Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Mshikamanifu kwa Yehova

Uwe Mshikamanifu kwa Yehova

“Yehova na awe kati yangu na wewe na kati ya uzao wangu na uzao wako mpaka wakati usio na kipimo.” —1 SAM. 20:42.

NYIMBO: 125, 62

1, 2. Kwa nini urafiki wa Yonathani na Daudi ni mfano bora wa ushikamanifu?

BILA shaka Yonathani alistaajabu sana jinsi kijana Daudi alivyolikabili lile jitu, Goliathi. Sasa Daudi alisimama mbele ya baba ya Yonathani, Mfalme Sauli wa Israeli, “akiwa na kichwa cha yule Mfilisti mkononi mwake.” (1 Sam. 17:57) Inaelekea Yonathani alivutiwa na ujasiri wa Daudi. Ilikuwa wazi kwamba Mungu alikuwa pamoja na Daudi, hivyo “nafsi ya Yonathani ikashikamana na nafsi ya Daudi.” Nao “wakafanya agano, kwa maana [Yonathani] alimpenda [Daudi] kama nafsi yake mwenyewe.” (1 Sam. 18:1-3) Katika maisha yake yote, Yonathani aliendelea kushikamana na Daudi.

2 Yonathani alishikamana na Daudi licha ya kwamba Mungu alimchagua Daudi awe mfalme wa pili wa Israeli. Sauli alipotaka kumuua Daudi, hilo lilimhangaisha sana Yonathani. Hivyo, Yonathani alienda katika jangwa la Yudea huko Horeshi, ili amtie moyo rafiki yake. Naye ‘akautia nguvu mkono wake kuhusiana na Mungu.’ Yonathani alimwambia: “Usiogope; . . .  wewe utakuwa mfalme juu ya Israeli, na mimi nitakuwa wa pili kwako.”—1 Sam. 23:16, 17.

3. Ni jambo gani lililokuwa muhimu zaidi kwa Yonathani kuliko kuwa mshikamanifu kwa Daudi, nasi tunajuaje? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

3 Ushikamanifu ni sifa inayowavutia watu wengi ulimwenguni. Hata hivyo, tungekosa somo muhimu sana ikiwa tungevutiwa na ushikamanifu wa Yonathani kwa Daudi bila kuzingatia ushikamanifu wake kwa Mungu. Kwa nini Yonathani alimwona Daudi kuwa rafiki badala ya mpinzani? Ni wazi kwamba kulikuwa na jambo fulani muhimu zaidi kwa Yonathani kuliko hata kuwa mfalme. Kumbuka kwamba ‘aliutia nguvu mkono wa Daudi kuhusiana na Mungu.’ Hivyo, ushikamanifu wake kwa Mungu ndio uliokuwa jambo muhimu zaidi moyoni mwa Yonathani. Kwa kweli, ushikamanifu wake kwa Yehova ndio uliokuwa msingi wa ushikamanifu wake kwa Daudi. Wanaume hao walishikamana na kiapo walichoapa: “Yehova na awe kati yangu na wewe na kati ya uzao wangu na uzao wako mpaka wakati usio na kipimo.”—1 Sam. 20:42.

4. (a) Ni nini kitakachotupatia shangwe ya kweli na kuridhika? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

4 Tukiwa Wakristo, hatuvutiwi tu na ushikamanifu wa wengine; bali sisi wenyewe ni washikamanifu kwa washiriki wa familia zetu, marafiki, na waabudu wenzetu. (1 The. 2:10, 11) Lakini tunapaswa kuwa washikamanifu kwa nani kwanza? Bila shaka ni kwa Yehova, Yule aliyetupatia uhai! (Ufu. 4:11) Tunapodumisha ushikamanifu wetu kwake, tunapata shangwe ya kweli na tunaridhika. Hata hivyo, ili tuonyeshe ushikamanifu wetu kwa Mungu, ni lazima tushikamane naye hata tunapokabili majaribu makali. Katika makala hii, tutazungumzia jinsi mfano wa Yonathani unavyoweza kutusaidia tushikamane na Yehova tunapokabili changamoto nne zifuatazo: (1) tunapoona kwamba mtu fulani mwenye mamlaka hastahili kupewa heshima, (2) tunapohitaji kuchagua tuwe washikamanifu kwa nani kwanza, (3) tunapoeleweka vibaya au kutendewa isivyo haki, na (4) inapokuwa vigumu kutimiza kiapo au ahadi.

TUNAPOONA KWAMBA MTU FULANI MWENYE MAMLAKA HASTAHILI KUPEWA HESHIMA

5. Kwa nini haikuwa rahisi kwa Waisraeli kuwa washikamanifu kwa Mungu Sauli alipokuwa mfalme?

5 Mungu alimtia mafuta Sauli, baba ya Yonathani, ili awe mfalme. Hata hivyo, baada ya muda Sauli aliacha kuwa mtiifu na Yehova alimkataa. (1 Sam. 15:17-23) Kwa kuwa Mungu hakumwondoa Sauli papo hapo kutoka kwenye kiti cha ufalme, matendo yake mabaya yalijaribu ushikamanifu wa raia zake na watu wake wa karibu. Haikuwa rahisi kwao kuwa washikamanifu kwa Mungu kwa sababu mfalme, ambaye aliketi juu ya “kiti cha ufalme cha Yehova,” alikuwa akifanya mambo mabaya.—1 Nya. 29:23.

6. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yonathani aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova?

6 Sauli alipoonyesha kwa mara ya kwanza mtazamo wa kutotii, Yonathani mwana wake, aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova. (1 Sam. 13:13, 14) Nabii Samweli alikuwa amesema hivi: “Yehova hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu.” (1 Sam. 12:22) Yonathani alionyesha kwamba aliamini jambo hilo wakati jeshi kubwa la Wafilisti lenye magari ya vita 30,000 lilipotishia kuvamia Israeli. Sauli alikuwa na wanaume 600 tu; isitoshe yeye na Yonathani tu ndio waliokuwa na silaha! Hata hivyo, Yonathani alivamia kikosi cha Wafilisti kilichokuwa na askari wachache akiwa na mchukua silaha wake. Yonathani alisema hivi: “Hakuna kizuizi chochote kwa Yehova kuokoa kwamba ni kwa wengi au ni kwa wachache.” Waisraeli hao wawili waliua wanaume 20 hivi katika kikosi hicho. Kisha “dunia ikaanza kutetemeka, nalo likawa ni tetemeko kutoka kwa Mungu.” Wakiwa wamechanganyikiwa, Wafilisti walianza kupigana wenyewe kwa wenyewe. Hivyo, Waisraeli walipata ushindi kwa sababu Yonathani alimwamini Mungu.—1 Sam. 13:5, 15, 22; 14:1, 2, 6, 14, 15, 20.

7. Yonathani alimtendeaje baba yake?

7 Hata ingawa uhusiano wa Sauli na Mungu uliharibika, Yonathani aliendelea kushirikiana na baba yake kila ilipowezekana. Kwa mfano, alishirikiana naye kupigana na adui za Israeli ili kuwalinda watu wa Mungu.—1 Sam. 31:1, 2.

8, 9. Kwa nini tunapaswa kuheshimu mamlaka?

8 Kama Yonathani, sisi pia tunaweza kuonyesha ushikamanifu wetu kwa Yehova kwa kujitiisha kwa kadiri chini ya mamlaka zilizo kubwa, kulingana na agizo la Mungu, hata kama tunaona baadhi ya mamlaka hazistahili kupewa heshima. Kwa mfano, huenda ofisa fulani wa serikali si mnyofu, lakini bado tunaheshimu cheo chake kwa sababu tunapofanya hivyo tunaonyesha kwamba tunajitiisha kwa kadiri chini ya “mamlaka zilizo kubwa” za serikali. (Soma Waroma 13:1, 2.) Kwa kweli, sisi sote tunaweza kuonyesha ushikamanifu wetu kwa Yehova kwa kuwaheshimu wale ambao amewapa mamlaka.—1 Kor. 11:3; Ebr. 13:17.

Njia moja ya kuonyesha kwamba sisi ni washikamanifu kwa Yehova ni kumheshimu mwenzi wa ndoa ambaye si Shahidi wa Yehova (Tazama fungu la 9)

9 Olga  [1] dada anayeishi huko Amerika Kusini, alidumisha ushikamanifu wake kwa Mungu kwa kumheshimu mume wake hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. Kwa miaka mingi, mume wake alimkasirikia kwa sababu ya kuwa Shahidi wa Yehova. Alimnyanyasa kihisia, alimtukana, alikataa kuongea naye, na alitishia kuwachukua watoto na kumwacha. Lakini Olga hakulipa uovu kwa uovu. Alifanya yote aliyoweza ili awe mke mzuri kwa kumpikia mume wake, kumfulia nguo, na kuwahudumia washiriki wengine wa familia. (Rom. 12:17) Ilipowezekana, aliandamana na mume wake alipowatembelea watu wake wa familia au marafiki. Kwa mfano, kabla ya kusafiri na mume wake kwenda jiji lingine kwa ajili ya mazishi ya baba mkwe wake, Olga aliwatayarisha watoto na kuandaa kila kitu kilichohitajika kwa ajili ya safari hiyo. Alimsubiri mume wake kwenye mlango wa kanisa hadi ibada ya mazishi ilipomalizika. Baada ya miaka mingi, mtazamo wa mume wake ulianza kubadilika kwa sababu ya subira na heshima ya Olga. Sasa anampeleka Olga kwenye Jumba la Ufalme, anamchochea kuhudhuria mikutano, na nyakati nyingine anahudhuria pamoja naye.—1 Pet. 3:1.

TUNAPOHITAJI KUCHAGUA TUWE WASHIKAMANIFU KWA NANI

10. Kwa nini Yonathani alichagua kuwa mshikamanifu kwa Daudi?

10 Kwa kuwa Sauli aliazimia kumuua Daudi, Yonathani alihitaji kuchagua awe mshikamanifu kwa nani. Ingawa alikuwa amefanya agano na Daudi, Yonathani alijitiisha pia kwa baba yake. Hata hivyo, Yonathani alijua kwamba Mungu alikuwa pamoja na Daudi, na si Sauli. Hivyo, alichagua kuwa mshikamanifu kwa Daudi kwanza badala ya Sauli. Alimwonya Daudi ajifiche na kisha akamweleza Sauli mambo mazuri kumhusu Daudi.—Soma 1 Samweli 19:1-6.

11, 12. Kumpenda Mungu hutusaidiaje tuwe washikamanifu kwake?

11 Kuwa mshikamanifu kwa Mungu kulimsaidia sana Alice, dada kutoka Australia, alipohitaji kuchagua awe mshikamanifu kwa nani. Alipoanza kujifunza Biblia, aliwaeleza washiriki wa familia yake kuhusu mambo mazuri aliyokuwa akijifunza. Baadaye, aliwaambia kwamba hangeungana nao tena kusherehekea Krismasi na aliwaeleza sababu za uamuzi wake. Mwanzoni familia yake ilikuwa na wasiwasi kidogo, lakini baada ya muda wasiwasi huo uligeuka na kuwa ghadhabu kali. Walihisi kwamba Alice aliwapuuza. Alice anasema hivi: “Hatimaye mama yangu alisema kwamba amenikana. Nilishtuka na niliumia sana kwa sababu niliipenda sana familia yangu. Hata hivyo, nilikata shauri kwamba Yehova na Mwana wake ndio watu muhimu zaidi maishani mwangu, na nikabatizwa katika kusanyiko lililofuata.”—Mt. 10:37.

12 Tusipojihadhari, ushikamanifu kwa taifa, shule, au timu za michezo unaweza kuchukua mahali pa ushikamanifu wetu kwa Mungu. Kwa mfano, Henry anapenda kucheza chesi. Shule yao ilikuwa na kawaida ya kushinda ubingwa wa mchezo huo, naye alitaka kufanya yote awezayo ili kuendeleza ushindi huo. Lakini alikiri hivi: “Hatua kwa hatua, nilianza kuwa mshikamanifu zaidi kwa timu ya shule kuliko kuwa mshikamanifu kwa Mungu. Mechi zilizochezwa mwishoni mwa juma zilianza kuchukua mahali pa huduma yangu ya Ufalme. Hivyo, niliamua kujiondoa kwenye timu.”—Mt. 6:33.

13. Kuwa washikamanifu kwa Mungu kunatusaidiaje kushughulikia matatizo ya familia?

13 Nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu kuwa washikamanifu kwa washiriki kadhaa wa familia kwa wakati mmoja. Kwa mfano, Ken anasema hivi: “Nilitaka kumtembelea kwa ukawaida mama yangu aliyekuwa amezeeka, na nyakati fulani kumchukua ili akae nasi. Lakini mama na mke wangu hawakuwa na uhusiano mzuri. Mwanzoni, nilikuwa njia panda kwa kuwa nisingeweza kumfurahisha mmoja bila kumkasirisha mwingine. Kisha nilitambua kwamba katika hali kama hiyo, nilipaswa kwanza kuwa mshikamanifu kwa mke wangu. Hivyo, kwa busara nilisuluhisha jambo hilo kwa njia iliyomfurahisha mke wangu.” Kuwa mshikamanifu kwa Mungu na kuheshimu Neno lake kulimpa Ken ujasiri wa kumweleza mke wake kwa nini alipaswa kumpokea mama yake kwa fadhili, na pia kumweleza mama yake kwa nini alihitaji kumheshimu mke wake.—Soma Mwanzo 2:24; 1 Wakorintho 13:4, 5.

TUNAPOELEWEKA VIBAYA AU KUTENDEWA ISIVYO HAKI

14. Sauli alimtendeaje Yonathani isivyo haki?

14 Huenda ikawa vigumu kuwa washikamanifu kwa Yehova mtu fulani mwenye mamlaka anapotutendea isivyo haki. Inawezekana Yonathani alikabili changamoto kama hiyo. Mfalme Sauli, mtiwa mafuta wa Mungu, alijua kwamba mwanaye alikuwa rafiki ya Daudi, lakini hakujua sababu za urafiki huo. Sauli alimkasirikia sana Yonathani na kumwaibisha. Hata hivyo, Yonathani hakulipiza kisasi. Alidumisha ushikamanifu wake kwa Mungu na kwa Daudi, ambaye baadaye angekuwa mfalme wa Israeli.—1 Sam. 20:30-41.

15. Tunapaswa kufanya nini ikiwa ndugu ametutendea isivyo haki?

15 Haielekei kwamba tunaweza kutendewa isivyo haki katika kutaniko la watu wa Yehova leo. Hata hivyo, wale wanaoongoza kati yetu ni wanaume ambao si wakamilifu na wanaweza kuelewa vibaya matendo yetu. (1 Sam. 1:13-17) Hivyo, tukitendewa isivyo haki au kueleweka vibaya, acheni tudumishe ushikamanifu wetu kwa Yehova.

INAPOKUWA VIGUMU KUTIMIZA AHADI

16. Ni katika hali gani tunapaswa kuwa washikamanifu kwa Mungu na kutokuwa na ubinafsi?

16 Sauli alimhimiza Yonathani afuatilie faida zake binafsi. (1 Sam. 20:31) Hata hivyo, ushikamanifu wa Yonathani kwa Mungu ulimchochea amsaidie Daudi badala ya kuhangaikia manufaa ambayo angepata kwa kuwa mfalme. Tunaweza kuchochewa kuiga sifa ya Yonathani ya kutokuwa na ubinafsi tukikumbuka kwamba mtu anayekubalika kwa Yehova ni yule ambaye ‘ameapa juu ya jambo lililo baya kwake, na bado habadiliki.’ (Zab. 15:4) Yonathani ‘hakubadili’ kiapo chake kwa Daudi; wala sisi hatupaswi kubadili kiapo au ahadi zetu. Kwa mfano, ikiwa makubaliano ya kibiashara yamekuwa magumu kuyatimiza kuliko tulivyotarajia, kuiheshimu Biblia na kudumisha ushikamanifu wetu kwa Mungu kunapaswa kutuchochea tutimize ahadi yetu. Vipi ikiwa tunakabili changamoto kubwa katika ndoa yetu kuliko tulivyotazamia? Bila shaka kumpenda Mungu kutatuchochea tuwe washikamanifu kwa mwenzi wa ndoa.—Soma Malaki 2:13-16.

Tunatimiza makubaliano yetu ya kibiashara kwa kuwa tunataka kubaki washikamanifu kwa Mungu na tunaiheshimu Biblia (Tazama fungu la 16)

17. Umejifunza nini katika makala hii?

17 Tunapotafakari mfano wa Yonathani, je, hatuchochewi kuiga ushikamanifu wake kwa Mungu na kuepuka ubinafsi? Kama Yonathani, acheni tushikamane na Yehova kwa kuwa washikamanifu kwa watu wake, hata wale ambao huenda wametuvunja moyo. Tunapodumisha ushikamanifu wetu kwa Yehova Mungu wakati wa majaribu, tunaufurahisha moyo wake, na hilo hutufanya turidhike sana. (Met. 27:11) Tukiendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova, tutashuhudia jinsi anavyowatendea mambo mengi mazuri wale wote wanaompenda. Katika makala inayofuata, tutachunguza mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwa watu washikamanifu na wasio washikamanifu ambao waliishi wakati mmoja na Daudi.

^ [1] (fungu la 9) Baadhi ya majina yamebadilishwa.