Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Mambo Gani Yanayoweza Kukusaidia Kujifunza kwa Ukawaida?

Ni Mambo Gani Yanayoweza Kukusaidia Kujifunza kwa Ukawaida?

JE, NI vigumu kwako kuendelea kufanya funzo lako la Biblia la kibinafsi kwa ukawaida na kulifurahia? Huenda sisi sote tumehisi hivyo nyakati fulani. Lakini fikiria mambo mengine tunayofanya kwa ukawaida, kama vile kuoga. Kuoga kunachukua muda na jitihada, lakini baada ya kuoga tunahisi tumeburudika! Kujifunza Biblia kunaweza kulinganishwa na ‘kuoshwa kwa maji kupitia neno’ kunakoburudisha. (Efe. 5:26) Fikiria baadhi ya mapendekezo yanayoweza kukusaidia:

  • Panga ratiba. Kujifunza Biblia kibinafsi ni mojawapo ya“mambo muhimu zaidi” ambayo Mkristo hapaswi kuyapuuza. (Flp. 1:10) Ili uweze kufuata ratiba yako, kwa nini usiiweke mahali ambapo inaonekana, kama vile kwenye ubao au mlango wa friji? Au unaweza kuweka mlio kwenye simu utakaokukumbusha muda wa kujifunza unapokaribia.

  • Zingatia hali yako. Je, ni rahisi zaidi kwako kukaza fikira kwa muda mrefu au kwa vipindi vifupi-vifupi vya wakati? Wewe ndiye unayejua hali zako vizuri zaidi. Hivyo, panga vipindi vyako vya kujifunza kulingana na hali zako. Ikiwa huna hamu ya kujifunza muda uliopanga unapofika, kwa nini usiamue kujifunza hata kwa dakika kumi tu? Kwa kujifunza hata kwa muda huo mfupi, utatimiza mengi zaidi kuliko ikiwa ungeamua kuacha kabisa. Na mara unapoanza, huenda ukachochewa kuendelea kujifunza zaidi.—Flp. 2:13.

  • Chagua mapema habari za kujifunza. Ikiwa utaketi kwanza ndipo uanze kufikiria utajifunza nini, huenda ukashindwa ‘kuutumia vizuri kabisa wakati wako.’ (Efe. 5:16) Kwa nini usiweke orodha ya makala au habari ambazo ungependa kujifunza? Unapojiuliza jambo fulani akilini, liandike swali hilo. Na mwishoni mwa kila kipindi cha kujifunza, unaweza kuongeza kwenye orodha yako mambo mengine ambayo ungependa kujifunza.

  • Uwe mwenye kunyumbulika. Jitahidi kuwa mwenye kunyumbulika unapopanga ratiba yako, inapohusu muda utakaotumia au habari utakazochagua kujifunza. Jambo muhimu si wakati, muda utakaotumia, au jambo unalojifunza, bali ni jinsi unavyojifunza kwa ukawaida.

Tunanufaika sana tunapokuwa na ratiba ya kujifunza kwa ukawaida. Tunamkaribia zaidi Yehova, tunajifunza kutenda kwa hekima, na tunahisi tumeburudishwa.—Yos. 1:8.