Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kinachokuongoza Unapofanya Maamuzi ya Kibinafsi?

Ni Nini Kinachokuongoza Unapofanya Maamuzi ya Kibinafsi?

“Endeleeni kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova.”EFE. 5:17.

NYIMBO: 69, 57

1. Taja baadhi ya sheria zilizo katika Biblia, na ueleze jinsi tunavyonufaika kwa kuzitii.

KUPITIA Neno lake lililoandikwa, Yehova ametupatia sheria hususa kuhusu mambo fulani. Kwa mfano, anakataza ukosefu wa maadili katika ngono, ibada ya sanamu, wizi, na ulevi. (1 Kor. 6:9, 10) Pia, Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliwapa wafuasi wake amri hii nzito, lakini yenye kusisimua: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Kwa kweli, sheria na amri za Mungu ni ulinzi mkubwa sana kwetu! Kutii amri hizo kumetusaidia tujiheshimu zaidi, tuwe na afya bora, na kumeongeza shangwe katika familia zetu. Zaidi ya yote, tunapofuata kwa ushikamanifu sheria za Yehova, ikiwemo amri ya kuhubiri, tunapata baraka na kibali chake.

2, 3. (a) Kwa nini Biblia haina sheria kuhusu kila hali tunayokabili maishani? (b) Tutazungumzia maswali gani katika makala hii? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

2 Hata hivyo, Biblia haitoi sheria hususa kuhusu kila jambo maishani mwetu. Kwa mfano, Maandiko hayana sheria hususa kuhusu mavazi yanayomfaa Mkristo. Hilo linaonyeshaje hekima ya Yehova? Tamaduni na mitindo ya mavazi inatofautiana katika sehemu mbalimbali ulimwenguni, na inabadilika kadiri wakati unavyopita. Ikiwa Biblia ingetoa orodha ya mitindo ya mavazi na mapambo yanayokubalika, kufikia sasa ingekuwa imepitwa na wakati. Kwa sababu hiyohiyo, Neno la Mungu lililoongozwa na roho halitoi sheria nyingi hususa kuhusu matibabu, burudani, na kazi inayomfaa Mkristo. Kwa hiyo, mtu mmojammoja na vichwa vya familia wana uhuru wa kujifanyia maamuzi kuhusu mambo hayo.

3 Je, hilo linamaanisha kwamba Yehova hajali maamuzi tunayofanya tunapokabili changamoto ya kufanya maamuzi muhimu, ambayo huenda yakaathiri maisha yetu? Je, Baba yetu wa mbinguni atakubaliana na uamuzi wowote tunaofanya maadamu hauvunji sheria ya Biblia? Na ikiwa hakuna sheria hususa, tutajuaje maamuzi yanayomfurahisha Yehova?

KWA NINI TUFIKIRIE KUHUSU MAAMUZI YA KIBINAFSI?

4, 5. Maamuzi yetu yanaweza kuwa na matokeo gani kwetu na kwa wengine?

4 Watu fulani wanahisi wana uhuru wa kuamua kufanya chochote watakacho. Hata hivyo, ili tufanye maamuzi ya hekima yanayomfurahisha Yehova, ni lazima tuzingatie sheria na kanuni zilizo katika Neno lake na kuzifuata maishani. Kwa mfano, ili tupate kibali cha Mungu, ni lazima tutende kulingana na sheria yake kuhusu damu. (Mwa. 9:4; Mdo. 15:28, 29) Sala itatusaidia tufanye maamuzi yanayopatana na kanuni na sheria za Kimaandiko.

5 Maamuzi mazito ya kibinafsi yanaweza kuathiri afya yetu ya kiroho. Kila uamuzi tunaofanya unaweza kuathiri uhusiano wetu na Yehova, iwe ni kwa njia nzuri au mbaya. Uamuzi mzuri utaimarisha uhusiano wetu na Mungu ilhali uamuzi mbaya utaharibu uhusiano huo. Isitoshe, uamuzi usiofaa unaweza kuwaumiza wengine kiroho kwa kuwasumbua, kuwakwaza, au kuharibu umoja wa kutaniko. Kwa kweli, ni muhimu tufikirie jinsi tunavyofanya maamuzi yetu ya kibinafsi.—Soma Waroma 14:19; Wagalatia 6:7.

6. Ni nini kinachopaswa kuongoza maamuzi yetu?

6 Tunapaswa kufanya nini ikiwa hakuna sheria ya moja kwa moja katika Biblia kuhusu jambo fulani? Chini ya hali hiyo, ni wajibu wetu kuchunguza mambo yanayohusika na kufanya maamuzi kwa kutegemea, si mapenzi yetu, bali mambo ambayo Yehova atakubali na kubariki.—Soma Zaburi 37:5.

FAHAMU MAPENZI YA YEHOVA

7. Ikiwa hakuna sheria hususa katika Biblia, tutajuaje mambo ambayo Yehova anataka tufanye?

7 Huenda ukajiuliza, ‘Tunaweza kujuaje mambo ambayo Yehova anakubali ikiwa Neno lake halina amri hususa kuhusu hali fulani?’ Andiko la Waefeso 5:17 linasema: “Endeleeni kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova.” Ikiwa hakuna sheria hususa katika Biblia, tunawezaje kufahamu mapenzi ya Mungu? Kwa kusali na kukubali mwongozo wa roho yake takatifu.

8. Yesu alifahamu jinsi gani mambo ambayo Yehova alitaka afanye? Toa mfano.

8 Fikiria jinsi ambavyo Yesu alifahamu mambo ambayo Baba yake alitaka afanye. Katika visa viwili, Yesu alisali kabla ya kuandaa kimuujiza chakula kwa ajili ya umati wa watu. (Mt. 14:17-20; 15:34-37) Hata hivyo, aliposhawishiwa na Ibilisi ageuze mawe yawe mkate, Yesu alikataa ingawa alikuwa na njaa. (Soma Mathayo 4:2-4.) Kwa kuwa alielewa maoni ya Baba yake, Yesu alijua kwamba hakupaswa kugeuza mawe yawe mkate. Alitambua kwamba kutumia nguvu zake kujinufaisha kulikuwa kinyume cha mapenzi ya Mungu. Alipokataa kufanya hivyo, alionyesha kwamba anamtegemea Yehova amwongoze na kumtunza.

9, 10. Ni nini kitakachotusaidia tufanye maamuzi ya hekima? Toa mfano.

9 Ili tufanye maamuzi ya hekima kama Yesu alivyofanya, ni lazima tutegemee mwongozo wa Yehova. Tunahitaji kutenda kulingana na maneno haya ya hekima: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako mwenyewe. Mwogope Yehova na ujiepushe na ubaya.” (Met. 3:5-7) Kuelewa maoni ya Yehova kupitia funzo la Biblia kutatusaidia tufahamu yale ambayo Mungu anataka tufanye katika hali fulani. Kadiri tunavyofahamu mawazo ya Yehova, ndivyo moyo wetu utakavyotambua mwongozo wake.—Eze. 11:19.

10 Kwa mfano: Wazia mwanamke aliyeolewa ambaye yuko dukani. Anaona viatu anavyovipenda, lakini vya bei ghali sana. Kwa hiyo anajiuliza, ‘Mume wangu atahisije nikitumia pesa nyingi hivyo?’ Inaelekea tayari anajua hisia za mume wake, ingawa hayupo pamoja naye. Kwa nini? Kwa sababu kuishi na mume wake kwa muda fulani kumemsaidia aelewe maoni yake kuhusu matumizi ya pesa. Kwa hiyo, anafahamu mawazo ya mume wake kuhusu kununua viatu hivyo. Kwa njia hiyohiyo, tunapozidi kujua mawazo na njia za Yehova, tunaboresha uwezo wetu wa kufahamu mambo ambayo Baba yetu wa mbinguni angependa tufanye katika hali mbalimbali.

UTAJUAJE MAONI YA YEHOVA?

11. Tunaweza kujiuliza maswali gani tunaposoma au kujifunza Biblia? (Ona sanduku lenye kichwa “ Unapojifunza Neno la Mungu, Jiulize Hivi.”)

11 Ili tuelewe vizuri maoni ya Yehova, ni muhimu sana tuwe na funzo la kibinafsi. Tunaposoma au kujifunza Neno la Mungu, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Habari hii inafunua nini kumhusu Yehova, njia zake za uadilifu, na maoni yake?’ Tunahitaji kuwa na mtazamo kama wa mtunga-zaburi, Daudi, aliyeimba hivi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova; nifundishe mapito yako mwenyewe. Nitembeze katika kweli yako na kunifundisha, kwa maana wewe ni Mungu wangu wa wokovu. Nimekutumainia mchana kutwa.” (Zab. 25:4, 5) Unapotafakari sehemu fulani ya Biblia, unaweza kujiuliza maswali kama haya: ‘Ninaweza kutumiaje habari hii? Ninaweza kuitumia wapi? Je, ninaweza kuitumia katika familia, kazini, shuleni, au katika huduma?’ Baada ya kujua ni wapi unapoweza kutumia habari hiyo, itakuwa rahisi zaidi kufahamu utaitumiaje.

12. Machapisho na mikutano yetu inaweza kutusaidiaje kujua maoni ya Yehova kuhusu mambo mbalimbali?

12 Njia nyingine itakayotusaidia kuelewa vizuri zaidi maoni ya Yehova ni kufuata kwa makini mwongozo unaotegemea Biblia unaotolewa na tengenezo lake. Kwa mfano, Fahirisi na Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova unatolewa ili kutusaidia tujifunze maoni ya Yehova kuhusu jinsi tunavyopaswa kufanya maamuzi ya kibinafsi katika hali tofauti-tofauti. Pia, tunanufaika sana tunaposikiliza kwa makini na kushiriki katika mikutano ya Kikristo. Kutafakari mambo tunayofundishwa kutatusaidia tutambue maoni ya Yehova na kuiga njia yake ya kufikiri. Tukitumia kikamili chakula cha kiroho kutoka kwa Yehova, hatua kwa hatua tutaelewa vizuri zaidi njia zake. Hivyo, tutafanya maamuzi ambayo Mungu wetu mwenye upendo atabariki.

FANYA MAAMUZI KWA KUTEGEMEA MAONI YA YEHOVA

13. Toa mfano unaoonyesha jinsi kuzingatia maoni ya Yehova kunavyoweza kutusaidia tufanye maamuzi ya hekima.

13 Fikiria mfano unaoonyesha jinsi maoni ya Yehova yanavyoweza kutusaidia tufanye maamuzi ya hekima. Tukiwa wahubiri wa Ufalme, huenda tukatamani kufanya utumishi wa wakati wote kama vile upainia wa kawaida. Ili tufanikiwe, tunachukua hatua ya kurahisisha maisha yetu. Wakati huohuo, huenda tukawa na wasiwasi kama kweli tutakuwa na furaha licha ya kuwa na vitu vichache vya kimwili. Bila shaka, hakuna amri katika Biblia inayotuamuru tuwe mapainia. Tunaweza kuendelea kumtumikia Yehova tukiwa wahubiri waaminifu. Hata hivyo, Yesu anatuhakikishia kwamba wale wanaojidhabihu kwa ajili ya Ufalme watapata baraka nyingi. (Soma Luka 18:29, 30.) Isitoshe, Maandiko yanaonyesha kwamba Yehova anafurahi tunapomtolea kwa shangwe “matoleo ya hiari” na kufanya yote tuwezayo kuendeleza ibada ya kweli. (Zab. 119:108; 2 Kor. 9:7) Kusoma Maandiko hayo na kusali ili tupate mwongozo, kunatusaidia tufahamu maoni ya Yehova. Tukitafakari mambo hayo tutafanya uamuzi mzuri ambao Baba yetu wa mbinguni atabariki.

14. Unaweza kujuaje ikiwa mtindo fulani wa mavazi unamfurahisha Yehova?

14 Fikiria mfano mwingine: Wazia kwamba unapenda mtindo fulani wa mavazi ambao unaweza kuwakwaza wengine kutanikoni. Lakini huenda hakuna sheria hususa ya Biblia inayopinga mtindo huo. Yehova ana maoni gani kuhusu jambo hilo? Mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kutoa ushauri huu: “Natamani wanawake wajipambe kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, si kwa mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mavazi yaliyo ghali sana, bali kwa njia inayowafaa wanawake wanaodai kumheshimu Mungu, yaani, kupitia matendo mema.” (1 Tim. 2:9, 10) Kanuni inayopatikana katika andiko hilo inawahusu pia wanaume Wakristo. Tukiwa watumishi wa Yehova waliojitoa kikamili, hatufikirii tu mambo tunayopenda, bali tunafikiria jinsi mavazi na mapambo yetu yanavyoweza kuwaathiri wengine. Sifa ya kiasi na upendo utatuchochea tujali maoni ya waabudu wenzetu ili tusiwakengeushe au kuwaudhi. (1 Kor. 10:23, 24; Flp. 3:17) Kuzingatia kile ambacho Biblia inasema kutatusaidia tufahamu maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo na kutuongoza tufanye maamuzi yanayomfurahisha.

15, 16. (a) Yehova anahisije tunapoendelea kufikiria mambo machafu kiadili? (b) Tunapochagua burudani, tunaweza kujuaje kinachomfurahisha Yehova? (c) Tunapaswa kufanya maamuzi mazito jinsi gani?

15 Biblia inaonyesha kwamba Yehova anahuzunika watu wanapofanya mambo maovu na ‘mwelekeo wa fikira za moyo wao unapokuwa mbaya wakati wote.’ (Soma Mwanzo 6:5, 6.) Andiko hilo linatusaidia kufahamu kwamba ni kosa kuwazawaza kuhusu ngono kwa sababu kunaweza kutuongoza kufanya dhambi nzito, ambayo inapingana na Maandiko na ni kinyume cha maoni ya Yehova. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.” (Yak. 3:17) Tukikumbuka jambo hilo, tutakataa burudani inayochochea mawazo na mwelekeo usiofaa. Wakristo wenye ufahamu hawahitaji kuuliza ikiwa ni sawa kusoma kitabu fulani, kutazama sinema au kucheza mchezo unaohusisha mambo ambayo Yehova anachukia. Maoni ya Yehova kuhusu mambo hayo yako wazi katika Neno lake.

16 Mara nyingi tunaweza kufanya uamuzi kwa njia tofauti-tofauti, na bado tumpendeze Yehova. Lakini tunapohitaji kufanya maamuzi mazito, nyakati nyingine huenda ikafaa kuomba ushauri kutoka kwa wazee au Wakristo wakomavu. (Tito 2:3-5; Yak. 5:13-15) Bila shaka, haifai kuwaomba wengine watufanyie maamuzi. Wakristo wanapaswa kuzoeza nguvu zao za ufahamu. (Ebr. 5:14) Sote tunapaswa kutenda kulingana na maneno haya ya Paulo yaliyoongozwa na roho: “Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.”—Gal. 6:5.

17. Tunanufaikaje tunapofanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova?

17 Tunapofanya maamuzi kwa kutegemea maoni ya Yehova, tunamkaribia zaidi. (Yak. 4:8) Anatubariki na tunapata kibali chake. Jambo hilo huimarisha imani yetu kwa Baba yetu wa mbinguni. Kwa hiyo, acheni tukubali kuongozwa na sheria na kanuni za Biblia, kwa kuwa zinafunua maoni ya Mungu. Bila shaka, sikuzote tutajifunza mambo mapya kumhusu Yehova. (Ayu. 26:14) Tukitia bidii, hata sasa tunaweza kupata hekima, ujuzi, na utambuzi tunaohitaji ili tufanye maamuzi ya hekima. (Met. 2:1-5) Mawazo na mipango ya wanadamu wasio wakamilifu hubadilika-badilika, lakini mtunga-zaburi anatukumbusha hivi: “Shauri la Yehova litasimama milele; mawazo ya moyo wake ni kwa kizazi kimoja baada ya kizazi kingine.” (Zab. 33:11) Ni wazi kwamba tunaweza kufanya maamuzi mazuri ikiwa mawazo na matendo yetu yanapatana na maoni ya Mungu wetu mwenye hekima yote, Yehova.