Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuza Urafiki wa Karibu Pamoja na Yehova

Kuza Urafiki wa Karibu Pamoja na Yehova

Kuza Urafiki wa Karibu Pamoja na Yehova

“MKARIBIENI Mungu, naye atawakaribia,” akaandika mwanafunzi Yakobo. (Yakobo 4:8) Naye mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Mwenyezi-Mungu ni rafiki ya wale wamchao.” (Zaburi 25:14, Biblia Habari Njema) Ni wazi kwamba Yehova Mungu hutaka tuwe na urafiki wa karibu pamoja naye. Hata hivyo, si wote wanaomwabudu Mungu na kutii sheria zake huhisi wakiwa karibu naye.

Vipi wewe? Je, una uhusiano wa kibinafsi wa karibu pamoja na Mungu? Bila shaka, wataka kumkaribia. Twaweza kukuzaje urafiki wa karibu pamoja na Mungu? Huo una umuhimu gani kwetu? Sura ya tatu ya kitabu cha Biblia cha Mithali yaandaa majibu.

Dhihirisha Fadhili-Upendo na Kweli

Mfalme Solomoni wa Israeli la kale aanza sura ya tatu ya Mithali kwa maneno haya: “Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku. Na miaka ya uzima, na amani.” (Mithali 3:1, 2) Kwa kuwa Solomoni alipuliziwa na Mungu kuandika hayo, shauri hilo kama la baba kwa kweli latoka kwa Yehova Mungu nasi ndio tunaoshauriwa. Hapa twashauriwa tutii vikumbusha vya Mungu—sheria, au mafundisho yake, na amri zake—zilizorekodiwa katika Biblia. Tukifanya hivyo, ‘wingi wa siku na miaka ya uzima na amani yetu zitaongezeka.’ Naam, hata sasa twaweza kuwa na maisha yenye amani na twaweza kuepuka ufuatiaji ambao hutuweka katika hatari ya kifo cha mapema ambacho mara nyingi huwapata watenda-maovu. Isitoshe, twaweza kutumainia uhai wa milele katika ulimwengu wenye amani.—Mithali 1:24-31; 2:21, 22.

Solomoni aendelea kusema hivi: “Rehema [“fadhili-upendo,” “NW”] na kweli zisifarakane nawe [“zisikuache,” “NW”]; zifunge shingoni mwako; ziandike juu ya kibao cha moyo wako. Ndivyo utakavyopata kibali na akili nzuri, mbele za Mungu na mbele ya mwanadamu.”Mithali 3:3, 4.

Neno la lugha ya awali linalomaanisha “fadhili-upendo” nyakati nyingine hutafsiriwa “upendo wenye uaminifu-mshikamanifu” nao huhusisha uaminifu, mshikamano, na uaminifu-mshikamanifu. Je, tumeazimia kuendelea kushikamana na Yehova hata iweje? Je, sisi huonyesha fadhili-upendo katika uhusiano wetu na waamini wenzetu? Je, sisi hujitahidi kubaki karibu nao? Katika shughuli za kila siku nao, je, sisi huwa na ‘sheria ya fadhili-upendo katika ulimi wetu’ hata chini ya hali ngumu?—Mithali 31:26, NW.

Kwa kuwa ni mwingi wa fadhili-upendo, Yehova yu “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Ikiwa tumetubu dhambi tulizofanya wakati uliopita na sasa twaifanyia miguu yetu mapito yaliyo manyofu, twahakikishiwa kwamba “majira ya kuburudisha” yatakuja kutoka kwa Yehova. (Matendo 3:19) Je, hatupaswi kumwiga Mungu wetu kwa kuwasamehe wengine makosa yao?—Mathayo 6:14, 15.

Yehova ni “Mungu wa kweli,” naye hutaka “kweli” kutoka kwa wale wanaotafuta urafiki wa karibu pamoja naye. (Zaburi 31:5) Je, kwa kweli twaweza kumtarajia Yehova awe Rafiki yetu ikiwa twaishi maisha maradufu—tukitenda kwa njia moja tunapokuwa na washiriki Wakristo na kwa njia nyingine wakati ambao hatuonekani—kama “watu wa ubatili” ambao huficha aina ya watu waliyo? (Zaburi 26:4) Huo ungekuwa upumbavu kama nini, kwa kuwa “vitu vyote viko uchi na vikiwa vimefunuliwa wazi machoni” pa Yehova!—Waebrania 4:13.

Fadhili-upendo na kweli zapasa kuthaminiwa kama mikufu ya thamani kubwa ‘iliyofungwa shingoni mwetu’ kwa kuwa sifa hizo hutusaidia ‘kupata kibali mbele za Mungu na mbele ya mwanadamu.’ Twahitaji kuonyesha sifa hizo nje na pia kuziandika ‘juu ya kibao cha moyo wetu,’ tukizifanya ziwe sehemu muhimu ya utu wetu.

Kuza Kumtumaini Yehova Kabisa-Kabisa

Mfalme huyo mwenye hekima aendelea kusema hivi: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.”Mithali 3:5, 6.

Kwa kweli twastahili kumtumaini Yehova kabisa. Akiwa Muumba wetu, yeye ni “hodari kwa nguvu zake” naye ndiye Chanzo cha “ukuu wa uweza.” (Isaya 40:26, 29) Aweza kutekeleza makusudi yake yote. Kwani, jina lake mwenyewe lamaanisha “Yeye Husababisha Iwe,” nalo hutuhakikishia uwezo wake wa kutimiza ahadi zake! Kwa kuwa “haiwezekani Mungu kusema uwongo,” yeye ndiye kielelezo kikuu cha ile kweli. (Waebrania 6:18) Sifa yake kuu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Yeye ni “mwenye haki katika njia zake zote, na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.” (Zaburi 145:17) Ikiwa hatuwezi kumtumaini Mungu, tutamtumaini nani basi? Bila shaka, ili tusitawishe kumtumaini, twahitaji ‘kuonja tuone ya kuwa Yehova yu mwema’ kwa kutumia maishani mwetu wenyewe mambo tunayojifunza katika Biblia na kwa kuzingatia manufaa ya mambo hayo.—Zaburi 34:8.

Twawezaje ‘kumkiri Yehova katika njia zetu zote’? Mtunga-zaburi aliyepuliziwa asema hivi: “Nitaitafakari kazi yako yote; Nitaziwaza habari za matendo yako.” (Zaburi 77:12) Kwa kuwa Mungu haonekani, ni muhimu kutafakari kazi zake kuu na jinsi alivyowatendea watu wake ili kukuza urafiki wa karibu pamoja naye.

Sala pia ni njia muhimu ya kumkiri Yehova. Mfalme Daudi alimlilia Yehova “mchana kutwa.” (Zaburi 86:3) Mara nyingi Daudi alisali usiku kucha, kama wakati alipokuwa mtoro nyikani. (Zaburi 63:6, 7) ‘Endelezeni sala kila wakati,’ akasihi mtume Paulo. (Waefeso 6:18) Sisi husali mara ngapi? Je, sisi hufurahia kuwasiliana na Mungu kutoka moyoni? Tunapokabili hali ngumu, je, sisi humwomba kwa bidii atusaidie? Je, sisi hutafuta mwongozo wake kwa bidii kabla ya kufanya maamuzi muhimu? Yehova hupendezwa nasi tunaposali kwake kutoka moyoni. Naye atuhakikishia kwamba atasikiliza sala zetu na ‘kunyosha mapito yetu.’

Ni upumbavu ulioje ‘kuzitegemea akili zetu wenyewe’ au za watu maarufu ulimwenguni ilhali twaweza kumtumaini Yehova kabisa! “Usiwe mwenye hekima machoni pako,” asema Solomoni. Badala yake, aonya hivi: “Mche BWANA, ukajiepushe na uovu. Itakuwa afya mwilini pako, na mafuta mifupani mwako.” (Mithali 3:7, 8) Hofu ifaayo ya kutomuudhi Mungu yapaswa kuongoza matendo, mawazo, na hisia zetu zote. Hofu hiyo yenye staha hutuzuia tusifanye lililo baya nayo huponya na kuburudisha kiroho.

Mpe Yehova Yaliyo Bora

Twaweza kumkaribia Mungu katika njia gani nyingine? “Mheshimu BWANA kwa mali yako, na kwa malimbuko ya mazao yako yote,” aagiza mfalme. (Mithali 3:9) Kumheshimu Yehova kwamaanisha kumstahi na kumkweza mbele za watu wote kwa kutangaza na kutegemeza jina lake hadharani. Mali tunazotumia kumheshimu Yehova ni wakati wetu, vipawa vyetu, nguvu zetu na mali zetu za kimwili. Lazima hizo ziwe malimbuko—bora zaidi tulizo nazo. Je, hatupaswi kuonyesha azimio letu la ‘kufuliza kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wa Mungu,’ kwa jinsi tunavyotumia mali zetu?—Mathayo 6:33.

Kumheshimu Yehova kwa mali zetu huthawabishwa sikuzote. “Ndipo ghala zako zitakapojazwa kwa wingi,” ahakikisha Solomoni, “na mashinikizo yako yatafurika divai mpya.” (Mithali 3:10) Ilhali ufanisi wenyewe wa kiroho hautokezi ufanisi wa kimwili, kutumia mali zetu kwa ukarimu ili kumheshimu Yehova hutokeza baraka nyingi. “Chakula” kilichomtegemeza Yesu kilikuwa kufanya mapenzi ya Mungu. (Yohana 4:34) Hali kadhalika, kushiriki kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ambayo humtukuza Yehova hututegemeza. Tukidumu katika kazi hiyo, ghala zetu za kiroho zitajazwa kwa wingi. Shangwe yetu—inayofananishwa na divai mpya—itafurika.

Je, hatumtegemei Yehova na kumwomba atutegemeze kwa chakula kila siku? (Mathayo 6:11) Kwa kweli, vyote tulivyo navyo, sisi huvipata kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo. Yehova atazidi kutubariki kwa kadiri tunavyotumia mali zetu kumsifu.—1 Wakorintho 4:7.

Kubali Nidhamu ya Yehova

Akijua fungu la nidhamu katika kupata urafiki wa karibu pamoja na Yehova, mfalme wa Israeli atushauri hivi: “Mwanangu, usidharau kuadhibiwa na [“nidhamu ya ,” “NW”] BWANA, wala usione ni taabu kurudiwa naye [“karipio lake,” “NW”]. Kwa kuwa BWANA ampendaye humrudi, kama vile baba mwanawe ampendezaye.”Mithali 3:11, 12.

Hata hivyo, huenda isiwe rahisi kukubali nidhamu. “Hakuna nidhamu ionekanayo kwa wakati wa sasa kuwa yenye shangwe, bali yenye kihoro; lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo hutoa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu,” akaandika mtume Paulo. (Waebrania 12:11) Karipio na nidhamu ni sehemu muhimu ya mazoezi ambayo hutuleta karibu na Mungu. Yehova huonyesha kwamba anatupenda kwa kuturekebisha, iwe ni kupitia wazazi, kutaniko la Kikristo, au kwa kutafakari Maandiko wakati wa funzo letu la kibinafsi. Ikiwa tuna hekima tutakubali kurekebishwa.

Shikamana na Hekima na Ufahamu

Kisha, Solomoni akazia umuhimu wa hekima na ufahamu katika kukuza uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Ajulisha hivi: “Heri mtu yule aonaye hekima, na mtu yule apataye ufahamu. Maana biashara yake ni bora kuliko biashara ya fedha, na faida yake ni nyingi kuliko dhahabu safi. . . . Yeye ni mti wa uzima kwao wamshikao sana; ana heri kila mtu ashikamanaye naye.”Mithali 3:13-18.

Akitukumbusha juu ya udhihirisho wa hekima na ufahamu katika kazi za ajabu za uumbaji wa Yehova, mfalme ataarifu hivi: “Kwa hekima BWANA aliiweka misingi ya nchi; kwa akili zake akazifanya mbingu imara; . . . Mwanangu, yasiondoke haya machoni pako, shika hekima kamili na busara. Basi yatakuwa uzima kwa nafsi yako, na neema shingoni mwako.”Mithali 3:19-22.

Hekima na ufahamu ni sifa za kimungu. Hatuhitaji kuzikuza tu bali pia kushikamana sana nazo kwa kutokuwa wazembe kamwe katika kujifunza Maandiko kwa bidii na kutumia mambo tunayojifunza. “Ndipo utakapokwenda katika njia yako salama,” Solomoni aendelea kusema, “wala mguu wako hautakwaa.” Aongeza kusema hivi: “Ulalapo hutaona hofu; naam, utalala na usingizi wako utakuwa mtamu.”Mithali 3:23, 24.

Naam, twaweza kutembea kwa usalama na kulala kwa amani ya akili huku tukingojea siku ijayo kama mwivi ya “uharibifu wa ghafula” dhidi ya ulimwengu mwovu wa Shetani. (1 Wathesalonike 5:2, 3; 1 Yohana 5:19) Hata katika dhiki kubwa ikaribiayo, twaweza kuwa na uhakika huu: “Usiogope hofu ya ghafula, wala uharibifu wa waovu utakapofika. Kwa kuwa BWANA atakuwa tumaini lako, naye atakulinda mguu wako usinaswe.”Mithali 3:25, 26; Mathayo 24:21.

Fanya Mema

“Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao,” Solomoni ashauri, “ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” (Mithali 3:27) Kufanyia wengine mema huhusisha kutumia mali zetu kwa ukarimu kwa niaba yao, na twaweza kufanya hivyo katika njia nyingi. Lakini je, kuwasaidia watu wapate uhusiano wa karibu na Mungu wa kweli silo jambo bora tuwezalo kuwafanyia katika “wakati [huu] wa mwisho”? (Danieli 12:4) Basi, hizi ndizo siku za kuonyesha bidii katika kufanya kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi.—Mathayo 28:19, 20.

Mfalme mwenye hekima aorodhesha pia mazoea ya kuepukwa, akisema: “Usimwambie jirani yako, Nenda, urudi halafu, na kesho nitakupa; nawe unacho kitu kile karibu nawe. Usiwaze mabaya juu ya jirani yako, ambaye anakaa karibu nawe na kujiona salama. Usishindane na mtu bila sababu, ikiwa hakukudhuru kwa lo lote. Usimhusudu mtu mwenye jeuri, wala usiichague mojawapo ya njia zake.”Mithali 3:28-31.

Akieleza kwa muhtasari sababu ya shauri lake, Solomoni asema hivi: “Maana mtu mkaidi ni chukizo kwa BWANA, bali siri yake ni pamoja na wanyofu. Laana ya BWANA i katika nyumba ya waovu, bali huibariki maskani ya mwenye haki. Hakika yake huwadharau wenye dharau, bali huwapa wanyenyekevu neema. Wenye hekima wataurithi utukufu, bali kukuzwa kwa wapumbavu ni fedheha.”Mithali 3:32-35.

Iwapo twataka kuwa na urafiki wa karibu pamoja na Yehova, hatupaswi kamwe kupanga njama wala kuwazia mambo yenye kuumiza. (Mithali 6:16-19) Tutapata upendeleo na baraka za Mungu iwapo tu twafanya yaliyo sawa machoni pake. Pia huenda tukapata heshima ambayo hatukujitafutia wakati ambapo wengine waona kwamba twatenda kulingana na hekima ya kimungu. Kwa hiyo na tukatae hila za ulimwengu huu mwovu na wenye jeuri. Kwa kweli, na tufuatie mwendo mnyofu na kukuza urafiki wa karibu pamoja na Yehova!

[Picha katika ukurasa wa 25]

“Mheshimu BWANA kwa mali yako”