Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutoka kwa Watumishi Washikamanifu wa Yehova

Jifunze Kutoka kwa Watumishi Washikamanifu wa Yehova

“Kwa mtu mshikamanifu utatenda kwa ushikamanifu.”—ZAB. 18:25.

NYIMBO: 63, 43

1, 2. Daudi alionyeshaje kwamba alikuwa mshikamanifu kwa Mungu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

NI USIKU wa manane, Daudi na Abishai wanatembea taratibu katikati ya askari 3,000 waliolala usingizi. Wakiwa katikati ya kambi, wanaume hao wawili wanamkuta Mfalme Sauli akiwa amelala fofofo. Alikuwa amesafiri hadi kwenye nyika ya Yudea ili amkamate Daudi na kumuua. Abishai anamnong’oneza hivi Daudi: “Acha nimpigilie chini kwa mkuki mara moja tu, nami sitafanya hivyo mara mbili.” Jibu la Daudi linashangaza! “Usimwangamize, kwani ni nani amepata kunyoosha mkono wake juu ya mtiwa-mafuta wa Yehova, naye akabaki bila hatia? . . . Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba ninyooshe mkono wangu juu ya mtiwa-mafuta wa Yehova!”—1 Sam. 26:8-12.

2 Daudi alielewa maana ya kuwa mshikamanifu kwa Mungu. Hakuwa na nia ya kumwangamiza Sauli. Kwa nini? Kwa sababu Sauli alikuwa mfalme mtiwa mafuta wa Mungu katika Israeli. Watumishi washikamanifu wa Yehova huwaheshimu wale waliochaguliwa na Mungu. Naam, Yehova anataka watu wake wote wawe washikamanifu.—Soma Zaburi 18:25.

3. Abishai alionyeshaje kwamba alikuwa mshikamanifu kwa Daudi?

3 Abishai alimheshimu Daudi. Kwa mfano, Daudi alipojaribu kuficha dhambi ya uzinzi aliyofanya na Bath-sheba, alimwagiza kaka ya Abishai, Yoabu, apange mume wa Bath-sheba auawe katika pambano. (2 Sam. 11:2-4, 14, 15; 1 Nya. 2:16) Huenda Abishai alijua kile ambacho Daudi alifanya, lakini aliendelea kumheshimu Daudi kama mfalme mteule wa Mungu. Isitoshe, Abishai hakujaribu kamwe kutumia mamlaka yake akiwa kiongozi wa kijeshi kunyakua ufalme wa Israeli. Badala yake, alimlinda Daudi dhidi ya wasaliti na maadui wengine.—2 Sam. 10:10; 20:6; 21:15-17.

4. (a) Ni kwa njia gani Daudi alikuwa mfano mzuri wa ushikamanifu kwa Mungu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Daudi alionyesha kwamba alikuwa mtumishi mshikamanifu wa Yehova alipokataa kumwangamiza Mfalme Sauli. Alipokuwa kijana, Daudi alilikabili lile jitu la Ufilisti, Goliathi, ambalo lilithubutu ‘kuvitukana vikosi vya Mungu aliye hai’! (1 Sam. 17:23, 26, 48-51) Daudi alipokuwa mfalme, alifanya dhambi nzito ya uzinzi na kuua kimakusudi, lakini alikubali karipio alilopewa na nabii Nathani, naye akatubu. (2 Sam. 12:1-5, 13) Hata alipozeeka, Daudi aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu. Kwa mfano, alitoa mchango mkubwa kwa ajili ya ujenzi wa hekalu la Yehova. (1 Nya. 29:1-5) Ni kweli kwamba Daudi alifanya makosa mengi mazito, lakini alikuwa mshikamanifu kwa Mungu. (Zab. 51:4, 10; 86:2) Tunapochunguza masimulizi mengine ya Daudi na watu walioishi wakati wake, acheni tutafute majibu ya maswali haya: Ni kwa njia gani tunaweza kuwa washikamanifu kwanza kwa Yehova? Tunahitaji sifa gani ili tuwe washikamanifu?

TUNAPASWA KUWA WASHIKAMANIFU KWA NANI KWANZA?

5. Tunajifunza nini kutokana na kosa la Abishai?

5 Abishai alipokuwa kwenye kambi ya Sauli, hakutambua alipaswa kuwa mshikamanifu kwa nani kwanza. Akitaka kuonyesha ushikamanifu wake kwa Daudi, Abishai alikuwa tayari kumuua Mfalme Sauli. Hata hivyo, Daudi alimzuia kwa sababu alitambua kwamba lingekuwa kosa kumuua “mtiwa-mafuta wa Yehova.” (1 Sam. 26:8-11) Kisa hicho kinatufundisha jambo hili muhimu: Tunapohitaji kuamua tuwe washikamanifu kwa nani kwanza, tunapaswa kufikiria ni kanuni gani za Biblia tunazoweza kutumia wakati huo.

6. Ingawa ni kawaida kushikamana na watu wa familia na marafiki, kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu?

6 Ushikamanifu huanzia moyoni, lakini moyo wa mwanadamu ni wenye hila. (Yer. 17:9) Kwa hiyo, inaweza kuwa rahisi kwa mtu ambaye ni mshikamanifu kwa Mungu kushikamana sana na rafiki wa karibu au mshiriki wa familia hata ikiwa anafanya mambo mabaya. Mtu wetu wa karibu anapoacha kweli, ni lazima tukumbuke kwamba sikuzote tunapaswa kuwa washikamanifu kwanza kwa Yehova.—Soma Mathayo 22:37.

7. Dada mmoja alidumishaje ushikamanifu wake kwa Mungu alipokabili hali ngumu?

7 Inaweza kuwa vigumu kubaki washikamanifu kwa Yehova mtu wa familia anapotengwa na ushirika. Kwa mfano, dada aitwaye Anne [1] alipigiwa simu na mama yake ambaye alikuwa ametengwa na ushirika. Mama huyo alitaka kumtembelea Anne kwa sababu alikuwa na huzuni iliyotokana na kutengwa na familia yake. Ombi hilo lilimsababishia Anne mkazo mkubwa sana, naye akaahidi kumjibu kwa barua. Kabla ya kumwandikia, alipitia tena kanuni za Biblia. (1 Kor. 5:11; 2 Yoh. 9-11) Anne alimwandikia mama yake na alimkumbusha kwa fadhili kuwa yeye mwenyewe ndiye aliyejitenga na familia kwa sababu ya kosa lake na mtazamo wake wa kutotubu. Anne aliandika hivi: “Njia pekee ya kuondoa huzuni yako ni kumrudia Yehova.”—Yak. 4:8.

8. Ni sifa gani zitakazotusaidia tuwe washikamanifu kwa Mungu?

8 Ushikamanifu wa watu walioishi wakati mmoja na Daudi unakazia sifa tatu ambazo zinaweza kutusaidia tuwe washikamanifu kwa Mungu. Sifa hizo ni: unyenyekevu, fadhili, na ujasiri. Acheni tuchunguze sifa moja baada ya nyingine.

TUNAHITAJI UNYENYEKEVU ILI TUWE WASHIKAMANIFU KWA MUNGU

9. Kwa nini Abneri alijaribu kumuua Daudi?

9 Daudi alipokuwa akizungumza na Mfalme Sauli huku akiwa na kichwa cha Goliathi mkononi mwake, angalau wanaume wawili walikuwa wakimtazama. Mmoja alikuwa mwana wa Sauli, Yonathani, ambaye alifanya agano la urafiki na Daudi. Mwingine alikuwa mkuu wa jeshi, Abneri. (1 Sam. 17:57–18:3) Baadaye, Abneri aliunga mkono jitihada za Sauli za kumuua Daudi. Daudi aliandika hivi: ‘Waonevu wanaitafuta nafsi yangu.’ (Zab. 54:3; 1 Sam. 26:1-5) Kwa nini Yonathani alimtendea Daudi kwa njia tofauti na Abneri? Kama Yonathani, Abneri alijua kwamba Mungu alimchagua Daudi awe mfalme wa Israeli. Baada ya kifo cha Sauli, Abneri angeweza kuonyesha unyenyekevu na kuwa mshikamanifu kwa Mungu kwa kumuunga mkono Daudi na si mwana na Sauli, Ish-boshethi. Baadaye Abneri alipolala na suria wa Mfalme Sauli, huenda alitaka yeye ndiye awe mfalme.—2 Sam. 2:8-10; 3:6-11.

10. Kwa nini Absalomu hakuwa mshikamanifu kwa Mungu?

10 Kukosa unyenyekevu kulimfanya Absalomu, mwana wa Daudi, ashindwe kuwa mshikamanifu kwa Mungu. Hiyo ndiyo sababu aliagiza “atengenezewe gari, pamoja na farasi na watu 50 wenye kukimbia mbele yake.” (2 Sam. 15:1) Isitoshe, aliiba ushikamanifu wa watu. Kama Abneri, Absalomu alitaka kumuua Daudi, hata ingawa alijua kwamba Yehova alimchagua Daudi awe mfalme wa Israeli.—2 Sam. 15:13, 14; 17:1-4.

11. Masimulizi ya Biblia kumhusu Abneri, Absalomu, na Baruku yanatufundisha nini?

11 Mfano wa Abneri na Absalomu unaonyesha wazi kwamba tamaa kubwa ya kupata kitu fulani inaweza kumfanya mtu asiwe mshikamanifu kwa Mungu. Kwa hakika, hakuna mtumishi mwaminifu wa Yehova ambaye angependa kuiga mfano wao mwovu na wenye ubinafsi. Hata hivyo, tamaa ya utajiri au kazi yenye mshahara mnono katika ulimwengu huu inaweza pia kumsababishia Mkristo madhara ya kiroho. Kwa njia fulani isiyotajwa, Baruku, mwandishi wa nabii Yeremia alikengeuka kwa muda. Baruku alipokea ujumbe huu kutoka kwa Yehova: “Tazama! Kile ambacho nimekijenga ninakibomoa, na kile ambacho nimekipanda ninaking’oa, ndiyo, nchi yote. Na wewe unaendelea kujitafutia makuu. Usiendelee kuyatafuta.” (Yer. 45:4, 5) Baruku alikubali kurekebishwa. Ni jambo la hekima kwetu kuzingatia maneno hayo ya Mungu tunapoendelea kusubiri mwisho wa ulimwengu huu mwovu.

12. Eleza ni kwa nini hatuwezi kuwa washikamanifu kwa Mungu ikiwa tuna ubinafsi.

12 Daniel, ndugu kutoka Mexico, alihitaji kuchagua kati ya kuwa mshikamanifu kwa Mungu na kufuatilia faida zake binafsi. Alitaka kumwoa msichana ambaye hakuwa mwabudu wa Yehova. Daniel anasema hivi: “Niliendelea kuwasiliana naye hata baada ya kuanza utumishi wa painia. Lakini baadaye, nilijinyenyekeza na nikamweleza mzee mwenye uzoefu kwamba nilikuwa nikikabili jaribu la ushikamanifu. Alinisaidia nitambue kwamba ili niwe mshikamanifu kwa Mungu nilihitaji kuacha kuwasiliana na msichana huyo. Baada ya kutoa sala nyingi na machozi, nilifanya hivyo. Kisha shangwe yangu katika huduma iliongezeka.” Baadaye Daniel alimwoa dada Mkristo mwenye sifa nzuri, na sasa anatumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko.

KUWA WASHIKAMANIFU KWA MUNGU HUTUSAIDIA TUWE WENYE FADHILI

Ukijua kwamba mwabudu mwenzako amefanya kosa zito, je, utaonyesha ushikamanifu kwa kumsaidia rafiki yako apate msaada wa kiroho? (Tazama fungu la 14)

13. Daudi alipofanya dhambi, Nathani alidumishaje ushikamanifu wake kwa Mungu na kwa Daudi?

13 Ushikamanifu wetu kwa Yehova unaweza kutusaidia tuwe washikamanifu kwa wanadamu wenzetu. Nabii Nathani alidumisha ushikamanifu wake kwa Daudi bila kuvunja ushikamanifu wake kwa Mungu. Nathani alijua kwamba Daudi alikuwa amefanya uzinzi na kupanga mume wa mwanamke huyo auawe katika pambano. Yehova alipomtuma Nathani kumkaripia Daudi, nabii huyo alitii na alitenda kwa ujasiri, licha ya kwamba alikuwa mshikamanifu kwa Daudi. Nathani alitenda kwa hekima na kumkaripia Daudi kwa fadhili. Ili kumsaidia Daudi aone uzito wa dhambi zake, Nathani alitumia mfano wa mwanaume fulani tajiri ambaye alitenda isivyo haki kwa kumchukua mwana kondoo wa mwanaume mwingine maskini. Daudi alipoonyesha kukasirishwa na kitendo cha mwanaume huyo tajiri, Nathani alimwambia hivi: “Wewe mwenyewe ndiye yule mwanamume!” Daudi alipata somo!—2 Sam. 12:1-7, 13..

14. Unawezaje kuwa mshikamanifu kwa Yehova na kwa rafiki au mtu wako wa familia?

14 Kuwa mwenye fadhili kunaweza kukusaidia unapohitaji kuamua uwe mshikamanifu kwa nani kwanza. Kwa mfano, huenda una uthibitisho kwamba mwabudu mwenzako amefanya dhambi nzito. Labda unataka kubaki mshikamanifu kwake, hasa ikiwa yeye ni rafiki yako wa karibu au mtu wa familia. Lakini kuficha dhambi yake, kungekufanya usiwe mshikamanifu kwa Mungu. Bila shaka, unapaswa kwanza kuwa mshikamanifu kwa Yehova. Kwa hiyo, kama nabii Nathani, uwe thabiti lakini tenda kwa fadhili. Mhimize mtu huyo atafute msaada wa wazee wa kutaniko. Ikiwa hatafanya hivyo haraka, ushikamanifu wako kwa Mungu utakuchochea uwajulishe wazee dhambi hiyo. Unapofanya hivyo, unadumisha ushikamanifu wako kwa Yehova na unamwonyesha fadhili rafiki au mtu wako wa familia, kwa kuwa wazee Wakristo watajaribu kumrekebisha upya mtu huyo kwa upole.—Soma Mambo ya Walawi 5:1; Wagalatia 6:1.

TUNAHITAJI UJASIRI ILI TUWE WASHIKAMANIFU KWA MUNGU

15, 16. Kwa nini Hushai alihitaji ujasiri ili awe mshikamanifu kwa Mungu?

15 Hushai alihitaji ujasiri ili awe mshikamanifu kwa Mungu. Alikuwa rafiki mshikamanifu wa Mfalme Daudi. Hata hivyo, ushikamanifu wake ulijaribiwa Absalomu, mwana wa Daudi, alipoiba mioyo ya wengi ili kunyakua jiji la Yerusalemu na kiti cha ufalme. (2 Sam. 15:13; 16:15) Daudi alipolikimbia jiji, Hushai angefanya nini? Je, angemsaliti Daudi na kuwa mshikamanifu kwa Absalomu, au angemfuata mfalme huyo mzee aliyekuwa akikimbia ili kuokoa uhai wake? Akiwa ameazimia kuwa mshikamanifu kwa mfalme aliyechaguliwa na Mungu, Hushai alimfuata Daudi kwenye Mlima wa Mizeituni.—2 Sam. 15:30, 32.

16 Daudi alimwomba Hushai arudi Yerusalemu na ajifanye kuwa rafiki ya Absalomu ili avunje ushauri wa Ahithofeli. Hushai alihatarisha uhai wake, na alionyesha kwamba alikuwa mshikamanifu kwa Yehova kwa kutenda kulingana na agizo la Daudi. Kama Daudi alivyosali, ushauri wa Hushai ulivunja ule wa Ahithofeli.—2 Sam. 15:31; 17:14.

17. Kwa nini tunahitaji ujasiri ili tuwe washikamanifu?

17 Tunahitaji ujasiri ili tuwe washikamanifu kwa Yehova. Wengi wetu tumesimama imara na kuonyesha kwamba sisi ni washikamanifu kwa Mungu licha ya kushinikizwa na washiriki wa familia, wafanyakazi wenzetu, au wenye mamlaka. Kwa mfano, Taro kutoka Japani, alijitahidi kuwa mshikamanifu na mtiifu kwa wazazi wake tangu utotoni. Hakufanya hivyo ili tu kutimiza wajibu, bali alitaka kuwafurahisha wazazi wake. Kwa hiyo, walipomzuia kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, jambo hilo lilimuumiza na ilikuwa vigumu sana kuwaeleza wazazi wake kwamba ameamua kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Taro anasema hivi: “Walikuwa na hasira kali hivi kwamba kwa miaka mingi nilikatazwa kuwatembelea nyumbani. Nilisali ili nipate ujasiri wa kushikamana na uamuzi wangu. Sasa mtazamo wao umebadilika, nami ninaweza kuwatembelea kwa ukawaida.”—Soma Methali 29:25.

18. Umejifunza nini katika makala hii?

18 Kama Daudi, Yonathani, Nathani, na Hushai, acheni sisi pia tudumishe ushikamanifu wetu kwa Yehova. Tukifanya hivyo tutaridhika sana! Kwa upande mwingine, tusingependa kamwe kukosa ushikamanifu kama Abneri na Absalomu. Kwa hakika, tunataka kushikamana na Yehova, kama Daudi alivyofanya. Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, hatuwezi kuepuka kufanya makosa. Hata hivyo, tunaweza kuonyesha kwamba ushikamanifu wetu kwa Yehova ndilo jambo la kwanza moyoni mwetu.

^ [1] (fungu la 7) Baadhi ya majina yamebadilishwa.