Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Inaweza Kubadili Maisha Yako

Imani Inaweza Kubadili Maisha Yako

Imani Inaweza Kubadili Maisha Yako

“INAWEZEKANA kabisa kuwa na maadili bila Mungu.” Ndivyo alivyosisitiza mwanamke mmoja mwagnosti. Alisema kwamba aliwalea watoto wake kwa maadili bora, nao pia wakawalea watoto wao kwa maadili bora—yote hayo bila imani katika Mungu.

Je, hilo lamaanisha kwamba hakuna haja ya kuwa na imani katika Mungu? Inaonekana ndivyo alivyofikiri mwanamke huyo. Na ni kweli kwamba si lazima iwe kwamba kila mtu ambaye hamwamini Mungu ni mbaya. Mtume Paulo aliwataja “watu wa mataifa” wasiomjua Mungu ambao ‘hufanya kwa asili mambo ya sheria.’ (Waroma 2:14) Watu wote—kutia ndani waagnosti—walizaliwa wakiwa na dhamiri. Wengi hujaribu kufuata dhamiri zao hata kama hawamwamini Mungu aliyewapa hisi hiyo ya asili ya kupambanua mema na mabaya.

Hata hivyo, imani thabiti katika Mungu—ambayo inategemea Biblia—hutuchochea zaidi kutenda mema kuliko mwongozo wa dhamiri usio na mwelekeo. Imani inayotegemea Neno la Mungu, Biblia, huiarifu dhamiri na kuifanya iweze kupambanua kwa urahisi mema na mabaya. (Waebrania 5:14) Isitoshe, imani huimarisha watu ili wadumishe maadili bora wanapokabili mkazo mkubwa. Kwa mfano, katika karne ya 20, nchi nyingi zilitawaliwa na mamlaka za kisiasa zenye ufisadi, ambazo ziliwalazimisha watu walioonekana kuwa wangwana kutenda ukatili wenye kutisha. Lakini, wale ambao wana imani ya kweli katika Mungu walikataa kuridhiana maadili yao, hata kama walihatarisha uhai wao. Na zaidi, imani inayotegemea Biblia inaweza kubadili watu. Inaweza kurekebisha maisha ya watu ambao huonekana kama wamepotea na kuwasaidia watu kuepuka kufanya makosa mazito. Ebu fikiria mifano michache.

Imani Inaweza Kubadili Maisha ya Familia

“Kwa imani yenu mmefanya maajabu.” Ndivyo alivyosema hakimu mmoja wa Uingereza alipotoa uamuzi wake juu ya malezi ya watoto wa John na Tania. Habari kuhusu John na Tania zilipowafikia wenye mamlaka, hawakuwa wamefunga ndoa na maisha yao ya nyumbani yalikuwa mabaya sana. John, ambaye alikuwa anatumia dawa za kulevya na kucheza-kamari, alikuwa ameingilia uhalifu ili kugharimia maovu hayo. Yeye hakuwajali watoto wake wala mama yao. Basi ni “mwujiza” gani uliotokea?

Siku moja, John alimsikia mpwa wake mchanga akitaja Paradiso. Kwa kuvutiwa, aliwauliza maswali wazazi wa mvulana huyo. Wazazi hao ni Mashahidi wa Yehova, nao walimsaidia John ajifunze juu ya paradiso katika Biblia. Hatua kwa hatua, John na Tania wakasitawisha imani inayotegemea Biblia ambayo ilibadili maisha zao. Walihalalisha ndoa yao na kuacha maovu yao. Wenye mamlaka waliokagua nyumba yao walipata mambo ambayo yalionekana kuwa hayangewezekana awali kidogo—familia yenye furaha katika makao safi yanayostahili kulelea watoto. Hakimu huyo alisema kweli alipotaja kwamba “mwujiza” huo umetokezwa na imani mpya ya John na Tania.

Maelfu ya kilometa kutoka Uingereza, mke mmoja mchanga katika nchi moja ya Mashariki ya Karibu alikuwa karibu kufanya jambo lenye kuhuzunisha. Alikuwa akipanga kutaliki mume wake na hivyo kuwa miongoni mwa mamilioni ya watu ambao ndoa zao huishia talaka. Alikuwa na mtoto, lakini mume wake alikuwa na umri mkubwa sana kuliko yeye. Basi, jamaa zake walikuwa wakimhimiza amtaliki, na hata alikuwa tayari ameanza kufanya mipango hiyo. Lakini, alikuwa akijifunza Biblia na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Shahidi huyo alipogundua jambo hilo, alimweleza maoni ya Biblia juu ya ndoa—kwa mfano, kwamba ndoa ni zawadi kutoka kwa Mungu na haipasi kuchukuliwa kijuu-juu tu. (Mathayo 19:4-6, 9) Mwanamke huyo akawaza, ‘Ni ajabu kwamba mwanamke huyu, ambaye hatujuani, anajaribu kuokoa familia yetu ilhali jamaa zangu wanataka kuivunja.’ Imani yake mpya ilimsaidia kuhifadhi ndoa yao.

Jambo lenye kuhuzunisha linaloathiri maisha ya familia lahusu utoaji-mimba. Ripoti moja ya Umoja wa Mataifa ilikadiria kwamba angalau mimba zipatazo milioni 45 hutolewa kimakusudi kila mwaka. Kila mimba inayotolewa ni msiba. Ujuzi wa Biblia ulimsaidia mwanamke mmoja nchini Filipino aepuke kuwa kati ya wale wanaotoa mimba.

Mashahidi wa Yehova walimpata mwanamke huyo, akakubali broshua ya kujifunzia Biblia yenye kichwa Mungu Anataka Tufanye Nini?, * akaanza kujifunza Biblia. Miezi kadhaa baadaye alieleza jambo lililomfanya akubali kujifunza. Alikuwa mja-mzito Mashahidi walipomtembelea kwa mara ya kwanza, lakini yeye na mume wake walikuwa wameamua kutoa mimba hiyo. Lakini ile picha iliyo kwenye ukurasa wa 24 wa broshua hiyo ikamgusa moyo. Maelezo ya Biblia yanayoambatana na picha hiyo yasemayo kwamba uhai ni mtakatifu kwa sababu ‘kwa Mungu iko chemchemi ya uzima’ yalimfanya asiitoe mimba hiyo. (Zaburi 36:9) Sasa ana mtoto mrembo mwenye afya nzuri.

Imani Huwasaidia Wale Wanaodharauliwa

Nchini Ethiopia, watu wawili ambao hawakuwa wamevalia vizuri walihudhuria mkutano wa ibada ya Mashahidi wa Yehova. Baada ya mkutano Shahidi mmoja akajijulisha kwao kwa njia ya kirafiki. Watu hao wakaomba pesa. Shahidi huyo akawapa kitu kizuri kuliko pesa. Aliwatia moyo wakuze imani katika Mungu, ambayo ‘ina thamani kubwa zaidi sana kuliko dhahabu.’ (1 Petro 1:7) Mmoja wao alikubali akaanza kujifunza Biblia. Jambo hilo likabadili maisha yake. Imani yake ilipozidi kukua, akaacha kuvuta sigareti, kunywa pombe kupindukia, kutafuna miraa na kisha akawa na maadili. Akajifunza kujiruzuku badala ya kuomba-omba na sasa anaishi maisha safi yenye manufaa.

Nchini Italia mtu mmoja mwenye umri wa miaka 47 alihukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani na kuzuiliwa katika hospitali ya gereza ya watu wenye matatizo ya akili. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova ambaye amepewa mamlaka ya kuingia katika gereza hilo ili kuwasaidia watu kiroho alijifunza Biblia pamoja na mtu huyo. Mtu huyo akafanya maendeleo haraka. Imani ilibadili maisha yake sana hivi kwamba sasa wafungwa wengine wanamwendea ili wapate mashauri ya jinsi wanavyoweza kutatua matatizo yao. Imani yake inayotegemea Biblia imefanya astahiwe sana, athaminiwe na kutumainiwa na wasimamizi wa magereza.

Katika miaka ya karibuni magazeti yameripoti juu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe katika Afrika. Habari zenye kuhofisha zaidi ni zile za wavulana ambao huzoezwa kuwa wanajeshi. Watoto hao hupewa dawa za kulevya, huteswa, na kulazimishwa kutenda ukatili dhidi ya jamaa zao ili kuhakikisha kwamba wanawajibika tu kwa kikosi chao pekee. Je, imani inayotegemea Biblia ina nguvu ya kutosha kubadili maisha ya vijana hao? Angalau iliwasaidia vijana wawili.

Nchini Liberia, Alex alitumikia akiwa mtoto-misa katika Kanisa Katoliki. Lakini alipofikia umri wa miaka 13, alijiunga na mojawapo ya vikundi vinavyozozana akawa mwanajeshi mwenye sifa mbaya sana. Alitumia uchawi ili awe jasiri vitani. Alex aliona wenzake wengi wakiuawa, lakini yeye aliokoka. Mnamo mwaka wa 1997 alikutana na Mashahidi wa Yehova akatambua kwamba hao hawakumdharau. Badala yake, walimsaidia ajifunze maoni ya Biblia juu ya ujeuri. Alex akaacha jeshi. Imani yake ilipoanza kukua, alitii amri hii ya Biblia: “Acheni ageuke mbali kutoka lililo baya na kufanya lililo jema; acheni atafute sana amani na kuifuatia.”—1 Petro 3:11.

Wakati uo huo, Samson ambaye pia alikuwa mwanajeshi akiwa angali mtoto alipitia mji ambako Alex alikuwa akiishi sasa. Alikuwa mvulana wa kwaya lakini mnamo mwaka wa 1993 akawa mwanajeshi, akaanza kutumia dawa za kulevya, kuwasiliana na roho, na kujiingiza kwenye ukosefu wa adili. Mnamo mwaka wa 1997 aliruhusiwa kutoka jeshini. Samson alikuwa akielekea Monrovia kujiunga na kikosi maalumu wakati rafikiye mmoja alipomshawishi ajifunze Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, basi akasitawisha imani inayotegemea Biblia. Jambo hilo lilimpa ujasiri wa kuacha njia zake za kivita. Sasa Alex na Samson wanaishi maisha matulivu na ya adili. Je, kuna jambo jingine lolote mbali na imani inayotegemea Biblia ambalo lingeweza kubadili maisha za watu hao ambao walikuwa wameteseka sana?

Imani Inayofaa

Hii ni mifano michache tu kati ya mifano mingi sana ambayo tungeweza kutaja inayoonyesha uwezo wa imani ya kweli inayotegemea Biblia. Bila shaka, si kila mtu ambaye hudai tu kumwamini Mungu huishi kwa kupatana na viwango vya juu vya Biblia. Hata watu fulani wasiomwamini Mungu wanaweza kuishi maisha mazuri kuliko wengine wanaodai kuwa Wakristo. Hiyo ni kwa sababu imani inayotegemea Biblia inahusisha mengi zaidi ya kumwamini tu Mungu.

Mtume Paulo alisema imani ni “taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo, wonyesho dhahiri wa mambo halisi ingawa hayaonwi.” (Waebrania 11:1) Kwa hiyo, imani inatia ndani itikadi yenye nguvu—inayotegemea uthibitisho usiokanushika—katika mambo yasiyoonekana. Hasa inahusu kutotilia shaka kamwe kuwapo kwa Mungu, kwamba anapendezwa nasi, na kwamba atabariki wale wanaofanya mapenzi yake. Mtume alisema hivi pia: “Amkaribiaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.

Ni imani ya aina hiyo ndiyo iliyobadili maisha ya John, Tania, na wengine waliotajwa katika makala hii. Iliwafanya wategemee kwa uhakika kabisa Neno la Mungu, Biblia, ili kupata mwongozo wa kufanya maamuzi. Iliwasaidia wajidhabihu kwa muda ili wasifuate mwenendo mbaya unaoonekana kuwa wenye kufaa. Japo kila moja ya mambo hayo yaliyoonwa ni tofauti, yote yalianza kwa njia moja. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova alijifunza Biblia pamoja na watu hawa, nao wakaona ukweli wa maneno haya ya Biblia: “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu.” (Waebrania 4:12) Nguvu za Neno la Mungu zilimsaidia kila mmoja wao kujenga imani yenye nguvu ambayo imebadili maisha yake yawe bora.

Mashahidi wa Yehova ni watendaji katika nchi na visiwa vya bahari zaidi ya 230. Wanakualika ujifunze Biblia. Kwa nini? Kwa sababu wamesadiki kwamba imani inayotegemea Biblia inaweza kufanya maisha yako pia yawe bora.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Imani inayotegemea Biblia hubadili maisha yawe bora

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

Title card of Biblia nieświeska by Szymon Budny, 1572