Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wajionaje?

Wajionaje?

Wajionaje?

ALIKUWA mtu mwenye kiburi. Alipokwezwa na kupewa wadhifa mkubwa serikalini, alijivunia sifa nyingi na upendezi aliopata. Lakini aliudhika sana, kwa kuwa ofisa mwingine alikataa kumpa heshima hiyo. Ili kulipa kisasi, ofisa huyo mwenye kiburi alipanga njama ya kuangamiza watu wote wa kabila la mkosaji huyo waliokuwa katika milki hiyo. Hayo ni maoni yaliyopotoka kama nini!

Mpanga-njama huyo alikuwa Hamani, ofisa mkuu katika nyumba ya Mfalme Ahasuero wa Uajemi. Naye alipanga kumfanyia nani uhasama huo? Myahudi aliyeitwa Mordekai. Ingawa Hamani alipita kiasi kwa kupanga kuangamiza kabila zima, jambo hilo laonyesha hatari na matokeo mabaya ya kiburi. Roho yake ya kujigamba ilitatiza wengine na pia ikamfanya atwezwe hadharani na hatimaye kufa.—Esta 3:1-9; 5:8-14; 6:4-10; 7:1-10.

Waabudu wa Kweli Waweza Kuwa na Kiburi

Yehova hutaka ‘twende kwa unyenyekevu [“kiasi,” NW] na Mungu wetu.’ (Mika 6:8) Biblia ina masimulizi kadha wa kadha ya watu walioshindwa kudumisha kiasi katika jinsi walivyojiona. Hilo liliwaletea matatizo na huzuni. Kufikiria baadhi ya vielelezo hivyo kwaweza kutusaidia kuona upumbavu na hatari ya kukosa maoni yenye usawaziko.

Maoni ya Yona, nabii wa Mungu, yalikosa usawaziko sana hivi kwamba alijaribu kukimbia alipopewa utume na Mungu akawaonye watu waovu wa Ninewi juu ya hukumu ya Yehova dhidi yao. (Yona 1:1-3) Baadaye, utendaji wake wa kuhubiri ulipofanikiwa kuwafanya Waninewi watubu, Yona akanuna. Alihangaikia sana sifa yake mwenyewe akiwa nabii hivi kwamba uhai wa maelfu ya Waninewi haukuwa na maana yoyote kwake. (Yona 4:1-3) Tukihangaikia kupita kiasi umuhimu wetu, huenda ikawa vigumu kwetu kuona watu na matukio yanayotuzunguka bila upendeleo na kwa njia ifaayo daima.

Mfikirie Uzia pia, ambaye alikuwa mfalme mzuri wa Yuda. Maoni yake yalipopoteza usawaziko, alijaribu kwa kiburi kunyakua wajibu fulani wa makuhani. Kwa sababu ya matendo yake yasiyo na kiasi na ya kimbelembele, afya yake iliathiriwa na akapoteza kibali cha Mungu.—2 Mambo ya Nyakati 26:3, 16-21.

Maoni yasiyo na usawaziko karibu yawanase mitume wa Yesu. Walihangaikia sana utukufu na mamlaka yao wenyewe. Wakati wa mtihani mkubwa ulipofika, walimwacha Yesu na kukimbia. (Mathayo 18:1; 20:20-28; 26:56; Marko 9:33, 34; Luka 22:24) Kukosa kwao kiasi na kujiona kwao kuwa watu wa maana sana karibu kuwafanye wasahau kusudi la Yehova na fungu lao kuhusiana na mapenzi yake.

Madhara ya Kujiona Kuwa wa Maana Sana

Maoni yasiyo na usawaziko yaweza kutokeza maumivu na kuharibu uhusiano wetu na wengine. Kwa kielelezo, twaweza kuwa tumeketi katika chumba na kuona watu wawili wakinong’onezeana na kucheka. Ikiwa twajifikiria sana, huenda tukadhania kwamba wanatudhihaki kwa kuwa wananong’onezeana. Huenda akili yetu isituruhusu kufikiria kwamba huenda wakawa wakiongea juu ya jambo jingine lolote. Kwani, wangeweza kuwa wanaongea juu ya nani mwingine? Huenda tukakasirika na kuamua kwamba hatutaongea nao tena kamwe. Kwa njia hiyo kukosa usawaziko na kujiona kuwa watu wa maana sana kwaweza kutokeza kutoelewana na kuharibu uhusiano na marafiki, washiriki wa familia, na wengine.

Huenda watu wanaojiona kuwa wa maana sana wakajigamba, na kujivunia daima eti vipawa, matendo, au mali zao nyingi. Au huenda wakatawala maongezi, nyakati zote wakitaja mambo fulani juu yao wenyewe. Mazungumzo ya aina hiyo huonyesha ukosefu wa upendo wa kweli na yaweza kukasirisha sana. Kwa hiyo, mara nyingi wenye kujiona kuwa wa maana sana hujitenga na wengine.—1 Wakorintho 13:4.

Tukiwa Mashahidi wa Yehova, huenda tukadhihakiwa na kukataliwa katika huduma yetu ya hadharani. Twahitaji kukumbuka kwamba si sisi wenyewe tunaopingwa bali ni Yehova, Chanzo cha ujumbe wetu. Hata hivyo, maoni yaliyopotoka juu ya umuhimu wetu yaweza kuwa na matokeo mabaya. Miaka kadhaa iliyopita, ndugu mmoja alikasirishwa na mambo ambayo mwenye nyumba alisema, naye akamtusi. (Waefeso 4:29) Tangu hapo, ndugu huyo hakushiriki tena kamwe katika huduma ya mlango kwa mlango. Naam, kiburi chaweza kutufanya tukasirike tunapohubiri. Na tujitahidi tusiruhusu hilo litukie kamwe. Badala yake, na tutafute msaada wa Yehova kwa unyenyekevu ili tuendelee kuthamini ifaavyo pendeleo la kushiriki katika huduma ya Kikristo.—2 Wakorintho 4:1, 7; 10:4, 5.

Kuwa na mtazamo wa kujiona kuwa wa maana sana kungeweza kutuzuia tusikubali shauri tunalohitaji sana. Miaka kadhaa katika nchi fulani ya Amerika ya Kati, mvulana tineja alitoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika mkutano wa Kikristo. Mwangalizi wa shule alipompa shauri la moja kwa moja, kijana huyo aliyekasirika alitupa Biblia yake sakafuni na kutoka nje ya Jumba la Ufalme kwa vishindo akinuia kutorudi kamwe. Lakini baada ya siku chache, akadhibiti kiburi chake, akafanya mapatano na mwangalizi wa shule, na kukubali shauri lake kwa unyenyekevu. Hatimaye, kijana huyo akawa Mkristo mkomavu.

Kukosa kiasi na kujiona kuwa watu wa maana sana kwaweza kuharibu uhusiano wetu na Mungu. Mithali 16:5 huonya hivi: “Kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa BWANA.”

Kujiona kwa Usawaziko

Ni wazi kwamba hatupaswi kujiona kuwa watu wa maana sana. Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba tusichukue kwa uzito tunayofanya au tunayosema. Biblia huonyesha kwamba waangalizi, watumishi wa huduma—kwa kweli, wote kutanikoni—wapaswa kuchukua mambo kwa uzito. (1 Timotheo 3:4, 8, 11; Tito 2:2) Kwa hiyo Wakristo wanawezaje kusitawisha na kudumisha kujiona kwa njia yenye kiasi, usawaziko, na kuchukua mambo kwa uzito?

Biblia huandaa vielelezo vingi vyenye kutia moyo vya watu waliodumisha usawaziko katika kujiona. Kielelezo chenye kutokeza ni kile cha unyenyekevu wa Yesu Kristo. Mwana wa Mungu aliacha kwa hiari wadhifa wake mtukufu huko mbinguni na kuwa mwanadamu duni duniani ili afanye mapenzi ya Baba yake na kuwaletea wanadamu wokovu. Licha ya matukano, kutendwa vibaya, na kifo cha kuaibisha, alidumisha sifa ya kujidhibiti na adhama. (Mathayo 20:28; Wafilipi 2:5-8; 1 Petro 2:23, 24) Yesu aliwezaje kufanya hayo? Alimtegemea Yehova kabisa naye aliazimia kufanya mapenzi yake. Yesu alijifunza Neno la Mungu kwa bidii, akasali kwa bidii, na kujikakamua katika huduma. (Mathayo 4:1-10; 26:36-44; Luka 8:1; Yohana 4:34; 8:28; Waebrania 5:7) Kufuata kielelezo cha Yesu kwaweza kutusaidia kusitawisha na kudumisha maoni yenye usawaziko juu yetu wenyewe.—1 Petro 2:21.

Pia fikiria kielelezo chema cha Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli. Kwa sababu ya kutotii kwa baba yake, Yonathani alipoteza fursa ya kumrithi Sauli akiwa mfalme. (1 Samweli 15:10-29) Je, Yonathani aliona uchungu kwa sababu ya hasara hiyo? Je, alimwonea wivu Daudi, kijana ambaye angetawala badala yake? Ingawa Yonathani alikuwa na umri mkubwa zaidi na huenda alikuwa na uzoefu mkubwa zaidi kuliko Daudi, alijipatanisha na mpango wa Yehova kwa kiasi na unyenyekevu naye akamtegemeza Daudi kwa uaminifu-mshikamanifu. (1 Samweli 23:16-18) Kuona mapenzi ya Mungu vizuri zaidi na kuwa tayari kujitiisha kwake kutatusaidia ‘kutojifikiria wenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’—Waroma 12:3.

Yesu alifundisha umuhimu wa kuonyesha kiasi na unyenyekevu. Alitolea jambo hilo kielezi kwa kusema kwamba wanafunzi wake wakiwa katika karamu ya ndoa, wasijitwalie “mahali pa kutokeza zaidi sana” kwa sababu huenda mtu fulani mashuhuri zaidi akaja nao wakaaibishwa kwa kulazimika kwenda mahali pa chini zaidi sana. Akielewesha fundisho hilo vizuri zaidi, Yesu aliongeza kusema hivi: “Kwa maana kila mtu ajikwezaye mwenyewe atanyenyekezwa na yeye ajinyenyekezaye mwenyewe atakwezwa.” (Luka 14:7-11) Ikiwa tuna hekima, tutalitii shauri la Yesu na ‘kujivika wenyewe hali ya akili ya kujishusha chini.’—Wakolosai 3:12; 1 Wakorintho 1:31.

Baraka za Kuwa na Maoni Yenye Usawaziko

Kuwa na roho ya kiasi na unyenyekevu huwawezesha watumishi wa Yehova kupata shangwe ya kweli katika huduma yao. Wazee hufikiwa kwa urahisi zaidi ‘wanapolitendea kundi kwa wororo.’ (Matendo 20:28, 29) Kisha wote kutanikoni hustarehe zaidi waongeapo nao na kutafuta msaada wao. Kwa hiyo washiriki wa kutaniko waweza kuvutwa karibu zaidi katika roho ya upendo, shauku, na kutumainiana.

Kutojiona kuwa wa maana sana hutuwezesha kuwa na marafiki wema. Sifa ya kiasi na unyenyekevu zitatuzuia tusisitawishe roho ya kushindana na kujaribu kuwashinda wengine katika matendo au katika vitu vya kimwili. Sifa hizo za kimungu zitatufanya tuwe wenye kujali zaidi, nazo zitatuwezesha kuwafariji na kuwategemeza wenye uhitaji. (Wafilipi 2:3, 4) Watu wanapochochewa na upendo na fadhili, kwa kawaida wao huitikia vema. Na je, uhusiano huo usio na ubinafsi sio msingi unaotegemeza urafiki mkubwa mbalimbali? Ni baraka iliyoje tuepukapo kujiona kupita kiasi kuwa wa maana sana!—Waroma 12:10.

Kujiona kwa usawaziko pia hufanya iwe rahisi kukubali makosa yetu tunapomkasirisha mtu fulani. (Mathayo 5:23, 24) Hilo hutokeza mahusiano mazuri zaidi, likiwezesha watu wapatane na kuheshimiana. Waangalizi, kama vile wazee Wakristo, wana fursa ya kufanyia wengine mema mengi iwapo wao ni wanyenyekevu na wenye kiasi. (Mithali 3:27; Mathayo 11:29) Mtu mnyenyekevu atawasamehe kwa urahisi wanaomtenda dhambi. (Mathayo 6:12-15) Hatachokozeka haraka akidhani amekosewa, naye atamtumainia Yehova arekebishe mambo ambayo hayawezi kurekebishwa vinginevyo.—Zaburi 37:5; Mithali 3:5, 6.

Baraka kubwa zaidi ipatikanayo kwa kujiona kwa kiasi na unyenyekevu ni ile ya kuwa na upendeleo na kibali cha Yehova. “Mungu hupinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili isiyostahiliwa.” (1 Petro 5:5) Na tusianguke kamwe katika mtego wa kujiona kuwa wa maana sana kuliko tulivyo. Badala yake, na tutambue kwa unyenyekevu sehemu yetu katika mpango wa mambo, wa Yehova. Wote wanaotimiza takwa lake la ‘kwenda kwa unyenyekevu na Mungu,’ watapata baraka nyingi.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Yonathani alimtegemeza Daudi kwa unyenyekevu