Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Mordekai alikuwa mtu halisi katika historia?

MYAHUDI aliyeitwa Mordekai alitimiza jukumu muhimu katika matukio ya kitabu cha Biblia cha Esta. Alikuwa Myahudi aliyepelekwa uhamishoni ambaye alifanya kazi katika jumba la mfalme wa Uajemi. Ilikuwa mwanzoni mwa karne ya tano K.W.K., “katika siku za [Mfalme] Ahasuero.” (Mfalme huyo leo kwa kawaida anatambuliwa kuwa Shasta wa Kwanza.) Mordekai alizuia njama ya kumuua mfalme. Mfalme alionyesha shukrani kwa kufanya mpango ili Mordekai aheshimiwe hadharani. Baadaye, baada ya kifo cha Hamani, adui ya Mordekai na Wayahudi wengine, mfalme alimpandisha Mordekai cheo na kumfanya kuwa waziri mkuu. Cheo hicho kilimruhusu Mordekai atoe agizo ambalo liliwakomboa Waisraeli katika Milki ya Uajemi wasiangamizwe.​—Esta 1:1; 2:5, 21-23; 8:1, 2; 9:16.

Baadhi ya wanahistoria wa mwanzoni mwa karne ya 20 walidai kwamba kitabu cha Esta ni hadithi ya kutungwa na kwamba Mordekai hakuwahi kuishi kamwe. Hata hivyo, mwaka wa 1941, wachimbuaji wa vitu vya kale walipata uthibitisho ambao huenda unaunga mkono simulizi la Biblia kumhusu Mordekai. Walipata nini?

Watafiti walipata maandishi yaliyochongwa ya kikabari ya Waajemi ambayo yanamtaja mwanamume anayeitwa Marduka (Kiswahili ni Mordekai). Alikuwa msimamizi, au labda mtunza-hesabu, huko Shushani. Arthur Ungnad, mtaalamu wa historia ya mashariki, aliripoti kwamba wakati huo maandishi hayo ya kuchongwa ndiyo yaliyokuwa “marejeo pekee ya ziada mbali na Biblia kumhusu Mordekai.”

Tangu kutolewa kwa ripoti ya Ungnad, wasomi wametafsiri maelfu ya maandishi mengine ya kuchongwa ya kikabari ya Waajemi. Kati ya maandishi hayo ni mabamba ya jiji la Persepolisi ambayo yalipatikana katika marundo ya Hazina karibu na kuta za jiji hilo. Mabamba hayo yaliandikwa wakati wa utawala wa Shasta wa Kwanza. Yameandikwa katika lugha ya Kielamu na yana majina kadhaa yanayopatikana katika kitabu cha Esta. a

Jina Mordekai (Marduka) kama lilivyoandikwa kwenye maandishi ya kuchongwa ya kikabari ya Waajemi

Mabamba kadhaa ya Persepolisi yanataja jina Marduka, ambaye alitumikia akiwa mwandishi wa mfalme kwenye jumba la mfalme huko Shushani wakati wa utawala wa Shasta wa Kwanza. Bamba moja linafafanua kwamba Marduka alikuwa mtafsiri. Maelezo hayo yanapatana na ufafanuzi wa Biblia kumhusu Mordekai. Alikuwa afisa ambaye alitumikia katika makao ya Mfalme Ahasuero (Shasta wa Kwanza) na ambaye alizungumza angalau lugha mbili. Kwa kawaida, Mordekai alikuwa akikaa kwenye lango la jumba la mfalme huko Shushani. (Esta 2:19, 21; 3:3) Lango hilo la mfalme lilikuwa jengo kubwa ambapo maofisa wa makao ya mfalme walifanya kazi.

Kuna ulinganifu mkubwa kati ya Marduka anayetajwa kwenye mabamba hayo na Mordekai anayetajwa katika Biblia. Waliishi katika kipindi kimoja na mahali palepale, na walitumikia wakiwa maofisa waliofanya kazi sehemu ileile. Ulinganifu huo wote kwa pamoja, unaonyesha kwamba mambo ambayo wachimbuaji wa vitu vya kale wamepata, huenda yanahusiana na Mordekai anayefafanuliwa katika kitabu cha Esta.

a Mwaka wa 1992, Profesa Edwin M. Yamauchi, alichapisha majina kumi kutoka kwenye maandishi ya jiji la Persepolisi ambayo pia yanapatikana katika kitabu cha Esta.