Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unamruhusu Mfinyanzi Mkuu Akufinyange?

Je, Unamruhusu Mfinyanzi Mkuu Akufinyange?

“Tazama! Kama udongo mkononi mwa mfinyanzi, ndivyo ninyi mlivyo mkononi mwangu.”—YER. 18:6.

NYIMBO: 60, 22

1, 2. Kwa nini Mungu alimwona Danieli kuwa “mtu mwenye kutamanika sana,” na tunawezaje kuwa watiifu kama yeye?

WAYAHUDI waliokuwa mateka walipoingia katika Babiloni la kale, waliona jiji lililojaa sanamu na watu waliokuwa watumwa wa roho waovu. Hata hivyo, Wayahudi waaminifu kama vile Danieli na waandamani wake watatu, walikataa kufinyangwa na mtazamo wa Wababiloni. (Dan. 1:6, 8, 12; 3:16-18) Danieli na waandamani wake waliazimia kujitoa kikamili kwa Yehova akiwa Mfinyanzi wao, na walifaulu. Danieli aliishi Babiloni karibu maisha yake yote; lakini malaika wa Mungu alisema kwamba alikuwa “mtu mwenye kutamanika sana.”—Dan. 10:11, 19.

2 Katika nyakati za Biblia, mfinyanzi angefinyanga udongo ndani ya kalibu ili kutokeza umbo alilotaka. Waabudu wa kweli leo wanamtambua Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu, na hivyo ana mamlaka ya kuwafinyanga watu na mataifa. (Soma Yeremia 18:6.) Pia, Mungu ana mamlaka ya kutufinyanga tukiwa mtu mmoja-mmoja. Hata hivyo, anatambua kwamba tuna uhuru wa kuchagua na anataka tujitiishe kwake kwa hiari. Acheni tufikirie jinsi tunavyoweza kuendelea kuwa kama udongo laini mikononi mwa Mungu, katika mambo matatu yafuatayo: (1) Tunaweza kuepukaje mazoea ambayo yanaweza kufanya iwe vigumu kwetu kukubali ushauri wa Mungu? (2) Tunaweza kusitawishaje sifa zitakazotusaidia kuwa udongo laini na tuendelee kujitiisha? (3) Wazazi Wakristo wanaweza kujitiishaje kwa Mungu wanapowafinyanga watoto wao?

EPUKA MAZOEA YANAYOWEZA KUFANYA MOYO WAKO UWE MGUMU

3. Ni mazoea gani yanayoweza kufanya moyo wetu uwe mgumu? Toa mfano.

3 Andiko la Methali 4:23 linasema hivi: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” Tunapaswa kuwa macho dhidi ya mazoea gani yanayoweza kufanya moyo wetu uwe mgumu? Yanatia ndani kiburi kinachopita kiasi, mazoea ya kufanya dhambi, na kukosa imani. Mambo hayo yanaweza kutokeza roho ya kutotii na uasi. (Dan. 5:1, 20; Ebr. 3:13, 18, 19) Mfalme Uzia wa Yuda alikuwa na kiburi. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 26:3-5, 16-21.) Mwanzoni, Uzia alifanya “yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova,” na “akaendelea kuwa na mwelekeo wa kumtafuta Mungu.” Lakini “mara tu alipopata nguvu, moyo wake ukawa na majivuno,” ingawa Mungu ndiye aliyempa nguvu hizo! Hata alijaribu kufukiza uvumba hekaluni, pendeleo ambalo lilikuwa la makuhani wa familia ya Haruni pekee. Kisha, makuhani walipomkataza, Uzia mwenye kiburi akawa na ghadhabu! Matokeo yalikuwa nini? Yehova alimnyenyekeza mfalme huyo mwenye kiburi, naye alikufa akiwa mwenye ukoma.—Met. 16:18.

4, 5. Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa tutashindwa kuepuka kiburi? Toa mfano.

4 Tusipokuwa macho ili kuepuka kiburi, sisi pia tunaweza kuanza ‘kujifikiria wenyewe kuliko ilivyo lazima kufikiri,’ na huenda tukafikia hatua ya kukataa ushauri wa Kimaandiko. (Rom. 12:3; Met. 29:1) Mfikirie mzee Mkristo anayeitwa Jim, ambaye alitofautiana na wazee wenzake kuhusu jambo fulani kutanikoni. Jim anaeleza hivi: “Niliwaambia ndugu hao kwamba hawakuwa na upendo, na nikawaacha wakiendelea na mkutano.” Miezi sita baadaye, alihamia kutaniko jirani lakini hakuwekwa kuwa mzee. Anakiri hivi: “Nilivunjika moyo sana. Nilijiona kuwa mwadilifu kupita kiasi, hivyo nikaacha kweli.” Jim hakutenda kwa miaka kumi. Anasema hivi: “Nilikuwa mwenye kiburi hivyo niliumia sana, na nikaanza kumlaumu Yehova kwa mambo yaliyokuwa yakinipata. Kwa miaka mingi, ndugu walinitembelea na kujaribu kunisaidia, lakini nilikataa msaada wao.”

5 Mfano wa Jim unaonyesha jinsi kiburi kinavyoweza kutufanya tutetee matendo yetu, na hivyo iwe vigumu kwetu kufinyangwa. (Yer. 17:9) Jim anasema hivi: “Nilishindwa kuacha kukazia fikira makosa ya watu wengine.” Je, umewahi kuumizwa kihisia na Mkristo mwenzako au kwa sababu ya kupoteza mapendeleo fulani? Ikiwa ndivyo, ulitendaje? Je, ulikuwa mwenye kiburi? Au ulijitahidi kufanya amani na ndugu yako na kubaki mshikamanifu kwa Yehova?—Soma Zaburi 119:165; Wakolosai 3:13.

6. Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa tunazoea kufanya dhambi?

6 Mazoea ya kufanya dhambi, kutia ndani kufanya dhambi kisiri, yanaweza kufanya iwe vigumu kwetu kukubali ushauri kutoka kwa Mungu. Hivyo inakuwa rahisi zaidi kwetu kufanya dhambi. Ndugu mmoja alisema kwamba baada ya muda fulani mwenendo wake usiofaa uliacha kumsumbua. (Mhu. 8:11) Ndugu mwingine aliyekuwa na zoea la kutazama ponografia, alikiri hivi: “Nilianza kuwachambua wazee.” Zoea lake lilikuwa likimwumiza kiroho. Mwishowe, mwenendo wake ulijulikana, na akapokea msaada ambao alihitaji sana. Bila shaka, sisi si wakamilifu. Hata hivyo, ikiwa tutaanza kuwachambua wengine au kutetea mwenendo wetu mbaya badala ya kumwomba Mungu atusamehe na atusaidie, huenda ikawa moyo wetu umeanza kuwa mgumu.

7, 8. (a) Waisraeli wa kale walionyeshaje jinsi ukosefu wa imani unavyoweza kufanya mioyo iwe migumu? (b) Tunajifunza nini?

7 Mfano unaotusaidia kuelewa jinsi ukosefu wa imani unavyoweza kufanya mioyo yetu iwe migumu ni Waisraeli waliokombolewa na Yehova kutoka Misri. Taifa hilo lilishuhudia miujiza mingi ambayo Mungu alifanya kwa niaba yao. Baadhi ya miujiza hiyo ilikuwa ya pekee sana! Hata hivyo, walipokaribia Nchi ya Ahadi, walianza kukosa imani. Badala ya kumtumaini Yehova, walianza kuogopa na kumnung’unikia Musa. Hata walitaka kurudi Misri ambako walikuwa watumwa! Yehova alihuzunika sana. Alisema hivi: “Watu hawa wataendelea kunitendea bila heshima mpaka wakati gani?” (Hes. 14:1-4, 11; Zab. 78:40, 41) Kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao na ukosefu wa imani, kizazi hicho kiliangamia nyikani.

8 Leo, kadiri tunavyokaribia dunia mpya, imani yetu inajaribiwa. Tunapaswa kuchunguza ubora wa imani yetu. Kwa mfano, tunaweza kuchunguza maoni yetu kuhusu maneno ya Yesu katika Mathayo 6:33. Jiulize hivi: ‘Je, mambo ninayotanguliza na maamuzi yangu yanaonyesha kwamba ninaamini kabisa maneno ya Yesu? Je, ningeamua kukosa mikutano au utumishi wa shambani ili nipate pesa zaidi? Nitafanya nini nikishinikizwa kutumia muda mrefu zaidi kazini? Je, nitaruhusu ulimwengu unifinyange nifanane nao na labda hata niache kweli?’

9. Kwa nini tunapaswa ‘kuendelea kujijaribu’ kama tuko katika imani, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

9 Kwa mfano, fikiria mtumishi wa Yehova ambaye anasitasita kufuata viwango vya Biblia kuhusu marafiki, watu waliotengwa na ushirika, au burudani. Jiulize hivi: ‘Je, nina maoni kama hayo?’ Tukigundua kwamba mioyo yetu imeanza kuwa migumu, tunahitaji kuchunguza imani yetu haraka iwezekanavyo! Biblia inatushauri hivi: “Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani, endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.” (2 Kor. 13:5) Tunapaswa kujichunguza kwa unyoofu na kutumia Neno la Mungu sikuzote ili kurekebisha fikira zetu.

ENDELEA KUWA KAMA UDONGO LAINI

10. Ni nini kitatusaidia tuwe kama udongo laini mikononi mwa Yehova?

10 Mungu anatumia Neno lake, kutaniko la Kikristo, na huduma ya shambani kutusaidia tuendelee kuwa kama udongo laini. Kama maji yanavyolainisha udongo, kusoma Biblia kila siku na kuitafakari kunaweza kutusaidia tuwe kama udongo laini mikononi mwa Yehova. Yehova aliwaamuru wafalme wa Israeli wajiandikie nakala ya Sheria ya Mungu na waisome kila siku. (Kum. 17:18, 19) Mitume walitambua kwamba ilikuwa muhimu kusoma Maandiko na kuyatafakari ili wafanikiwe katika huduma. Walinukuu na kutaja Maandiko mengi ya Kiebrania walipoandika barua na waliwatia moyo wengine waliowahubiria wafanye vivyo hivyo. (Mdo. 17:11) Leo, sisi pia tunaona umuhimu wa kusoma Neno la Mungu kila siku na kulitafakari. (1 Tim. 4:15) Kufanya hivyo kutatusaidia tubaki wanyenyekevu machoni pa Yehova na tuendelee kuwa udongo laini mikononi mwake.

Tumia maandalizi ya Mungu ili uendelee kuwa udongo laini (Tazama fungu la 10 hadi 13)

11, 12. Yehova anaweza kutumiaje kutaniko la Kikristo kutufinyanga kulingana na mahitaji yetu? Toa mfano.

11 Kupitia kutaniko la Kikristo, Yehova anatufinyanga kulingana na mahitaji yetu tukiwa mtu mmoja-mmoja. Jim, aliyetajwa mwanzoni alianza kubadili mtazamo wake mzee mmoja alipoanza kupendezwa naye kibinafsi. Jim anasema: “Mzee huyo hakunilaumu hata mara moja wala kunichambua. Badala yake alidumisha mtazamo mzuri kunielekea na kuonyesha kwamba kwa kweli alitaka kunisaidia.” Baada ya miezi mitatu hivi, mzee huyo alimwalika Jim ahudhurie mikutano ya Kikristo. Jim anasema, “Kutaniko lilinikaribisha kwa uchangamfu na upendo walionionyesha ulinisaidia kubadilika. Nilianza kugundua kwamba sikupaswa kuzingatia sana hisia zangu. Ndugu zangu na mke wangu mpendwa, ambaye alibaki imara kiroho, walinisaidia kupata tena nguvu za kiroho. Pia nilitiwa moyo sana na makala zenye kichwa, ‘Yehova Si wa Kulaumiwa’ na ‘Mtumikie Yehova kwa Uaminifu-Mshikamanifu,’ katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1992.”

12 Baada ya muda, Jim aliwekwa rasmi tena kuwa mzee. Tangu wakati huo amesaidia ndugu wengine washinde majaribu kama hayo na kupata tena nguvu za kiroho. Anamalizia kusema hivi: “Nilifikiri kwamba nilikuwa na uhusiano mzuri sana na Yehova lakini haikuwa hivyo! Ninajuta kwamba niliruhusu kiburi kinipofushe nisione mambo muhimu zaidi na kunifanya nikazie fikira kupita kiasi makosa ya wengine.”—1 Kor. 10:12.

13. Huduma ya shambani inaweza kutusaidia kusitawisha sifa gani, na tutapata manufaa gani?

13 Huduma ya shambani inawezaje kutufinyanga tuwe watu bora? Kuwahubiria wengine habari njema kunaweza kutusaidia tusitawishe unyenyekevu na sifa nyingine za tunda la roho ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Fikiria sifa nzuri ambazo umesitawisha kwa kushiriki katika huduma. Zaidi ya hilo, tunapoonyesha utu kama wa Kristo, tunapamba ujumbe wetu, jambo linaloweza kubadili mtazamo wa baadhi ya wale tunaohubiria. Kwa mfano, Mashahidi wawili nchini Australia walimsikiliza kwa heshima mwenye nyumba mmoja aliyezungumza nao bila fadhili. Hata hivyo, baadaye, alijuta jinsi alivyowatendea na akaindikia ofisi ya tawi barua. Alisema hivi: “Ningependa kuomba msamaha dada hao wawili wanyenyekevu na wenye subira kwa kuwadharau na kujiona kuwa mwadilifu kupita kiasi. Ninajihisi kuwa mjinga kwa sababu niliwafukuza watu hao wawili waliokuwa wakitangaza Neno la Mungu.” Je, mwenye nyumba huyo angeandika barua hiyo iwapo wahubiri hao wangeonyesha hasira hata kidogo? Hapana. Naam, huduma yetu hutunufaisha sisi na pia majirani wetu!

JITIISHE KWA MUNGU UNAPOWAFINYANGA WATOTO WAKO

14. Wazazi wanapaswa kufanya nini ili wafanikiwe kuwafinyanga watoto wao?

14 Mara nyingi watoto ni wanyenyekevu na huwa tayari kujifunza. (Mt. 18:1-4) Hivyo, wazazi wenye hekima wanaweza kujitahidi kuwafundisha watoto wao kweli na kuwasaidia kuipenda. (2 Tim. 3:14, 15) Bila shaka ili wafanikiwe, lazima wazazi wakazie kweli mioyoni mwao wenyewe, na kuifanya iwe njia yao ya maisha. Wazazi wanapofanya hivyo, inakuwa rahisi kwa watoto wao kuipenda kweli. Isitoshe, wanajifunza kwamba wazazi wao wanawapenda wanapowatia nidhamu na pia ni njia ya Yehova ya kuwaonyesha upendo.

15, 16. Wazazi wanapaswa kuonyeshaje kwamba wanamtegemea Mungu ikiwa mtoto wao ametengwa na ushirika?

15 Licha ya kulelewa katika familia ya Kikristo, baadhi ya watoto huiacha kweli au kutengwa na ushirika na kuumiza hisia za familia yao. Dada mmoja kutoka Afrika Kusini alisema hivi: “Ndugu yangu alipotengwa na ushirika ni kana kwamba alikuwa amekufa. Nilivunjika moyo sana!” Yeye na wazazi wake walitendaje? Walifuata mwongozo unaopatikana katika Neno la Mungu. (Soma 1 Wakorintho 5:11, 13.) Wazazi wake wanasema hivi: “Tuliazimia kutumia ushauri wa Biblia tukitambua kwamba kufanya mambo kwa kufuata njia ya Mungu huleta matokeo mazuri. Tuliona mpango wa kutenga na ushirika kuwa nidhamu kutoka kwa Mungu na tulisadiki kwamba Yehova hutoa nidhamu kwa sababu ya upendo naye hufanya hivyo kwa kiwango kinachofaa. Kwa hiyo tuliwasiliana na mwana wetu katika mambo ya lazima yanayohusu familia tu.”

16 Mwana huyo alihisije? Alisema hivi baadaye: “Nilijua kwamba familia yangu hainichukii lakini walikuwa wakimtii Yehova na tengenezo lake.” Pia alisema: “Unapolazimika kumwomba Yehova msaada na msamaha, unatambua kwamba unamhitaji sana.” Wazia jinsi familia hiyo ilivyoshangilia kijana huyo aliporudishwa! Naam, tukimtambua Mungu katika njia zetu zote, tutapata matokeo mazuri.—Met. 3:5, 6; 28:26.

17. Kwa nini tuendelee kujitiisha kwa Yehova katika maisha yetu yote, na tutanufaikaje kwa kufanya hivyo?

17 Nabii Isaya alitabiri kwamba mwishoni mwa kipindi cha uhamisho Wayahudi wangetubu na kusema hivi: “Ee Yehova, wewe ni Baba yetu. Sisi ni udongo, nawe ni Mfinyanzi wetu; nasi sote ni kazi ya mkono wako.” Kisha wangemsihi hivi: “Usilikumbuke milele kosa letu. Tazama, sasa, tafadhali: sisi sote ni watu wako.” (Isa. 64:8, 9) Vivyo hivyo, tukijitiisha kwa unyenyekevu kwa Yehova na kuendelea kufanya hivyo katika maisha yetu yote, atatuona kuwa watu wenye kutamanika sana, kama alivyomwona nabii Danieli. Zaidi ya hilo, Yehova ataendelea kutufinyanga kwa kutumia Neno lake, roho yake, na tengenezo lake ili siku moja tusimame mbele zake tukiwa “watoto wa Mungu” wakamilifu.—Rom. 8:21.