Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 47

Usiruhusu Chochote Kikutenganishe na Yehova

Usiruhusu Chochote Kikutenganishe na Yehova

“Ninakutumaini wewe, Ee Yehova.”​—ZAB. 31:14.

WIMBO 122 Iweni Imara, Thabiti!

MUHTASARI a

1. Tunajuaje kwamba Yehova anataka tuwe na uhusiano wa karibu pamoja naye?

 YEHOVA anatukaribisha tusitawishe uhusiano wa karibu pamoja naye. (Yak. 4:8) Anataka kuwa Mungu wetu, Baba yetu, na rafiki yetu. Anajibu sala zetu na kutusaidia tunapokabili hali ngumu. Naye hutumia tengenezo lake kutufundisha na kutulinda. Hata hivyo, ni lazima tufanye nini ili tuwe na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova?

2. Tunawezaje kumkaribia Yehova?

2 Tunaweza kumkaribia Yehova kwa kusali kwake, kusoma Neno lake, na kulitafakari. Tunapofanya hivyo, tunachochewa kumpenda na kumthamini hata zaidi. Tunachochewa kumtii na kumsifu​—mambo ambayo anastahili kabisa kupokea. (Ufu. 4:11) Kadiri tunavyozidi kumjua Yehova, ndivyo tutakavyozidi kumtegemea yeye na tengenezo lake ambalo ametuandalia ili kutulinda.

3. Ibilisi hutumia njia gani kututenganisha na Yehova, lakini ni nini kitakachotusaidia ili tusimwache kamwe Mungu wetu na tengenezo lake? (Zaburi 31:13, 14)

3 Hata hivyo, Ibilisi hujaribu kututenganisha na Yehova, hasa tunapokabili changamoto. Yeye hutumia mbinu gani? Yeye hujaribu kutufanya tuache hatua kwa hatua kumtegemea Yehova na tengenezo lake. Lakini tunaweza kupinga ujanja wake. Ikiwa imani yetu ni yenye nguvu na tunamtumaini kabisa Yehova, hatutamwacha Mungu wetu na tengenezo lake.​—Soma Zaburi 31:13, 14.

4. Tutazungumzia nini katika makala hii?

4 Katika makala hii, tutazungumzia changamoto tatu ambazo huenda zikatoka nje ya kutaniko; kila moja inaweza kufanya tuache kumtumaini Yehova na tengenezo lake. Changamoto hizo zinawezaje kututenganisha na Yehova? Na tunaweza kufanya nini ili kupinga jitihada za Shetani?

TUNAPOKABILI HALI NGUMU

5. Hali ngumu zinawezaje kufanya tuache kumtumaini Yehova na tengenezo lake?

5 Wakati mwingine, tunakabili hali ngumu​—kama vile upinzani kutoka kwa watu wa familia au kupoteza kazi. Matatizo kama hayo yanawezaje kufanya tuache kutumaini tengenezo la Yehova na kututenganisha naye? Tunapokabiliana na hali ngumu kwa muda mrefu, huenda tukashuka moyo na kuhisi kwamba hatuna tumaini. Shetani hutumia fursa kama hizo kujaribu kutufanya tutilie shaka kwamba Yehova anatupenda. Ibilisi anataka tuanze kujiuliza ikiwa Yehova au tengenezo lake ndilo linalotusababishia mateso. Jambo kama hilo liliwapata baadhi ya Waisraeli huko Misri. Mwanzoni walikuwa wameamini kwamba Mungu alimweka rasmi Musa na Haruni wawakomboe kutoka utumwani. (Kut. 4:29-31) Lakini baadaye Farao alipofanya maisha yao yawe magumu zaidi, walimlaumu Musa na Haruni kwa sababu ya matatizo yao, waliwaambia hivi: “Mmefanya Farao na watumishi wake watudharau nanyi mmeweka upanga mkononi mwao ili watuue.” (Kut. 5:19-21) Waliwalaumu watumishi washikamanifu wa Mungu. Hilo linasikitisha sana! Ikiwa umekuwa ukivumilia hali ngumu kwa muda mrefu, unawezaje kuimarisha tumaini lako katika Yehova na tengenezo lake?

6. Tunajifunza nini kutoka kwa nabii Habakuki kuhusu jinsi ya kukabiliana na hali ngumu? (Habakuki 3:17-19)

6 Mmiminie Yehova moyo wako katika sala, na utafute msaada kutoka kwake. Nabii Habakuki alikabili hali nyingi ngumu. Pindi moja, inaonekana alitilia shaka ikiwa Yehova alimjali. Basi, alimmiminia Yehova hisia zake katika sala. Alisema hivi: “Ee Yehova, nililie msaada mpaka lini, lakini wewe hunisikii? . . . Kwa nini unavumilia ukandamizaji?” (Hab. 1:2, 3) Yehova alijibu sala ya kutoka moyoni ya mtumishi wake mshikamanifu. (Hab. 2:2, 3) Baada ya kutafakari matendo ya Yehova ya wokovu, Habakuki alipata tena shangwe nyingi. Alipata usadikisho kwamba Yehova alimjali na angemsaidia avumilie jaribu lolote. (Soma Habakuki 3:17-19.) Tunapata somo gani? Unapokabili hali ngumu, sali kwa Yehova na umwambie jinsi unavyohisi. Kisha utafute msaada kutoka kwake. Ikiwa utafanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakupatia nguvu unazohitaji ili kuvumilia. Na unapoona jinsi anavyokutegemeza, imani yako kwake itakuwa yenye nguvu zaidi.

7. Watu wa ukoo wa Shirley walijaribu kumsadikisha aamini jambo gani, na ni nini kilichomsaidia asipoteze imani yake katika Yehova?

7 Dumisha ratiba yako ya kiroho. Fikiria jinsi kufanya hivyo kulivyomsaidia Shirley, dada anayeishi huko Papua New Guinea alipokabili hali ngumu. b Familia ya Shirley ilikuwa maskini na nyakati nyingine ilikuwa vigumu kwao kupata chakula cha kutosha. Mtu fulani wa ukoo alijaribu kumfanya aache kumtumaini Yehova. Alisema hivi: “Unasema kwamba roho takatifu ya Mungu inakusaidia, lakini msaada huo uko wapi? Bado familia yenu ni maskini. Unapoteza muda wako ukihubiri.” Shirley anakiri hivi: “Nilijiuliza hivi: ‘Je, Mungu anatujali au la?’ Basi papo hapo nikasali kwa Yehova na kumwambia mambo yote niliyokuwa nikiwaza. Sikuacha kusoma Biblia na machapisho yetu, na niliendelea kuhubiri na kuhudhuria mikutano.” Baada ya muda, Shirley alianza kutambua kwamba Yehova alikuwa akiitunza familia yao. Familia yao haikukosa chakula na walikuwa na furaha. Shirley anasema hivi: “Nilihisi kwamba Yehova alikuwa akijibu sala zangu.” (1 Tim. 6:6-8) Ikiwa utashikamana na ratiba yako ya kiroho, wewe pia hutaruhusu hali ngumu au shaka zikutenganishe na Yehova.

NDUGU WANAOONGOZA WANAPOTENDEWA KWA NJIA ISIYOFAA

8. Ni nini ambacho huenda kikawapata ndugu wanaoongoza katika tengenezo la Yehova?

8 Kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, maadui wetu hueneza uwongo au habari zisizo sahihi kuhusu ndugu wanaoongoza katika tengenezo la Yehova. (Zab. 31:13) Baadhi ya akina ndugu wamekamatwa na kushtakiwa kuwa wahalifu. Wakristo wa karne ya kwanza walikabili hali kama hiyo wakati mtume Paulo alipokamatwa na kushtakiwa kimakosa. Walitendaje?

9. Baadhi ya Wakristo walitendaje mtume Paulo alipofungwa gerezani?

9 Baadhi ya Wakristo katika karne ya kwanza waliacha kumtegemeza mtume Paulo alipofungwa gerezani huko Roma. (2 Tim. 1:8, 15) Kwa nini? Je, walimwonea aibu Paulo kwa sababu watu walimwona kuwa mhalifu? (2 Tim. 2:8, 9) Au je, walipatwa na hofu, na kuogopa kwamba wao pia wangeteswa? Hata iwe walikuwa na sababu gani, wazia jinsi Paulo alivyohisi. Alikuwa amevumilia hali nyingi ngumu na hata alikuwa amehatarisha uhai wake kwa ajili yao. (Mdo. 20:18-21; 2 Kor. 1:8) Tusiwe kamwe kama wale waliomwacha mtume Paulo wakati alipohitaji msaada! Tunapaswa kukumbuka jambo gani ndugu wanaoongoza wanapoteswa?

10. Tunapaswa kukumbuka nini ndugu wanaoongoza wanapoteswa, na kwa nini?

10 Kumbuka kwa nini tunateswa na yule anayesababisha mateso hayo. Andiko la 2 Timotheo 3:12 linasema hivi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” Basi, hatupaswi kushangaa kwamba Shetani anawalenga ndugu wanaoongoza katika mashambulizi yake. Lengo lake ni kwamba anataka mashambulizi hayo yavunje utimilifu wa ndugu hao na kututisha sisi.​—1 Pet. 5:8.

Ingawa Paulo alikuwa amefungwa gerezani, kwa ujasiri Onesiforo alimtegemeza. Leo, ndugu na dada zetu huwategemeza waabudu wenzao waliofungwa gerezani, kama inavyoonyeshwa kwenye igizo hili (Tazama fungu la 11 na 12)

11. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Onesiforo? (2 Timotheo 1:16-18)

11 Endelea kuwategemeza ndugu zako na uendelee kushikamana nao. (Soma 2 Timotheo 1:16-18.) Mkristo wa karne ya kwanza aliyeitwa Onesiforo alitenda kwa njia tofauti Paulo alipofungwa gerezani. “Hakuaibika kwa sababu ya minyororo [ya Paulo] ya gereza.” Badala yake, Onesiforo alimtafuta Paulo, na alipompata akatafuta njia za kumsaidia kihususa. Kwa kufanya hivyo, Onesiforo aliuhatarisha uhai wake mwenyewe. Tunapata somo gani? Hatupaswi kuruhusu kuogopa wanadamu kututishe au kutuzuie kuwategemeza ndugu zetu ambao wanateswa. Badala yake, acheni tuwatetee na kufanya yote tunayoweza ili kuwasaidia. (Met. 17:17) Wanahitaji upendo na utegemezo wetu.

12. Tunajifunza nini kutokana na ndugu na dada zetu nchini Urusi?

12 Fikiria jinsi ambavyo ndugu na dada zetu nchini Urusi wamewasaidia waabudu wenzao ambao wamefungwa gerezani. Kesi za wengi wao zinapoendeshwa, ndugu na dada wengi huja mahakamani ili kuwategemeza. Tunapata somo gani? Ndugu wanaoongoza wanaposhtakiwa kwa uwongo, kukamatwa, au kuteswa, hilo halipaswi kukutisha. Sali kwa ajili yao, watunze watu wa familia yao, na utafute njia nyingine hususa za kuwategemeza.​—Mdo. 12:5; 2 Kor. 1:10, 11.

TUNAPODHIHAKIWA

13. Dhihaka zinawezaje kufanya tuache kumtumaini Yehova na tengenezo lake?

13 Watu wa ukoo ambao si Mashahidi, wafanyakazi wenzetu, au wanashule wenzetu huenda wakatudhihaki kwa sababu tunahubiri au tunaishi kulingana na viwango vya juu vya maadili vya Yehova. (1 Pet. 4:4) Huenda wakasema: “Mimi sina tatizo na wewe, lakini dini yako ina sheria kali mno na imepitwa na wakati.” Huenda wengine wakatukosoa kwa sababu ya jinsi tunavyowatendea watu waliotengwa na ushirika, wakisema hivi: “Unawezaje kusema kwamba una upendo?” Maelezo kama hayo yanaweza kupanda mbegu za shaka katika akili zetu. Huenda tukaanza kujiuliza hivi: ‘Je, Yehova anatarajia mengi mno kutoka kwangu? Je, tengenezo lake lina sheria kali sana?’ Ikiwa unakabili hali kama hiyo, unawezaje kuendelea kuwa karibu na Yehova na tengenezo lake?

Ayubu alikataa kuamini uwongo wa wale waliodai kuwa rafiki zake ambao pia walimdhihaki. Badala yake, alikuwa ameazimia kuendelea kudumisha utimilifu wake kwa Yehova (Tazama fungu la 14)

14. Tunapaswa kutendaje wengine wanapotudhihaki kwa sababu ya kuishi kulingana na viwango vya Yehova? (Zaburi 119:50-52)

14 Azimia kuishi kulingana na viwango vya Yehova. Ayubu alikuwa mwanamume ambaye aliishi kulingana na viwango vya Yehova licha ya kudhihakiwa kwa sababu ya kufanya hivyo. Mmoja wa wale waliodai kuwa marafiki wa Ayubu hata alijaribu kumsadikisha Ayubu aamini kwamba Mungu hakujali ikiwa Ayubu alifuata viwango vyake au la. (Ayu. 4:17, 18; 22:3) Lakini Ayubu alikataa kuamini uwongo huo. Alijua kwamba viwango vya Yehova kuhusu mema na mabaya vilikuwa sahihi, na alikuwa ameazimia kuishi kulingana navyo. Hakuruhusu watu wengine wavunje utimilifu wake. (Ayu. 27:5, 6) Tunapata somo gani? Usiruhusu dhihaka zikufanye utilie shaka viwango vya Yehova. Fikiria mambo ambayo umejionea maishani. Je, hujajionea tena na tena kwamba viwango vya Yehova vinafaa na kwamba vinakunufaisha? Azimia kwamba utaunga mkono tengenezo ambalo linafuata viwango hivyo. Ukifanya hivyo, hata watu wakijaribu kukudhihaki jinsi gani, hutaacha kumtumikia Yehova.​—Soma Zaburi 119:50-52.

15. Kwa nini Brizit alidhihakiwa?

15 Fikiria kisa cha Brizit, dada anayeishi nchini India. Watu wa familia yake walimdhihaki kwa sababu ya imani yake. Muda mfupi baada ya kubatizwa mwaka wa 1997, mume wake ambaye si Shahidi alipoteza kazi. Basi mume wake akaamua kwamba yeye, Brizit, na binti zao wanapaswa kwenda kuishi na wazazi wake ambao waliishi katika jiji lingine. Lakini Brizit angekabili changamoto kubwa hata zaidi. Kwa kuwa mume wake hakuwa na kazi, Brizit alilazimika kufanya kazi ya muda wote ili kutegemeza familia yake. Isitoshe, kutaniko lililokuwa karibu lilikuwa umbali wa kilomita 350. Kwa kusikitisha, familia ya mume wake ilimpinga kwa sababu ya imani yake. Upinzani ulikuwa mbaya sana hivi kwamba familia ya Brizit ikalazimika kuhama tena. Kisha ghafla, mume wake akafa. Baadaye, mmoja wa binti zake alikufa kwa sababu ya kansa akiwa na umri wa miaka 12 tu. Jambo baya hata zaidi, watu wa ukoo wa Brizit walimlaumu kwa sababu ya mambo hayo yote. Walidai kwamba ikiwa hangekuwa Shahidi wa Yehova, misiba hiyo yote haingempata. Lakini bado Brizit aliendelea kumtumaini Yehova na kukaa karibu na tengenezo lake.

16. Brizit alibarikiwaje kwa kukaa karibu na Yehova na tengenezo lake?

16 Kwa kuwa Brizit aliishi mbali sana kutoka kwenye kutaniko, mwangalizi wa mzunguko alimtia moyo awahubirie watu katika eneo aliloishi na kuongoza mikutano nyumbani kwake. Mwanzoni alihisi kwamba hilo ni jambo gumu sana. Lakini alifuata mwongozo huo. Aliwahubiria wengine habari njema, akafanya mikutano nyumbani kwake, na kutenga muda kwa ajili ya kufanya ibada ya familia pamoja na binti zake. Matokeo yalikuwaje? Brizit alifaulu kuanzisha na kuongoza mafunzo mengi ya Biblia, na wengi kati ya wanafunzi wake wakabatizwa. Mwaka wa 2005, alianza kutumikia akiwa painia wa kawaida. Alithawabishwa kwa sababu ya kumtumaini Yehova na kuwa mshikamanifu kwa tengenezo lake. Binti zake wanamtumikia Yehova kwa uaminifu, na sasa kuna makutaniko mawili katika eneo hilo! Brizit anasadiki kwamba Yehova alimpa nguvu za kukabiliana na hali ngumu na kuvumilia dhihaka kutoka kwa watu wa familia yake.

ENDELEA KUWA MSHIKAMANIFU KWA YEHOVA NA TENGENEZO LAKE

17. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Shetani anataka tuamini kwamba Yehova hutuacha tunapokabili hali ngumu na kwamba ikiwa tutaunga mkono tengenezo la Yehova mambo yatazidi kuwa magumu kwetu. Shetani anataka tuogope ndugu wanaoongoza wanaposhtakiwa kwa uwongo, kuteswa, au kufungwa gerezani. Na tunapodhihakiwa, anataka tuache kutumaini viwango vya Yehova na tengenezo Lake. Hata hivyo, tunazijua vizuri mbinu zake za uovu na hawezi kutudanganya. (2 Kor. 2:11) Azimia kuendelea kupinga uwongo wa Shetani na uendelee kuwa mshikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake. Kumbuka kwamba Yehova hatakuacha kamwe. (Zab. 28:7) Kwa hiyo, usiruhusu chochote kikutenganishe na Yehova!​—Rom. 8:35-39.

18. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

18 Katika makala hii, tumezungumzia changamoto ambazo huenda tukakabili kutoka nje ya kutaniko. Lakini huenda pia changamoto zinazotoka ndani ya kutaniko zikajaribu azimio letu la kumtumaini Yehova na tengenezo lake. Tunawezaje kufanikiwa kushinda changamoto hizo? Tutazungumzia hilo katika makala inayofuata.

WIMBO 118 “Tusaidie Tuwe na Imani Zaidi”

a Ili tufaulu kuvumilia kwa uaminifu katika siku hizi za mwisho, ni lazima tuendelee kumtegemea Yehova na tengenezo lake. Ibilisi hujaribu kutumia majaribu ili kufanya tusimtumaini Yehova na tengenezo lake. Makala hii itazungumzia changamoto tatu ambazo Ibilisi hutumia na mambo tunayoweza kufanya ili kupinga jitihada zake.

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.