Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Twahitaji Tengenezo la Yehova

Twahitaji Tengenezo la Yehova

Twahitaji Tengenezo la Yehova

JE, UMEWAHI kumsikia mtu fulani akisema, “Naamini katika Mungu lakini si katika dini iliyopangwa kitengenezo”? Mara nyingi maoni kama hayo hutolewa na watu ambao wakati mmoja walikuwa wakifurahia kwenda kanisani lakini wakakata tamaa dini yao iliposhindwa kuwatimizia mahitaji yao ya kiroho. Ijapokuwa kwa ujumla watu wengi wametamaushwa na matengenezo ya kidini, bado wanasisitiza kwamba wanataka kumwabudu Mungu. Hata hivyo, wanaamini kwamba ni afadhali kumwabudu kwa njia yao wenyewe badala ya kumwabudu wakishirikiana na kanisa au tengenezo jingine.

Biblia husema nini? Je, Mungu awataka Wakristo washirikiane na tengenezo fulani?

Wakristo wa Mapema Waliopangwa Kitengenezo Walinufaika

Kwenye Pentekoste mwaka wa 33 W.K., Yehova alimwaga roho takatifu yake, si juu ya waamini wachache, bali juu ya kikundi cha wanaume na wanawake waliokusanyika pamoja “mahali palepale,” yaani, katika chumba cha juu katika jiji la Yerusalemu. (Matendo 2:1) Wakati huo, kutaniko la Kikristo, ambalo lilikuja kuwa tengenezo la kimataifa, lilifanyizwa. Jambo hilo lilithibitika kuwa baraka halisi kwa wanafunzi hao wa mapema. Kwa nini? Kwanza, walikuwa wamepewa mgawo wa maana—wa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu hatimaye “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Katika makutaniko wageuzwa-imani wapya wangeweza kujifunza kutoka kwa waamini wenzao wenye uzoefu jinsi ya kuendeleza kazi ya kuhubiri.

Punde si punde ujumbe wa Ufalme ulienea na kufika mbali kabisa na Yerusalemu. Kati ya mwaka wa 62 na 64 W.K., mtume Petro aliandika barua yake ya kwanza kwa Wakristo waliokuwa ‘wametawanyika huku na huku katika Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia,’ zilizo katika Uturuki ya kisasa. (1 Petro 1:1) Pia kulikuwa na waamini katika Palestina, Lebanoni, Siria, Ugiriki, Krete, na Italia. Paulo alipokuwa akiwaandikia Wakolosai mwaka wa 60 hadi 61 W.K., habari njema ilikuwa ‘imehubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’—Wakolosai 1:23.

Manufaa ya pili ya kushirikiana na tengenezo ilikuwa kitia-moyo ambacho Wakristo wangetoa kwa mmoja na mwenzake. Kwa kushirikiana na kutaniko, Wakristo wangeweza kusikia hotuba zenye kuchochea, kujifunza Maandiko Matakatifu pamoja, kushiriki mambo yaliyoonwa yenye kujenga, na kujiunga na waamini wenzao katika sala. (1 Wakorintho sura ya 14) Na wanaume wakomavu wangeweza ‘kulichunga kundi la Mungu.’—1 Petro 5:2.

Wakiwa washiriki wa kutaniko, Wakristo pia walipata kujuana, wakapendana. Badala ya kuhisi kuwa wamelemewa kwa kushirikiana na kutaniko, Wakristo wa mapema walijengwa na kuimarishwa na ushirika huo.—Matendo 2:42; 14:27; 1 Wakorintho 14:26; Wakolosai 4:15, 16.

Sababu nyingine iliyofanya kutaniko la ulimwenguni pote lililoungana, au tengenezo lihitajike, ilikuwa ni kudumisha muungano. Wakristo walijifunza ‘kusema kwa upatano.’ (1 Wakorintho 1:10) Lilikuwa jambo muhimu. Washiriki wa kutaniko walitoka kwenye malezi ya kielimu na ya kijamii ya namna mbalimbali. Walisema lugha tofauti-tofauti, na bila shaka walikuwa na tofauti za kiutu. (Matendo 2:1-11) Nyakati fulani, kulikuwa na tofauti halisi za maoni. Hata hivyo, Wakristo walisaidiwa kutatua tofauti hizo ndani ya kutaniko. —Matendo 15:1, 2; Wafilipi 4:2, 3.

Maswali mazito ambayo hayangeweza kushughulikiwa na wazee wenyeji yalipelekwa kwa waangalizi wasafirio waliokomaa, kama vile Paulo. Mambo muhimu ya kimafundisho yalipelekwa kwa baraza kuu linaloongoza lililokuwa Yerusalemu. Mwanzoni baraza linaloongoza lilifanyizwa na mitume wa Yesu Kristo lakini baadaye lilipanuliwa ili kutia ndani wanaume wazee wa kutaniko katika Yerusalemu. Kila kutaniko lilitambua kwamba baraza linaloongoza na wawakilishi wake walipewa mamlaka na Mungu ili kupanga huduma, kuweka rasmi wanaume kwenye nyadhifa za utumishi, na kufanya maamuzi kuhusu mambo ya kimafundisho. Suala lilipotatuliwa na baraza linaloongoza, makutaniko yalikubali uamuzi huo na ‘kushangilia juu ya kitia-moyo hicho.’—Matendo 15:1, 2, 28, 30, 31.

Naam, Yehova alitumia tengenezo katika karne ya kwanza. Lakini vipi leo?

Twahitaji Tengenezo Leo

Kama vile wenzao wa karne ya kwanza, Mashahidi wa Yehova leo huchukua kwa uzito utume wa kuhubiri habari njema za Ufalme. Njia moja wanayotumia kutimiza kazi hiyo ni kwa kugawanya Biblia na vichapo vya Biblia, kazi ambayo huhitaji kuwe na tengenezo.

Vichapo vya Kikristo lazima vitayarishwe kwa uangalifu, vikaguliwe kuwa ni sahihi, vichapwe, kisha kupelekwa kwenye makutaniko. Kisha, Wakristo mmoja-mmoja lazima wajitolee kupeleka fasihi kwa wale wanaotaka kuisoma. Ujumbe wa Ufalme umewafikia mamilioni ya watu kwa njia hiyo. Wahubiri wa habari njema hujitahidi kutekeleza kazi yao ya kuhubiri kwa njia ya utaratibu, wakihakikisha kwamba hakuna sehemu yoyote ya eneo inayofanyiwa kazi mara nyingi huku sehemu nyingine zikisahaulika. Mambo hayo yote hutaka kuwe na tengenezo.

Kwa kuwa “Mungu si mwenye ubaguzi,” lazima Biblia na fasihi ya Biblia itafsiriwe. (Matendo 10:34) Kwa sasa, gazeti hili hupatikana katika lugha 132, na gazeti jenzi, Amkeni! huchapishwa katika lugha 83. Hilo hutaka kuwe na vikundi vya watafsiri vilivyopangwa vizuri ulimwenguni pote.

Washiriki wa kutaniko hupokea kitia-moyo wanapohudhuria mikutano na makusanyiko ya Kikristo. Wakiwa huko wao husikiza hotuba za Biblia zenye kuchochea, hujifunza Maandiko pamoja, hushiriki mambo yaliyoonwa yenye kujenga, na kujiunga na waabudu wenzao katika sala. Na kama ndugu zao wa karne ya kwanza, wanafurahia ziara zenye kuimarisha imani za waangalizi wasafirio wenye upendo. Hivyo, Wakristo leo hufanyiza “kundi moja, mchungaji mmoja.”—Yohana 10:16.

Bila shaka, Mashahidi wa Yehova si wakamilifu, wala wenzao wa mapema. Hata hivyo, wanajitahidi kufanya kazi pamoja kwa muungano. Kama tokeo, kazi ya kuhubiri Ufalme inatimizwa duniani kote.—Matendo 15:36-40; Waefeso 4:13.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wakristo leo hufanyiza “kundi moja, mchungaji mmoja”