Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Katika utimizo wa kisasa wa unabii huo, mwanamume mwenye kidau cha wino anawakilisha Yesu Kristo ambaye anawatia alama wale watakaookoka

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mwanamume mwenye kidau cha wino na wanaume sita wenye silaha za kuponda katika maono ya Ezekieli wanafananisha nini?

Wanafananisha majeshi ya mbinguni yaliyohusika kuharibu Yerusalemu na yatakayohusika kuharibu mfumo mwovu wa Shetani katika Har–Magedoni. Kwa nini ilifaa kurekebisha uelewaji huo?

Ezekieli alipoona mambo maovu yaliyokuwa yakifanywa katika jiji la Yerusalemu lililoasi kabla halijaharibiwa katika mwaka wa 607 K.W.K., alipewa maono kuhusu mambo ambayo yangetukia kabla ya uharibifu huo. Aliona wanaume sita wakiwa na silaha za kuponda. Pia aliona mwanamume kati yao “aliyevaa kitani” na alikuwa na “kidau cha wino.” (Eze. 8:6-12; 9:2, 3) Mwanamume huyo aliambiwa: “Pita katikati ya jiji, . . . nawe lazima utie alama kwenye mapaji ya uso ya watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanywa katikati yake.” Kisha wanaume waliokuwa na silaha za kuponda waliambiwa waue wote jijini ambao hawakuwa na alama. (Eze. 9:4-7) Tunajifunza nini kutokana na maono hayo, na mwanamume mwenye kidau cha wino ni nani?

Unabii huo ulitolewa mwaka wa 612 K.W.K., na ulitimizwa mara ya kwanza miaka mitano baadaye Yerusalemu lilipoharibiwa na jeshi la Babiloni. Ingawa Wababiloni waliokuwa wapagani waliruhusiwa kuharibu jiji hilo, walikuwa wakitekeleza hukumu ya Yehova. (Yer. 25:9, 15-18) Hii ni kwa sababu Yehova aliwatumia kuadhibu watu wake walioasi. Hata hivyo, si kila mtu ambaye angeuawa. Waadilifu hawangeangamizwa pamoja na waovu. Kwa upendo, Yehova alihakikisha kwamba Wayahudi waliochukizwa na mambo mabaya yaliyofanyika kwenye jiji hilo wangeokolewa.

Ezekieli hakuhusika katika kutia alama au kuangamiza watu. Badala yake, malaika wangeelekeza jinsi ambavyo hukumu ingetolewa. Kwa hiyo kupitia unabii huu, tunaruhusiwa kuona mambo yasiyoonekana huko mbinguni kwenyewe. Yehova alikuwa amewaagiza malaika zake ahakikishe kwamba waovu wameharibiwa na waadilifu wameokoka. *

Zamani tulisema kwamba katika utimizo wa kisasa wa maono hayo, mwanamume mwenye kidau cha wino aliwakilisha watiwa-mafuta. Tulifikiri kwamba wale wanaoitikia ujumbe unaohubiriwa wanatiwa alama ya wokovu. Hata hivyo, katika miaka ya karibuni imekuwa wazi kwamba maelezo hayo yanahitaji kurekebishwa. Kulingana na andiko la Mathayo 25:31-33, Yesu ndiye anayewahukumu watu. Atatoa hukumu ya mwisho wakati wa dhiki kuu, akiwatenganisha kondoo watakaookoka, na mbuzi watakaoharibiwa.

Hivyo, kwa kufikiria uelewaji huo mpya, tunajifunza mambo gani kutokana na maono ya Ezekieli? Tunajifunza mambo matano hivi:

  1. Katika kipindi kilichotangulia uharibifu wa Yerusalemu, Ezekieli alikuwa mlinzi pamoja na Yeremia, kama vile Isaya alivyokuwa mlinzi hapo awali. Leo, Yehova anatumia kikundi kidogo cha watiwa-mafuta wake kulisha watu wake na kuwaonya wengine kabla ya dhiki kuu kuanza. Kwa kweli, watumishi wote wa nyumbani wa Kristo wanashiriki kutoa onyo hilo.—Mt. 24:45-47.

  2. Ezekieli hakuhusika katika kutia alama wale waliookoka; na leo pia watumishi wa Mungu hawahusiki. Wanatangaza ujumbe wa Yehova ambao ni sehemu ya kazi yao ya kuhubiri inayoelekezwa na malaika.—Ufu. 14:6.

  3. Katika siku za Ezekieli hakuna mtu aliyepata alama halisi kwenye paji la uso wake. Ndivyo ilivyo leo. Watu wanahitaji kufanya nini ili watiwe alama ya wokovu? Wanahitaji kukubali habari njema, kuvaa utu wa Kikristo, kujiweka wakfu kwa Yehova, na kutegemeza kwa ushikamanifu ndugu za Kristo. (Mt. 25:35-40) Wale wanaofanya mambo hayo, watapata alama ya wokovu wakati wa dhiki kuu.

  4. Katika utimizo wa kisasa wa unabii huo, mwanamume mwenye kidau cha wino anawakilisha Yesu Kristo, ambaye anawatia alama wale watakaookoka. Umati mkubwa utapokea alama yao wakati wa dhiki kuu. Kisha watakuwa na nafasi ya kuishi milele hapa duniani.—Mt. 25:34, 46. *

  5. Katika utimizo wa kisasa wa unabii huo, wale wanaume sita wenye silaha za kuponda wanawakilisha majeshi ya Yesu mbinguni, Yesu mwenyewe akiyaongoza. Hivi karibuni, wataharibu mataifa na uovu wote.—Eze. 9:2, 6, 7; Ufu. 19:11-21.

Kuelewa mambo hayo muhimu kunaimarisha usadikisho wetu kwamba Yehova hawaharibu waadilifu pamoja na waovu. (2 Pet. 2:9; 3:9) Pia tunakumbushwa umuhimu wa kazi ya kuhubiri katika siku zetu. Kila mtu anahitaji kuonywa kabla mwisho uje!—Mt. 24:14.

^ fu. 6 Baruku (mwandishi wa Yeremia), Ebedmeleki Mwethiopia, na Warekabu waliokolewa ingawa hawakupata alama halisi kwenye mapaji ya nyuso zao. (Yer. 35:1-19; 39:15-18; 45:1-5) Walipata alama ya mfano ya wokovu.

^ fu. 12 Watiwa-mafuta waaminifu hawahitaji kupata alama hiyo ya wokovu. Badala yake, wanatiwa muhuri wa mwisho kabla ya kufa au kabla ya dhiki kuu kuanza.—Ufu. 7:1, 3.