Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Alituimarisha Katika Kipindi cha Vita na cha Amani

Yehova Alituimarisha Katika Kipindi cha Vita na cha Amani

Paul: Tulikuwa tumefurahi sana! Ilikuwa Novemba 1985, na tulikuwa tukielekea kwenye mgawo wetu wa kwanza wa umishonari nchini Liberia, Afrika Magharibi. Ndege yetu ilitua nchini Senegal. Anne alisema hivi: “Baada ya saa moja tu, tutakuwa tumefika Liberia!” Kisha, tukasikia tangazo hili: “Abiria wa Liberia ni lazima mshuke kwenye ndege. Baadhi ya watu wamejaribu kuipindua serikali, hivyo hatuwezi kwenda huko.” Kwa siku kumi zilizofuata, tuliishi na wamishonari wengine nchini Senegal, tukisikiliza taarifa za habari kutoka nchini Liberia kuhusu watu wengi waliouawa na kuhusu vizuizi vya kutotoka nje jioni vilivyowekwa na serikali, na ikiwa mtu angeonekana nje, angeuawa.

Anne: Kwa kawaida, sisi ni watu ambao huepuka matukio yenye kusisimua sana. Isitoshe, tangu utotoni nilijulikana kama Annie Mwenye Wasiwasi Sana. Mimi huwa na wasiwasi hata ninapotaka kuvuka barabara! Hata hivyo, tulikuwa tumeazimia kufika kwenye mgawo wetu.

Paul: Mimi na Anne tulizaliwa kwenye maeneo yaliyo na umbali wa kilomita nane tu, magharibi mwa Uingereza. Sote tulianza upainia tulipomaliza tu shule ya sekondari; mimi nilitiwa moyo sana na wazazi wangu na Anne alitiwa moyo na mama yake. Waliunga mkono kikamili tamaa yetu ya kuwa watumishi wa wakati wote. Nikiwa na umri wa miaka 19, nilipata pendeleo la kutumikia Betheli, na Anne akajiunga nami tulipofunga ndoa, mwaka wa 1982.

Tulipohitimu Shule ya Gileadi, Septemba 8, 1985

Anne: Tulipenda utumishi wa Betheli, lakini sikuzote tulitamani kutumikia kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa. Tamaa hiyo iliongezeka tulipofanya kazi Betheli pamoja na wamishonari wa zamani. Tulisali kihususa kuhusu jambo hilo kila usiku kwa miaka mitatu, na tulifurahi sana tulipopata mwaliko wa kuhudhuria darasa la 79 la Shule ya Gileadi, mwaka wa 1985! Tulipata mgawo wa kutumikia nchini Liberia, Afrika Magharibi.

TULIIMARISHWA NA UPENDO WA NDUGU NA DADA ZETU

Paul: Tulisafiri kwenye ndege ya kwanza iliyoruhusiwa kuingia nchini Liberia. Watu walikuwa wakiogopa sana na bado vizuizi vya kutotoka nje jioni vilikuwepo. Watu walikuwa wakiogopa sana hivi kwamba ikiwa gari lingetoa mlio mkubwa wenye kushtua katika eneo la soko, watu wangepiga kelele na kukimbia. Tulisoma pamoja sehemu za kitabu cha Zaburi kila usiku ili tupate utulivu. Lakini kwa kweli tuliupenda sana mgawo wetu. Anne alitumikia shambani akiwa mmishonari, nami nilitumikia Betheli, nikifanya kazi pamoja na John Charuk. a Alikuwa mzoefu na alielewa vizuri hali za ndugu na dada zetu, mambo yaliyomsaidia kunizoeza.

Anne: Ni nini kilichotusaidia kuupenda haraka mgawo wetu nchini Liberia? Ni ndugu na dada zetu. Walikuwa wachangamfu, wenye urafiki, na waaminifu. Tulijenga uhusiano wa karibu pamoja nao; nao wakawa familia yetu mpya. Ushauri waliotupatia ulituimarisha kiroho. Tulifurahia sana kuhubiri huko. Wenye nyumba wangekasirika ikiwa ungeondoka mapema! Watu walizungumzia maswali ya Biblia mitaani, hivyo, ilikuwa rahisi kujiunga katika mazungumzo yao. Tulikuwa na wanafunzi wengi wa Biblia hivi kwamba ilikuwa vigumu kujifunza nao wote. Hilo lilikuwa tatizo zuri sana!

TULIIMARISHWA LICHA YA KUOGOPA

Kuwatunza wakimbizi katika Betheli ya Liberia, mwaka wa 1990

Paul: Mwaka wa 1989, baada ya miaka minne ya amani ya kadiri, kulitokea mabadiliko yenye kushtua—vita vya wenyewe kwa wenyewe. Julai 2, 1990, vikosi vya waasi viliteka maeneo yaliyo karibu na Betheli. Kwa miezi mitatu, tulipoteza mawasiliano na watu wote, kutia ndani familia zetu na makao makuu ya ulimwenguni pote. Kulikuwa na vurugu, upungufu wa chakula, na watu walibakwa. Hali hiyo mbaya iliendelea kwa miaka 14 na kuathiri nchi nzima.

Anne: Watu katika baadhi ya makabila walikuwa wakipigana na watu wa makabila mengine na kuwauwa. Wapiganaji wenye silaha nzito waliovaa mavazi ya ajabu walikuwa wakitembea mitaani, na walipora vitu katika kila nyumba. Baadhi yao walisema kwamba kwa maoni yao kuua wanadamu ni kama tu “kuchinja kuku.” Kulikuwa na rundo la maiti kwenye vizuizi vya barabarani, na baadhi ya vizuizi hivyo vilikuwa karibu na ofisi ya tawi. Mashahidi waaminifu waliuawa, kutia ndani wamishonari wetu wapendwa wawili.

Mashahidi walihatarisha uhai wao kwa kuwaficha Mashahidi kutoka katika makabila yaliyokuwa yakiwindwa na kuuawa. Wamishonari na Wanabetheli waliwaficha watu pia. Baadhi ya Mashahidi waliokimbia na kuja Betheli walilala ghorofa ya chini, na wengine waliishi pamoja nasi katika vyumba vyetu kwenye ghorofa ya juu. Kwenye chumba chetu tuliishi pamoja na familia ya watu saba.

Paul: Kila siku, wapiganaji walijaribu kuingia Betheli ili kuona kama tumewaficha watu. Tulikuwa na mfumo wa ulinzi uliohusisha watu wanne: wawili walitazama kupitia dirishani na wawili walienda kwenye lango ili kuzungumza na wapiganaji. Ikiwa wale wawili waliokuwa langoni wangeweka mikono yao mbele, basi hakukuwa na hatari. Lakini ikiwa wangeweka mikono yao nyuma, ilimaanisha kwamba wapiganaji wana hasira, hivyo wale waliotazama dirishani wangewaficha ndugu na dada zetu haraka.

Anne: Baada ya majuma mengi, kikundi kimoja cha wapiganaji wenye hasira kililazimisha kuingia Betheli. Mimi na dada mwingine tulijifungia bafuni ambapo kulikuwa na kabati lenye sehemu ambayo mtu angeweza kujificha. Kabati hilo lilikuwa na rafu ambayo iliweza kuchomoka, na mtu angeweza kujificha kwenye sehemu ndogo iliyo ndani yake. Kisha, rafu ingerudishwa mahali pake. Dada yetu alijificha humo. Wapiganaji walikuja mahali tulipokuwa, wakiwa na bunduki zao. Wakagonga kwa hasira mlango wetu. Paul aliwasihi hivi: “Mke wangu yuko bafuni.” Ile rafu ilipiga kelele nilipokuwa nikiirudisha, na kupanga tena vitu kwenye kabati kulichukua muda mrefu. Nilihisi huenda wapiganaji hao wangejiuliza ninafanya nini, hivyo niliogopa na kuanza kutetemeka kwa nguvu mwili mzima. Ningewezaje kufungua mlango wa bafuni nikiwa na wasiwasi huo? Nilisali kimyakimya, nikimsihi Yehova anisaidie. Kisha, nikafungua mlango na nikafaulu kuwasalimu kwa utulivu. Mmoja wao alinisukuma na kuingia kwa nguvu bafuni, akaenda moja kwa moja kwenye lile kabati, akalifungua, na kuhamisha-hamisha vitu. Hakuamini kwamba hakupata chochote. Kisha, yeye na kikundi chake walipekua vyumba vingine na pia kwenye dari. Lakini kwa mara nyingine tena, hawakupata chochote.

KWELI ILIZIDI KUNG’AA

Paul: Kwa miezi mingi, hatukuwa na chakula cha kutosha. Lakini chakula cha kiroho ndicho kilichotuimarisha. Ibada ya asubuhi ya Betheli ndiyo ilikuwa “kiamsha kinywa” pekee tulichopata, na sote tulithamini sana nguvu za kiroho tulizopata kutokana na ibada hiyo.

Ikiwa hatungekuwa na chakula na maji, tungelazimika kuondoka kwenye ofisi ya tawi, hivyo, wale waliokuwa wamejificha wangeweza kuuawa. Mara nyingi, Yehova alitupatia mahitaji yetu kwa wakati unaofaa na kwa njia zenye kustaajabisha. Yehova alitutimizia mahitaji yetu na alitusaidia kudhibiti woga wetu.

Kadiri ulimwengu ulivyozidi kuwa na giza, ndivyo nuru ya kweli ilivyozidi kung’aa. Ndugu na dada zetu wengi walihitaji kukimbia tena na tena ili kuokoa uhai wao, lakini imani yao iliendelea kuwa imara na walibaki wakiwa watulivu licha ya hali ngumu. Baadhi yao walisema kwamba kuvumilia hali ngumu wakati wa vita kuliwapa “mazoezi mazuri kwa ajili ya dhiki kuu.” Wazee wa makutaniko na akina ndugu vijana wenye ujasiri walijitoa ili kusimamia mambo. Walipohamia eneo lingine, akina ndugu na dada walishikamana, wakaanzisha maeneo mapya ya kuhubiri na kufanya mikutano kwenye Majumba ya Ufalme ya muda yaliyokuwa msituni. Mikutano ilikuwa kama mahali pa kujificha wakati wa dhoruba, na kazi ya kuhubiri iliwasaidia Mashahidi kukabiliana na hali ngumu. Tulipokuwa tukisambaza misaada, tuliguswa moyo kupokea maombi mengi ya mikoba kwa ajili ya huduma badala ya nguo. Watu waliohuzunika na kukatishwa tamaa walisikiliza habari njema. Walishangaa sana kuona jinsi Mashahidi walivyokuwa na furaha na mtazamo mzuri; waling’aa kama nuru kwenye giza hilo. (Mt. 5:​14-16) Bidii waliyokuwa nayo akina ndugu hata iliwasaidia baadhi ya wapiganaji katili kuwa ndugu zetu.

TULIIMARISHWA TULIPOKABILI TUKIO LENYE KUVUNJA MOYO

Paul: Pindi fulani tulihitaji kuondoka nchini, mara tatu tuliondoka kwa muda mfupi na mara mbili kwa mwaka mzima. Dada mmoja mmishonari alifafanua vizuri hisia zetu aliposema hivi: “Kwenye Shule ya Gileadi, tulifundishwa kuweka moyo wetu kwenye mgawo wetu, nasi tulifanya hivyo. Kwa hiyo, kuwaacha ndugu zetu katika hali kama hizo kulikuwa kama kuung’oa moyo wetu!” Tulifurahi kwamba tungeweza kusaidia utendaji nchini Liberia tukiwa katika nchi zilizo jirani.

Tukirudi kwa furaha nchini Liberia, mwaka wa 1997

Anne: Mei 1996, tukiwa watu wanne tulianza safari kwa gari la ofisi ya tawi ambalo lilikuwa na rekodi nyingi muhimu za ofisi ya tawi. Tulitaka kusafiri kwenda kwenye eneo la mji lililokuwa salama ambalo lilikuwa umbali wa kilomita 16. Wakati huohuo eneo tulilokuwa lilivamiwa. Wapiganaji wenye hasira walipiga risasi hewani, wakasimamisha gari letu, wakatutoa nje watatu kati yetu, na wakaendesha gari huku Paul akiwa bado ndani ya gari. Tulisimama hapo tukiwa tumeshtuka sana. Ghafla, tulimwona Paul akitembea katikati ya umati kuelekea mahali tulipokuwa, huku damu zikitiririka kwenye paji la uso. Mwanzoni, tulifikiri kwamba amepigwa risasi, lakini hatimaye tulitambua kwamba ikiwa angekuwa amepigwa risasi asingeweza kutembea! Mpiganaji mmoja alikuwa amempiga usoni alipokuwa akimsukuma ili atoke kwenye gari. Tunashukuru kwamba halikuwa jeraha kubwa.

Kulikuwa na gari la jeshi karibu yetu lililokuwa limejaa watu wenye woga na lilikuwa tayari kuondoka. Tuliamua kupanda, lakini kwa kuwa ndani hakukuwa na nafasi, tulining’inia nje. Dereva aliendesha gari kwa kasi sana, hivi kwamba karibu tuanguke. Tulimwomba asimamishe gari, lakini aliogopa kufanya hivyo. Kwa njia fulani tulifaulu kushikilia mpaka mwisho wa safari, lakini gari liliposimama tulikuwa tumechoka sana na tulikuwa tukitetemeka kwa sababu ya woga.

Paul: Tukiwa hatuna kitu chochote isipokuwa nguo chafu na zilizochanika ambazo tulikuwa tumevaa, tulitazamana na kushangaa inawezekanaje kwamba bado tuko hai. Tulilala kwenye eneo la wazi kando ya helikopta iliyochakaa na yenye mashimo ya risasi, ambayo siku iliyofuata ilitubeba mpaka Sierra Leone. Tulishukuru sana kwamba tuko hai, lakini tulikuwa na wasiwasi sana kuhusu hali ya ndugu na dada zetu nchini Liberia.

TULIIMARISHWA TULIPOKABILI CHANGAMOTO NYINGINE AMBAYO HATUKUTARAJIA

Anne: Tulipofika Betheli jijini Freetown, Sierra Leone, tulikuwa salama na tulitunzwa vizuri. Lakini nilianza kukumbuka mambo mabaya yaliyotokea nchini Liberia. Mchana nilikuwa na hofu kwamba huenda jambo baya litatokea na nisingeweza kufikiri vizuri. Kila kitu kilichonizunguka hakikuonekana kuwa halisi. Usiku ningeamka nikitokwa na jasho, nilitetemeka na kuhisi jambo baya lilikuwa karibu kutokea. Sikuweza kupumua vizuri. Paul alinishika na kusali pamoja nami. Tuliimba nyimbo za Ufalme mpaka nilipoacha kutetemeka. Nilihisi kwamba nilikuwa nikirukwa na akili na nisingeweza kuendelea kutumikia nikiwa mmishonari.

Sitasahau kamwe kilichotokea baada ya hapo. Juma hilohilo tulipokea magazeti mawili. Moja lilikuwa gazeti la Amkeni! la Juni 8, 1996. Gazeti hilo lilikuwa na makala yenye kichwa, “Kukabiliana na Mishiko ya Hofu ya Ghafla.” Sasa nilielewa kilichokuwa kikinipata. Gazeti la pili lilikuwa la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1996, lililokuwa na makala yenye kichwa, “Wao Hupata Wapi Nguvu Zao?” Gazeti hilo la Mnara wa Mlinzi lilikuwa na picha ya kipepeo aliyejeruhiwa. Makala hiyo ilieleza kwamba kama kipepeo anavyoweza kuendelea kula na kupepea licha ya mabawa yake kujeruhiwa vibaya, ndivyo sisi pia, kwa msaada wa roho ya Yehova tunavyoweza kuwasaidia wengine hata ikiwa tumeumizwa kihisia. Hicho kilikuwa chakula chenye kuimarisha kutoka kwa Yehova kwa wakati unaofaa kabisa. (Mt. 24:45) Kufanya utafiti kuhusiana na jambo hilo na kukusanya makala ambazo zilizungumzia jambo hilo kulinisaidia. Baada ya muda, dalili nilizokuwa nazo za ugonjwa wa kupata wasiwasi sana baada ya tukio lenye kutisha, zilipotea.

TULIIMARISHWA TULIPOHITAJI KUZOEA MGAWO MPYA

Paul: Tulikuwa na furaha sana kila mara tuliporudi Liberia baada ya kulazimika kuondoka. Kufikia mwishoni mwa 2004, tulikuwa kwenye mgawo wetu kwa karibu miaka 20. Vita vilikuwa vimekwisha. Kulikuwa na mipango ya ujenzi katika ofisi ya tawi. Lakini ghafla tulipewa mgawo mpya.

Hiyo ilikuwa hali ngumu sana kwetu. Tulikuwa na uhusiano wa karibu sana na familia yetu ya kiroho nchini Liberia. Tungewezaje kuwaacha? Kwa kuwa tulikuwa tumeacha familia zetu tulipoenda katika Shule ya Gileadi, tulikuwa tumejionea jinsi kujikabidhi mikononi mwa Yehova kunavyoleta baraka nyingi, hivyo tulikubali mgawo huo. Mgawo wetu mpya ulikuwa katika nchi jirani ya Ghana.

Anne: Tulilia sana tulipoondoka Liberia. Tulishangaa wakati Frank, ndugu mwenye umri mkubwa na mwenye hekima, alipotuambia hivi: “Ni lazima mtusahau!” Kisha akafafanua hivi: “Tunajua kwamba hamtatusahau kamwe, lakini ni lazima mfanye mgawo wenu mpya kwa moyo wenu wote. Mgawo huo umetoka kwa Yehova, hivyo wakazieni fikira ndugu na dada wa huko.” Hilo lilituimarisha ili tuweze kukabiliana na changamoto ya kuanza maisha mapya mahali ambapo watu wachache walitufahamu na kila kitu kilikuwa kipya kwetu.

Paul: Hata hivyo, haikuchukua muda mrefu kuipenda familia yetu mpya ya kiroho nchini Ghana. Kulikuwa na Mashahidi wengi huko! Tulijifunza mambo mengi kutokana na ushikamanifu na imani yenye nguvu ya marafiki wetu wapya. Kisha, baada ya kutumikia nchini Ghana kwa miaka 13, tulipata mgawo mwingine ambao hatukutarajia. Tulipewa mgawo wa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Afrika Mashariki, nchini Kenya. Ingawa tuliwakosa sana rafiki zetu katika migawo yetu iliyopita, mara moja tulihisi tukiwa na uhusiano wa karibu na ndugu na dada waaminifu nchini Kenya. Na bado tunatumikia katika eneo kubwa ambalo lina uhitaji mkubwa sana.

Tukiwa na marafiki wapya katika eneo la ofisi ya tawi ya Afrika Mashariki, mwaka wa 2023

MAMBO TULIYOJIFUNZA KATIKA MIGAWO YETU

Anne: Kwa miaka mingi, nimekabili hali ngumu zilizofanya nitetemeke kwa hofu. Hali za hatari na zinazoleta mkazo zinaweza kutuathiri kihisia na kimwili pia. Hatulindwi kimuujiza kutokana na mambo hayo. Ninaposikia sauti za risasi zikifyatuliwa, tumbo linasokota kwa sababu ya wasiwasi na mikono inakufa ganzi. Lakini nimejifunza kutegemea msaada wote ambao Yehova anatupatia ili kutuimarisha, kutia ndani utegemezo wa ndugu na dada zetu. Na nimejionea kwamba ninapodumisha ratiba yangu ya kiroho, Yehova anaweza kunisaidia kuendelea na mgawo wangu.

Paul: Huenda baadhi ya watu wakauliza, “Je, mnapenda mgawo wenu?” Nchi unayotumikia inaweza kuwa maridadi, lakini pia inaweza kubadilika na kuwa eneo lenye misukosuko na hatari. Hivyo, ni jambo gani tunalopenda zaidi ya nchi tunayotumikia? Ni ndugu na dada wenye thamani ambao ni familia yetu. Licha ya kwamba tuna malezi tofauti, kwa kweli sisi sote tuna akili moja. Tulifikiri kwamba tumetumwa ili kuwatia moyo, lakini ukweli ni kwamba wao ndio wametuimarisha sisi.

Kila mara tunapohama, tunajionea muujiza wa siku zetu, yaani, undugu wetu. Maadamu sisi ni sehemu ya kutaniko, tuna familia na mahali ambapo tunahisi tuko nyumbani. Tuna uhakika kwamba ikiwa tutaendelea kumtegemea Yehova, atatupatia nguvu tunazohitaji.—Flp. 4:13.

a Tazama simulizi la maisha la John Charuk, “I Am Grateful to God and Christ,” katika toleo la Kiingereza la gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1973.