Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kumtumikia Yehova kwa Shangwe

Endelea Kumtumikia Yehova kwa Shangwe

NI SIKU gani ulikuwa na shangwe zaidi maishani mwako? Je, ni siku uliyofunga ndoa au siku ambayo mtoto wako wa kwanza alizaliwa? Au je, ni siku ulioonyesha wakfu wako kwa Yehova kwa kubatizwa? Inaelekea unaiona siku hiyo kuwa muhimu na yenye shangwe zaidi kuliko zote! Bila shaka, waabudu wenzako walifurahi sana ulipoonyesha hadharani kwamba unampenda Mungu kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zako zote.—Marko 12:30.

Bila shaka umefurahia sana kumtumikia Yehova tangu ulipobatizwa. Hata hivyo, baadhi ya wahubiri wa Ufalme wamepoteza kwa kadiri fulani shangwe waliyokuwa nayo mwanzoni. Kwa nini? Na ni sababu gani zinazotuchochea tuendelee kumtumikia Yehova kwa shangwe?

KWA NINI WENGINE WAMEPOTEZA SHANGWE YAO?

Bila shaka ujumbe wa Ufalme, unaohusisha ahadi ya Yehova ya kukomesha mfumo mwovu wa sasa na kuleta ulimwengu mpya hivi karibuni, hutupatia sababu za kuwa na shangwe. Zaidi ya hilo, andiko la Sefania 1:14 linatuhakikishia hivi: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu. Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” Hata hivyo, kusubiri kwa muda mrefu kuliko tulivyotarajia kunaweza kupunguza shangwe tuliyokuwa nayo mwanzoni, na kufanya tupunguze bidii yetu katika utumishi mtakatifu wa Mungu.—Met. 13:12.

Ushirika wenye kujenga wa watu wa Mungu hutupatia sababu ya kuendelea kumtumikia Yehova kwa shangwe. Huenda mwenendo mzuri wa watumishi wa Yehova ndio uliotuvuta kwenye ibada ya kweli na kutusaidia tuanze kumtumikia Mungu kwa shangwe. (1 Pet. 2:12) Lakini vipi ikiwa Mkristo mwenzetu ametiwa nidhamu kwa sababu ya kushindwa kuishi kulingana na viwango vya Mungu? Katika hali kama hizo, wengine ambao walivutwa kwenye kweli kwa sababu ya mwenendo mzuri wa watu wa Yehova, huenda wakavunjika moyo na kupoteza shangwe yao.

Propaganda za kibiashara za ulimwengu mwovu wa Shetani zinaweza pia kusababisha tupoteze shangwe yetu. Ibilisi hutumia ulimwengu wake kutufanya tuamini kwamba tunahitaji vitu ambavyo kwa kweli si vya lazima. Lakini ni vizuri tukumbuke maneno haya ya Yesu: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” (Mt. 6:24) Hatuwezi kumtumikia Yehova kwa shangwe huku tukijaribu kuutumia kikamili ulimwengu huu.

‘KUWA NA SHANGWE KATIKA MUNGU WA WOKOVU WETU’

Kumtumikia Yehova si mzigo mzito kwa wale wanaompenda. (1 Yoh. 5:3) Kumbuka kwamba Yesu alisema, “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Kuchukua nira ya kuwa mwanafunzi Mkristo ni jambo lenye kuburudisha na huleta shangwe. Bila shaka tuna sababu za kuwa na shangwe kubwa katika utumishi wa Yehova. Acheni sasa tuchunguze sababu tatu muhimu za ‘kuwa na shangwe katika Mungu wa wokovu wetu.’—Hab. 3:18.

Tunamtumikia Mpaji wetu wa Uhai, Mungu mwenye furaha. (Mdo. 17:28; 1 Tim. 1:11) Tunatambua kwamba tupo hai kwa sababu Yeye ndiye aliyetuumba. Hivyo, tunaendelea kumtumikia kwa shangwe haidhuru miaka mingapi imepita tangu tulipobatizwa.

Héctor hudumisha shangwe yake kwa kukazia fikira tumaini la Ufalme na kuhubiri kwa bidii

Mfikirie Héctor, ambaye amemtumikia Yehova akiwa mwangalizi anayesafiri kwa miaka 40. Anaendelea kusitawi hata “wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi.” (Zab. 92:12-14) Ugonjwa wa mke wake umepunguza mambo ambayo Héctor anaweza kutimiza katika utumishi wa Mungu, lakini haujapunguza shangwe yake. Anasema hivi: “Ingawa ninahuzunika kuona afya ya mke wangu ikidhoofika na kufanya iwe vigumu kumtunza, sijaruhusu hilo liondoe shangwe yangu ya kumtumikia Mungu wa kweli. Kujua kwamba chanzo cha uhai wangu ni Yehova, ambaye aliwaumba wanadamu akiwa na kusudi fulani, ni sababu tosha ya kumpenda sana na kumtumikia kwa moyo wote. Ninajitahidi kudumisha bidii yangu ya kuhubiri na kukazia fikira tumaini la Ufalme ili nisipoteze shangwe yangu.”

Yehova ametupatia zawadi ya fidia ili tuwe na maisha yenye furaha. Kwa kweli, “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Naam, dhambi zetu zinaweza kusamehewa na tunaweza kupata uzima wa milele kwa msingi wa imani katika dhabihu ya Yesu ambayo Mungu aliitoa kwa upendo. Je, hiyo si sababu nzuri ya kuwa na shukrani? Na je, shukrani zetu hazipaswi kutuchochea tumtumikie Yehova kwa shangwe?

Jesús alirahisisha maisha yake na kumtumikia Yehova kwa shangwe kwa miaka mingi

Ndugu aitwaye Jesús, kutoka Mexico, alisema hivi: “Nilikuwa mtumwa wa kazi yangu, wakati mwingine nilifanya zamu tano mfululizo ingawa haikuwa lazima kufanya hivyo. Nilifanya hivyo ili tu nipate pesa zaidi. Kisha nilijifunza kumhusu Yehova na jinsi alivyomtoa Mwana wake mpendwa kwa ajili ya wanadamu. Hilo lilinifanya nitamani sana kumtumikia. Hivyo, nilijiweka wakfu kwa Yehova, nikaacha kazi yangu niliyoifanya kwa miaka 28 na kuanza utumishi wa wakati wote.” Huo ulikuwa mwanzo wa miaka mingi ya kumtumikia Yehova kwa shangwe.

Tunda tulilo nalo hutokeza shangwe kubwa, si huzuni. Je, unakumbuka maisha yako yalikuwaje kabla hujamjua Yehova? Mtume Paulo aliwakumbusha Wakristo wa Roma kwamba zamani walikuwa “watumwa wa dhambi” lakini walikuja “kuwa watumwa wa uadilifu.” Walikuwa wakitokeza tunda “katika utakatifu,” ambao mwisho wake ni uzima wa milele. (Rom. 6:17-22) Sisi pia tunaishi maisha matakatifu na hivyo tunaepuka huzuni inayotokana na mwenendo mpotovu au wenye jeuri. Bila shaka, hiyo ni sababu kubwa ya kuwa na shangwe!

“Miaka yenye furaha zaidi maishani mwangu ni ile ambayo nimetumia kumtumikia Yehova.”—Jaime

Fikiria kisa cha Jaime, aliyejihusisha katika mchezo wa ndondi. Aliamini mageuzi na hakuamini kwamba kuna Mungu. Jaime alianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo na alivutiwa na upendo alioonyeshwa. Ili aache mwenendo wake wa zamani, Jaime alihitaji kumwomba Yehova amsaidie aamini kwamba kuna Mungu. Jaime anasema hivi: “Hatua kwa hatua, nilitambua kwamba kuna Mungu mwenye rehema ambaye ni Baba mwenye upendo. Kuishi kulingana na viwango vya Yehova vya uadilifu kumenilinda. Ikiwa nisingebadilika, huenda ningeuawa kama baadhi ya rafiki zangu waliokuwa katika mchezo wa ndondi. Miaka yenye furaha zaidi maishani mwangu ni ile ambayo nimetumia kumtumikia Yehova.”

USIFE MOYO!

Unafikiri tunapaswa kuhisije tunaposubiri mwisho wa ulimwengu huu mwovu wa mambo? Kumbuka, ‘tunapanda kwa roho’ na ‘tutavuna uzima wa milele.’ Kwa hiyo, “tusife moyo katika kufanya yaliyo mema, kwa maana katika majira yanayofaa tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.” (Gal. 6:8, 9) Kwa msaada wa Yehova, acheni tuvumilie, tujitahidi sana kusitawisha sifa zinazohitajiwa ili tuokoke “dhiki kuu,” na tuendelee kumtumikia Yehova kwa shangwe, hata tunapokabili majaribu.—Ufu. 7:9, 13, 14; Yak. 1:2-4

Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutathawabishwa kwa sababu ya uvumilivu wetu, kwa maana Mungu anajua vizuri kazi yetu na jinsi tunavyompenda yeye na jina lake. Tukiendelea kumtumikia Yehova kwa shangwe, tutakuwa kama mtunga zaburi, Daudi, aliyesema hivi: “Nimemweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yuko upande wa mkono wangu wa kuume, sitatikiswa. Kwa hiyo moyo wangu unashangilia, nao utukufu wangu una mwelekeo wa kuwa na shangwe. Pia, mwili wangu mwenyewe utakaa katika usalama.”—Zab. 16:8, 9.