Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova ‘Anakujali’

Yehova ‘Anakujali’

KWA NINI unaweza kuwa na uhakika kwamba maneno hayo ni ya kweli? Unajuaje kuwa Yehova anakujali? Sababu moja ni kwamba Biblia inasema hivyo. Andiko la 1 Petro 5:7 linasema hivi: “[Tupeni] mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.” Ni nini kinachokuthibitishia kwamba Yehova Mungu anakujali?

MUNGU ANAANDAA MAHITAJI YA KIMWILI

Yehova ameweka mfano wa kuwa mwenye fadhili na mkarimu

Kwanza, Mungu ana sifa ambazo kwa kawaida tungependa rafiki zetu wa karibu wawe nazo. Mara nyingi watu wanaoonyeshana fadhili na ukarimu huwa marafiki wa karibu. Ni rahisi kuona jinsi Yehova anavyowaonyesha wanadamu fadhili na ukarimu kila siku. Fikiria mfano mmoja: “Hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mt. 5:45) Jua na mvua hutimiza nini? Pamoja na mambo mengine, Mungu hutumia vitu hivyo ‘kuijaza mioyo yetu kikamili kwa chakula na uchangamfu.’ (Mdo. 14:17) Naam, Yehova anahakikisha kwamba dunia inatoa chakula kingi, nasi hufurahi sana tunapopata mlo mzuri.

Lakini kwa nini watu wengi wanakosa chakula? Kwa sababu mara nyingi watawala wa kibinadamu hufikiria zaidi kupata mamlaka na kufaidika kifedha badala ya kuboresha maisha ya watu. Hivi karibuni, Yehova atasuluhisha tatizo hilo linalotokana na pupa, kwa kuondoa mfumo wa kisiasa uliopo na kuleta Ufalme wa mbinguni unaotawaliwa na Mwana wake. Wakati huo, hakuna mtu atakayekosa chakula. Kwa sasa, Mungu anawategemeza watumishi wake waaminifu. (Zab. 37:25) Je, hilo halithibitishi kwamba anatujali?

YEHOVA HUTUMIA WAKATI WAKE KWA UKARIMU

Yehova ameweka mfano wa kutumia wakati wake kwa ukarimu

Rafiki mzuri anatumia wakati kuwa pamoja nawe. Anaweza kutumia saa nyingi kuzungumza nawe mambo yanayowahusu nyote. Na rafiki mzuri atakusikiliza kwa makini unapomweleza matatizo na mahangaiko yako. Je, Yehova hutusikiliza kwa njia hiyo? Bila shaka! Yeye husikiliza sala zetu. Hivyo, Biblia inatutia moyo ‘tudumu katika sala’ na ‘tusali bila kuacha.’—Rom. 12:12; 1 The. 5:17.

Yehova yuko tayari kusikiliza sala zetu kwa muda gani? Tunaweza kupata jibu kwa kuchunguza mfano fulani katika Biblia. Kabla ya kuwachagua mitume wake, Yesu “[aliendelea] kusali kwa Mungu usiku wote.” (Luka 6:12) Katika sala hiyo, inaelekea Yesu aliwataja wanafunzi wake wengi kwa majina, alifikiria sifa zao na udhaifu wao, na akamwomba Baba yake amsaidie kuwachagua. Asubuhi ilipofika, Yesu alikuwa na uhakika kwamba wanafunzi aliowachagua ni wale ambao walistahili zaidi kuwa mitume wake. Akiwa “msikiaji wa sala,” Yehova anapenda kusikiliza sala zetu za kutoka moyoni. (Zab. 65:2) Hata ikiwa mtu atasali kwa muda mrefu kuhusu jambo linalomhangaisha sana, Yehova yuko tayari kuendelea kumsikiliza.

MUNGU YUKO TAYARI KUSAMEHE

Yehova ameweka mfano wa kuwa tayari kusamehe

Nyakati nyingine inakuwa vigumu hata kwa marafiki wa karibu kusameheana. Nyakati fulani watu huvunja urafiki ambao umedumu kwa muda mrefu kwa sababu wameshindwa kusameheana. Yehova hayuko hivyo. Biblia inawaalika wote wenye mioyo minyoofu wamwombe msamaha, “kwa maana atasamehe kwa njia kubwa.” (Isa. 55:6, 7) Ni nini humchochea Mungu asamehe kwa hiari?

Ni kwa sababu Mungu ana upendo usio na kifani. Anawapenda wanadamu sana hivi kwamba amemtoa Mwanaye, Yesu, ili awakomboe kutoka katika dhambi na madhara yake. (Yoh. 3:16) Kwa kweli, fidia inatimiza mambo mengi zaidi. Kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo, Mungu huwasamehe kwa hiari wale anaowapenda. Mtume Yohana aliandika hivi: “Tukiungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na mwadilifu hata atusamehe dhambi zetu.” (1 Yoh. 1:9) Kwa kuwa Yehova anasamehe, watu wanaweza kuendelea kufurahia urafiki wake na kujua jambo hilo hugusa mioyo yetu sana.

ANAKUSAIDIA UNAPOHITAJI MSAADA WAKE

Yehova ameweka mfano wa kutusaidia tunapohitaji msaada

Rafiki wa kweli huwasaidia wengine wanapohitaji msaada. Je, Yehova hufanya hivyo? Neno lake linasema hivi: “Ijapokuwa huenda [mtumishi wa Mungu] akaanguka, yeye hatatupwa chini, kwa maana Yehova anautegemeza mkono wake.” (Zab. 37:24) Yehova ‘huwategemeza watumishi wake’ kwa njia mbalimbali. Fikiria kisa hiki kilichotokea katika kisiwa cha St. Croix, kilicho Karibea.

Msichana fulani alikataa kusalimu bendera kwa sababu ya imani yake na hilo likafanya ashinikizwe na wanafunzi wenzake. Baada ya kumwomba Yehova msaada, aliamua kutetea imani yake. Baadaye, alipotoa ripoti mbele ya darasa, aliamua kuzungumzia suala la kusalimu bendera. Akitumia Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, alifafanua jinsi simulizi la Shadraki, Meshaki, na Abednego lilivyomsaidia kufanya uamuzi. Alisema hivi: “Yehova aliwalinda Waebrania hao watatu kwa sababu hawakukubali kuabudu sanamu.” Kisha akawaonyesha wale waliokuwepo kitabu hicho. Wanafunzi wenzake 11 waliomba kitabu hicho. Akitambua kwamba Yehova alimpa nguvu na hekima, msichana huyo alifurahi sana kutoa ushahidi kuhusu mada inayoweza kuzua ubishi.

Ikiwa wakati wowote utashuku kwamba Yehova anakujali, tafakari maandiko kama vile Zaburi 34:17-19; 55:22; na 145:18, 19. Waulize Mashahidi ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu kuhusu jinsi alivyowatunza. Na unapohitaji msaada wa Mungu, sali kuhusu jambo hilo. Baada ya muda mfupi utajionea jinsi Yehova ‘anavyokujali.’