Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 23

Sikuzote Yehova Yuko Pamoja Nawe, Hauko Peke Yako

Sikuzote Yehova Yuko Pamoja Nawe, Hauko Peke Yako

“Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia.”​—ZAB. 145:18.

WIMBO 28 Kuwa Rafiki wa Yehova

MUHTASARI *

1. Kwa nini nyakati nyingine watumishi wa Yehova huhisi upweke?

NYAKATI nyingine, wengi wetu huhisi upweke. Kwa baadhi yetu, hisia hizo huisha haraka. Kwa wengine, hisia hizo za upweke zinaweza kubaki kwa muda mrefu. Huenda tukahisi upweke hata ikiwa tumezungukwa na watu wengi. Kwa wengine, si rahisi kuzoea kutaniko jipya. Wengine wanatoka katika familia zenye uhusiano wa karibu sana, hivyo huhisi upweke wanapokuwa mbali na watu wa familia yao. Ilhali wengine wanakosa ushirika wa mpendwa wao aliyekufa. Na baadhi ya Wakristo, hasa wale waliojifunza kweli hivi karibuni, wanahisi wako peke yao wanapotengwa au kunyanyaswa na watu wa familia wasio waamini, na marafiki wa zamani.

2. Tutajibu maswali gani?

2 Yehova anajua na anaelewa kila kitu kutuhusu. Ikiwa tunahisi upweke anaelewa hali yetu, na anataka kutusaidia tushinde hisia hizo. Yehova anatusaidiaje? Tunaweza kufanya nini ili tukabiliane na hisia hizo? Na tunaweza kuwasaidiaje wengine kutanikoni wanaohisi upweke? Acheni tuzungumzie majibu ya maswali hayo.

YEHOVA ANATAMBUA HALI YETU

Yehova alimtuma malaika ili kumhakikishia Eliya kwamba hakuwa peke yake (Tazama fungu la 3)

3. Yehova alionyeshaje kwamba alimjali Eliya?

3 Yehova anahangaikia sana hali njema ya waabudu wake wote. Yuko karibu na kila mmoja wetu, naye hutambua tunapolemewa na hisia za kuvunjika moyo. (Zab. 145:18, 19) Fikiria jinsi alivyomkazia uangalifu Eliya, nabii wake. Mwanamume huyo mwaminifu aliishi katika kipindi kigumu katika historia ya Israeli. Waabudu wa Yehova walikuwa wakiteswa vikali, na Eliya ndiye hasa aliyekuwa akilengwa na maadui wenye nguvu waliompinga Mungu. (1 Fal. 19:1, 2) Jambo lingine ambalo huenda lilimhangaisha Eliya ni kuhisi kwamba alikuwa nabii pekee aliyekuwa anamtumikia Yehova. (1 Fal. 19:10) Mara moja, Yehova alitambua hisia za Eliya. Yehova alimtuma malaika ili kumhakikishia nabii wake kwamba hakuwa peke yake—bado kulikuwa na Waisraeli wengi waliomwogopa Mungu!—1 Fal. 19:5, 18.

4. Andiko la Marko 10:29, 30 linaonyeshaje jinsi Yehova anavyowajali wale waliopoteza utegemezo kutoka kwa watu wa familia na marafiki?

4 Yehova anajua kwamba tulipochagua kumtumikia, huenda baadhi yetu tulihitaji kudhabihu mambo mengi. Mambo hayo yanaweza kutia ndani kukosa kutegemezwa na watu wetu wa ukoo na rafiki zetu wa zamani wasio waamini. Pindi moja huenda sababu ya wasiwasi, mtume Petro alimuuliza hivi Yesu: “Tumeacha kila kitu na kukufuata; basi tutapata nini?” (Mt. 19:27) Kwa wororo, Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba wangepata familia kubwa ya kiroho. (Soma Marko 10:29, 30.) Na Yehova, kichwa cha familia yetu ya kiroho, anaahidi kwamba atawategemeza wale wanaomtumikia. (Zab. 9:10) Fikiria baadhi ya mambo unayoweza kufanya ili kupata msaada wa Yehova unapokabiliana na hisia za upweke.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA UNAPOHISI UKO PEKE YAKO

5. Utapata faida gani kwa kukazia jinsi ambavyo Yehova amekutegemeza?

5 Kazia jinsi Yehova anavyokutegemeza. (Zab. 55:22) Kufanya hivyo, kutakusaidia kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu hali yako. Dada mseja anayeitwa Carol, * ambaye watu wake wa familia hawako katika kweli, anasema hivi: “Ninapokumbuka na kutafakari jinsi ambavyo Yehova amenitegemeza wakati wa majaribu, kunanisaidia nisihisi kwamba niko peke yangu. Ninapata uhakika kwamba Yehova atanitegemeza wakati ujao.”

6. Andiko la 1 Petro 5:9, 10 linaweza kuwatiaje moyo wale wanaokabiliana na hisia za upweke?

6 Fikiria jinsi Yehova anavyowasaidia waamini wenzetu wanaohisi upweke. (Soma 1 Petro 5:9, 10.) Hiroshi, ndugu ambaye kwa miaka mingi amekuwa Shahidi wa Yehova pekee katika familia yake, anasema hivi: “Kutanikoni, ni rahisi kuona kwamba hakuna aliye na hali kamilifu. Kujua kwamba sote tunafanya yote tunayoweza ili kumtumikia Yehova kunaweza kututia moyo sisi tulio peke yetu katika kweli.”

7. Sala inakusaidiaje?

7 Dumisha ratiba nzuri ya kiroho. Hilo linatia ndani kumweleza waziwazi Yehova hisia zetu. (1 Pet. 5:7) Massiel anasema hivi: “Jambo moja muhimu sana lililonisaidia kukabiliana na upweke lilikuwa kusali kwa bidii kwa Yehova.” Massiel ni dada kijana aliyehisi ametengwa na familia yake alipoamua kumtumikia Yehova. Anaeleza hivi: “Yehova alikuwa Baba halisi kwangu, nilisali kwake mara nyingi kwa siku, nikimweleza jinsi nilivyohisi.”

Kusikiliza rekodi za sauti za Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia kunaweza kuwasaidia wale walio peke yao wasihisi upweke sana (Tazama fungu la 8) *

8. Kusoma na kutafakari Neno la Mungu kumekusaidiaje?

8 Soma Neno la Mungu kwa ukawaida, ukitafakari masimulizi hususa ambayo yanaonyesha upendo wa Yehova kwako. Bianca, dada aliyehitaji kuvumilia maneno yenye kuvunja moyo kutoka kwa familia yake, anasema hivi: “Kusoma na kutafakari kuhusu masimulizi ya Biblia na masimulizi ya maisha ya watumishi wa Yehova ambao wamekabiliana na hali kama zangu kumenisaidia.” Baadhi ya Wakristo hukariri maandiko yanayofariji sana kama vile Zaburi 27:10 na Isaya 41:10. Wengine wametambua kwamba kusikiliza machapisho ya kujifunza yaliyorekodiwa kunawasaidia wasihisi upweke wanapojitayarisha kwa ajili ya mikutano au wanapofanya usomaji wao wa Biblia.

9. Kuhudhuria mikutano kunakunufaishaje?

9 Jitahidi kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Utanufaika na programu zenye kutia moyo na pia utawafahamu ndugu na dada zako. (Ebr. 10:24, 25) Massiel, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Ingawa nilikuwa na haya sana, niliazimia kuhudhuria kila mkutano wa kutaniko na kutoa maelezo. Kufanya hivyo, kulinisaidia nihisi nikiwa sehemu ya kutaniko.”

10. Kwa nini ni muhimu kusitawisha urafiki na Wakristo waaminifu?

10 Sitawisha urafiki pamoja na Wakristo waaminifu. Tafuta marafiki kutanikoni ambao unaweza kujifunza kutoka kwao, hata ikiwa umri au malezi yenu yanatofautiana. Biblia inatukumbusha kwamba hekima ‘inapatikana miongoni mwa waliozeeka.’ (Ayu. 12:12) Wenye umri mkubwa wanaweza pia kujifunza kutoka kwa vijana waaminifu. Daudi alikuwa na umri mdogo sana kuliko Yonathani, lakini hilo halikuwazuia kufurahia urafiki wa karibu. (1 Sam. 18:1) Daudi na Yonathani walisaidiana ili wamtumikie Yehova licha ya changamoto kubwa walizokabili. (1 Sam. 23:16-18) Irina, dada ambaye kwa sasa ni Shahidi pekee katika familia yake, anasema hivi: “Kwa kweli ndugu na dada zetu wanaweza kuwa kama wazazi wetu au watoto wenzetu wa kiroho. Yehova anaweza kuwatumia ili kutimiza mahitaji yetu.”

11. Ni lazima ufanye nini ili kusitawisha urafiki imara?

11 Huenda isiwe rahisi kupata marafiki wapya, hasa ikiwa una haya. Ratna, dada mwenye haya aliyejifunza kweli licha ya upinzani, anasema hivi: “Nilitambua kwamba nilihitaji msaada na utegemezo kutoka kwa familia yangu ya kiroho.” Si rahisi kumwambia mtu mwingine hisia zako, lakini mawasiliano ya aina hiyo ndiyo msingi wa urafiki wa karibu. Rafiki zako wanapenda kukutia moyo na kukutegemeza, hata hivyo, wanahitaji kujua jinsi wanavyoweza kukusaidia.

12. Huduma inaweza kukusaidiaje kuwa na marafiki wazuri?

12 Mojawapo ya njia bora za kuanzisha urafiki ni kushirikiana na Wakristo wenzetu katika huduma. Carol, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Nimepata marafiki wengi wazuri kwa kutumia muda pamoja na akina dada katika huduma na utendaji mwingine wa kitheokrasi. Kwa miaka mingi, Yehova amenitegemeza kupitia marafiki hao.” Bila shaka, kusitawisha urafiki na Wakristo waaminifu, kuna matokeo mazuri. Yehova huwatumia marafiki hao ili kukusaidia kukabiliana na hisia zenye kutaabisha kama vile upweke.—Met. 17:17.

WASAIDIE WENGINE WAJIHISI KUWA SEHEMU YA FAMILIA YETU

13. Wote kutanikoni wana wajibu gani?

13 Wote kutanikoni wana wajibu wa kufanya kutaniko liwe sehemu yenye upendo na amani ambapo hakuna anayehisi yuko peke yake. (Yoh. 13:35) Kwa kweli, mambo tunayofanya na kusema yanaweza kuwatia moyo sana wengine! Dada mmoja alisema hivi: “Nilipojifunza kweli, kutaniko likawa familia yangu. Nisingekuwa Shahidi wa Yehova bila utegemezo wao.” Unaweza kufanya nini ili kuwasaidia wale walio peke yao katika kweli wahisi kwamba wao pia ni sehemu ya kutaniko?

14. Unaweza kufanya nini ili kuanzisha urafiki na wapya kutanikoni?

14 Chukua hatua ya kwanza kuanzisha urafiki. Tunaweza kuanza kwa kuwakaribisha kwa uchangamfu wapya kutanikoni. (Rom. 15:7) Hata hivyo, tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kuwasalimia tu. Hatimaye tunataka kuanzisha urafiki imara. Hivyo, uwe mwenye fadhili na uonyeshe kwamba unawajali sana wapya. Jitahidi kuelewa mambo ambayo huenda wakawa wanapitia bila kuwauliza maswali yenye kuaibisha. Huenda isiwe rahisi kwa wengine kueleza hisia zao, hivyo uwe mwangalifu usiwalazimishe kujieleza. Badala yake, waulize maswali kwa busara na kuwasikiliza kwa subira. Kwa mfano, unaweza kuwauliza jinsi walivyopata kweli.

15. Wakristo wakomavu wanaweza kuwasaidiaje wengine kutanikoni?

15 Wote kutanikoni wataimarika kiroho ikiwa Wakristo wakomavu, hasa wazee wa kutaniko, watapendezwa nao. Melissa, aliyelelewa katika kweli na mama yake, anasema hivi: “Siwezi kuelezea kikamili jinsi ninavyowathamini akina ndugu ambao kwa mingi wamekuwa baba zangu wa kiroho. Wakati wowote ninapohitaji mtu wa kuzungumza naye, wanakuwa tayari kunisikiliza.” Mauricio, ndugu kijana ambaye alihisi kwamba ametelekezwa wakati mwalimu wake wa Biblia alipoacha kweli, anasema hivi: “Wazee wa kutaniko walipendezwa nami kibinafsi na hilo lilinisaidia sana. Walizungumza nami kwa ukawaida. Waliandamana nami katika huduma, walinieleza hazina walizopata katika funzo lao la kibinafsi la Biblia, na hata walicheza michezo pamoja nami.” Melissa na Mauricio wamekuwa wakimtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote.

Je, kuna yeyote katika kutaniko lako ambaye atathamini sana ukarimu na ushirika wako? (Tazama fungu la 16 hadi 19) *

16-17. Ni njia gani hususa tunazoweza kutumia kuwasaidia wengine?

16 Wasaidie kwa njia hususa. (Gal. 6:10) Leo, ndugu anayetumikia akiwa mmishonari katika nchi iliyo mbali na familia yake, anasema hivi: “Mara nyingi unachohitaji ni tendo la fadhili linalofanywa kwa wakati unaofaa. Ninakumbuka siku moja nilipopata aksidenti ya gari. Nilipofika nyumbani nilikuwa na mkazo sana. Lakini wenzi fulani wa ndoa walinialika nyumbani kwao kwa ajili ya mlo rahisi. Sikumbuki tulichokula, lakini ninakumbuka kwamba walinisikiliza kwa fadhili. Nilipoondoka, nilihisi nafuu!”

17 Sote tunafurahia matukio ya kitheokrasi kama vile makusanyiko, kwa sababu tunatumia muda pamoja na wengine. Hata hivyo, Carol, aliyetajwa awali, anasema hivi: “Hasa kwenye makusanyiko ninakuwa na wakati mgumu sana.” Kwa nini? Anasema hivi: “Ingawa ninakuwa nimezungukwa na mamia na hata maelfu ya ndugu na dada, mara nyingi wote wanakuwa pamoja na familia zao. Ninapowaona mimi huhisi upweke sana.” Inakuwa vigumu kwa wengine kuhudhuria kusanyiko baada ya kufiwa na mwenzi wao. Je, unamfahamu yeyote anayekabili changamoto kama hizo? Je, unaweza kumwalika ahudhurie pamoja na familia yenu tukio la kitheokrasi linalofuata?

18. Tunaweza kutumiaje 2 Wakorintho 6:11-13 tunapoonyesha ukarimu?

18 Tumieni wakati pamoja. Jitahidi kuwaalika ndugu na dada mbalimbali kwa ajili ya tafrija na burudani, hasa wale ambao huenda wanahisi upweke. Tunataka ‘kufungua mioyo yetu kabisa,’ hasa kwa ajili yao. (Soma 2 Wakorintho 6:11-13.) Melissa aliyenukuliwa awali, anakumbuka hivi: “Sikuzote tulifurahi ndugu na dada walipotualika nyumbani kwao ili tutumie wakati pamoja na familia yao au kusafiri nao.” Je, kuna yeyote kutanikoni ambaye unaweza kumwonyesha ukarimu?

19. Ni pindi gani ambazo huenda zikafaa zaidi kutumia wakati pamoja na Wakristo wenzetu?

19 Kuna pindi ambazo huenda Wakristo wenzetu wakathamini zaidi ushirika wetu. Huenda wengine wanaona kuwa vigumu kushirikiana na ndugu zao wa ukoo wasio waamini wakati wa sikukuu. Huenda wengine wanapata huzuni sana kwenye siku fulani, kama vile tarehe ambayo mpendwa wao alikufa. Tunapokuwa tayari kutumia wakati pamoja na ndugu na dada ambao wanapitia hali hizo ngumu, tunaonyesha kwamba ‘tunawajali kwa unyoofu.’—Flp. 2:20.

20. Maneno ya Yesu kwenye Mathayo 12:48-50 yanaweza kutusaidiaje tunapohisi upweke?

20 Kuna sababu nyingi zinazoweza kumfanya Mkristo ahisi upweke. Hata hivyo, hatupaswi kusahau kamwe kwamba Yehova anaelewa kikamili hisia hizo. Anatupatia kile tunachohitaji, na mara nyingi kupitia Wakristo wenzetu. (Soma Mathayo 12:48-50.) Na sisi tunaonyesha kwamba tunathamini mpango wake wenye upendo tunapofanya yote tunayoweza ili kuitegemeza familia yetu ya kiroho. Hata tuhisije nyakati fulani, kamwe hatuko peke yetu kwa sababu sikuzote Yehova yuko pamoja nasi!

WIMBO 46 Asante, Yehova

^ fu. 5 Je, nyakati nyingine wewe hupambana na hisia za upweke? Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba Yehova anaelewa kikamili hali yako, naye yuko tayari kukupa msaada unaohitaji. Katika makala hii, tutazungumzia mambo unayoweza kufanya ili kukabiliana na hisia za upweke. Pia, tutajifunza jinsi unavyoweza kuwatia moyo waamini wenzako wanaohisi upweke.

^ fu. 5 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Ndugu ambaye mke wake alikufa ananufaika kwa kusikiliza rekodi za sauti za Biblia na machapisho ya kujifunzia.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: Ndugu na binti yake wanamtembelea na kumwonyesha ukarimu ndugu mwenye umri mkubwa kutanikoni.