Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 45

Jinsi Yehova Anavyotusaidia Kutimiza Huduma Yetu

Jinsi Yehova Anavyotusaidia Kutimiza Huduma Yetu

“Watajua kwa hakika kwamba nabii alikuwa miongoni mwao.”​—EZE. 2:5.

WIMBO 67 “Lihubiri Neno”

MUHTASARI a

1. Tunaweza kutarajia nini, na tunaweza kuwa na uhakika gani?

 TUNAWEZA kutarajia kukabili upinzani tunapotimiza kazi yetu ya kuhubiri. Inawezekana kwamba upinzani huo utaongezeka wakati ujao. (Dan. 11:44; 2 Tim. 3:12; Ufu. 16:21) Ingawa hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatupatia msaada tunaohitaji. Kwa nini? Sikuzote Yehova amewasaidia watumishi wake watimize migawo yao​—haidhuru kazi hiyo ni ngumu kadiri gani. Ili kuona mfano wa jambo hilo, acheni tuchunguze baadhi ya matukio katika maisha ya nabii Ezekieli ambaye aliwahubiria Wayahudi waliokuwa uhamishoni huko Babiloni.

2. Yehova aliwafafanuaje watu ambao Ezekieli angewahubiria, na tutachunguza nini katika makala hii? (Ezekieli 2:3-6)

2 Ezekieli aliwahubiria watu wa aina gani? Yehova aliwafafanua kuwa “wakaidi,” “wenye moyo mgumu,” na ‘waasi.’ Walikuwa wenye madhara kama miiba na hatari kama nge. Ndiyo sababu Yehova alimwambia Ezekieli tena na tena: “Usiogope”! (Soma Ezekieli 2:3-6.) Ezekieli alifaulu kutimiza kazi yake ya kuhubiri kwa sababu (1) alitumwa na Yehova, (2) alitiwa nguvu na roho ya Mungu, na (3) aliimarishwa na maneno ya Mungu. Mambo hayo matatu yalimsaidiaje Ezekieli? Na yanatusaidiaje leo?

EZEKIELI​—ALITUMWA NA YEHOVA

3. Ni maneno gani ambayo yalimwimarisha Ezekieli, na Yehova alimhakikishiaje kwamba angemtegemeza?

3 Yehova alimwambia hivi Ezekieli: “Ninakutuma.” (Eze. 2:3, 4) Ni wazi kwamba maneno hayo yalimwimarisha Ezekieli. Kwa nini? Bila shaka alikumbuka kwamba Yehova alitumia maneno kama hayo alipomweka rasmi Musa na Isaya wawe manabii Wake. (Kut. 3:10; Isa. 6:8) Ezekieli alijua pia jinsi Yehova alivyowasaidia manabii hao wawili washinde changamoto walizokabili. Basi, Yehova alipomwambia hivi Ezekieli mara mbili: “Ninakutuma,” nabii huyo alikuwa na sababu nzuri za kutumaini kwamba Yehova angemtegemeza. Isitoshe, katika kitabu cha Ezekieli tunapata maneno haya mara kadhaa: “Neno la Yehova likanijia.” (Eze. 3:16) Pia, maneno “Neno la Yehova likanijia tena” yanarudiwa mara nyingi. (Eze. 6:1) Kwa kweli, Ezekieli alikuwa na usadikisho kwamba alikuwa ametumwa na Yehova. Isitoshe, akiwa mwana wa kuhani, inaelekea kwamba Ezekieli alifundishwa na baba yake jinsi ambavyo katika historia yote Yehova aliwahakikishia manabii Wake kwamba angewasaidia. Yehova alikuwa amemwambia Isaka, Yakobo, na Yeremia maneno haya: “Niko pamoja nawe.”​—Mwa. 26:24; 28:15; Yer. 1:8.

4. Ni maneno gani yenye kufariji ambayo yalimwimarisha Ezekieli?

4 Waisraeli wengi wangeitikiaje ujumbe wa Ezekieli? Yehova alisema hivi: “Watu wa nyumba ya Israeli watakataa kukusikiliza, kwa maana hawataki kunisikiliza mimi.” (Eze. 3:7) Walipomkataa Ezekieli, watu hao walikuwa wakimkataa Yehova. Maneno hayo yalimhakikishia Ezekieli kwamba ingawa watu wangekataa kumsikiliza, hilo halingemaanisha kwamba ameshindwa kutimiza mgawo wake akiwa nabii. Pia, Yehova alimhakikishia kwamba wakati ambapo hukumu alizotangaza zingetimia, watu wangejua kwamba “nabii alikuwa miongoni mwao.” (Eze. 2:5; 33:33) Bila shaka, maneno hayo yenye kufariji yalimwimarisha Ezekieli ili atimize huduma yake.

LEO​—TUMETUMWA NA YEHOVA

Kama Ezekieli, huenda watu wasipendezwe na ujumbe wetu na hata wakatupinga, lakini tunajua kwamba Yehova yuko pamoja nasi (Tazama fungu la 5 na 6)

5. Kulingana na Isaya 44:8, ni nini kinachotupatia nguvu?

5 Sisi pia tunaimarishwa tunapojua kwamba tumetumwa na Yehova. Ametuheshimu kwa kutuita “mashahidi” wake. (Isa. 43:10) Hilo ni pendeleo kubwa sana! Kama vile Yehova alivyomhimiza Ezekieli: “Usiogope,” Yehova anatuhimiza hivi: “Msiogope.” Kwa nini hatupaswi kuwaogopa wapinzani wetu? Kama Ezekieli, tumetumwa na Yehova naye anatutegemeza.​—Soma Isaya 44:8.

6. (a) Yehova anatuhakikishiaje kwamba atatusaidia? (b) Ni nini kinachotupatia faraja na nguvu?

6 Yehova anatuhakikishia kwamba atatusaidia. Kwa mfano, kabla ya Yehova kusema: “Ninyi ni mashahidi wangu,” alisema: “Unapopita katika maji, nitakuwa pamoja nawe, na unapopita katika mito, haitafurika na kukufunika. Unapotembea katika moto, hutateketea, wala mwali wa moto hautakuunguza.” (Isa. 43:2) Tunapotimiza huduma yetu, wakati mwingine tunakabili vizuizi vilivyo kama mafuriko na majaribu makali kama moto. Ingawa hivyo, kwa msaada wa Yehova tunaendelea kuhubiri. (Isa. 41:13) Kama ilivyokuwa katika siku za Ezekieli, leo watu wengi hawataki kusikiliza ujumbe wetu. Tunakumbuka kwamba wanapokataa kusikiliza, hilo halimaanishi kwamba tumeshindwa kutimiza kazi yetu tukiwa Mashahidi wa Mungu. Tunafarijiwa na kutiwa moyo kwa kujua kwamba Yehova anafurahi tunapoendelea kuwa waaminifu kwa kutangaza ujumbe wake. Mtume Paulo alisema hivi: “Kila mtu atapokea thawabu yake kulingana na kazi yake mwenyewe.” (1 Kor. 3:8; 4:1, 2) Dada mmoja ambaye amekuwa painia kwa miaka mingi alisema hivi: “Ninapata shangwe kujua kwamba Yehova anabariki jitihada zetu.”

EZEKIELI​—ALITIWA NGUVU NA ROHO YA MUNGU

Ezekieli anaona maono ya gari la kimbingu la Yehova ambayo yanaimarisha usadikisho wake kwamba Yehova atamsaidia kutimiza huduma yake (Tazama fungu la 7)

7. Ni lazima Ezekieli alihisije kila mara alipotafakari maono aliyoona? (Tazama picha kwenye jalada.)

7 Ezekieli aliona jinsi roho ya Mungu ilivyo yenye nguvu sana. Katika maono, aliona roho takatifu ikitenda juu ya viumbe wa kiroho wenye nguvu na kwenye magurudumu makubwa sana ya gari la kimbingu. (Eze. 1:20, 21) Ezekieli aliitikiaje? Aliandika jambo lililotokea. “Nilipouona, nikaanguka chini kifudifudi.” Ezekieli alistaajabu sana hivi kwamba akaanguka chini. (Eze. 1:28) Baadaye, kila mara Ezekieli alipotafakari kuhusu maono hayo yenye kuimarisha, ni lazima hilo liliimarisha usadikisho wake kwamba kwa msaada wa roho ya Mungu, angetimiza huduma yake.

8-9. (a) Amri ambayo Yehova alimpa Ezekieli ilimsaidiaje? (b) Yehova alimwimarishaje zaidi Ezekieli ili ahubiri katika eneo gumu?

8 Yehova alimwamuru Ezekieli hivi: “Mwana wa binadamu, simama kwa miguu yako ili nizungumze nawe.” Amri hiyo pamoja na roho ya Mungu ilimpa Ezekieli nguvu ambayo alihitaji ili kusimama. Ezekieli aliandika hivi: “Roho ikaingia ndani yangu na kunifanya nisimame kwa miguu yangu.” (Eze. 2:1, 2) Baadaye, na katika huduma yake yote, Ezekieli aliongozwa na “mkono” wa Mungu, yaani, roho yake takatifu. (Eze. 3:22; 8:1; 33:22; 37:1; 40:1) Roho ya Mungu ilimwimarisha Ezekieli kwa ajili ya kazi aliyopewa​—kazi ya kuwahubiria watu wenye “vichwa vigumu na mioyo migumu” katika eneo lake. (Eze. 3:7) Yehova alimwambia Ezekieli hivi: “Nimeufanya uso wako uwe mgumu kama nyuso zao na paji la uso wako liwe gumu kama mapaji ya nyuso zao. Nimelifanya paji la uso wako kuwa kama almasi, gumu kuliko jiwe gumu. Usiwaogope, wala usitishwe na nyuso zao.” (Eze. 3:8, 9) Ni kana kwamba Yehova alimwambia hivi Ezekieli: ‘Usiruhusu ukaidi wa watu ukuvunje moyo. Mimi nitakuimarisha.’

9 Baada ya hapo, roho ya Mungu ilimbeba Ezekieli katika kazi yake ya kuhubiri. Ezekieli aliandika hivi: “Mkono wa Yehova ukatulia juu yangu kwa nguvu.” Ilimchukua nabii huyo juma moja kutafakari na kuelewa kikamili ujumbe ambao alipaswa kutangaza ili azungumze kwa usadikisho. (Eze. 3:14, 15) Kisha Yehova akamwagiza aende kwenye bonde tambarare, akiwa huko “roho ikaingia ndani [yake].” (Eze. 3:23, 24) Sasa Ezekieli alikuwa tayari kuanza huduma yake.

LEO​—TUNAIMARISHWA NA ROHO YA MUNGU

Kama ilivyokuwa kwa Ezekieli, ni nini kinachotusaidia leo kutimiza huduma yetu? (Tazama fungu la 10)

10. Tunahitaji msaada gani ili kutimiza kazi yetu ya kuhubiri, na kwa nini?

10 Tunahitaji msaada gani ili kutimiza kazi yetu ya kuhubiri? Ili kujibu swali hilo, fikiria mambo ambayo Ezekieli alijionea. Kabla ya kuanza kuhubiri, roho ya Mungu ilimpa nguvu alizohitaji. Leo, kama ilivyokuwa kwa Ezekieli, tunaweza tu kutimiza kazi ya kuhubiri kwa msaada wa roho ya Mungu. Kwa nini? Kwa sababu Shetani anapigana vita dhidi yetu ili kusimamisha kazi yetu ya kuhubiri. (Ufu. 12:17) Kwa maoni ya kibinadamu, inaweza kuonekana kwamba hatuwezi kumshinda Shetani. Lakini kupitia kazi yetu ya kuhubiri, tunamshinda! (Ufu. 12:9-11) Jinsi gani? Tunaposhiriki katika huduma, tunaonyesha kwamba hatuogopi vitisho vya Shetani. Kila mara tunapohubiri, tunamshinda Shetani. Basi, kwa kuwa tunaendelea kutimiza kazi yetu ya kuhubiri licha ya upinzani, tunaweza kufikia mkataa gani? Tunasadiki kabisa kwamba tunaimarishwa na roho takatifu na kwamba tuna kibali cha Yehova.​—Mt. 5:10-12; 1 Pet. 4:14.

11. Roho ya Mungu itatusaidiaje, na tunawezaje kuendelea kuipokea?

11 Tunapata uhakikisho gani zaidi kwa kujua kwamba kwa njia ya mfano, Yehova alikuwa amefanya uso na paji la uso wa Ezekieli kuwa gumu? Roho ya Mungu inaweza kutupatia nguvu tunazohitaji ili kukabiliana na changamoto yoyote katika huduma yetu. (2 Kor. 4:7-9) Basi, tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tutaendelea kupokea roho ya Mungu? Tunapaswa kuendelea kusali ili tupate roho hiyo, tukiwa na uhakika kwamba Yehova atasikiliza sala zetu. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake hivi: “Endeleeni kuomba, . . . endeleeni kutafuta, . . . endeleeni kupiga hodi.” Matokeo ni kwamba Yehova ‘atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.’—Luka 11:9, 13; Mdo. 1:14; 2:4.

EZEKIELI​—ALIIMARISHWA NA MANENO YA MUNGU

12. Kulingana na Ezekieli 2:9–3:3, kile kitabu cha kukunjwa kilitoka wapi, nacho kilikuwa na ujumbe gani?

12 Ezekieli hakutiwa nguvu tu na roho ya Mungu, bali pia aliimarishwa na maneno ya Mungu. Katika maono, Ezekieli aliona mkono ulioshika kitabu cha kukunjwa. (Soma Ezekieli 2:9–3:3.) Kitabu hicho cha kukunjwa kilitoka wapi? Kilikuwa na ujumbe gani? Kilimwimarishaje Ezekieli? Acheni tuone. Kitabu hicho cha kukunjwa kilitoka kwenye kiti cha enzi cha Mungu. Inaelekea kwamba Yehova alitumia mmoja kati ya malaika wanne ambao Ezekieli alikuwa amewaona hapo awali ili kumpa kitabu hicho cha kukunjwa. (Eze. 1:8; 10:7, 20) Kitabu hicho kilikuwa na maneno ya Mungu, yaani, ujumbe mrefu wa hukumu ambao Ezekieli alipaswa kuwatangazia wahamishwa walioasi. (Eze. 2:7) Ujumbe huo ulikuwa umeandikwa upande wa mbele na nyuma wa kitabu hicho cha kukunjwa.

13. Yehova alimwambia Ezekieli afanye nini na kile kitabu cha kukunjwa, na kwa nini kilikuwa kitamu?

13 Yehova alimwambia nabii wake ale kitabu hicho cha kukunjwa na ‘akijaze tumboni mwake.’ Ezekieli alitii na akala kitabu hicho chote. Sehemu hiyo ya maono ilimaanisha nini? Ezekieli alihitaji kuelewa kikamili ujumbe ambao alipaswa kutangaza. Alipaswa kuamini kabisa ujumbe huo ili uchochee hisia zake za ndani kabisa. Kisha jambo la kushangaza likatokea. Ezekieli alitambua kwamba kitabu hicho “kilikuwa kitamu kama asali.” (Eze. 3:3) Kwa nini? Ezekieli aliona heshima ya kumwakilisha Yehova kuwa jambo tamu, au lenye kufurahisha. (Zab. 19:8-11) Alikuwa mwenye shukrani kwa sababu Yehova alikuwa amemchagua kuwa nabii wake.

14. Ni nini kilichomsaidia Ezekieli awe tayari kukubali mgawo wake?

14 Baadaye, Yehova alimwambia hivi Ezekieli: “Yatie moyoni mwako na kuyasikiliza maneno yangu yote nitakayokuambia.” (Eze. 3:10) Kupitia maagizo hayo, Yehova alimwambia Ezekieli atunze katika kumbukumbu yake maneno yaliyoandikwa kwenye kile kitabu cha kukunjwa na ayatafakari. Kufanya hivyo kulimwimarisha Ezekieli kibinafsi. Pia, kulimpatia ujumbe wenye nguvu ambao angewatangazia watu. (Eze. 3:11) Akiwa na ujumbe wa Mungu moyoni mwake na kwenye midomo yake, sasa Ezekieli alikuwa tayari kuanza mgawo wake na kuutimiza.​—Linganisha Zaburi 19:14.

LEO​—TUNAIMARISHWA NA MANENO YA MUNGU

15. Ili tuendelee kutimiza huduma yetu, tunapaswa ‘kutia nini moyoni mwetu’?

15 Ili tuendelee kutimiza huduma yetu, sisi pia tunahitaji kuendelea kuimarishwa na maneno ya Mungu. Tunahitaji ‘kutia moyoni’ mambo yote ambayo Yehova anatuambia. Leo, Yehova anazungumza nasi kupitia Neno lake lililoandikwa, Biblia. Tunawezaje kuhakikisha kwamba Neno la Mungu linaendelea kuchochea fikira, hisia, na nia yetu?

16. Ni lazima tufanye nini na Neno la Mungu, na tunawezaje kulielewa vizuri zaidi moyoni mwetu?

16 Kama vile tunavyoimarishwa kimwili tunapokula chakula na kukimeng’enya, hivyo ndivyo tunavyoimarishwa kiroho tunapojifunza Neno la Mungu na kulitafakari. Tunakumbuka somo tunalojifunza kutokana na kile kitabu cha kukunjwa. Kuhusu Neno la Mungu, Yehova anataka ‘tulijaze tumboni mwetu,’ yaani, tulielewe vizuri. Tunaweza kufanya hivyo kwa kusali, kusoma, na kutafakari. Kwanza, tunasali ili kutayarisha moyo wetu upokee mawazo ya Mungu. Kisha tunasoma sehemu fulani ya Biblia. Halafu, tunatua ili kutafakari na kufikiria kwa undani kuhusu mambo ambayo tumesoma. Matokeo yatakuwaje? Kadiri tunavyotafakari, ndivyo moyo wetu wa mfano unavyozidi kulielewa Neno la Mungu.

17. Kwa nini ni muhimu kutafakari mambo tunayosoma katika Biblia?

17 Kwa nini ni muhimu kusoma Biblia na kuitafakari? Kufanya hivyo kunatupatia nguvu tunazohitaji ili kuhubiri ujumbe wa Ufalme sasa na kutangaza ujumbe mkali wa hukumu ambao huenda tutatangaza hivi karibuni. Pia, tunapotafakari sifa za Yehova zenye kuvutia, uhusiano wetu pamoja naye utazidi kuimarika. Matokeo ni kwamba tutafurahia jambo tamu, au lenye kufurahisha, yaani, tutaridhika na kuwa na amani moyoni.​—Zab. 119:103.

TUNACHOCHEWA KUVUMILIA

18. Watu katika eneo letu watalazimika kutambua jambo gani, na kwa nini?

18 Ezekieli alikuwa nabii, lakini sisi si manabii. Hata hivyo, tumeazimia kuendelea kutangaza ujumbe ulioongozwa na roho ya Mungu ambao Yehova ametunza katika Neno lake lililoandikwa, hadi kazi ya kuhubiri itakapokamilishwa kwa njia ambayo itamridhisha. Wakati wa hukumu utakapofika, watu katika eneo letu hawatakuwa na kisingizio cha kusema kwamba hawakupokea onyo au kwamba Mungu aliwapuuza. (Eze. 3:19; 18:23) Badala yake, watalazimika kutambua kwamba ujumbe tuliokuwa tukihubiri ulitoka kwa Mungu.

19. Ni nini ambacho kitatuimarisha ili tutimize huduma yetu?

19 Ni nini ambacho kitatuimarisha ili kutimiza huduma yetu? Ni yale mambo matatu yaliyomwimarisha Ezekieli. Tunaendelea kuhubiri kwa sababu tunajua kwamba tumetumwa na Yehova, tunatiwa nguvu na roho takatifu ya Mungu, na tunaimarishwa na Neno la Mungu. Kwa msaada wa Yehova, tunachochewa kuendelea kutimiza huduma yetu na kuvumilia “mpaka mwisho.”​—Mt. 24:13.

WIMBO 65 Songa Mbele!

a Katika makala hii, tutachunguza mambo matatu yaliyomsaidia nabii Ezekieli atimize mgawo wake wa kuhubiri. Tunapochunguza jinsi Yehova alivyomsaidia nabii huyo, tutaimarisha uhakika wetu kwamba Yehova atatusaidia pia ili tutimize huduma yetu.