Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 45

WIMBO 138 Kichwa Chenye Mvi —Taji la Uzuri

Jifunze Kutokana na Maneno ya Mwisho ya Wanaume Waaminifu

Jifunze Kutokana na Maneno ya Mwisho ya Wanaume Waaminifu

“Je, hekima haipatikani miongoni mwa waliozeeka, na je, uelewaji hauji kwa sababu ya kuishi muda mrefu?”AYU. 12:12.

JAMBO KUU

Kumtii Yehova Mungu hutuletea baraka sasa na uzima wa milele wakati ujao.

1. Kwa nini tunaweza kujifunza kutoka kwa wale wenye umri mkubwa?

 SISI sote tunahitaji mwongozo tunapofanya maamuzi muhimu maishani. Tunaweza kupata sehemu kubwa ya mwongozo huo kutoka kwa wazee wa kutaniko na Wakristo wengine wakomavu. Ikiwa wana umri mkubwa sana kuliko sisi, hatupaswi kupuuza ushauri wao na kuuona kuwa umepitwa na wakati. Yehova anataka tujifunze kutoka kwa wale wenye umri mkubwa. Wamekuwa na muda mrefu zaidi wa kupata uzoefu, uelewaji, na hekima kuliko sisi.—Ayu. 12:12.

2. Makala hii itazungumzia nini?

2 Katika nyakati za Biblia, Yehova aliwatumia watu waaminifu wenye umri mkubwa kuwatia moyo na kuwaongoza watu wake. Kwa mfano, mfikirie Musa, Daudi, na mtume Yohana. Waliishi katika nyakati tofauti, na hali zao zilitofautiana sana. Walipokaribia mwisho wa maisha yao, waliwapa ushauri wenye hekima wale walio na umri mdogo kuliko wao. Kila mmoja wa wanaume hao waaminifu wenye umri mkubwa alikazia umuhimu wa kumtii Mungu. Yehova alihifadhi maneno yao yenye hekima kwa ajili yetu leo. Iwe sisi ni vijana au wazee, tunaweza kunufaika kwa kuchunguza ushauri waliotoa. (Rom. 15:4; 2 Tim. 3:16) Katika makala hii, tutachunguza maneno ya mwisho ya wanaume hao watatu wenye umri mkubwa na mambo tunayoweza kujifunza kutokana na maneno hayo.

“MTAISHI KWA MUDA MREFU”

3. Ni katika njia zipi Musa alimtumikia Mungu?

3 Musa alijitoa kikamili kwa Yehova. Alitumikia akiwa nabii, mwamuzi, kamanda, na mwanahistoria. Musa alikuwa na uzoefu mwingi sana! Aliliongoza taifa la Israeli kutoka utumwani Misri na alijionea miujiza mingi ya Yehova. Yehova alimtumia kuandika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, Zaburi ya 90, na inawezekana Zaburi ya 91. Pia, inaelekea aliandika kitabu cha Ayubu.

4. Musa aliwatia moyo akina nani, na kwa nini?

4 Muda mfupi kabla ya kifo chake, akiwa na umri wa miaka 120, Musa aliwakusanya Waisraeli wote ili kuwakumbusha kuhusu mambo yote ambayo Yehova alikuwa amewafanyia. Walipokuwa vijana, baadhi ya wasikilizaji wake walikuwa wamejionea ishara na miujiza mingi ambayo Yehova alikuwa amefanya, pamoja na hukumu Zake dhidi ya Misri. (Kut. 7:​3, 4) Walikuwa wametembea katikati ya maji yaliyogawanyika ya Bahari Nyekundu na kujionea jeshi la Farao likiangamizwa. (Kut. 14:​29-31) Wakiwa nyikani, walijionea ulinzi na utunzaji wa Yehova. (Kum. 8:​3, 4) Sasa taifa hilo likiwa tayari kuingia katika Nchi ya Ahadi, Musa alitumia fursa hiyo ya mwisho kabla ya kifo chake ili kuwatia moyo. a

5. Maneno ya mwisho ya Musa yanayopatikana kwenye Kumbukumbu la Torati 30:​19, 20 yaliwahakikishia nini Waisraeli?

5 Musa alisema nini? (Soma Kumbukumbu la Torati 30:​19, 20.) Taifa la Israeli lilikuwa na tarajio zuri sana la wakati ujao. Wakiwa na baraka za Yehova, Waisraeli wangeweza kuishi kwa muda mrefu katika nchi ambayo alikuwa amewaahidi. Na kwa kweli nchi hiyo ilikuwa maridadi na yenye rutuba! Musa aliifafanua nchi hiyo kuwa yenye “majiji makubwa na yenye kupendeza ambayo hamkujenga, nyumba zilizojaa vitu vizuri vya aina mbalimbali ambavyo hamkufanya kazi ili kuvipata, visima ambavyo hamkuchimba, na mashamba ya mizabibu na mizeituni ambayo hamkupanda.”—Kum. 6:​10, 11.

6. Kwa nini Mungu aliruhusu mataifa mengine yalishinde taifa la Israeli?

6 Pia, Musa aliwapa Waisraeli onyo. Ili waendelee kuishi katika nchi hiyo maridadi, walihitaji kutii amri za Yehova. Musa aliwahimiza ‘wachague uzima’ kwa kumsikiliza Yehova na “kushikamana naye.” Hata hivyo, Waisraeli walimkataa Yehova. Hivyo, baada ya muda Mungu aliwaruhusu Waashuru na baadaye Wababiloni kuwashinda Waisraeli na kuwapeleka uhamishoni.—2 Fal. 17:​6-8, 13, 14; 2 Nya. 36:​15-17, 20.

7. Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Musa? (Tazama pia picha.)

7 Tunajifunza nini? Utii huongoza kwenye uzima wa milele. Kama Waisraeli ambao walikuwa wamekaribia kuingia kwenye Nchi ya Ahadi, sisi pia tumekaribia kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa, ambapo tutaona dunia ikibadilishwa na kuwa paradiso. (Isa. 35:1; Luka 23:43) Ibilisi na roho wake waovu hawatakuwepo tena. (Ufu. 20:​2, 3) Dini za uwongo hazitawapotosha tena watu wamwache Yehova. (Ufu. 17:16) Serikali za wanadamu hazitawakandamiza tena watu walio chini ya utunzaji wao. (Ufu. 19:​19, 20) Yehova hataruhusu waasi wawepo katika Paradiso. (Zab. 37:​10, 11) Watu wote wanaoishi katika Paradiso watatii sheria za Yehova za uadilifu, zinazoendeleza umoja na amani. Hivyo, watu wote watapendana na kutumainiana. (Isa. 11:9) Hilo ni tumaini zuri sana! Zaidi ya hilo, ikiwa tutamtii Yehova, tutaweza kuendelea kuishi katika paradiso duniani, si tu kwa karne kadhaa, bali kwa umilele wote.—Zab. 37:29; Yoh. 3:16.

Ikiwa tutamtii Yehova, tutaweza kuishi katika dunia Paradiso, si tu kwa karne kadhaa bali kwa umilele wote (Tazama fungu la 7)


8. Ahadi ya uzima wa milele ilimsaidiaje mmishonari mmoja aliyetumikia kwa muda mrefu barani Afrika? (Yuda 20, 21)

8 Ikiwa tutaendelea kuweka karibu akilini ahadi ya Mungu ya kuishi milele, tutatamani kushikamana naye haidhuru matatizo ambayo huenda tukakabili. (Soma Yuda 20, 21.) Pia, ahadi hiyo inaweza kutusaidia kushinda udhaifu mbalimbali wa kibinafsi. Mmishonari aliyetumikia kwa miaka mingi barani Afrika, ambaye alipambana kwa muda mrefu na udhaifu fulani alisema hivi: “Kutambua kwamba tumaini langu la kuishi milele lilikuwa hatarini, kulifanya niazimie hata zaidi kuendelea kupambana na tatizo langu na kutoa dua kwa Yehova kwa bidii. Kwa msaada wake, niliweza kulishinda tatizo hilo.”

“NDIPO UTAKAPOFANIKIWA”

9. Daudi alikabili majaribu gani maishani?

9 Daudi alikuwa mfalme wa watu wa Yehova na alikuwa mshikamanifu kwa Mungu. Pia, alikuwa mwanamuziki, mshairi, shujaa, na nabii. Alikabili majaribu mengi. Kwa miaka kadhaa, aliishi akiwa mkimbizi, alipokuwa akimkimbia Mfalme Sauli mwenye wivu. Baada ya kuwa mfalme, Daudi alihitaji kukimbia ili kuokoa uhai wake wakati Absalomu, mwana wake, alipojaribu kuunyakua ufalme kutoka kwake. Licha ya matatizo ambayo Daudi alikabili na udhaifu wake mwenyewe, aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu hadi mwisho wa maisha yake. Yehova alimfafanua Daudi kuwa ‘mtu aliyeupendeza moyo Wake.’ Kwa kweli, tunapaswa kusikiliza ushauri wenye hekima wa Daudi!—Mdo. 13:22; 1 Fal. 15:5.

10. Kwa nini Daudi alimpa ushauri Sulemani, mwana wake ambaye angekuwa mfalme?

10 Kwa mfano, fikiria shauri ambalo Daudi alimpatia Sulemani, mwana wake ambaye angekuwa mfalme anayefuata. Mwanamume huyo kijana alikuwa amechaguliwa na Yehova ili aendeleze ibada safi na kujenga hekalu ambalo lingemtukuza Mungu. (1 Nya. 22:5) Sulemani angekabili hali ngumu. Daudi angemwambia nini? Acheni tuone.

11. Kulingana na andiko la 1 Wafalme 2:​2, 3, Daudi alimpa ushauri gani Sulemani, na matokeo yalikuwaje alipotii ushauri huo? (Tazama pia picha.)

11 Daudi alisema nini? (Soma 1 Wafalme 2:​2, 3.) Daudi alimwambia mwana wake kwamba ikiwa angemtii Yehova, angefanikiwa maishani. Na kwa miaka mingi, Yehova alimsaidia Sulemani kupata mafanikio kwa njia nyingi. (1 Nya. 29:​23-25) Alijenga hekalu lenye utukufu na kuandika vitabu kadhaa vya Biblia, na baadhi ya maneno yake yanapatikana katika sehemu nyingine za Biblia. Alijulikana sana kwa sababu ya hekima na utajiri wake. (1 Fal. 4:34) Lakini kama Daudi alivyoeleza, Sulemani angefanikiwa ikiwa tu angemtii Yehova Mungu. Kwa kusikitisha, baadaye Sulemani alianza kuabudu miungu mingine. Hivyo, alipoteza kibali cha Yehova na hekima ya kutawala kwa uadilifu na haki.—1 Fal. 11:​9, 10; 12:4.

Maneno ya mwisho ya Daudi kwa Sulemani, mwana wake, yanatusaidia kuelewa kwamba ikiwa tutamtii Yehova, atatupatia hekima ya kufanya maamuzi mazuri (Tazama fungu la 11-12) b


12. Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Daudi?

12 Tunajifunza nini? Utii hutuletea mafanikio. (Zab. 1:​1-3) Bila shaka, Yehova hajaahidi kutupatia utajiri na utukufu ambao alimpa Sulemani. Lakini ikiwa tutamtii Mungu wetu, atatupatia hekima ambayo itatusaidia kufanya maamuzi mazuri. (Met. 2:​6, 7; Yak. 1:5) Kanuni zake zinaweza kutusaidia katika mambo hususa kama vile kazi, elimu, burudani, na pesa. Kutumia hekima inayotoka kwa Mungu kutatulinda dhidi ya madhara ya kudumu. (Met. 2:​10, 11) Tutakuwa na marafiki wazuri. Na tutapata mwongozo tunaohitaji ili kuwa na maisha ya familia yenye furaha.

13. Carmen alipataje mafanikio maishani?

13 Carmen, anayeishi nchini Msumbiji, alifikiri kwamba elimu ya juu ndiyo siri ya mafanikio maishani. Alijiunga na chuo kikuu na kusomea usanifu majengo. Dada huyo aliandika hivi: “Nilipenda mambo niliyokuwa nikijifunza. Lakini masomo hayo yalichukua muda wangu mwingi na kutumia nguvu zangu nyingi. Nilikuwa chuoni kuanzia saa moja na nusu asubuhi hadi saa kumi na mbili jioni. Ilikuwa vigumu kuhudhuria mikutano, na hali yangu ya kiroho ilidhoofika. Moyoni mwangu nilitambua kwamba nilikuwa nikijaribu kuwatumikia mabwana wawili.” (Mt. 6:24) Carmen alisali kuhusu hali yake na kufanya utafiti kwenye machapisho yetu. Anaongezea hivi: “Baada ya kupata ushauri mzuri kutoka kwa ndugu wakomavu na kutoka kwa mama yangu, niliamua kuacha chuo kikuu na kuanza utumishi wa wakati wote. Hilo lilinisaidia kufanya maamuzi bora kabisa maishani, na sijutii uamuzi wangu.”

14. Musa na Daudi walikuwa na ujumbe gani wa msingi?

14 Musa na Daudi walimpenda Yehova na walijua kwamba ni muhimu sana kumtii. Katika maneno yao ya mwisho, waliwatia moyo watu waliowasikiliza wafuate mfano wao kwa kushikamana na Yehova Mungu wao. Pia, waliwaonya watu hao kwamba ikiwa wangemwacha Yehova wangepoteza kibali chake na pia baraka ambazo alikuwa amewaahidi. Ushauri wao ni wenye thamani kwetu leo. Karne nyingi baadaye, mtumishi mwingine wa Yehova alionyesha umuhimu wa kuwa waaminifu kwa Mungu.

“SINA SHANGWE KUBWA KULIKO HII”

15. Mtume Yohana alijionea nini katika maisha yake?

15 Yohana alikuwa mtume ambaye alipendwa na Yesu Kristo. (Mt. 10:2; Yoh. 19:26) Yohana alishirikiana na Yesu katika huduma yake yote, aliona miujiza ya Yesu, na alishikamana naye katika nyakati ngumu. Alimwona Yesu alipokuwa akiuawa na alimwona baada ya kufufuliwa. Pia, alijionea jinsi Ukristo ulivyoenea katika karne ya kwanza, kutoka kuwa kikundi kidogo cha waaminifu hadi habari njema ilipokuwa “[imehubiriwa] katika uumbaji wote chini ya mbingu.”—Kol. 1:23.

16. Ni nani ambao wamenufaika na barua za Yohana?

16 Karibu na mwishoni mwa maisha yake marefu, Yohana alipata pendeleo la kutumiwa kuandika Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Alirekodi ‘ufunuo wenye kustaajabisha aliopata kupitia Yesu Kristo.’ (Ufu. 1:1) Yohana aliandika kitabu cha Injili kinachoitwa kwa jina lake. Pia, aliandika barua tatu zilizoongozwa na roho. Aliandika barua yake ya tatu kwa Mkristo mwaminifu aliyeitwa Gayo, ambaye Yohana alimwona kuwa mtoto wake mpendwa wa kiroho. (3 Yoh. 1) Kufikia wakati huo, ni lazima kulikuwa na watu wengi ambao Yohana aliwaona kuwa watoto wake wa kiroho. Mambo ambayo mwanamume huyo mwaminifu mwenye umri mkubwa aliandika, yamewatia moyo wafuasi wote wa Yesu mpaka sasa.

17. Kulingana na 3 Yohana 4, ni jambo gani linalotupatia shangwe kubwa?

17 Yohana aliandika nini? (Soma 3 Yohana 4.) Yohana aliandika kuhusu shangwe inayotokana na kumtii Mungu. Kufikia wakati ambao Yohana aliandika barua yake ya tatu, baadhi ya watu walikuwa wakieneza mafundisho ya uwongo na kusababisha migawanyiko. Hata hivyo, wengine waliendelea ‘kutembea katika kweli.’ Walimtii Yehova na walikuwa wakiendelea ‘kutembea kulingana na amri zake.’ (2 Yoh. 4, 6) Wakristo hao waaminifu walimfurahisha Yohana na Yehova pia.—Met. 27:11.

18. Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Yohana?

18 Tunajifunza nini? Uaminifu hutuletea shangwe. (1 Yoh. 5:3) Kwa mfano, tuna shangwe kwa sababu tunajua kwamba tunamfurahisha Yehova. Anashangilia anapoona tukipinga majaribu ya ulimwengu huu na kuikubali kweli. (Met. 23:15) Malaika mbinguni wanashangilia pia. (Luka 15:10) Sisi pia tunafurahi tunapoona ndugu na dada zetu wakiendelea kuwa waaminifu, hasa wanapokabili majaribu. (2 The. 1:4) Kisha, mfumo huu utakapoharibiwa, tutaridhika kujua kwamba tulionyesha ushikamanifu wetu kwa Yehova hata katika ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani.

19. Dada anayeitwa Rachel alisema nini kuhusu kuwafundisha wengine kweli? (Tazama pia picha.)

19 Tunapata shangwe, hasa tunapowafundisha wengine ile kweli. Rachel, anayeishi katika Jamhuri ya Dominika, anahisi ni pendeleo kubwa sana kuwafundisha watu kumhusu Yehova, Mungu wetu. Anasema hivi anapowakumbuka watoto wake wa kiroho: “Ni vigumu kuelezea shangwe ninayohisi ninapoona wale ambao ninawafundisha wakisitawisha upendo wao kwa Yehova, wakimfanya kuwa nanga yao, na kufanya mabadiliko maishani ili kumfurahisha. Hisia hizo za shangwe zinazidi kwa mbali jitihada na mambo yoyote ambayo huenda nilijidhabihu ili kuwafundisha.”

Tunapata shangwe tunapowafundisha wengine kumpenda na kumtii Yehova (Tazama fungu la 19)


NUFAIKA KUTOKANA NA MANENO YA MWISHO YA WANAUME WAAMINIFU

20. Ni katika njia gani tunafanana na Musa, Daudi, na Yohana?

20 Musa, Daudi, na Yohana waliishi katika nyakati na hali ambazo zilikuwa tofauti na zetu. Lakini tumefanana nao kwa njia nyingi. Walimtumikia Mungu wa kweli, kama sisi tunavyofanya. Kama wao, tunasali kwa Yehova, tunamtegemea, na tunatafuta mwongozo wake. Na kama wanaume hao wa zamani, tuna uhakika kwamba Yehova huwabariki sana wale wanaomtii.

21. Tukifuata ushauri wa wanaume waaminifu wenye umri mkubwa kama vile Musa, Daudi, na Yohana, tutapata baraka gani?

21 Hivyo, acheni tufuate ushauri ulio katika maneno ya mwisho ya wanaume hao wenye umri mkubwa, kwa kutii amri za Yehova. Kisha, tutakuwa na mafanikio ya kweli katika mambo yote tunayofanya. Tutapata uzima na ‘tutaishi kwa muda mrefu,’ naam, milele! (Kum. 30:20) Na tutakuwa na shangwe inayotokana na kumfurahisha Baba yetu wa mbinguni, ambaye hutimiza ahadi zake zote kwa njia ambazo hatuwezi kuwazia kamwe.—Efe. 3:20.

WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia

a Waisraeli wengi ambao waliona miujiza ya Yehova katika Bahari Nyekundu walikufa kabla ya kuiona Nchi ya Ahadi. (Hes. 14:​22, 23) Yehova alisema kwamba wanaume wenye umri wa miaka 20 na zaidi wangekufa nyikani. (Hes. 14:29) Hata hivyo, Yoshua, Kalebu, na wengi kati ya wale wenye umri chini ya miaka 20, na kabila la Lawi walifaulu kuona Yehova akitimiza ahadi yake wakati taifa la Israeli lilipovuka Mto Yordani na kuingia Kanaani.—Kum. 1:​24-40.

b MAELEZO YA PICHA: Kushoto: Daudi akimpatia ushauri wa mwisho Sulemani, mwana wake. Kulia: Wanafunzi katika Shule ya Utumishi wa Painia wakinufaika na elimu ya kitheokrasi.