Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Amenisaidia Nifanikiwe Katika Utumishi Wake

Yehova Amenisaidia Nifanikiwe Katika Utumishi Wake

Nilimweleza ofisa kwamba tayari nilikuwa nimetumikia kifungo cha gereza kwa sababu ya kukataa kwenda vitani.Nilimuuliza hivi: “Unataka kunifunga tena gerezani?” Tulikuwa na mazungumzo hayo nilipoitwa mara ya pili ili nijiandikishe katika Jeshi la Marekani.

NILIZALIWA mwaka wa 1926 katika kijiji cha Crooksville, Ohio, Marekani. Baba na Mama hawakuwa wanadini, lakini walituambia sisi watoto nane twende kanisani. Nilichagua kwenda katika Kanisa la Methodisti. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, mhudumu wa kanisa alinipa zawadi kwa sababu sikukosa ibada ya Jumapili hata mara moja kwa mwaka mzima.

Margaret Walker (dada wa pili kushoto) alinisaidia kujifunza kweli

Katika kipindi hicho, jirani yetu aliyeitwa Margaret Walker, ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova, alianza kumtembelea mama na kuzungumza naye kuhusu Biblia. Siku moja, niliamua kusikiliza. Lakini Mama alifikiri ningevuruga funzo lake, hivyo akaniambia nitoke nje. Hata hivyo, niliendelea kutafuta nafasi za kusikiliza mazungumzo yao. Baada ya ziara kadhaa, Margaret aliniuliza hivi: “Unajua jina la Mungu?” Nilimjibu, “Kila mtu anajua ni Mungu.” Akaniambia, “Chukua Biblia yako na usome Zaburi 83:18.” Baada ya kusoma, nilitambua kwamba jina la Mungu ni Yehova. Kisha nilikimbia nje na kuwaambia hivi rafiki zangu: “Mkifika nyumbani leo jioni, someni Zaburi 83:18 katika Biblia zenu mwone Mungu anaitwa nani.” Unaweza kusema kwamba nilianza kuhubiri mara moja.

Nilijifunza Biblia na nikabatizwa mwaka wa 1941. Muda mfupi baadaye, nilipewa mgawo wa kuongoza funzo la kitabu la kutaniko. Niliwatia moyo mama, dada yangu na wadogo zangu wahudhurie, na wote walianza kuja kwenye funzo la kitabu nililoongoza. Hata hivyo, Baba hakupenda ujumbe wa Biblia.

NAKABILI UPINZANI NYUMBANI

Nilipewa majukumu mengi kutanikoni, na nilikuwa na maktaba ya vitabu vya kitheokrasi. Siku moja, Baba alinyoosha kidole chake kuelekea vitabu vyangu na kusema, “Unaona vitabu vile? Sitaki kuviona ndani ya nyumba hii, na uondoke navyo.” Niliondoka nyumbani na nilipata chumba katika jiji jirani la Zanesville, Ohio, lakini mara kwa mara niliwatembelea watu wa familia yetu ili kuwatia moyo.

Baba alijaribu kumzuia Mama kuhudhuria mikutano. Wakati mwingine akiwa njiani kwenda mkutanoni, Baba angemfuata na kumrudisha nyumbani. Lakini Mama angeondoka kupitia mlango mwingine na kwenda mkutanoni. Nilimwambia Mama hivi: “Usihofu. Mwishowe atachoka kukufuatilia.” Baada ya muda, Baba alikata tamaa, na Mama aliendelea kuhudhuria mikutano bila tatizo.

Mwaka wa 1943, kutaniko letu lilianza kufanya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na nilianza kutoa hotuba za wanafunzi. Ushauri niliopokea baada ya kutoa hotuba zangu katika shule hiyo ulinisaidia kuboresha uwezo wangu wa kufundisha.

KUTOUNGA MKONO UPANDE WOWOTE WAKATI WA VITA

Wakati huo, mataifa yalikuwa yakipigana Vita vya Pili vya Ulimwengu. Mwaka wa 1944, niliitwa ili nijiandikishe katika utumishi wa kijeshi. Nilifika Fort Hayes jijini Columbus, Ohio, nikapima afya, na kujaza fomu. Pia, niliwaambia maofisa kwamba sitakuwa mwanajeshi. Waliniruhusu niondoke. Siku kadhaa baadaye, ofisa mmoja alisimama mlangoni pangu na kuniambia hivi: “Corwin Robison, nina hati ya kukukamata.”

Majuma mawili baadaye, hakimu alisema hivi: “Ungekuwa uamuzi wangu, ningekuhukumu kifungo cha maisha gerezani. Una jambo lolote la kusema?” Nilijibu hivi: “Mheshimiwa, ninapaswa kuonwa kuwa mhudumu. Huwa ninawatembelea watu nyumbani kwao, na nimewahubiria watu wengi habari njema ya Ufalme.” Hakimu aliliambia hivi baraza la mahakama: “Hamkuja hapa kuamua ikiwa kijana huyu ni mhudumu au la. Mmekuja kuamua ikiwa alijiunga na jeshi au la.” Kwa muda usiozidi nusu saa, baraza la mahakama lilikata shauri kwamba nina hatia. Hakimu alinihukumu kifungo cha miaka mitano katika gereza la kitaifa la Ashland, Kentucky.

YEHOVA ALINILINDA NIKIWA GEREZANI

Nilifungwa kwa majuma mawili kwenye gereza la Columbus, Ohio, na siku ya kwanza nilibaki ndani ya chumba changu cha gereza. Nilisali hivi kwa Yehova: “Siwezi kukaa ndani ya chumba hiki kwa miaka mitano. Sijui nifanye nini.”

Siku iliyofuata, walinzi waliniruhusu nitoke nje. Nilimkaribia mfungwa mmoja mrefu na mwenye nguvu, nasi tukasimama tukitazama nje dirishani. Aliniuliza hivi: “Ewe Mfupi, kwa nini umefungwa?” Nilijibu, “Mimi ni Shahidi wa Yehova.” Akasema, “Kweli? Basi kwa nini upo hapa?” Nikamwambia, “Mashahidi wa Yehova hawaendi vitani na hawaui watu.” Akasema, “Wamekufunga gerezani kwa sababu hutaki kuua watu. Wanawafunga watu wengine gerezani kwa sababu wanaua watu. Mimi siwaelewi.” Nikasema, “Hata mimi sielewi.”

Kisha alisema, “Nilikuwa kwenye gereza lingine kwa miaka 15 na huko nilisoma baadhi ya machapisho yenu.” Aliposema hivyo nilisali, “Yehova, nisaidie ili mtu huyu awe upande wangu.” Wakati huohuo, mfungwa huyo, aliyeitwa Paul, akasema hivi: “Mfungwa yeyote akikusumbua tu, niambie. Nitapambana naye.” Matokeo yake, sikusumbuliwa na mfungwa yeyote kati ya wafungwa 50 waliokuwa katika gereza hilo.

Nilikuwa kati ya Mashahidi waliofungwa gerezani huko Ashland, Kentucky, kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote

Maofisa wa gereza waliponihamishia katika gereza la Ashland, niliwakuta ndugu kadhaa wakomavu ambao walikuwa wakitumikia kifungo hapo. Ushirika wao ulinisaidia mimi na wengine kuendelea kuwa imara kiroho. Walitupatia mgawo wa usomaji wa Biblia kila juma, nasi tulitayarisha maswali na majibu kwa ajili ya mkutano uliopangwa na ndugu hao. Kulikuwa pia na mtumishi wa maeneo ya kuhubiri. Tulikuwa tukilala ndani ya chumba kikubwa chenye vitanda kuzunguka pande zote. Mtumishi wa eneo angeniambia hivi: “Robison, utahubiri kwenye kitanda hiki na hiki. Yeyote atakayelala kwenye vitanda hivyo, yupo kwenye eneo lako. Hakikisha kwamba unamhubiria kabla hajaondoka.” Hivyo ndivyo tulivyohubiri kwa utaratibu.

BAADA YA KUTOKA GEREZANI

Vita vya Pili vya Ulimwengu viliisha mwaka wa 1945, lakini nilibaki gerezani kwa muda fulani. Nilikuwa na wasiwasi kuhusu familia yetu kwa kuwa Baba alikuwa ameniambia, “Nikifanikiwa kukuondoa wewe, hawa wengine hawatanishinda.” Baada ya kuachiliwa, nilishangazwa na maendeleo mazuri niliyokuta katika familia yetu. Licha ya upinzani wa Baba, watu saba kwenye familia yetu walikuwa wakihudhuria mikutano na mdogo wangu mmoja wa kike alikuwa amebatizwa.

Tukielekea katika huduma pamoja na Demetrius Papageorge, ndugu mtiwa mafuta aliyeanza kumtumikia Yehova mwaka wa 1913

Vita vya Korea vilipoanza mwaka wa 1950, niliitwa mara ya pili ili nijiunge na jeshi na nilienda huko Fort Hayes. Baada ya kutahiniwa, ofisa fulani aliniambia hivi: “Wewe ni kati ya watu wanaostahili zaidi katika kikundi chako.” Nilisema hivi: “Ni sawa, lakini sitajiunga na jeshi.” Kisha nilinukuu andiko la 2 Timotheo 2:3 na kusema, “Tayari mimi ni askari-jeshi wa Kristo.” Baada ya kimya kirefu, alisema hivi: “Unaweza kuondoka.”

Muda mfupi baadaye, nilihudhuria mkutano wa wale wanaotaka kutumikia Betheli katika kusanyiko la wilaya lililofanywa jijini Cincinnati, Ohio. Ndugu Milton Henschel alituambia kwamba ikiwa ndugu yeyote angependa kufanya kazi kwa bidii kwa ajili ya Ufalme, tengenezo linaweza kumtumia Betheli. Nilijaza fomu ya Betheli, nilikubaliwa, na niliwasili Betheli ya Brooklyn, mnamo Agosti 1954. Nimekuwa Betheli tangu wakati huo.

Sijawahi kukosa kazi ya kufanya Betheli. Kwa miaka kadhaa, nilishughulikia matangi ya kupasha maji katika jengo la uchapishaji na majengo ya ofisi, nilifanya kazi ya kurekebisha mashine, na kukarabati vitasa. Nilifanya kazi pia katika Majumba ya Kusanyiko huko New York City.

Kutunza matangi ya kupasha maji kwenye jengo la ofisi katika Betheli ya Brooklyn

Nilipenda sana ratiba ya Betheli, ambayo inahusisha kuhudhuria ibada ya asubuhi na Funzo la familia la Mnara wa Mlinzi na vilevile kushiriki katika huduma pamoja na kutaniko. Kwa kweli, mambo hayo yanaweza na yanapaswa kuwapo katika kila familia ya Mashahidi wa Yehova. Wazazi na watoto wanapochunguza andiko la siku pamoja, kufanya Ibada ya Familia, na kushiriki kwa bidii katika mikutano ya kutaniko na katika kazi ya kuhubiri, wote katika familia wanaweza kuwa wenye afya kiroho.

Nimepata marafiki wengi hapa Betheli na kutanikoni. Baadhi yao walikuwa watiwa mafuta na tayari wamepokea thawabu yao mbinguni. Wengine hawakuwa watiwa mafuta. Hata hivyo, watumishi wote wa Yehova si wakamilifu, wakiwemo Wanabetheli. Ninapokosa kuelewana na ndugu yangu, sikuzote ninajitahidi kufanya amani. Huwa ninafikiria andiko la Mathayo 5:23, 24 na jinsi tunavyopaswa kusuluhisha hali ya kutoelewana. Si rahisi kuomba msamaha, lakini mara nyingi matatizo huisha ninapomwomba rafiki msamaha.

MATOKEO MAZURI KATIKA UTUMISHI WANGU

Kwa sababu ya umri, sasa ni vigumu kwangu kuhubiri nyumba kwa nyumba, lakini sijaacha kuhubiri. Nimejifunza Kichina cha Kimandarini na ninafurahia kuwahubiria Wachina katika mahubiri ya barabarani. Wakati mwingine, ninatoa magazeti 30 au 40 hivi kwa watu wanaopendezwa.

Kuwahubiria Wachina jijini Brooklyn, New York

Nimewahi kufanya ziara ya kurudia ya mtu akiwa nchini China! Siku moja, msichana fulani mwenye shauku alitabasamu aliponiona. Alikuwa akisambaza vipeperushi vya matangazo ya kibanda cha matunda. Nilitabasamu na nikampa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika lugha ya Kichina. Aliyachukua na akaniambia kwamba anaitwa Katie. Baadaye, alikuwa akija kuzungumza nami kila aliponiona. Nilimfundisha majina ya matunda na mboga katika Kiingereza, naye alirudia kutaja majina hayo. Nilimfafanulia pia maandiko ya Biblia, na alikubali kitabu Biblia Inafundisha. Hata hivyo, baada ya majuma kadhaa, sikumwona tena.

Miezi kadhaa baadaye, msichana mwingine aliyekuwa akitoa vipeperushi vya matangazo alikubali magazeti. Juma lililofuata alinipa simu yake na kusema, “Zungumza na mtu kutoka China.” Nilisema, “Simjui mtu yeyote nchini China.” Lakini aliendelea kusisitiza, hivyo nilichukua simu na kusema, “Habari, mimi ni Robison.” Sauti kwenye simu ilisema, “Robby, unazungumza na Katie. Nilirudi China.” Nilishangaa, “China?” Katie alijibu, “Ndiyo. Robby, unamjua msichana ambaye amekupa simu? Ni mdogo wangu. Ulinifundisha mambo mengi mazuri. Tafadhali mfundishe kama ulivyokuwa ukinifundisha.” Nilisema hivi: “Katie, nitafanya yote niwezayo. Asante kwa kuniambia mahali ulipo.” Muda mfupi baadaye, nilizungumza na mdogo wa Katie kwa mara ya mwisho. Natumaini kwamba wasichana hao wataendelea kujifunza kumhusu Yehova popote walipo.

Nimemtumikia Yehova katika utumishi mtakatifu kwa miaka 73. Ninashukuru kwamba alinisaidia kutounga mkono upande wowote na kuwa mwaminifu nilipokuwa gerezani. Pia, wadogo zangu waliniambia kwamba walitiwa moyo walipoona nikikabili upinzani kutoka kwa Baba bila kukata tamaa. Hatimaye, Mama na wadogo zangu sita walibatizwa. Hata Baba alilegeza msimamo wake, na alihudhuria mikutano kadhaa kabla hajafa.

Ikiwa ni mapenzi ya Mungu, watu wa familia yetu na marafiki ambao wamekufa watafufuliwa katika ulimwengu mpya. Wazia shangwe tutakayopata tutakapomwabudu Yehova pamoja na wale tunaowapenda kwa umilele wote! *

^ fu. 32 Makala hii ilipokuwa ikitayarishwa, Corwin Robison alikufa akiwa mwaminifu kwa Yehova.