Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sifa ya Kimungu Yenye Thamani Zaidi Kuliko Almasi

Sifa ya Kimungu Yenye Thamani Zaidi Kuliko Almasi

Almasi zimethaminiwa sana kwa miaka mingi. Baadhi ya almasi zina thamani ya mamilioni ya dola. Hata hivyo, je, inawezekana kwamba Mungu anaona vitu vingine kuwa vyenye thamani kuliko almasi au mawe mengine ya thamani?

Haykanush, mhubiri ambaye hajabatizwa anayeishi Armenia, alipata hati ya kusafiria karibu na nyumba yake. Ndani ya hati hiyo kulikuwemo kadi za benki na pesa nyingi. Haykanush alimsimulia jambo hilo mume wake ambaye pia ni mhubiri ambaye hajabatizwa.

Wenzi hao walikuwa na matatizo makubwa ya kifedha na walikuwa na madeni; hata hivyo waliamua kupeleka pesa hizo kwenye anwani iliyokuwa katika hati hiyo. Mtu aliyepoteza hati hiyo pamoja na familia yake walishangaa sana. Haykanush na mume wake walieleza kwamba walikuwa wanyoofu kwa sababu ya mambo waliyojifunza katika Biblia. Walihisi kwamba ni lazima wawe wanyoofu na walitumia nafasi hiyo kuzungumza kuhusu Mashahidi wa Yehova na kuwaachia machapisho.

Familia hiyo walitaka kumthawabisha Haykanush kwa kumpa pesa, lakini alikataa. Ili kuonyesha uthamini wao, siku iliyofuata mke wa mwanamume huyo aliwatembelea wenzi hao nyumbani na kusisitiza kwamba Haykanush akubali pete ya almasi.

Kama familia hiyo, watu wengi wangeshangazwa na unyoofu wa Haykanush na mumewe. Lakini je, Yehova angeshangazwa na unyoofu huo? Angeuonaje unyoofu wao? Je, walipata faida yoyote kwa kuwa wanyoofu?

SIFA ZENYE THAMANI KULIKO VITU VYA KIMWILI

Ni rahisi kujibu maswali hayo kwa sababu watumishi wa Mungu wanaamini kwamba kuonyesha sifa za Yehova ni jambo la thamani zaidi machoni pake kuliko almasi, dhahabu, au vitu vingine vya kimwili. Naam, maoni ya Yehova kuhusu vitu vyenye thamani na visivyo na thamani yanatofautiana na maoni ya wanadamu. (Isa. 55:8, 9) Na watumishi wake wanaona kwamba kuonyesha sifa za Yehova kwa kiwango kikubwa zaidi ni jambo lenye thamani sana.

Hilo linaonekana wazi tunaposoma mambo ambayo Biblia inasema kuhusu utambuzi na hekima. Andiko la Methali 3:13-15 linasema hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amepata hekima, na mtu anayepata utambuzi, kwa maana kuwa nayo kama mapato ni bora kuliko kuwa na mapato ya fedha na kuwa nayo kama mazao ni bora kuliko dhahabu yenyewe. Ina thamani kuliko marijani, na mapendezi yako mengine yote hayawezi kulinganishwa nayo.” Ni wazi kwamba Yehova anathamini sifa hizo kuliko hazina zozote za kimwili.

Vipi kuhusu unyoofu?

Yehova ni mnyoofu, ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Alitumia roho yake kumwongoza mtume Paulo awaandikie Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza hivi: “Endeleeni kusali kwa ajili yetu, kwa maana sisi tuna uhakika kwamba tuna dhamiri nyoofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Ebr. 13:18.

Yesu Kristo aliweka mfano mzuri wa unyoofu. Kwa mfano, kumbuka Kuhani Mkuu Kayafa aliposema: “Kwa Mungu aliye hai ninakuweka chini ya kiapo utuambie kama wewe ndiye Kristo Mwana wa Mungu!” Kwa unyoofu, Yesu alijitambulisha kuwa Masihi ingawa hilo lingefanya Sanhedrini idai kwamba anakufuru na hivyo kumuua.—Mt. 26:63-67.

Namna gani sisi? Je, tutakuwa wanyoofu tusiposema ukweli wote au kuupotosha kusudi tufaidike kimwili?

CHANGAMOTO ZA KUWA MNYOOFU

Ni kweli kwamba si rahisi kuwa wanyoofu katika siku hizi za mwisho ambazo wengi ni “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa.” (2 Tim. 3:2) Wengi wanabadili maoni yao kuhusu unyoofu wanapokabili hali ngumu za kiuchumi au inapokuwa vigumu kupata kazi. Wengi wanahisi si vibaya kuiba, kudanganya, au kufanya mambo mengine yasiyo ya unyoofu. Watu wengi wana maoni ya kwamba haiwezekani kuwa wanyoofu iwapo watafaidika kimwili. Hata Wakristo fulani wamefanya maamuzi mabaya kuhusiana na hilo na wamepoteza msimamo wao mzuri kutanikoni kwa sababu ya “pato lisilo la haki.”—1 Tim. 3:8; Tito 1:7.

Hata hivyo, Wakristo wengi wanamwiga Yesu. Wanatambua kwamba sifa za kimungu ni muhimu zaidi kuliko mali au faida zozote. Hivyo, vijana Wakristo hawadanganyi ili wapite mtihani shuleni. (Met. 20:23) Ni kweli kwamba huenda tusithawabishwe sikuzote kwa kuwa wanyoofu kama Haykanush. Hata hivyo, Mungu anasema kwamba tunapaswa kuwa wanyoofu machoni pake, na hilo linatuwezesha kudumisha kitu chenye thamani sana, yaani, dhamiri safi.

Mfano wa Gagik unaonyesha ukweli wa jambo hilo. Anasema hivi: “Kabla ya kuwa Mkristo, nilikuwa nikifanya kazi katika kampuni kubwa ambapo mmiliki wake aliepuka kulipa kodi kwa kuripoti sehemu kidogo tu ya faida ya kampuni. Nikiwa msimamizi, nilitarajiwa ‘kukubaliana’ na wakala wa kukusanya kodi kwa kumhonga ili apuuze ufisadi wa kampuni hiyo. Kwa sababu hiyo, nilijulikana kuwa mtu asiye mnyoofu. Nilipojifunza kweli, nilikataa kufanya hivyo, hata ingawa nilikuwa nikipata mshahara mnono. Badala yake, nilianzisha biashara. Na tangu siku ya kwanza nilisajili kampuni yangu na kulipa kodi zote.”—2 Kor. 8:21.

Gagik anasimulia hivi: “Katika kampuni niliyoanzisha, nilipata nusu ya mapato ya awali, kwa hiyo ilikuwa vigumu kuiandalia familia yangu. Hata hivyo, nina furaha zaidi sasa. Nina dhamiri safi mbele za Yehova. Nimewawekea wana wangu wawili mfano mzuri, na nina mapendeleo kutanikoni. Wakaguzi wa kodi na watu wengine ninaofanya biashara pamoja nao sasa wananijua kuwa mtu mnyoofu.”

YEHOVA HUTUSAIDIA

Yehova anawapenda wale wanaopamba fundisho lake kwa kuonyesha sifa zake bora kutia ndani unyoofu. (Tito 2:10) Alimwongoza Mfalme Daudi kutuhakikishia hivi: “Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate.”—Zab. 37:25.

Simulizi la Ruthu mwaminifu linaonyesha ukweli wa jambo hilo. Alishikamana na mama-mkwe wake, Naomi, badala ya kumwacha alipokuwa mzee. Ruthu alihamia Israeli ambapo angeweza kumwabudu Mungu wa kweli. (Rut. 1:16, 17) Alipokuwa Israeli, Ruthu alifanya kazi kwa unyoofu na bidii, akijitahidi kukusanya masalio kulingana na Sheria. Na kama vile Daudi alivyojionea baadaye, Yehova hakuwaacha Ruthu na Naomi. (Rut. 2:2-18) Yehova alimtimizia Ruthu mambo mengi zaidi kuliko mahitaji ya kimwili. Alimchagua kuwa nyanya ya Mfalme Daudi na hata Masihi aliyeahidiwa!—Rut. 4:13-17; Mt. 1:5, 16.

Huenda baadhi ya watumishi wa Yehova wakajikuta katika hali ambayo wanapata mshahara mdogo mpaka inakuwa vigumu kutimiza mahitaji yao. Badala ya kutafuta njia ya mkato isiyo ya unyoofu, wanajitahidi kufanya kazi kwa bidii. Hivyo, wanaonyesha kwamba wanathamini sifa bora za Mungu, kutia ndani unyoofu kuliko vitu vyovyote vya kimwili.—Met. 12:24; Efe. 4:28.

Kama Ruthu katika nyakati za kale, Wakristo ulimwenguni pote wanaamini kwamba Yehova ana nguvu za kuwasaidia. Wanamtegemea kabisa yule aliyetoa ahadi hii katika Neno lake: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Ebr. 13:5) Mara kwa mara Yehova ameonyesha kwamba anaweza na anawasaidia wale wanaokabili hali ngumu na wanaoonyesha sifa ya unyoofu nyakati zote. Ametimiza ahadi yake ya kutosheleza mahitaji yetu maishani.—Mt. 6:33.

Naam, wanadamu wanathamini almasi na vitu vingine vyenye thamani. Lakini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Baba yetu wa mbinguni anapoona tukionyesha sifa ya unyoofu pamoja na sifa zake nyingine, tunakuwa wenye thamani kubwa sana kuliko vito vya thamani!

Tukiwa wanyoofu tutadumisha dhamiri safi na tutakuwa na uhuru wa kusema katika huduma