Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waige Marafiki wa Karibu wa Yehova

Waige Marafiki wa Karibu wa Yehova

“Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wanaomwogopa.”—ZAB. 25:14.

NYIMBO: 106, 118

1-3. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba tunaweza kuwa rafiki za Mungu? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

BIBLIA inataja kihususa kwamba Abrahamu alikuwa rafiki ya Mungu. (Isa. 41:8; Yak. 2:23; 2 Nya. 20:7) Kwa kweli, yeye ndiye mtu pekee mwaminifu anayetajwa kwa njia hiyo katika Biblia. Je, hilo linamaanisha kwamba Abrahamu ndiye mwanadamu pekee aliyekuwa rafiki ya Yehova? Hapana. Biblia inaonyesha kwamba sisi sote tunaweza kuwa rafiki za Mungu.

2 Neno la Mungu lina masimulizi mengi ya wanaume na wanawake waliomwogopa Yehova, waliomwamini na waliokuwa rafiki zake wa karibu. (Soma Zaburi 25:14.) Mtume Paulo alieleza kuhusu ‘wingu kubwa la mashahidi,’ ambao ni wazi kwamba walikuwa rafiki za Mungu. (Ebr. 12:1) Na miongoni mwao kuna watu wa aina mbalimbali.

3 Acheni tuzungumzie marafiki watatu wa Yehova wanaotajwa katika Maandiko matakatifu. Nao ni: (1) Ruthu, mjane mshikamanifu kutoka Moabu; (2) Hezekia, mfalme mwadilifu wa Yuda; na (3) Maria, mama mnyenyekevu wa Yesu. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi kila mmoja wao alivyositawisha urafiki na Mungu?

ALIONYESHA UPENDO MSHIKAMANIFU

4, 5. Ruthu alihitaji kufanya uamuzi gani mgumu, na kwa nini ilikuwa vigumu kufanya uamuzi huo? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

4 Hebu wazia wajane watatu wakitembea katika nyanda za Moabu huku mavazi yao yakipepea kwa sababu ya upepo. Ni Naomi na binti wakwe zake, Ruthu na Orpa. Unamwona Orpa akiachana nao, kwa kuwa ameamua kurudi nyumbani, Moabu. Naye Naomi ameazimia kwenda katika nchi yake, Israeli. Yuko pamoja na Ruthu, ambaye anahitaji kufanya uamuzi muhimu sana maishani mwake. Anaweza kuamua kurudi Moabu kwa watu wake au kushikamana na mama mkwe wake, Naomi, na kwenda naye Bethlehemu.—Rut. 1:1-8, 14.

5 Ingekuwa rahisi kwa Ruthu kuwafikiria watu wake wa familia waliokuwa Moabu, yaani mama yake na ndugu zake wengine wa ukoo ambao wangeweza kumtunza na kumsaidia. Moabu kulikuwa nyumbani. Alijua vizuri utamaduni wa nchi hiyo, wakazi wake, na lugha waliyozungumza. Naomi hangeweza kumhakikishia Ruthu kwamba angepata mambo hayo huko Bethlehemu. Hata alimshauri Ruthu abaki Moabu. Naomi alijua kwamba hangeweza kuwapatia binti wakwe zake waume wala mahali pa kuishi. Ruthu angefanya nini? Fikiria tofauti kati ya Ruthu na Orpa, ambaye alikuwa “amerudi kwa watu wake na kwa miungu yake.” (Rut. 1:9-15) Je, Ruthu alitaka kurudi kwa miungu ya uwongo ya watu wake? La hasha!

6. (a) Ruthu alifanya uamuzi gani wa hekima? (b) Kwa nini Boazi alimsifu Ruthu kwa kutafuta kimbilio chini ya mabawa ya Yehova?

6 Inaonekana kwamba Ruthu alijifunza kumhusu Yehova Mungu, labda kutoka kwa mume wake au kutoka kwa Naomi. Yehova hakuwa kama miungu ya Moabu. Ruthu alimpenda Yehova na alijua kwamba yeye ndiye anayestahili kuabudiwa. Hata hivyo, haikutosha tu kuwa na ujuzi. Ruthu alihitaji kufanya uamuzi. Je, angemchagua Yehova kuwa Mungu wake? Ruthu alifanya uamuzi wa hekima. Alimwambia hivi Naomi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu.” (Rut. 1:16) Inatia moyo kutafakari jinsi Ruthu alivyompenda Naomi, lakini jambo muhimu hata zaidi ni upendo wake kwa Yehova. Baadaye, Boazi alimsifu Ruthu kwa kuwa alitafuta kimbilio chini ya mabawa ya Yehova. (Soma Ruthu 2:12.) Jambo hilo linatukumbusha jinsi kifaranga anavyotafuta ulinzi chini ya mabawa ya mzazi wake mwenye nguvu. (Zab. 36:7; 91:1-4) Yehova alikuwa kama mzazi huyo kwa Ruthu. Alimthawabisha kwa sababu ya imani yake, na Ruthu hakuwa na sababu yoyote ya kujutia uamuzi wake.

7. Ni nini kinachoweza kuwasaidia wale wanaosita kujiweka wakfu kwa Yehova?

7 Watu wengi wanajifunza kumhusu Yehova lakini wanasita kutafuta kimbilio kwake. Hawachukui hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Ikiwa unasita kujiweka wakfu kwa Yehova, je, umewahi kujiuliza ni kwa nini unaogopa? Kila mtu aliye hai anamtumikia mungu fulani. (Yos. 24:15) Kwa nini usitafute kimbilio kwa Mungu wa pekee wa kweli, ambaye anastahili kutumikiwa? Kujiweka wakfu kwa Yehova ni njia bora ya kuonyesha kwamba unamwamini. Atakusaidia uishi kulingana na wakfu wako na ukabiliane na changamoto zozote zinazoweza kutokea. Hivyo ndivyo Mungu alivyomfanyia Ruthu.

‘ALISHIKAMANA NA YEHOVA’ —LICHA YA MALEZI YAKE

8. Hezekia alilelewa katika mazingira gani?

8 Tofauti na Ruthu, kijana Hezekia alizaliwa katika taifa lililokuwa wakfu kwa Yehova. Lakini si Waisraeli wote walioishi kulingana na wakfu wao. Mmoja wao alikuwa baba ya Hezekia, Mfalme Ahazi. Mwanaume huyo mwovu aliliongoza taifa la Yuda kuabudu sanamu na akalitia unajisi hekalu la Yehova lililokuwa Yerusalemu. Kwa kweli, Hezekia alilelewa katika mazingira hatari sana, kwa kuwa Ahazi aliwateketeza baadhi ya watoto wake wakiwa hai ili kutoa dhabihu kwa mungu wa uwongo.—2 Fal. 16:2-4, 10-17; 2 Nya. 28:1-3.

9, 10. (a) Kwa nini ingekuwa rahisi kwa Hezekia kuwa mwenye ghadhabu? (b) Kwa nini hatupaswi kuwa na ghadhabu dhidi ya Mungu? (c) Kwa nini hatupaswi kufikiri kwamba malezi yetu huamua jinsi maisha yetu yatakavyokuwa?

9 Ingekuwa rahisi kwa Hezekia kuwa mwovu kama baba yake au kuwa mwenye ghadhabu dhidi ya Mungu. Wengine ambao wamevumilia hali ambazo si ngumu sana ukilinganisha na zile za Hezekia, wanahisi kwamba wana sababu ya msingi ya kuwa na “ghadhabu juu ya Yehova” au kulichukia tengenezo lake. (Met. 19:3) Isitoshe, wengine wanafikiri kwamba historia mbaya ya familia yao ndiyo inayowafanya waishi maisha mapotovu, labda wakirudia makosa ya wazazi wao. (Eze. 18:2, 3) Je, maoni hayo ni sahihi?

10 Tunapochunguza maisha ya Hezekia tunaona wazi kwamba jibu la swali hilo ni hapana. Hakuna sababu yoyote ya msingi ya kuwa na ghadhabu dhidi ya Yehova kwa kuwa yeye si chanzo cha mambo mabaya yanayowapata watu katika ulimwengu huu mwovu. (Ayu. 34:10) Ni kweli kwamba wazazi wanaweza kuwaathiri watoto wao, iwe ni kwa njia nzuri au mbaya. (Met. 22:6; Kol. 3:21) Lakini jambo hilo halimaanishi kwamba historia ya familia ndiyo inayoamua maisha ya mtu. Badala yake, Yehova ametupatia sote zawadi yenye thamani sana, yaani uhuru wa kuchagua tutafanya nini na tutakuwa watu wa aina gani. (Kum. 30:19) Hezekia alitumiaje zawadi hiyo?

Vijana wengi wanakubali kweli haidhuru wamelelewa katika familia za aina gani (Tazama fungu la 9 na 10)

11. Kwa nini Hezekia alikuwa miongoni mwa wafalme bora wa Yuda?

11 Hezekia alikuwa mwana wa mfalme mbaya sana wa Yuda, lakini yeye alikuwa miongoni mwa wafalme bora sana. (Soma 2 Wafalme 18:5, 6.) Ingawa baba yake alimwekea mfano mbaya sana, kulikuwa na watu wengine ambao angeweza kuchagua kuwaiga. Kwa mfano, Isaya alikuwa nabii wakati huo, kama vile Mika na Hosea. Tunaweza kumwazia Mfalme Hezekia akitafakari kwa kina maagizo yaliyoongozwa na roho kutoka kwa wanaume hao waaminifu, na kukubali kwa moyo mkunjufu ushauri na rekebisho kutoka kwa Yehova. Hivyo, Hezekia aliazimia kurekebisha mambo maovu ambayo baba yake alikuwa amefanya. Alifanya hivyo kwa kulisafisha hekalu, kufanya upatanisho kwa ajili ya dhambi za watu, na kuongoza kwa bidii kampeni kubwa ya kuharibu sanamu za kipagani. (2 Nya. 29:1-11, 18-24; 31:1) Hata alipokabili hali ngumu sana, kama vile mfalme Senakeribu wa Ashuru alipotishia kushambulia Yerusalemu, Hezekia alionyesha imani na uhodari mkubwa. Alitegemea wokovu wa Mungu na aliwaimarisha watu kwa maneno na kwa kuwawekea mfano. (2 Nya. 32:7, 8) Baadaye, Hezekia aliporekebishwa kwa sababu ya kuwa na majivuno, alijinyenyekeza naye akatubu. (2 Nya. 32:24-26) Ni wazi kwamba Hezekia hakuruhusu malezi yake yaharibu maisha yake au wakati wake ujao. Badala yake, alionyesha kwamba yeye ni rafiki ya Yehova na ni mfano mzuri wa kuigwa.

12. Watu wengi leo wamethibitishaje kwamba wao ni rafiki za Yehova?

12 Kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu wenye watu wakatili na wasio na upendo, haishangazi kwamba watoto wengi hawalelewi na wazazi wenye upendo na wanaojali. (2 Tim. 3:1-5) Wakristo wengi leo wamelelewa katika familia zenye historia mbaya, lakini wamesitawisha urafiki wa karibu na Yehova. Kama Hezekia, wanathibitisha kwamba malezi ya mtu hayapaswi kuamua wakati wake ujao. Mungu ametupatia zawadi bora sana ya uhuru wa kuchagua, na ni heshima kubwa sana kutumia zawadi hiyo kushikamana na Yehova na kumpa heshima na utukufu, kama Hezekia alivyofanya.

ALISEMA HIVI: “TAZAMA! KIJAKAZI WA YEHOVA!”

13, 14. Kwa nini mgawo ambao Maria alipewa ulionekana kuwa mgumu sana, lakini Maria aliitikiaje maneno ya Gabrieli?

13 Karne kadhaa baada ya siku za Hezekia, mwanamke mnyenyekevu kutoka Nazareti alisitawisha urafiki wa pekee na Yehova. Hakuna mwanadamu yeyote ambaye amewahi kupewa mgawo kama wake. Aliambiwa kwamba angechukua mimba, angemzaa na kumlea Mwana mzaliwa pekee wa Mungu! Bila shaka Yehova alimtumaini sana Maria, binti ya Heli, hivi kwamba akampa mgawo huo wa pekee. Lakini Maria alihisije alipofikiria mambo yaliyohusika katika kutimiza mgawo huo?

“Tazama! Kijakazi wa Yehova!” (Tazama fungu la 13 na 14)

14 Ni rahisi kufikiria tu heshima kubwa ambayo Maria alipewa kwa kukabidhiwa jukumu hilo, na kupuuza wasiwasi ambao huenda alikuwa nao kuhusu mgawo huo ulioonekana kuwa wenye kuogopesha. Malaika wa Mungu, Gabrieli, alimwambia kwamba angepata mimba kimuujiza, yaani bila kulala na mwanaume. Gabrieli hakusema kwamba angeenda kuwafafanulia watu wa familia na majirani wa Maria chanzo cha mimba hiyo. Wangekuwa na maoni gani? Bila shaka Maria alikuwa na wasiwasi kuhusu mchumba wake, Yosefu. Angemthibitishiaje Yosefu kwamba bado yeye ni mwaminifu kwake licha ya kwamba alikuwa na mimba? Zaidi ya hayo, lilikuwa jukumu zito sana kumlea, kumtunza, na kumzoeza Mwana mzaliwa pekee wa Aliye Juu! Hatujui wasiwasi wote ambao Maria alikuwa nao malaika Gabrieli alipozungumza naye. Hata hivyo, tunajua kwamba alijibu hivi: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.”—Luka 1:26-38.

15. Kwa nini Maria alikuwa na imani ya pekee sana?

15 Maria alikuwa na imani ya pekee sana. Alikuwa kama kijakazi aliye tayari kutumiwa na bwana wake kwa njia yoyote. Hivyo, Maria alimtumaini Bwana wake, Yehova, ili amtunze na kumwongoza kufanya maamuzi. Alitaka kumtumikia kwa njia yoyote ile. Ni nini kilichofanya awe na imani? Mtu hazaliwi akiwa na imani. Bali imani inatokana na jitihada za mtu na baraka za Mungu. (Gal. 5:22; Efe. 2:8) Je, kuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba Maria alijitahidi kuimarisha imani yake? Ndiyo. Fikiria jinsi alivyosikiliza na mambo aliyosema.

16. Ni nini kinachoonyesha kwamba Maria alikuwa msikilizaji mzuri?

16 Jinsi Maria alivyosikiliza. Biblia inamshauri kila mtu awe “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.” (Yak. 1:19) Je, Maria alikuwa msikilizaji mzuri? Bila shaka. Injili ya Luka inataja visa viwili vinavyoonyesha kwamba Maria alisikiliza kwa makini maneno ambayo yalikuwa na maana kubwa ya kiroho, na baadaye alitafakari kile alichosikia. Yesu alipozaliwa, wachungaji wanyenyekevu walimweleza Maria mambo waliyoambiwa na malaika. Miaka 12 baadaye, akiwa bado mvulana, Yesu alisema jambo lililokuwa na maana kubwa sana kiroho. Katika visa hivyo vyote, Maria alisikiliza, alikumbuka, na alitafakari kwa kina mambo aliyosikia.—Soma Luka 2:16-19, 49, 51.

17. Maneno ya Maria yanafunua nini?

17 Maneno ya Maria. Biblia haina maneno mengi ambayo Maria alisema. Maelezo yake marefu zaidi yanapatikana kwenye Luka 1:46-55. Maneno hayo yanafunua kwamba Maria aliyaelewa vizuri sana Maandiko. Inaonekana maneno yake yanafanana na maneno ambayo Hana, mama ya nabii Samweli, alisema katika sala. (1 Sam. 2:1-10) Inakadiriwa kwamba katika mazungumzo yake, Maria alinukuu Maandiko mara 20 hivi. Ni wazi kwamba alikuwa mwanamke ambaye alizungumza kwa uhuru kuhusu mambo ya kiroho. Maria alitoa mambo yaliyokuwa katika hazina ya moyo wake, hifadhi ya kweli ambazo alikuwa amejifunza kutoka kwa Rafiki yake mkubwa, Yehova Mungu.

18. Tunawezaje kuiga imani ya Maria?

18 Kama Maria, wakati mwingine tunaweza kupokea mgawo kutoka kwa Yehova ambao unaonekana mgumu. Acheni tujinyenyekeze chini ya mkono wa Yehova, tukitumaini kwamba atatusaidia kwa njia bora kabisa. Tunaweza kuiga imani ya Maria kwa kusikiliza kwa makini mambo tunayojifunza kumhusu Yehova na makusudi yake, kutafakari kweli za kiroho, na kuwaeleza wengine kwa shangwe mambo ambayo tumejifunza.—Zab. 77:11, 12; Luka 8:18; Rom. 10:15.

19. Tunapoiga imani ya pekee ya watu wanaotajwa katika Biblia, tunaweza kuwa na uhakika gani?

19 Ni nani anayeweza kusema kwamba Ruthu, Hezekia, na Maria hawakuwa rafiki za Yehova kama alivyokuwa Abrahamu? Wao, pamoja na wote walio katika ‘wingu kubwa la mashahidi’ na vilevile waaminifu wengine katika historia, walifurahia sana kuwa rafiki za Mungu. Acheni tuendelee kuiga imani yao. (Ebr. 6:11, 12) Tunapofanya hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutapata baraka kubwa, yaani kuwa na urafiki wa karibu na Yehova milele!