote 12 hivi: “Yeyote anayetaka kuwa mkubwa kati yenu lazima awe mhudumu wenu, na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kati yenu lazima awe mtumwa wa wote.” (Marko 10:​35-37, 43, 44) Ndugu wanaojitahidi kufikia mapendeleo wakiwa na nia nzuri, yaani, ya kuwatumikia wengine, watakuwa baraka kutanikoni.—1 The. 2:8.

NI NINI KINACHOWEZA KUIMARISHA TAMAA YAKO YA KUJITAHIDI KUFIKIA MAPENDELEO?

9. Unawezaje kuimarisha tamaa yako ya kujitahidi kufikia mapendeleo?

9 Ni wazi kwamba unampenda Yehova na unataka kuwatumikia wengine. Ingawa hivyo, huenda ukakosa hamu ya kufanya kazi ambazo hufanywa na watumishi wa huduma. Unawezaje kuimarisha tamaa yako ya kutumikia? Kwa nini usifikirie shangwe utakayopata kwa kuwatumikia ndugu na dada zako? Yesu alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Mdo. 20:35) Yesu aliishi kulingana na kanuni hiyo. Alipata shangwe ya kweli kwa kuwatumikia wengine. Wewe pia unaweza kupata shangwe hiyo.

10. Yesu alionyeshaje kwamba alifurahia kuwatumikia wengine? (Marko 6:​31-34)

10 Fikiria mfano unaoonyesha jinsi Yesu alivyopata furaha kwa kuwatumikia wengine. (Soma Marko 6:​31-34.) Pindi moja, Yesu na mitume wake walikuwa wamechoka. Walikuwa wakielekea mahali pasipo na watu ili wapumzike. Lakini umati wa watu ulitangulia kufika huko, wakitarajia kufundishwa na Yesu. Angeweza kusema hapana kwa sababu yeye na wanafunzi wake “hawakuwa na wakati hata wa kula.” Au Yesu angeweza kuwaambia waondoke baada ya kuwafundisha mambo machache. Lakini kwa kuwa alichochewa na upendo, ‘alianza kuwafundisha mambo mengi.’ Na aliendelea kuwafundisha hadi “ilipokaribia jioni.” (Marko 6:35) Alifanya hivyo, si kwa sababu alilazimika, bali kwa sababu “aliwasikitikia.” Alitaka kuwafundisha kwa sababu aliwapenda. Yesu alipata shangwe kubwa kwa kuwatumikia wengine.

11. Yesu aliwasaidiaje wasikilizaji wake kwa njia hususa? (Tazama pia picha.)

11 Yesu alifanya mengi zaidi ya kuwafundisha tu watu. Aliwaandalia pia mahitaji yao ya kimwili. Aliandaa chakula kimuujiza, kisha wanafunzi wake wakawagawia watu. (Marko 6:41) Kwa kufanya hivyo, aliwafundisha wanafunzi wake jinsi ya kuwatumikia wengine. Pia, aliwaonyesha kwamba kazi za mikono, kama ambazo mara nyingi hufanywa na watumishi wa huduma, ni muhimu. Wazia shangwe ambayo mitume walikuwa nayo walipofanya kazi pamoja na Yesu ya kugawa chakula kilichoandaliwa kimuujiza hadi ‘wote wakala na kushiba’! (Marko 6:42) Bila shaka, hiyo si pindi pekee ambayo Yesu alitanguliza masilahi ya wengine. Alitumia maisha yake yote akiwa duniani kuwatumikia watu. (Mt. 4:23; 8:16) Yesu alipata shangwe nyingi na aliridhika alipowafundisha wengine na kuwaandalia mahitaji yao. Hapana shaka kwamba wewe pia utapata shangwe nyingi unapojitahidi bila ubinafsi kufikia pendeleo la kuwa mtumishi wa huduma.

Upendo wako kwa Yehova na tamaa yako ya kuwatumikia wengine itakuchochea kulitumikia kutaniko kwa njia yoyote (Tazama fungu la 11) a


12. Kwa nini hatupaswi kuhisi kwamba hatuna kipawa chochote tunachoweza kutumia ili kulisaidia kutaniko?

12 Usivunjike moyo ikiwa unahisi kwamba huna kipawa au uwezo wowote wa pekee. Ni wazi kwamba una sifa nzuri ambazo unaweza kuzitumia ili kulisaidia kutaniko. Unaweza kunufaika kwa kusali na kutafakari maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 12:​12-30, na kuona jinsi unavyoweza kuyatumia. Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba wewe pia, kama watumishi wengine wote wa Yehova, unahitajika na unatimiza jukumu muhimu kutanikoni. Ikiwa kwa sasa huna sifa za kustahili kuwa mtumishi wa huduma, usivunjike moyo. Badala yake, endelea kufanya yote unayoweza ili kumtumikia Yehova na kuwasaidia ndugu na dada zako. Uwe na uhakika kwamba wazee wa kutaniko watazingatia uwezo wako na kukupatia migawo unayoweza kutimiza.—Rom. 12:​4-8.

13. Sifa nyingi za kustahili za wanaume waliowekwa rasmi zinawahusu nani wengine?

13 Fikiria sababu nyingine moja inayopaswa kukuchochea kujitahidi kufikia pendeleo la kuwa mtumishi wa huduma: Sifa nyingi za kustahili kuwa mtumishi wa huduma zinawahusu Wakristo wote. Kwa kweli, Wakristo wote wanapaswa kumkaribia Yehova, kupata shangwe inayotokana na kutoa, na kuweka mfano mzuri katika maisha ya Kikristo. Sifa ambazo tayari unazo. Hivyo, ni mambo gani hususa ambayo ndugu anaweza kufanya ili kujitahidi kufikia pendeleo hilo?

JINSI YA KUFIKIA PENDELEO LA KUWA MTUMISHI WA HUDUMA

14. “Kuchukua mambo kwa uzito” kunamaanisha nini? (1 Timotheo 3:​8-10, 12)

14 Acheni sasa tuchunguze baadhi ya sifa za kustahili kuwa mtumishi wa huduma zinazotajwa kwenye 1 Timotheo 3:​8-10, 12. (Soma.) Mtumishi wa huduma anapaswa “kuchukua mambo kwa uzito.” Maneno hayo yanaweza pia kutafsiriwa kuwa “anayestahili kuheshimiwa,” au “mwenye staha.” Hilo halimaanishi kwamba hupaswi kamwe kucheka au kufurahia utani. (Mhu. 3:​1, 4) Hata hivyo, unapaswa kuchukua migawo yako yote kwa uzito. Ikiwa unajulikana kuwa mwenye kutegemeka, utaheshimiwa kutanikoni.

15. Maneno ‘si mwenye ndimi mbili’ na ‘si mwenye pupa ya mapato yasiyo ya haki’ yanamaanisha nini?

15 ‘Si mwenye ndimi mbili’ inamaanisha kwamba wewe ni mnyoofu na unategemeka. Unatimiza ahadi zako, na huwadanganyi wengine. (Met. 3:32) ‘Si mwenye pupa ya mapato yasiyo ya haki” inamaanisha kwamba wewe ni mnyoofu katika mambo ya kibiashara na unaposhughulikia masuala ya pesa. Hutawatumia vibaya Wakristo wenzako ili kujinufaisha kifedha.

16. (a) Maneno ‘si mwenye kunywa divai nyingi’ yanamaanisha nini? (b) Kuwa na “dhamiri safi” kunamaanisha nini?

16 ‘Si mwenye kunywa divai nyingi’ inamaanisha kwamba hutumii kileo kupita kiasi au kujulikana kuwa mtu anayekunywa kileo kupita kiasi. Kuwa na “dhamiri safi” kunamaanisha kwamba unaishi kulingana na viwango vya Yehova. Ingawa wewe si mkamilifu, unafurahia amani inayotokana na kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu.

17. Ndugu anawezaje kuonyesha kwamba anategemeka ‘anapojaribiwa kama anafaa’? (1 Timotheo 3:10; tazama pia picha.)

17 ‘Kujaribiwa kama unafaa’ kunamaanisha umeonyesha kwamba wewe ni mwenye kutegemeka unapopewa migawo mbalimbali. Kwa hiyo, wazee wanapokupa mgawo, fuata kwa uangalifu maagizo yao na miongozo inayotolewa na tengenezo. Hakikisha unaelewa mgawo wako unahusisha nini na wakati unaopaswa kuukamilisha. Unapotimiza kila mgawo kwa bidii, wengine kutanikoni watatambua jambo hilo na kuona maendeleo yako mazuri. Wazee, jitahidini kuwazoeza akina ndugu waliobatizwa. (Soma 1 Timotheo 3:10.) Je, kuna ndugu waliobatizwa katika kutaniko lenu ambao wako katika miaka ya mapema ya utineja au wadogo zaidi? Je, wao ni mfano mzuri katika mazoea yao ya kujifunza kibinafsi? Je, wao hutoa maelezo katika mikutano na kushiriki katika huduma ya shambani kwa ukawaida? Ikiwa ndivyo, wapeni migawo inayowafaa kulingana na umri wao na hali zao. Kwa njia hiyo, ndugu hao vijana wanaweza “kujaribiwa kama wanafaa.” Kisha, wanapofikia miaka ya mwisho ya utineja wanaweza kustahili kuwa watumishi wa huduma.

Kwa kuwapatia migawo akina ndugu waliobatizwa, wazee wanaweza kuwajaribu “kama wanafaa” (Tazama fungu la 17)


18. Maneno “hawana shtaka” yanamaanisha nini?

18 Maneno “hawana shtaka” yanamaanisha kwamba hakuna shtaka lolote la kweli la kufanya kosa zito linaloweza kuletwa dhidi yako. Bila shaka, huenda Wakristo wakashtakiwa kwa uwongo. Yesu alishtakiwa kwa uwongo, na alitabiri kwamba wafuasi wake wangekabili hali hiyo. (Yoh. 15:20) Hata hivyo, ikiwa utadumisha mwenendo wako ukiwa safi, kama Yesu alivyofanya, utajulikana kuwa mwenye sifa nzuri kutanikoni.—Mt. 11:19.

19. Kuwa “waume wa mke mmoja” kunahusisha nini?

19 “Waume wa mke mmoja.” Ikiwa umefunga ndoa, ni lazima ushikamane na mpango wa awali wa Yehova wa ndoa, yaani, ndoa ya mume mmoja na mke mmoja. (Mt. 19:​3-9) Mwanamume Mkristo hapaswi kamwe kufanya uasherati. (Ebr. 13:4) Lakini mengi zaidi yanahusika. Ni lazima uwe mshikamanifu kwa mke wako, na hupaswi kamwe kuwakazia fikira wanawake wengine kwa njia isiyofaa.—Ayu. 31:1.

20. Mwanamume anawezaje kuisimamia “vizuri” nyumba yake?

20 “Wanaosimamia vizuri watoto wao na nyumba zao wenyewe.” Ikiwa wewe ni kichwa cha familia, ni lazima uchukue kwa uzito majukumu yako. Ongoza ibada ya familia kwa ukawaida. Shiriki katika huduma pamoja na kila mtu katika familia yako mara nyingi iwezekanavyo. Wasaidie watoto wako wasitawishe uhusiano wa karibu na Yehova. (Efe. 6:4) Mwanamume anayetunza familia yake anaonyesha kwamba anaweza kulitunza kutaniko.—Linganisha 1 Timotheo 3:5.

21. Ikiwa kwa sasa wewe si mtumishi wa huduma, unaweza kufanya nini?

21 Akina ndugu, ikiwa kwa sasa wewe si mtumishi wa huduma, tafadhali sali na ufikirie mambo yaliyotajwa katika makala hii. Jifunze kuhusu sifa za kustahili kuwa mtumishi wa huduma na ujitahidi kuzifikia. Tafakari kuhusu upendo wako kwa Yehova na kwa ndugu na dada zako. Na uimarishe tamaa yako ya kuwatumikia. (1 Pet. 4:​8, 10) Jitahidi ili ujionee shangwe inayotokana na kuwatumikia ndugu na dada zako kutanikoni. Na Yehova atabariki sana jitihada zako za kufikia pendeleo la kuwa mtumishi wa huduma!—Flp. 2:13.

WIMBO 17 “Nataka”

a MAELEZO YA PICHA: Kushoto, kwa unyenyekevu, Yesu anawahudumia wanafunzi wake; kulia, mtumishi wa huduma akimsaidia ndugu aliyezeeka.