Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

“Nilitaka Kufanya Kazi ya Yehova”

“Nilitaka Kufanya Kazi ya Yehova”

TULIPUNGA mkono na kukiaga kikundi kidogo cha watu ambao tulikuwa tumewatembelea karibu na kijiji cha Granbori, kilicho ndani ya msitu wa mvua huko Suriname. Kisha tukapanda mashua ya mbao kwenye Mto Tapanahoni. Baadaye, tukapita kwenye maporomoko ya mto na propela ya mashua ikagonga mwamba. Papo hapo, mashua ikaanguka kwenye maporomoko na tukazama ndani ya maji. Moyo wangu ukaanza kupiga mbiombio. Ingawa nilikuwa nimesafiri kwenye mto kwa mashua kwa miaka mingi nikiwa mwangalizi wa mzunguko, sikujua jinsi ya kuogelea.

Kabla sijawasimulia kilichofuata, acheni niwaambie jinsi nilivyoanza utumishi wa wakati wote.

Nilizaliwa mwaka wa 1942, kwenye kisiwa maridadi cha Karibea kinachoitwa Curaçao. Baba yangu alitokea Suriname, lakini tulihamia kwenye kisiwa hicho kwa sababu ya kazi ya baba. Miaka kadhaa kabla sijazaliwa, baba alikuwa kati ya Mashahidi wa kwanza wa Yehova kubatizwa huko Curaçao. a Alijifunza Biblia pamoja nasi watoto kila juma, ingawa si sikuzote tulipenda kujifunza. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, baba yangu aliihamisha familia yetu kwenda Suriname ili kumtunza mama yake aliyekuwa akizeeka.

KUSHIRIKIANA NA MARAFIKI WAZURI KULINISAIDIA

Huko Suriname nilianza kushirikiana na vijana kutanikoni ambao walikuwa wakimtumikia Yehova kwa bidii. Walikuwa wamenizidi umri kwa miaka michache na walitumikia kama mapainia wa kawaida. Walipokuwa wakizungumzia mambo waliyojionea kwenye utumishi wa shambani, nyuso zao ziling’aa kwa shangwe. Baada ya mikutano ya kutaniko, mimi na rafiki zangu pia tulikuwa na mazungumzo kuhusu habari za Biblia, nyakati nyingine tukiwa tumeketi nje usiku chini ya anga lenye nyota. Marafiki hao walinisaidia kutambua jambo ambalo nilitaka maishani; nilitaka kufanya kazi ya Yehova. Basi nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 16. Baadaye, nilipokuwa na umri wa miaka 18, nilianza upainia wa kawaida.

KUJIFUNZA MASOMO MUHIMU

Nilipokuwa nikifanya upainia huko Paramaribo

Nilijifunza masomo mengi nilipokuwa painia, na masomo hayo yamenisaidia kipindi chote ambacho nimekuwa katika utumishi wa wakati wote. Kwa mfano, somo la kwanza ambalo nilijifunza ni umuhimu wa kuwazoeza wengine. Nilipoanza kufanya upainia, mmishonari aliyeitwa Willem van Seijl alipendezwa nami kibinafsi. b Alinifundisha mambo mengi sana kuhusu jinsi ya kushughulikia migawo ya kitheokrasi. Wakati huo sikujua kwamba nilihitaji sana kupata mazoezi hayo. Mwaka uliofuata niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee, na baada ya hapo nikaanza kusimamia vikundi vilivyo mbali, ndani kabisa ya msitu wa mvua wa Suriname. Ninathamini sana mazoezi ambayo akina ndugu walinipa! Tangu wakati huo, nimejitahidi kuiga mfano wao kwa kutenga muda ili kuwazoeza wengine.

Somo la pili nililojifunza ni umuhimu wa kuishi maisha rahisi yenye mpangilio mzuri. Mwanzoni mwa kila mwezi, mimi na painia wa pekee mwenzangu tulifanya mipango ya kupata mahitaji yetu ya kimwili kwa ajili ya majuma ambayo yangefuata. Kisha mmoja wetu angefunga safari ndefu ya kwenda kwenye mji mkuu ili kununua vitu tulivyohitaji. Tulihitaji kutumia pesa tulizopata kila mwezi kwa makini na kugawa chakula kwa makini ili kiweze kutosha kwa mwezi mzima. Tulipoishiwa na kitu fulani tukiwa katika msitu wa mvua, ni watu wachache sana ambao wangeweza kutusaidia. Ninaamini kwamba kujifunza kuishi maisha rahisi yenye mpangilio mzuri nilipokuwa kijana, kumenisaidia kukazia fikira kazi ya Yehova katika maisha yangu yote.

Somo la tatu nililojifunza ni manufaa ya kuwafundisha watu kwa kutumia lugha yao ya asili. Nililelewa nikizungumza Kiholanzi, Kiingereza, Papiamento, na Sranantongo (pia, inajulikana kama Sranan), lugha inayozungumzwa na watu wengi huko Suriname. Lakini katika msitu wa mvua, niliona kwamba watu waliitikia kwa njia nzuri zaidi habari njema tulipowahubiria kwa kutumia lugha yao ya asili. Ilikuwa vigumu kwangu kuzungumza baadhi ya lugha hizo, kwa mfano, lugha ya Saramaccan ambayo inatumia sauti za juu na chini. Hata hivyo, jitihada zetu hazikuwa za bure. Kwa miaka mingi, nimefaulu kuwafundisha watu wengi zaidi ukweli kwa sababu ninaweza kuzungumza lugha yao ya asili.

Bila shaka, pindi fulani nilisema mambo yenye kuaibisha. Kwa mfano, pindi moja nilitaka kumuuliza mwanafunzi wa Biblia aliyezungumza lugha ya Saramaccan jinsi alivyokuwa akihisi, kwa sababu alikuwa na maumivu ya tumbo. Lakini kihalisi nilimuuliza kama alikuwa mjamzito! Kwa kweli, hakufurahishwa na swali nililomuuliza. Lakini licha ya changamoto kama hizo, sikuzote nilijitahidi kuzungumza lugha ya asili ya watu katika migawo yangu.

KUKUBALI MAJUKUMU YA ZIADA

Mwaka wa 1970, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko. Mwaka huo nilionyesha programu ya picha za slaidi yenye kichwa “Kutembelea Makao Makuu ya Mashahidi wa Yehova” kwa vikundi vingi vilivyo mbali kwenye msitu wa mvua. Ili kufikia vikundi hivyo, kikundi cha akina ndugu pamoja nami tungesafiri kwenye mito ya msitu wa mvua tukitumia mashua ndefu, nyembamba ya mbao. Mashua yetu ilibeba jenereta, tangi la petroli, taa za petroli, na projekta ya kuonyesha picha za slaidi. Tulipofika mwisho wa safari, tulibeba vifaa ndani ya msitu hadi mahali ambapo tungeonyesha programu hiyo ya slaidi. Hata hivyo, jambo ninalokumbuka zaidi kuhusu safari hizo ni jinsi watu katika maeneo hayo ya mbali walivyopenda programu hizo. Nilifurahi sana kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova na sehemu ya kidunia ya tengenezo lake. Baraka za kiroho zilizidi kwa mbali mambo yoyote niliyodhabihu nilipokuwa nikifanya kazi ya Yehova.

KUSUKA KAMBA YA NYUZI TATU

Mimi na Ethel tulifunga ndoa Septemba 1971

Ingawa niliona kwamba useja ulinisaidia katika utumishi wangu, bado nilihisi uhitaji wa kupata mwenzi wa ndoa. Basi, nilianza kusali kihususa ili nipate mke ambaye angefurahia kwa shangwe hali ngumu katika utumishi wa wakati wote kwenye msitu wa mvua. Mwaka mmoja hivi baadaye, nilianza kufanya uchumba na Ethel, painia wa pekee ambaye alikuwa na roho ya kujidhabihu. Tangu alipokuwa na umri mdogo, Ethel alipendezwa sana na mtume Paulo na alitaka kujitolea kwenye huduma ya Kikristo kama alivyofanya Paulo. Tulifunga ndoa Septemba 1971, na tukaanza kutumikia katika mgawo wa mwangalizi wa mzunguko tukiwa wenzi wa ndoa.

Ethel alilelewa katika familia ambayo haikuwa na vitu vingi vya kimwili. Basi, ilikuwa rahisi kwake kuzoea maisha ya kazi ya kusafiri kwenye msitu wa mvua. Kwa mfano, tulipokuwa tukijitayarisha kutembelea makutaniko yaliyokuwa ndani kabisa ya msitu, tulibeba vitu vichache. Tulifua nguo na kuoga kwenye mito. Pia, tulizoea kula chochote ambacho wale ambao walitukaribisha walituandalia​—mjusi mkubwa aliyeitwa iguana, samaki aina ya piranha, au chochote kile ambacho waliwinda msituni au kuvua kwenye mito. Mahali ambapo hawakuwa na sahani tulikula kwa kutumia majani ya migomba. Ikiwa hawakuwa na vijiko, tulikula kwa mikono. Mimi na Ethel tunahisi kwamba kujidhabihu tukiwa pamoja katika kazi ya Yehova kumetuunganisha kwenye kamba imara yenye nyuzi tatu. (Mhu. 4:12) Hatuwezi kamwe kubadilisha mambo hayo tuliyojionea na kitu kingine chochote!

Jambo lililoonwa nililosimulia mwanzoni lilitokea tulipokuwa tukirudi kutoka kwenye eneo lililo mbali ndani ya msitu. Mashua ilipofika kwenye eneo lenye maporomoko, ilizama ndani ya maji kwa muda mfupi, lakini ghafla ikarudi juu. Jambo zuri ni kwamba tulikuwa tumevaa majaketi ya kuokolea uhai na hatukuanguka nje ya mashua. Lakini mashua yetu ilijaa maji. Tulimwaga vyakula tulivyokuwa tumebeba kwenye vyombo vyetu na tukatumia vyombo hivyo kumwaga maji yaliyokuwa ndani ya mashua.

Kwa kuwa tulipoteza chakula chetu, tulianza kuvua samaki tulipoendelea na safari kwenye mto. Lakini hatukuvua samaki hata mmoja. Basi, tukasali kwa Yehova na kumwomba atupe chakula cha siku hiyo. Papo hapo ndugu mmoja akatupa kamba ya kuvua samaki na kumvua samaki mkubwa ambaye angetutosha sisi watu watano usiku huo.

MUME, BABA, NA MWANGALIZI ANAYESAFIRI

Baada ya kufanya kazi ya kuzunguka kwa miaka mitano, Ethel na mimi tulipata baraka ambayo hatukutarajia​—tungekuwa wazazi. Nilifurahia kusikia habari hizo ingawa sikuwa na uhakika jinsi ambavyo wakati wetu ujao ungekuwa. Ethel na mimi tulitamani sana kuendelea na utumishi wa wakati wote ikiwa ingewezekana. Mwaka wa 1976, mwana wetu Ethniël alizaliwa. Mwana wetu wa pili, Giovanni, alizaliwa miaka miwili na nusu baadaye.

Nilipohudhuria ubatizo kwenye Mto Tapanahoni karibu na Godo Holo Mashariki mwa Suriname​—1983

Kwa sababu ya uhitaji nchini Suriname wakati huo, ofisi ya tawi ilifanya mpango ili niendelee kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko huku tukiwalea watoto wetu. Wana wetu walipokuwa wadogo, nilipewa mgawo wa kuzungukia mizunguko yenye makutaniko machache. Kwa kawaida, hilo liliniruhusu nitumikie kwa majuma mawili kila mwezi nikiwa mwangalizi wa mzunguko na kutumia kipindi kilichobaki cha mwezi huo nikiwa painia katika kutaniko ambalo tulikuwa tumepewa mgawo. Ethel na wavulana wetu waliambatana nami nilipokuwa nikitembelea makutaniko yaliyokuwa karibu na nyumbani. Hata hivyo, nilisafiri peke yangu nilipotembelea makutaniko na makusanyiko katika msitu wa mvua.

Nilipokuwa mwangalizi wa mzunguko, mara nyingi nilisafiri kwa mashua ili kutembelea makutaniko yaliyo mbali

Nilihitaji kupanga mambo kwa makini ili nitimize majukumu yangu. Nilihakikisha kwamba tulifanya funzo la familia kila juma. Nilipokuwa nikitembelea makutaniko yaliyokuwa mbali msituni, Ethel aliongoza funzo la familia pamoja na wavulana wetu nyumbani. Hata hivyo, mara nyingi ilivyowezekana, tulifanya mambo pamoja kama familia. Ethel na mimi tulishiriki kwa ukawaida katika tafrija pamoja na wavulana wetu​—iwe ni kucheza michezo au kutembelea sehemu fulani. Mara nyingi nilichelewa kulala usiku, kwa sababu nilikuwa nikijitayarisha kwa ajili ya migawo ya kitheokrasi. Na Ethel, akiwa mke mwenye uwezo anayefafanuliwa kwenye Methali 31:15, alikuwa akiamka kabla hakujapambazuka ili kuhakikisha kwamba tunasoma andiko la siku tukiwa familia na kula kiamsha kinywa pamoja kabla ya wana wetu kwenda shuleni. Ninathamini sana kwamba nina mke mwenye sifa ya kujidhabihu ambaye sikuzote amenisaidia kutimiza majukumu yangu ya Kimaandiko.

Tukiwa wazazi, tulijitahidi sana kuwasaidia wavulana wetu wampende Yehova na huduma ya Kikristo. Tulitaka wana wetu watumie maisha yao katika utumishi wa wakati wote, si kwa sababu sisi tulitaka wafanye hivyo, bali kwa sababu ni uamuzi wao. Sikuzote tulizungumza nao kuhusu shangwe za utumishi wa wakati wote. Bila kupuuza hali ngumu tulizokabili, tulikazia jinsi Yehova alivyotusaidia na kutubariki tukiwa familia. Pia, tulihakikisha kwamba wana wetu walishirikiana na Mashahidi ambao walimtanguliza Yehova maishani mwao.

Yehova alituandalia mahitaji yetu yote tulipokuwa tukiwalea wana wetu. Bila shaka, sikuzote nilijitahidi kutimiza majukumu yangu. Mambo niliyojionea kwenye msitu wa mvua nikiwa painia wa pekee mseja, yalinifundisha jinsi ya kufanya mipango mapema kwa ajili ya mahitaji ya kimwili. Hata hivyo, wakati mwingine licha ya jitihada zetu hatukupata kila kitu tulichohitaji. Katika pindi hizo, ninaamini kwamba Yehova alitusaidia. Kwa mfano, mwishoni mwa miaka ya 1980, na mwanzoni mwa miaka ya 1990, kulikuwa na machafuko ya kisiasa nchini Suriname. Katika miaka hiyo, wakati mwingine ilikuwa vigumu kupata hata mahitaji ya msingi. Hata hivyo, Yehova alituandalia mahitaji yetu.​—Mt. 6:32.

NINAPOTAFAKARI MAISHA YANGU

Kushoto kwenda kulia: Nikiwa na mke wangu, Ethel

Mwana wetu mkubwa, Ethniël, pamoja na mke wake, Natalie

Mwana wetu Giovanni pamoja na mke wake, Christal

Katika maisha yetu yote, sikuzote Yehova ametutunza na ametusaidia kuridhika na kuwa na furaha sana. Watoto wetu wamethibitika kuwa baraka kwetu na limekuwa pendeleo kuwalea ili wawe watumishi wa Yehova. Pia, tunafurahi kwamba walichagua kutumia maisha yao katika utumishi wa wakati wote. Ethniël na Giovanni, wote wamehitimu kutoka kwenye shule za kitheokrasi na sasa wanatumikia kwenye ofisi ya tawi ya Suriname pamoja na wake zao.

Sasa umri wangu na wa Ethel umesonga, lakini bado tunafanya kazi ya Yehova kwa bidii tukiwa mapainia wa pekee. Kwa kweli, tuna shughuli nyingi sana hivi kwamba bado sijapata muda wa kujifunza jinsi ya kuogelea! Lakini sijuti kamwe. Ninapotafakari maisha yangu, kwa kweli ninahisi kwamba uamuzi niliofanya nilipokuwa kijana wa kutumia maisha yangu katika kazi ya utumishi wa wakati wote, ni mojawapo ya maamuzi bora ambayo niliwahi kufanya.

a Tazama Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2002 uku. 70.

b Simulizi la maisha la Willem van Seijl, “Mambo Halisi Yamezidi Mataraja Yangu,” limechapishwa katika gazeti la Amkeni! la Oktoba 8, 1999.