Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Alimwita “Rafiki Yangu”

Yehova Alimwita “Rafiki Yangu”

“Wewe, Ee Israeli, ni mtumishi wangu, wewe, Ee Yakobo, ambaye nimemchagua, uzao wa Abrahamu rafiki yangu.” —ISA. 41:8.

NYIMBO: 91, 22

1, 2. (a) Tunajuaje kwamba wanadamu wanaweza kuwa rafiki za Mungu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

TANGU tunapozaliwa hadi tunapokufa, uhitaji wetu mkubwa zaidi ni upendo. Wanadamu wanahitaji sana upendo, na si tu upendo wa kimahaba. Tunatamani kuwa na marafiki na kushirikiana na wengine. Lakini kuna aina ya upendo tunaohitaji zaidi kuliko aina nyingine yoyote, yaani upendo wa Yehova. Ni vigumu kwa wengi kuamini kwamba wanadamu wanaweza kuwa na urafiki wa karibu na wenye upendo pamoja na Mungu Mweza Yote, ambaye ni Roho asiyeonekana. Je, sisi pia tuna maoni kama hayo? La, hasha!

2 Biblia inaeleza kuhusu wanadamu wasio wakamilifu ambao walikuwa rafiki za Mungu. Ni muhimu tutafakari mfano wao, kwa kuwa kujenga urafiki na Mungu ndilo jambo bora zaidi tunaloweza kufanya maishani. Abrahamu ni mfano bora wa mtu aliyesitawisha urafiki wa aina hiyo. (Soma Yakobo 2:23.) Ni nini kilichofanya Abrahamu awe rafiki wa karibu wa Yehova? Jambo kuu lilikuwa imani. Kwa kweli, Biblia inamwita Abrahamu “baba ya wale wote walio na imani.” (Rom. 4:11) Acheni tuone jinsi imani ilivyomsaidia Abrahamu awe rafiki wa karibu wa Mungu. Tunapofanya hivyo, kila mmoja wetu anaweza kujiuliza hivi: ‘Ninawezaje kuiga imani ya Abrahamu na kuimarisha urafiki wangu na Yehova?’

ABRAHAMU AWA RAFIKI YA YEHOVA

3, 4. (a) Abrahamu alikabili jaribu gani kubwa la imani? (b) Kwa nini Abrahamu alikuwa tayari kumdhabihu Isaka?

3 Hebu wazia mwanaume mzee, Abrahamu, akipanda mlima. Huenda hiyo ndiyo safari ngumu zaidi maishani mwake. Safari hiyo haikuwa ngumu kwa sababu ya umri, kwa kuwa bado Abrahamu alikuwa na nguvu ingawa alikuwa na umri wa miaka 125 hivi. [1] Nyuma yake alifuatwa na mwana wake, Isaka, ambaye huenda alikuwa na umri wa miaka 25. Kijana huyo alikuwa amebeba kuni. Naye Abrahamu alibeba kisu na vitu vya kuwashia moto. Yehova alikuwa amemwagiza amtoe dhabihu mwana wake!—Mwa. 22:1-8.

4 Inaelekea hilo ndilo jaribu kubwa zaidi la imani ambalo Abrahamu alikabili. Baadhi ya watu wanasema kwamba Mungu alikuwa mkatili kwa kumwagiza Abrahamu amtoe mwanaye, na wengine wanasema kwamba Abrahamu alitii bila kufikiri wala kujali. Wanasema hivyo kwa sababu hawana imani wala hawaelewi jinsi inavyofanya kazi. (1 Kor. 2:14-16) Abrahamu hakumtii Mungu bila kufikiri. Badala yake, alitii kwa sababu aliona. Kwa macho ya imani ya kweli, alimwona Baba yake wa mbinguni, Yehova, ambaye hawaagizi kamwe watumishi Wake waaminifu wafanye jambo lolote litakalowaletea madhara ya kudumu. Abrahamu alijua kwamba ikiwa angemtii Yehova, basi yeye na mwanaye mpendwa wangebarikiwa. Imani hiyo ilitegemea nini? Ilitegemea ujuzi na mambo aliyopitia maishani.

5. Inaelekea Abrahamu alijifunza jinsi gani kumhusu Yehova, na ujuzi huo ulimsaidiaje?

5 Ujuzi. Ingawa alilelewa Uru, jiji la Wakaldayo lililojaa ibada ya sanamu, Abrahamu alimjua Yehova. Hilo liliwezekanaje, wakati baba yake, Tera, alikuwa mwabudu sanamu? (Yos. 24:2) Biblia haisemi kihususa, lakini inafunua kwamba Abrahamu alikuwa wa kizazi cha tisa kutoka kwa Shemu, mtoto wa Noa na mwanaume mwenye imani thabiti. Shemu aliishi hadi Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 150 hivi. Hatuna uhakika ikiwa Abrahamu alijifunza kumhusu Yehova kutoka kwa Shemu. Hata hivyo, inaelekea Shemu aliwafundisha watu wake wa familia kile alichojua kumhusu Yehova. Kwa njia fulani, ujuzi huo ulimfikia Abrahamu na kugusa moyo wake. Naye alianza kumpenda Mungu, na ujuzi aliopata ulimsaidia ajenge imani.

6, 7. Mambo ambayo Abrahamu alipitia yaliimarishaje imani yake?

6 Mambo aliyopitia maishani. Abrahamu alipitia mambo gani yaliyoimarisha imani yake katika Yehova? Kuna msemo usemao, mawazo huchochea hisia na hisia huchochea matendo. Mambo ambayo Abrahamu alijifunza kumhusu Mungu yalimfanya amwogope na kumheshimu sana “Yehova Mungu Aliye Juu Zaidi, Mtokezaji wa mbingu na dunia.” (Mwa. 14:22) Biblia inaita hisia hizo “kumwogopa Mungu,” nazo ni muhimu sana katika kujenga urafiki wa karibu na Mungu. (Ebr. 5:7; Zab. 25:14) Kumwogopa Mungu kulimchochea Abrahamu atende.

7 Mungu aliwaagiza Abrahamu na Sara, ambao walikuwa wamezeeka, waondoke Uru na kwenda kwenye nchi ya kigeni. Wangeishi kwenye mahema katika maisha yao yote. Kwa kutii, Abrahamu alimpa Yehova nafasi ya kumbariki na kumlinda. Kwa mfano, Abrahamu aliogopa kwamba mke wake mrembo, Sara, angechukuliwa na yeye angeuawa. Alikuwa na sababu nzuri za kuogopa, lakini hakuruhusu wasiwasi huo umkengeushe asimtii Yehova. Mara kadhaa Yehova aliingilia kati na kuwalinda Abrahamu na Sara, hata alifanya hivyo kimuujiza. (Mwa. 12:10-20; 20:2-7, 10-12, 17, 18) Mambo hayo yaliimarisha imani ya Abrahamu.

8. Tunawezaje kupata ujuzi na uzoefu utakaoimarisha urafiki wetu na Yehova?

8 Je, tunaweza kuwa rafiki za Yehova? Ndiyo, inawezekana kabisa! Leo, ujuzi na mifano ya watu mbalimbali inapatikana katika Biblia. Abrahamu alikuwa na sehemu ndogo tu ya utajiri mwingi wa hekima inayopatikana sasa katika Biblia. (Dan. 12:4; Rom. 11:33) Neno la Mungu limejaa hazina zinazotupatia ujuzi wa kina kumhusu “Mtokezaji wa mbingu na dunia” na kutusaidia tumheshimu na kumpenda. Hisia hizo zinapotuchochea tumtii Mungu, tunapata uzoefu kwa sababu tunaona matokeo ya kumtii. Tunaelewa kuwa sheria zake hutulinda na tunatambua kwamba anatubariki na kutuimarisha. Tunajifunza kwamba kumtumikia Mungu kwa moyo wote hutufanya tuwe na amani, turidhike, na tuwe na shangwe. (Zab. 34:8; Met. 10:22) Tunapozidi kupata ujuzi na uzoefu, imani yetu katika Yehova na urafiki wetu pamoja naye unakua pia.

ABRAHAMU ALIDUMISHAJE URAFIKI WAKE NA MUNGU?

9, 10. (a) Ni nini kinachohitajika ili kuwa na urafiki imara? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Abrahamu alithamini na aliimarisha urafiki wake na Yehova?

9 Urafiki unaweza kuwa hazina yenye thamani. (Soma Methali 17:17.) Hata hivyo, urafiki si kama kitu kisicho hai ambacho unanunua na kukiweka tu mahali fulani kiendelee kupigwa na vumbi. Urafiki ni kama kiumbe hai kinachohitaji kutunzwa ili kiendelee kuwapo na kusitawi. Abrahamu alithamini na alidumisha urafiki wake na Yehova. Alifanya hivyo jinsi gani?

10 Abrahamu hakuhisi kamwe kwamba historia yake ya kumwogopa na kumtii Mungu ilitosha. Alipokuwa akielekea Kanaani pamoja na familia yake kubwa, aliendelea kumruhusu Yehova amwongoze anapofanya maamuzi yake yote, makubwa kwa madogo. Alipokuwa na umri wa miaka 99, mwaka mmoja kabla ya Isaka kuzaliwa, Yehova alimwagiza awatahiri wanaume wote wa nyumba yake. Je, Abrahamu alitilia shaka amri hiyo au kutafuta njia ya kuikwepa? Hapana. Alimtumaini Mungu na alitekeleza agizo Lake “siku hiyo hiyo.”—Mwa. 17:10-14, 23.

11. Kwa nini Abrahamu alikuwa na wasiwasi kuhusu Sodoma na Gomora, na Yehova alimsaidiaje?

11 Abrahamu alizoea kumtii Yehova hata katika mambo yaliyoonekana kuwa madogo, na hilo lilifanya urafiki wake na Mungu uendelee kusitawi na kuimarika. Alikuwa huru kumweleza Yehova mambo yaliyokuwa moyoni mwake, na alimwomba msaada alipotatanishwa na maswali magumu. Kwa mfano, alipojua kwamba Mungu anakusudia kuharibu majiji ya Sodoma na Gomora, Abrahamu alikuwa na wasiwasi kwamba huenda watu waadilifu wangeangamizwa pamoja na waovu. Labda Abrahamu alikuwa na wasiwasi kuhusu mpwa wake Loti pamoja na familia yake, ambao walikuwa wakiishi Sodoma. Abrahamu aliuliza maswali yake kwa unyenyekevu mkubwa na alimtumaini Mungu, “Mwamuzi wa dunia yote.” Kwa subira, Yehova alimfundisha Abrahamu kwamba Yeye ni Mungu wa rehema, anayesoma mioyo na kutafuta watu waadilifu ili awaokoe, hata wakati wa hukumu.—Mwa. 18:22-33.

12, 13. (a) Ujuzi na mambo ambayo Abrahamu alipitia yalimsaidiaje baadaye? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Abrahamu alikuwa na uhakika na Yehova?

12 Bila shaka, kila jambo ambalo Abrahamu alijifunza na kujionea maishani lilimsaidia kudumisha urafiki wa karibu na Yehova. Baadaye, alipokabili jaribu kubwa sana, Yehova alipomwambia amdhabihu mwana wake Isaka, Abrahamu angeweza kutafakari mambo aliyojua kuhusu utu wa Rafiki yake wa mbinguni. Acheni sasa tumfikirie tena mwanaume mwaminifu anayepanda mlima huko Moria. Je, alifikiri kwamba Yehova angebadilika ghafla na kuwa mkatili na asiye na rehema? Kwa maoni ya Abrahamu, hilo lilikuwa jambo lisilowezekana kabisa! Tunajuaje?

13 Kabla ya kuwaacha watumishi alioandamana nao, Abrahamu alisema hivi: “Ninyi kaeni hapa pamoja na punda, lakini mimi na huyu mvulana tunataka kwenda mbele huko tukaabudu, halafu tutarudi hapa mlipo.” (Mwa. 22:5) Abrahamu alimaanisha nini? Je, alikuwa akiwadanganya watumishi wake, akiwaambia kuwa Isaka atarudi wakati alijua kwamba angetolewa dhabihu? Hapana. Biblia inatusaidia kuelewa kile ambacho Abrahamu alikuwa akifikiria. (Soma Waebrania 11:19.) Abrahamu “alifikia uamuzi kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumfufua [Isaka] hata kutoka kwa wafu.” Naam, Abrahamu aliamini ufufuo. Alijua kwamba Yehova alikuwa amemrudishia nguvu za uzazi yeye na mke wake katika siku za uzeeni. (Ebr. 11:11, 12, 18) Abrahamu alitambua kwamba hakuna jambo lisilowezekana kwa Yehova. Kwa hiyo, haidhuru ni nini kingetokea katika siku hiyo ngumu maishani mwake, alikuwa na uhakika kwamba mwana wake mpendwa angerudishwa kwake ili ahadi za Mungu zitimie. Basi haishangazi kwamba Abrahamu anaitwa “baba ya wale wote walio na imani”!

14. Unakabili changamoto gani katika utumishi wako kwa Yehova, na mfano wa Abrahamu unaweza kukusaidiaje?

14 Namna gani sisi? Ni kweli kwamba Yehova hatuagizi tufanye jambo kama hilo leo. Lakini anataka tumtii hata wakati ambapo ni vigumu kufanya hivyo au hatuelewi kwa nini tunapaswa kutii. Je, kuna agizo lolote kutoka kwa Mungu ambalo unaona ni vigumu kulitii? Kwa wengine, huenda changamoto kubwa ni kuhubiri. Labda wana aibu, hivyo inakuwa vigumu kwao kuwaeleza habari njema watu wasiowajua. Au huenda ikawa vigumu kwa baadhi yetu kuwa tofauti na wengine, labda shuleni au kazini. (Kut. 23:2; 1 The. 2:2) Je, unahisi kama Abrahamu, kana kwamba unapanda mlima huko Moria ili kwenda kufanya kazi ambayo unaona iko nje ya uwezo wako? Ikiwa ndivyo, jipe moyo kutokana na ujasiri na imani ya Abrahamu! Kutafakari mifano ya wanaume na wanawake waaminifu kutatuchochea tuwaige na kutufanya tuwe na urafiki wa karibu zaidi na Yehova.—Ebr. 12:1, 2.

URAFIKI UNAOLETA BARAKA

15. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Abrahamu hakujutia kamwe uamuzi wake wa kumtii Yehova kwa ushikamanifu?

15 Je, unafikiri Abrahamu aliwahi kujutia uamuzi wake wa kumtii Yehova kwa ushikamanifu? Fikiria jinsi ambavyo Biblia inafafanua mwisho wa maisha yake: “Abrahamu akakata pumzi, akafa katika umri mwema wa uzee, akiwa mzee na mwenye kutosheka.” (Mwa. 25:8) Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 175, hakuwa na nguvu tena za kuendelea kuishi, lakini angeweza kutafakari maisha yenye kuridhisha ambayo aliishi. Jambo kuu maishani mwake lilikuwa urafiki wake pamoja na Yehova Mungu. Hata hivyo, Biblia inaposema kwamba Abrahamu alikuwa “mzee na mwenye kutosheka,” haimaanishi kwamba hakuwa na tamaa ya kuishi tena wakati ujao.

16. Abrahamu atafurahia nini katika Paradiso?

16 Biblia inasema kwamba Abrahamu “alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mjenzi na mtengenezaji wa jiji hilo ni Mungu.” (Ebr. 11:10) Abrahamu aliamini kwamba siku moja angeliona jiji hilo, yaani Ufalme wa Mungu, ukitawala dunia—na bila shaka ataliona! Wazia jinsi Abrahamu atakavyosisimuka kuishi katika Paradiso duniani na kupata fursa ya kuendelea kuimarisha urafiki wake na Yehova! Bila shaka ataguswa moyo sana atakapotambua kwamba imani yake iliwasaidia watumishi wa Yehova kwa maelfu ya miaka baada ya kifo chake! Atajifunza kwamba dhabihu aliyoagizwa atoe katika Mlima Moria ilikuwa “mfano” wa jambo kubwa zaidi. (Ebr. 11:19) Isitoshe, atajifunza kwamba maumivu aliyopata alipokuwa akijitayarisha kumtoa Isaka, yamewasaidia mamilioni ya watu waaminifu kuwazia maumivu ambayo Yehova alipata alipomtoa Mwana wake, Yesu Kristo, awe fidia. (Yoh. 3:16) Mfano wa Abrahamu umetusaidia sisi sote tuthamini zaidi fidia, tendo kubwa zaidi la upendo katika historia!

17. Umeazimia kufanya nini, na tutachunguza nini katika makala inayofuata?

17 Acheni kila mmoja wetu aazimie kuiga imani ya Abrahamu. Tunapoendelea kumjua vizuri Yehova, tunajiwekea rekodi ya uaminifu kwake na tunajionea thawabu ya kumtumikia kwa ushikamanifu. (Soma Waebrania 6:10-12.) Yehova na awe rafiki yetu milele! Katika makala inayofuata, tutachunguza mifano mingine mitatu ya watu waaminifu ambao walikuwa marafiki wa karibu wa Mungu.

^ [1] (fungu la 3) Mwanzoni mwanaume huyo aliitwa Abramu na mke wake aliitwa Sarai, lakini katika makala hii tutatumia majina waliyopewa baadaye na Yehova, yaani Abrahamu na Sara.