Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 48

Tunza Akili Zako Ushikamanifu Wako Unapojaribiwa

Tunza Akili Zako Ushikamanifu Wako Unapojaribiwa

“Tunza akili zako katika mambo yote.”​—2 TIM. 4:5.

WIMBO 123 Kutii Utaratibu wa Kitheokrasi kwa Ushikamanifu

MUHTASARI a

1. Inamaanisha nini kutunza akili zetu? (2 Timotheo 4:5)

 TUNAPOKABILI hali ngumu ushikamanifu wetu kwa Yehova na tengenezo lake unaweza kujaribiwa. Tunawezaje kushinda changamoto kama hizo? Tunahitaji kutunza akili zetu na kukaa macho, tukisimama imara katika imani. (Soma 2 Timotheo 4:5.) Tunatunza akili zetu kwa kuendelea kuwa watulivu, kufikiria mambo kwa njia nzuri, na kujitahidi kuona mambo kulingana na maoni ya Yehova. Tukifanya hivyo, mawazo yetu hayataongozwa na hisia.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Katika makala iliyotangulia, tulichunguza changamoto tatu zinazotoka nje ya kutaniko ambazo huenda tukakabili. Katika makala hii, tutachunguza changamoto tatu kutoka ndani ya kutaniko ambazo zinaweza kujaribu ushikamanifu wetu kwa Yehova. Changamoto hizo ni (1) tunapohisi kwamba Mkristo mwenzetu ametutendea kwa njia isiyofaa, (2) tunapotiwa nidhamu, na (3) inapokuwa vigumu kufuata mabadiliko ya kitengenezo. Tunawezaje kutunza akili zetu na kuendelea kushikamana na Yehova na tengenezo lake tunapokabili changamoto hizo?

TUNAPOHISI KWAMBA MKRISTO MWENZETU AMETUTENDEA KWA NJIA ISIYOFAA

3. Huenda tukatendaje tunapohisi kwamba Mkristo mwenzetu ametutendea kwa njia isiyofaa?

3 Je, umewahi kuhisi kwamba Mkristo mwenzako amekutendea kwa njia isiyofaa, labda ni ndugu mwenye mapendeleo kutanikoni? Inawezakana kwamba ndugu huyo hakukusudia kukuumiza. (Rom. 3:23; Yak. 3:2) Hata hivyo, huenda matendo yake yalikuumiza. Labda ulikosa usingizi ukifikiria kuhusu jambo hilo. Huenda ulijiuliza hivi, ‘Ikiwa ndugu anaweza kutenda kwa njia hii, je, kweli hili ni tengenezo la Mungu? ’ Hivyo ndivyo Shetani anavyotaka tufikiri. (2 Kor. 2:11) Kufikiria kwa njia hiyo isiyofaa kunaweza kutufanya tujitenge kutoka kwa Yehova na tengenezo lake. Basi, ikiwa ndugu au dada ametutendea kwa njia isiyofaa, tunawezaje kutunza akili zetu na kuepuka kufikiri kwa njia itakayotusababishia madhara?

4. Yosefu alitunzaje akili zake alipotendewa kwa njia isiyofaa, na tunajifunza nini kutokana na mfano wake? (Mwanzo 50:19-21)

4 Usiweke kinyongo. Yosefu alipokuwa tineja, ndugu zake wakubwa walimtendea kwa njia isiyofaa. Walimchukia, na hata baadhi yao walitaka kumuua. (Mwa. 37:4, 18-22) Mwishowe, walimuuza utumwani. Matokeo ni kwamba Yosefu alikabili majaribu makali yaliyodumu kwa miaka 13 hivi. Yosefu angeweza kutilia shaka ikiwa kweli Yehova anampenda. Na huenda alijiuliza ikiwa Yehova alikuwa amemwacha wakati alipohitaji msaada. Lakini Yosefu hakuweka kinyongo. Badala yake, alitunza akili zake kwa kuendelea kuwa mtulivu. Alipopata nafasi ya kulipiza kisasi dhidi ya ndugu zake, alijizuia kufanya hivyo na akawaonyesha upendo na kuwasamehe. (Mwa. 45:4, 5) Yosefu alitenda hivyo kwa sababu alifikiria mambo kwa njia nzuri. Badala ya kukazia fikira matatizo yake, aliona mambo kwa njia pana​—alitambua kusudi la Yehova. (Soma Mwanzo 50:19-21.) Tunapata somo gani? Unapotendewa kwa njia isiyofaa, usiwe na uchungu kumwelekea Yehova au kujiuliza ikiwa amekuacha. Badala yake, tafakari kuhusu jinsi anavyokusaidia kuvumilia jaribu hilo. Isitoshe, wengine wanapokutendea kwa njia isiyofaa, jitahidi kufunika udhaifu wao kwa upendo.​—1 Pet. 4:8.

5. Miqueas alitunzaje akili zake alipohisi kwamba ametendewa kwa njia isiyofaa?

5 Fikiria mfano wa nyakati zetu wa mzee wa kutaniko kutoka Amerika Kusini anayeitwa Miqueas. b Anakumbuka pindi moja ambayo alihisi kwamba ametendwa kwa ukali na baadhi ya akina ndugu wenye mapendeleo katika tengenezo. Alisema hivi: “Sikuwa nimewahi kukabili mkazo kama huo hapo awali. Nilikuwa naogopa. Nilishindwa kulala usiku, nililia na kuhisi sina la kufanya.” Hata hivyo, Miqueas alitunza akili zake na akajitahidi sana kudhibiti hisia zake. Alisali mara kwa mara, akimwomba Yehova ampe roho yake takatifu na nguvu za kuvumilia. Pia, alitafuta habari katika machapisho yetu ambazo zingeweza kumsaidia. Somo ni nini? Ikiwa unahisi kwamba ndugu au dada amekutendea kwa njia isiyofaa, endelea kuwa mtulivu na ujitahidi kudhibiti hisia zisizofaa ambazo huenda ukawa nazo. Huenda usijue hali ambazo zilimfanya mtu huyo azungumze au kutenda kwa njia hiyo. Basi, zungumza na Yehova katika sala na umwombe akusaidie uone mambo kulingana na maoni ya mtu huyo. Kufanya hivyo huenda kukakusaidia usitilie shaka nia ya mwabudu mwenzako na kuachilia kosa lake. (Met. 19:11) Kumbuka kwamba Yehova anaelewa hali unayokabili, naye atakupa nguvu unazohitaji ili kuvumilia.​—2 Nya. 16:9; Mhu. 5:8.

TUNAPOTIWA NIDHAMU

6. Kwa nini ni muhimu tuone nidhamu ya Yehova kama wonyesho wa upendo wake kwetu? (Waebrania 12:5, 6, 11)

6 Nidhamu inaweza kutuumiza kihisia. Lakini ikiwa tutakazia fikira tu maumivu, huenda tukaanza kupunguza uzito wa nidhamu hiyo, tukihisi kwamba hatukustahili kupewa nidhamu au imetolewa kwa ukali sana. Matokeo ni kwamba huenda tukakosa kutambua jambo muhimu sana, yaani, kuona nidhamu hiyo kama wonyesho wa upendo wa Yehova kwetu. (Soma Waebrania 12:5, 6, 11.) Na ikiwa tutaruhusu hisia zetu zituongoze, tutampa Shetani nafasi ya kutumia vibaya hisia zetu. Anataka tukatae nidhamu hiyo, na jambo baya hata zaidi, tujitenge na Yehova na kutaniko. Ikiwa umetiwa nidhamu, unawezaje kutunza akili zako?

Kwa unyenyekevu Petro alikubali shauri na nidhamu, na hivyo akawa mwenye thamani zaidi kwa Yehova (Tazama fungu la 7)

7. (a) Kama inavyoonyeshwa kwenye picha, Yehova alimtumiaje Petro baada ya kukubali nidhamu? (b) Unajifunza nini kutokana na mfano wa Petro?

7 Kubali nidhamu, na ufanye marekebisho yanayohitajika. Zaidi ya mara moja, Yesu alimrekebisha Petro mbele ya mitume wengine. (Marko 8:33; Luka 22:31-34) Bila shaka, hilo lilimwaibisha sana Petro! Hata hivyo, Petro aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Yesu. Alikubali nidhamu na akajifunza kutokana na makosa yake. Matokeo ni kwamba Yehova alimthawabisha Petro kwa sababu ya ushikamanifu wake na akampa majukumu mazito kutanikoni. (Yoh. 21:15-17; Mdo. 10:24-33; 1 Pet. 1:1) Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Petro? Tunajinufaisha sisi wenyewe na wengine tunapoepuka kukazia fikira aibu tunayohisi, tunapokubali shauri, na kufanya marekebisho yanayohitajika. Tunapofanya hivyo, tunakuwa wenye thamani zaidi kwa Yehova na ndugu zetu.

8-9. Baada ya kutiwa nidhamu, mwanzoni Bernardo alihisije, lakini ni nini kilichomsaidia kurekebisha njia yake ya kufikiri?

8 Fikiria jambo lililompata Bernardo, ndugu anayeishi Msumbiji. Aliondolewa kuwa mzee wa kutaniko. Bernardo alihisije mwanzoni? Anasema hivi: “Niliweka kinyongo kwa sababu sikupenda nidhamu niliyopata.” Alihangaikia jinsi ambavyo wengine wangemwona kutanikoni. Anasema hivi: “Ilinichukua miezi kadhaa kusitawisha maoni yanayofaa kuhusu hali hiyo na kuanza tena kumtumaini Yehova na tengenezo lake.” Ni nini kilichomsaidia Bernardo asitawishe mtazamo unaofaa?

9 Bernardo alirekebisha njia yake ya kufikiri. Anaeleza hivi: “Nilipotumikia nikiwa mzee, nilikuwa nikitumia andiko la Waebrania 12:7 kuwasaidia wengine wawe na maoni yanayofaa kuhusu nidhamu ya Yehova. Sasa nikajiuliza, ‘Ni nani anayehitaji kutumia andiko hili?’ Ni watumishi wote wa Yehova​—kutia ndani mimi.” Kisha Bernardo akachukua hatua za ziada ili kuanza tena kumtumaini Yehova na tengenezo lake. Aliimarisha ratiba yake ya kiroho ya kusoma Biblia na kutafakari kwa undani. Ingawa alikuwa na wasiwasi kuhusu maoni ya akina ndugu na dada kumwelekea, alihubiri pamoja nao katika huduma na kushiriki kwenye mikutano ya kutaniko. Baadaye, Bernardo aliwekwa rasmi tena kuwa mzee. Ikiwa kama Bernardo umepewa nidhamu, usikazie fikira hisia za aibu, kubali shauri, na ufanye marekebisho yanayohitajika. c (Met. 8:33; 22:4) Ukifanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakuthawabisha kwa kuendelea kuwa mshikamanifu kwake na tengenezo lake.

INAPOKUWA VIGUMU KUFUATA MABADILIKO YA KITENGENEZO

10. Ni badiliko gani la kitengenezo ambalo huenda lilijaribu ushikamanifu wa baadhi ya wanaume Waisraeli?

10 Mabadiliko ya kitengenezo yanaweza kujaribu ushikamanifu wetu. Tusipokuwa waangalifu hata tunaweza kuyaruhusu yatutenganishe na Yehova. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo huenda badiliko la kitengenezo chini ya Sheria ya Musa lilivyowaathiri baadhi ya Waisraeli. Kabla ya Sheria ya Musa, vichwa vya familia walitimiza majukumu ya kikuhani. Walijenga madhabahu na wakamtolea Yehova dhabihu kwa niaba ya familia zao. (Mwa. 8:20, 21; 12:7; 26:25; 35:1, 6, 7; Ayu. 1:5) Lakini Sheria ilipoanzishwa, vichwa vya familia walipoteza pendeleo hilo. Yehova aliwachagua makuhani kutoka katika familia ya Haruni ili watoe dhabihu. Baada ya badiliko hilo la kitengenezo kufanywa, ikiwa kichwa cha familia ambaye hakuwa mzao wa Haruni angeanza kutenda kama kuhani, angeweza kuuawa. d (Law. 17:3-6, 8, 9) Je, inawezekana kwamba badiliko hilo ndilo lilifanya Kora, Dathani, Abiramu, na wakuu 250 wapinge mamlaka ya Musa na Haruni? (Hes. 16:1-3) Hatuna uhakika. Vyovyote vile, Kora na wale walioshirikiana naye hawakuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova. Ikiwa mabadiliko ya kitengenezo yanajaribu ushikamanifu wako, unaweza kufanya nini?

Wakohathi walipobadilishiwa mgawo, walitumikia kwa hiari wakiwa waimbaji, walinzi, na watunza maghala (Tazama fungu la 11)

11. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa baadhi ya Walawi Wakohathi?

11 Unga mkono kikamili mabadiliko ya kitengenezo. Walipokuwa wakisafiri nyikani, Wakohathi walikuwa na pendeleo la pekee sana. Kila mara Waisraeli walipohamisha kambi, baadhi ya Wakohathi walibeba sanduku la agano mbele ya watu wote. (Hes. 3:29, 31; 10:33; Yos. 3:2-4) Hilo lilikuwa pendeleo kubwa! Hata hivyo, mambo yalibadilika Waisraeli walipoanza kuishi katika Nchi ya Ahadi. Sanduku la agano halikuhitaji kuhamishwa mara kwa mara. Basi, kufikia wakati ambapo Sulemani alianza kutawala akiwa mfalme, baadhi ya Wakohathi walipewa mgawo wa kuwa waimbaji, wengine kati yao walitumikia wakiwa walinzi, na wengine walikuwa watunza maghala. (1 Nya. 6:31-33; 26:1, 24) Hakuna rekodi yoyote inayoonyesha kwamba Wakohathi walilalamika au kudai kwamba wapewe pendeleo la pekee zaidi kwa sababu ya pendeleo walilokuwa nalo zamani. Tunajifunza somo gani? Unga mkono kwa moyo wote mabadiliko ambayo tengenezo la Yehova linafanya, kutia ndani mabadiliko yoyote yanayoathiri mgawo wako. Pata shangwe katika mgawo wowote ule utakaopewa. Kumbuka kwamba mgawo wako si kipimo cha thamani yako machoni pa Yehova. Yehova anathamini sana utii wako kuliko mgawo wowote ulio nao.​—1 Sam. 15:22.

12. Zaina alihisije alipobadilishiwa mgawo na kutoka Betheli?

12 Fikiria mfano wa Zaina, dada anayeishi Mashariki ya Kati, ambaye alipewa badiliko la mgawo na kupoteza pendeleo alilothamini sana. Alipewa mgawo wa kutumikia shambani baada ya kutumikia Betheli kwa zaidi ya miaka 23. Anasema hivi: “Nilipobadilishiwa mgawo nilishtuka sana. Nilihisi kwamba sifai na nikawa nikijiuliza, ‘Nilikosea wapi?’” Kwa kusikitisha, baadhi ya akina ndugu na dada katika kutaniko walimfanya ahisi maumivu zaidi kwa kumwambia: “Ikiwa wangeona kwamba unafaa, tengenezo halingekuondoa.” Kwa muda fulani, Zaina alishuka moyo sana hivi kwamba alilia kila usiku. Lakini anasema hivi: “Sikujiruhusu kamwe nitilie shaka tengenezo wala upendo wa Yehova.” Zaina alifauluje kutunza akili zake?

13. Zaina alifanya nini ili kushinda hisia zake zisizofaa?

13 Zaina alifaulu kushinda hisia zake zisizofaa. Jinsi gani? Alisoma makala katika machapisho yetu ambazo zilizungumzia changamoto aliyokuwa akipitia. Makala yenye kichwa “Unaweza Kukabiliana na Kivunja-Moyo!” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 2001, lilimsaidia sana. Makala hiyo ilifafanua jinsi ambavyo huenda Marko, mwandikaji wa Biblia, alipambana na hisia kama hizo alipobadilishiwa mgawo. Zaina anakumbuka hivi: “Mfano wa Marko ndiyo dawa iliyonisaidia kushinda hisia za kuvunjika moyo.” Pia, Zaina alidumisha uhusiano wa karibu pamoja na rafiki zake. Hakujitenga; wala hakujiruhusu alemewe na hisia za kujisikitikia. Alifikia mkataa kwamba roho ya Yehova inafanya kazi kupitia tengenezo lake na kwamba wale wanaoongoza walimjali sana. Lakini pia, alitambua kwamba lazima tengenezo la Mungu lichukue hatua zinazostahili ili kutimiza kazi ya Yehova.

14. Ilikuwa vigumu kwa Vlado kukubaliana na mabadiliko gani ya kitengenezo, na ni nini kilichomsaidia?

14 Ilikuwa vigumu kwa Vlado, mzee wa kutaniko mwenye umri wa miaka 73 kutoka Slovenia, wakati kutaniko lao lilipounganishwa na kutaniko lingine, na Jumba la Ufalme alilokuwa akihudhuria mikutano likafungwa. Anasema hivi: “Sikuelewa kwa nini Jumba la Ufalme maridadi kama hilo lingefungwa. Niliumia kwa sababu tulikuwa tumefanya marekebisho hivi karibuni katika Jumba la Ufalme. Mimi ni fundi seremala, na nilikuwa nimetengeneza baadhi ya vitu katika Jumba hilo. Pia, makutaniko hayo yalipounganishwa, tulihitaji kufanya mabadiliko mengi na haikuwa rahisi kwetu wahubiri wenye umri mkubwa.” Ni nini kilichomsaidia Vlado aunge mkono mwongozo huo? Anaeleza hivi: “Kuunga mkono mabadiliko yanayofanywa na tengenezo la Yehova sikuzote huleta baraka. Marekebisho hayo yanatutayarisha kwa ajili ya mabadiliko makubwa zaidi ya wakati ujao.” Je, ni vigumu kwako kukubali mabadiliko yanayotokea makutaniko yanapounganishwa au kwa sababu ya badiliko la mgawo? Uwe na hakika kwamba Yehova anaelewa hisia zako. Unapounga mkono mabadiliko hayo na kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake ambalo analitumia, kwa hakika utabarikiwa.​—Zab. 18:25.

TUNZA AKILI ZAKO KATIKA MAMBO YOTE

15. Tunawezaje kutunza akili zetu tunapokabili changamoto kutoka ndani ya kutaniko?

15 Tunapozidi kukaribia mwisho wa mfumo huu wa mambo, tunaweza kutarajia changamoto kutoka ndani ya kutaniko. Changamoto hizo zinaweza kujaribu ushikamanifu wetu kwa Yehova. Basi, tunapaswa kutunza akili zetu. Ukihisi kwamba Mkristo mwenzako amekutendea kwa njia isiyofaa, usijiruhusu kuweka kinyongo. Ukipewa nidhamu, usikazie fikira hisia za aibu, badala yake kubali shauri, na ufanye marekebisho yanayohitajika. Na tengenezo la Yehova linapofanya mabadiliko ambayo yanakuathiri wewe binafsi, yakubali kwa moyo wote na utii mwongozo huo.

16. Unawezaje kuendelea kumtumaini Yehova na tengenezo lake?

16 Unaweza kuendelea kumtumaini Yehova na tengenezo lake ushikamanifu wako unapojaribiwa. Lakini ili ufanye hivyo, unahitaji kutunza akili zako, yaani, uendelee kuwa mtulivu, ufikirie mambo kwa njia inayofaa, na uone mambo kulingana na maoni ya Yehova. Azimia kujifunza kuhusu watu wanaotajwa katika Biblia ambao walifaulu kukabiliana na hali kama hizo na utafakari kuhusu mifano yao. Sali kwa Yehova ili upate msaada. Na usijitenge kamwe na wengine kutanikoni. Hivyo, hata jambo gani litokee, Shetani hataweza kukutenganisha na Yehova au tengenezo Lake.​—Yak. 4:7.

WIMBO 126 Uwe Macho, Simama Imara, Uwe na Nguvu

a Ushikamanifu wetu kwa Yehova na tengenezo lake unaweza kujaribiwa, hasa tunapokabili changamoto ndani ya kutaniko. Makala hii itazungumzia changamoto tatu kati ya hizo na mambo tunayoweza kufanya ili kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake.

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.

c Unaweza kupata mapendekezo zaidi katika makala “Umewahi Kuwa na Mapendeleo ya Utumishi? Je, Unaweza Kutumikia Tena? ” kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 2009, uku. 30.

d Kulingana na Sheria, kichwa cha familia ambaye alitaka kumchinja mnyama wa kufugwa kwa ajili ya nyama alipaswa kumpeleka mnyama huyo mahali patakatifu. Ruhusa ya pekee ilitolewa kwa ajili ya vichwa vya familia ambao waliishi mbali na mahali patakatifu.​—Kum. 12:21.