Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Yehova Mungu Wetu Ni Yehova Mmoja”

“Yehova Mungu Wetu Ni Yehova Mmoja”

“Sikiliza, Ee Israeli: Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.” —KUM. 6:4.

NYIMBO: 138, 112

1, 2. (a) Kwa nini maneno ya Kumbukumbu la Torati 6:4 yanajulikana sana? (b) Kwa nini Musa alisema maneno hayo?

KWA karne nyingi, maneno sita ya Kiebrania katika Kumbukumbu la Torati 6:4 yametumiwa na watu wenye imani ya Kiyahudi yakiwa sehemu ya sala ya pekee. Wanatoa sala hiyo kila siku, asubuhi na jioni. Sala hiyo inaitwa Shema, ambalo ni neno la kwanza katika mstari huo. Wayahudi wenye bidii hutoa sala hiyo ili kuonyesha jinsi walivyojitoa kikamili kwa Mungu.

2 Maneno hayo yalikuwa sehemu ya hotuba ya mwisho ya Musa kwa taifa la Israeli walipokuwa wamekusanyika kwenye nyanda za Moabu mwaka wa 1473 K.W.K. Taifa hilo lilikuwa karibu kuvuka Mto Yordani na kurithi Nchi ya Ahadi. (Kum. 6:1) Musa aliyekuwa kiongozi wao kwa miaka 40 alitaka watu hao wawe jasiri walipokabiliana na hali ngumu iliyokuwa mbele yao. Walipaswa kumtegemea Yehova na kuwa waaminifu kwake akiwa Mungu wao. Bila shaka, maneno hayo ya Musa yangewachochea sana Waisraeli. Baada ya kutaja zile Amri Kumi na maagizo mengine ambayo Yehova alikuwa amewapa, Musa alitoa tangazo lenye nguvu linalopatikana katika Kumbukumbu la Torati 6:4, 5. (Soma.)

3. Tutachunguza maswali gani katika makala hii?

3 Je, Waisraeli waliokusanyika pamoja na Musa hawakujua kwamba Yehova Mungu wao ni “Yehova mmoja”? Bila shaka walijua. Waisraeli waaminifu walimjua na kumwabudu Mungu mmoja tu, yaani, Mungu wa mababu zao Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Basi kwa nini Musa aliwakumbusha kwamba Yehova Mungu wao ni “Yehova mmoja”? Kutambua kwamba Yehova ni mmoja, kunahusianaje na kumpenda kwa moyo, nafsi, na nguvu zetu zote kama inavyotajwa katika mstari wa 5? Na maneno ya Kumbukumbu la Torati 6:4, 5 yanatuhusuje leo?

MUNGU WETU NI “YEHOVA MMOJA”

4, 5. (a) Maana moja ya maneno “Yehova mmoja” ni nini? (b) Yehova anatofautianaje na miungu ya mataifa?

4 Ni wa pekee. Katika Kiebrania na lugha nyingine nyingi, neno “moja” halitumiwi kuonyesha idadi tu. Linaweza kudokeza kitu cha kipekee, cha aina yake. Haielekei Musa alikuwa akipinga fundisho la utatu la dini za uwongo. Yehova ndiye Muumba wa mbingu na dunia, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. Yeye ndiye Mungu halisi na wa kweli, hakuna mungu kama yeye. (2 Sam. 7:22) Hivyo, Musa alikuwa akiwakumbusha Waisraeli kwamba wanapaswa kumwabudu Yehova pekee. Hawakupaswa kuwaiga watu waliowazunguka ambao waliabudu miungu mingi, ya kiume na ya kike. Baadhi ya miungu hiyo ya uwongo ilionwa kuwa inatawala vitu fulani vya asili. Mungu fulani aliwakilishwa na miungu mingine ambayo ilikuwa na maumbo tofauti.

5 Kwa mfano, Wamisri waliabudu mungu wa jua aliyeitwa Ra, mungu wa kike wa anga Nut, mungu wa dunia Geb, mungu wa Nile Hapi, na wanyama wengi walioonwa kuwa watakatifu. Yehova alionyesha kwamba alikuwa mkuu kuliko miungu hiyo ya uwongo alipoleta yale Mapigo Kumi. Mungu mkuu wa Wakanaani alikuwa Baali, mungu wa uzazi, ambaye pia alikuwa mungu wa anga, mvua, na dhoruba. Katika sehemu nyingi, watu walimtegemea Baali ili awalinde. (Hes. 25:3) Waisraeli walipaswa kukumbuka kwamba Mungu wao, “Mungu wa kweli,” ni “Yehova mmoja.”—Kum. 4:35, 39.

6, 7. Ni nini maana nyingine ya maneno “Yehova mmoja,” naye alionyeshaje kwamba yeye ni “mmoja”?

6 Habadiliki na ni Mshikamanifu. Maneno “Yehova mmoja” yanamaanisha kwamba kusudi na matendo yake yanategemeka sikuzote. Yehova Mungu habadiliki-badiliki. Badala yake, sikuzote yeye ni mwaminifu, mshikamanifu, na wa kweli. Alimwahidi Abrahamu kwamba wazao wake wangerithi Nchi ya Ahadi, naye akafanya matendo yenye nguvu ili atimize ahadi hiyo. Ingawa miaka 430 ilipita, Yehova alikuwa ameazimia kutimiza ahadi hiyo.—Mwa. 12:1, 2, 7; Kut. 12:40, 41.

7 Karne nyingi baadaye, Yehova alipowaambia Waisraeli kwamba wao ni mashahidi wake, alisema hivi: “Mimi ni Yeye yuleyule. Kabla yangu hakuna Mungu yeyote aliyefanyizwa, na baada yangu hapakuendelea kuwapo yeyote.” Akisisitiza kwamba kusudi lake halibadiliki, Yehova aliongeza kusema hivi: “Wakati wote mimi ni Yeye yuleyule.” (Isa. 43:10, 13; 44:6; 48:12) Lilikuwa pendeleo kubwa sana kwa Waisraeli na kwetu pia kuwa watumishi wa Yehova, Mungu ambaye habadiliki na ni mshikamanifu katika njia zake zote!—Mal. 3:6; Yak. 1:17.

8, 9. (a) Yehova anataka waabudu wake wafanye nini? (b) Yesu alikaziaje maana ya maneno ya Musa?

8 Naam, Musa aliwakumbusha Waisraeli kwamba Yehova aliwapenda na kuwajali sikuzote. Kwa sababu hiyo, walipaswa kujitoa kabisa kwake, kumpenda bila masharti kwa moyo, nafsi, na nguvu zao zote. Watoto pia walitarajiwa kujitoa kikamili kwa kuwa wazazi walipaswa kuwafundisha nyakati zote.—Kum. 6:6-9.

9 Kwa kuwa makusudi na mapenzi ya Yehova hayabadiliki, ni wazi kwamba anatarajia waabudu wake watimize matakwa yaleyale. Ili akubali ibada yetu, lazima sisi pia tujitoe kikamili na kumpenda kwa moyo, akili, na nguvu zetu zote. Yesu Kristo alimwambia hivyo mtu fulani aliyemwuliza swali. (Soma Marko 12:28-31.) Kwa hiyo, acheni tujifunze jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunaelewa “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.”

JITOE KIKAMILI KWA YEHOVA

10, 11. (a) Ni katika njia gani ibada yetu kwa Yehova ni ya pekee? (b) Vijana Waebrania walionyeshaje kwamba wamejitoa kikamili kwa Yehova?

10 Ili Yehova awe Mungu wa pekee kwetu, tunapaswa tujitoe kikamili kwake. Hatuwezi kuabudu miungu mingine au kuingiza mawazo na mazoea ya uwongo katika ibada yetu kwa Yehova. Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova hawezi kulinganishwa kamwe na miungu mingine. Ni Yehova peke yake anayepaswa kuabudiwa.—Soma Ufunuo 4:11.

11 Katika kitabu cha Danieli, tunasoma kuhusu vijana Waebrania Danieli, Hanania, Mishaeli, na Azaria. Walionyesha kwamba walijitoa kikamili kwa Yehova kwa kukataa kula vyakula visivyo safi na pia kukataa kuinamia sanamu ya dhahabu ya Nebukadneza. Walijua mambo ya kutangulizwa; waliazimia kubaki washikamanifu kwake.—Dan. 2:1–3:30.

12. Tunapaswa kuepuka nini tunapojitoa kikamili kwa Yehova?

12 Ili kujitoa kikamili kwa Yehova, ni lazima tuwe waangalifu tusiruhusu kitu chochote kichukue mahali pa Yehova maishani mwetu. Ni vitu gani vinavyoweza kuingilia ibada yetu? Katika Amri Kumi, Yehova alionyesha wazi kwamba watu wake hawapaswi kuwa na miungu mingine na hawapaswi kuabudu sanamu. (Kum. 5:6-10) Leo kuna ibada mbalimbali za sanamu, na huenda tusitambue baadhi yake kwa urahisi. Lakini matakwa ya Yehova hayajabadilika, bado yeye ni “Yehova mmoja.” Acheni tuone jinsi tunavyoweza kuepuka ibada ya sanamu leo.

13. Tunaweza kupenda nini zaidi kuliko Yehova?

13 Andiko la Wakolosai 3:5 (soma), linatoa ushauri mkali kwa Wakristo kuhusu mambo yanayoweza kuharibu uhusiano wao wa pekee pamoja na Yehova. Ona kwamba pupa inahusianishwa na ibada ya sanamu. Andiko hilo linasema hivyo kwa sababu kitu ambacho mtu anapenda kama vile mali au raha kinaweza kumwongoza maishani na kuwa kama mungu mwenye nguvu. Lakini tunapotazama mstari wote, tunaona kwamba mazoea mengine yote yenye dhambi yanayotajwa yanahusiana na pupa na ibada ya sanamu kwa njia fulani. Tunaweza kutamani sana vitu hivyo hadi tupoteze upendo wetu kwa Mungu. Tukifanya hivyo, Yehova hatakuwa “Yehova mmoja” kwetu. Hatungependa jambo hilo litukie kamwe.

14. Mtume Yohana alitoa onyo gani?

14 Mtume Yohana alizungumzia wazo hilohilo alipoonya kwamba mtu akipenda vitu vilivyo katika ulimwengu, yaani, “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani,” basi “kumpenda Baba hakumo ndani yake.” (1 Yoh. 2:15, 16) Kwa hiyo tunahitaji kuchunguza moyo wetu nyakati zote tuone ikiwa unashawishiwa na burudani, marafiki, na mitindo ya mavazi na mapambo ya ulimwengu. Au tunaweza kuonyesha kwamba tunaupenda ulimwengu tukijitahidi “kujitafutia makuu,” kama vile kufuatia elimu ya juu. (Yer. 45:4, 5) Tuko karibu sana kuingia katika ulimwengu mpya. Hivyo, ni muhimu sana kukumbuka maneno ya Musa yenye nguvu! Tukielewa na kuamini kabisa kwamba “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja,” tutafanya yote tuwezayo kujitoa kikamili, na kumtumikia kwa njia anayokubali.—Ebr. 12:28, 29.

DUMISHA UMOJA WA KIKRISTO

15. Kwa nini Paulo aliwakumbusha Wakristo kwamba Mungu ni “Yehova mmoja”?

15 Maneno “Yehova mmoja” yanatusaidia kuelewa kwamba Yehova anawataka watumishi wake wawe na umoja na wawe na kusudi lilelile maishani. Kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza lilikuwa na Wayahudi, Wagiriki, Waroma, na watu wa mataifa mengine. Walilelewa katika mazingira tofauti ya kidini, na walikuwa na desturi na mapendezi tofauti-tofauti. Kwa sababu hiyo, ilikuwa vigumu kwa baadhi yao kukubali njia mpya ya kuabudu au kuacha kabisa njia zao za zamani. Mtume Paulo aliona inafaa kuwakumbusha kwamba Wakristo wana Mungu mmoja, Yehova.—Soma 1 Wakorintho 8:5, 6.

16, 17. (a) Ni unabii gani unaotimizwa leo, na kumekuwa na matokeo gani? (b) Ni nini kinachoweza kuharibu umoja wetu?

16 Hali ikoje katika kutaniko la Kikristo leo? Nabii Isaya alitabiri kwamba “katika siku za mwisho,” watu wa mataifa yote wangemiminika katika ibada ya kweli ya Yehova iliyoinuliwa. Wangesema: “[Yehova] atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.” (Isa. 2:2, 3) Tunafurahi sana kuona unabii huo ukitimia leo! Kwa sababu hiyo makutaniko mengi yana watu wa rangi, utamaduni, na lugha mbalimbali, wanaomtukuza Yehova. Hata hivyo, tofauti hizo zinaweza kutokeza changamoto ambazo tunapaswa kuzifikiria kwa uzito.

Je, unachangia umoja wa kutaniko la Kikristo? (Tazama fungu la 16 hadi 19)

17 Kwa mfano, unawaonaje Wakristo wenzako kutoka utamaduni tofauti kabisa na wako? Huenda hujazoea lugha yao, mtindo wao wa mavazi, tabia, na chakula chao. Je, unajitenga nao na kushirikiana na wale walio na malezi kama yako? Au vipi ikiwa waangalizi wa kutaniko, mzunguko, au ofisi yenu wana umri mdogo kuliko wako au wana utamaduni au rangi tofauti na yako? Je, unaruhusu mambo hayo yaharibu umoja unaopaswa kuwa kati ya watu wa Yehova?

18, 19. (a) Tunapata ushauri gani katika Waefeso 4:1-3? (b) Tunaweza kufanya nini ili kudumisha umoja kutanikoni?

18 Tunaweza kuepukaje mitego hiyo? Paulo alitoa ushauri mzuri kwa Wakristo walioishi Efeso, jiji lenye ufanisi na wakazi kutoka malezi mbalimbali. (Soma Waefeso 4:1-3.) Paulo alitangulia kutaja sifa kama vile unyenyekevu, upole, subira, na upendo. Sifa hizo zinaweza kulinganishwa na nguzo zinazoitegemeza nyumba. Licha ya kuwa na nguzo zenye nguvu, nyumba inahitaji kudumishwa kwa ukawaida; la sivyo, inaweza kuanza kuharibika. Paulo aliwasihi Wakristo Waefeso wajitahidi sana “kuushika umoja wa roho.”

19 Kila mmoja wetu ana jukumu la kuchangia kudumisha umoja wa kutaniko. Tunaweza kufanya nini? Kwanza, sitawisha na kuonyesha sifa alizotaja Paulo, yaani, unyenyekevu, upole, subira, na upendo. Kisha, jitahidi sana kuchangia “kifungo chenye kuunganisha cha amani.” Hali za kutoelewana ni kama nyufa ndogo katika umoja wetu; hivyo tunapaswa kujitahidi kusuluhisha hali hizo ili tudumishe amani na umoja tunaothamini sana miongoni mwetu.

20. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaelewa “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja”?

20 “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.” Hayo ni maneno yenye nguvu kama nini! Kikumbusho hicho kiliwaimarisha Waisraeli kukabili changamoto walipoingia na kuirithi Nchi ya Ahadi. Tukizingatia maneno hayo, tutaimarishwa kukabiliana na dhiki kuu iliyo karibu na baadaye kuchangia amani na umoja katika Paradiso. Acheni tuendelee kujitoa kikamili kwa Yehova kwa kumpenda na kumtumikia kwa nafsi yote na kujitahidi sana kudumisha umoja wa Kikristo. Tukiendelea kufanya hivyo, tunaweza kutazamia kwa uhakika utimizo wa maneno haya ambayo Yesu aliwaambia wale atakaowachagua kuwa kondoo: “Njooni, ninyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.”—Mt. 25:34.