Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Katika siku za Yesu, watu walipaswa kulipa kodi za aina gani?

TANGU zamani, Waisraeli walizoea kutoa pesa ili kutegemeza ibada ya kweli. Lakini kufikia wakati wa Yesu, Wayahudi walihitaji kulipa kodi nyingi, zilizofanya maisha yawe magumu.

Ili kutegemeza ibada ya Mungu kwenye hema la ibada na baadaye kwenye hekalu, Wayahudi wote waliokuwa watu wazima walihitaji kulipa nusu shekeli (drakma mbili). Katika karne ya kwanza, michango hiyo ilitumika kwa ajili ya dhabihu na utunzaji wa hekalu ambalo Herode alijenga. Baadhi ya Wayahudi walimuuliza Petro msimamo wa Yesu kuhusu suala hilo, na Kristo alionyesha kwamba si vibaya kulipa kodi hiyo. Isitoshe, alimwamuru Petro achukue sarafu moja ili akalipe kodi hiyo.—Mt. 17:24-27.

Wakati huo, watu wa Mungu walikuwa pia wakitoa fungu la kumi, yaani, sehemu ya kumi ya mazao yao au ya kipato chao. (Law. 27:30-32; Hes. 18:26-28) Viongozi wa kidini walisisitiza kwamba fungu la kumi kila mboga, hata “mnanaa na dili na bizari” lilipaswa kulipwa kwa uangalifu sana. Yesu hakusema kwamba ilikuwa vibaya kutoa fungu la kumi, lakini alifunua jinsi ambavyo waandishi na Mafarisayo walivyokuwa wanafiki kwa kutumia sheria hiyo vibaya.—Mt. 23:23.

Wakati huohuo Waroma walikuwa wakitawala na waliwatoza watu kodi nyingi za aina tofauti-tofauti. Mojawapo ilikuwa kodi waliyotozwa wale waliomiliki mashamba, na wangeweza kulipa kodi hiyo kwa pesa au bidhaa. Inakadiriwa kwamba watu walilipa kati ya asilimia 20-25 ya mazao waliyovuna. Pia, kulikuwa na kodi ya kichwa kwa ajili ya kila Myahudi. Mafarisayo walimuuliza Yesu kuhusu kodi hiyo. Naye alionyesha maoni sahihi kuhusu kodi aliposema hivi: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.”—Mt. 22:15-22.

Pia, kulikuwa na ushuru kwa ajili ya bidhaa zilizoingia au kutoka eneo moja hadi lingine. Kodi hiyo ilikusanywa kwenye bandari, madarajani, njia panda, au kwenye miingilio ya miji au masoko.

Kwa ujumla kodi ambayo watu waliokuwa chini ya utawala wa Roma walilipa, ilikuwa kubwa sana na yenye kulemea. Kulingana na mwanahistoria Mroma Tacitus, wakati wa utawala wa Maliki Tiberio wakati Yesu alipokuwa duniani, “Siria na Yudea waliomba wapunguziwe kodi kwa sababu ilikuwa mzigo mkubwa kwao.”

Njia iliyotumika kukusanya kodi hizo ilifanya ziwalemee zaidi. Kazi ya kukusanya kodi ilipewa mtu ambaye angetoa pesa nyingi zaidi ili kupata kazi hiyo. Waliotoa pesa nyingi zaidi wangepata faida kwa kukusanya kodi hizo na waliwaajiri watu wengine waende kukusanya kodi hizo, ambao pia walitaka kujipatia faida. Inawezekana Zakayo aliwaajiri wakusanya kodi wa aina hiyo. (Luka 19:1, 2) Inaeleweka ni kwa nini watu walichukizwa na jambo hilo na kuwachukia wale waliokuwa wakikusanya kodi.