Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufanikiwa Kupitia Udumifu

Kufanikiwa Kupitia Udumifu

Kufanikiwa Kupitia Udumifu

UDUMIFU umekuwa sifa haba sana siku hizi. Watu wengi huamini kwamba mtu hufanikiwa kwa kuwa mahali pafaapo wakati ufaao, bali si kwa kuwa mdumifu. Ni nani awezaye kuwalaumu? Vyombo vya habari vimejaa matangazo ya biashara ambayo, bila wewe kujua, hukufanya ufikiri kwamba unaweza kupata chochote utakacho bila kujitahidi sana ukiongezea fedha kidogo tu. Magazeti huchapisha mfululizo wa habari nyingi sana juu ya mafanikio yanayopatikana haraka-haraka na juu ya wafanya-biashara vijana ambao hufanikiwa kuchuma mamilioni ya fedha punde tu baada ya kumaliza shule.

Mwandishi wa habari za magazeti Leonard Pitts asikitika: “Katika jamii inayozingatia sana mambo hayo, hilo huonekana kuwa jambo rahisi. . . . Laonekana kama jambo ambalo mtu yeyote angeweza kufanya kama angejua tu mbinu za kulifanya, kama angekuwa na uwezo, au kama angepata msaada wa Mungu.”

Udumifu Ni Nini?

Udumifu humaanisha ‘kushikilia kwa imara kusudi, hali, au shughuli fulani bila kuacha, kujapokuwa vizuizi au vipingamizi.’ Humaanisha kuazimia kabisa kuendelea kujapokuwa matatizo, kuwa wenye kushikamana na wasiokufa moyo. Biblia hukazia umuhimu wa sifa hiyo. Kwa mfano, Neno la Mungu latushauri hivi: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme,” “fulizeni kubisha hodi, nanyi mtafunguliwa,” “dumuni katika sala,” na “shikeni sana lililo bora.”—Mathayo 6:33; Luka 11:9; Waroma 12:12; 1 Wathesalonike 5:21.

Kukabiliana na vipingamizi visivyoepukika ni sehemu muhimu ya udumifu. Mithali 24:16 lasema: “Mwenye haki huanguka mara saba akaondoka tena.” (Italiki ni zetu.) Badala ya ‘kuacha’ anapopatwa na tatizo au anapokosa kufanikiwa, mtu mwenye udumifu ‘huondoka tena,’ ‘hufuliza,’ na kujaribu tena.

Hata hivyo, wengi hawako tayari kukabili matatizo na kutofanikiwa ambako huenda kukawapata. Kwa kuwa hawajasitawisha tamaa ya udumifu, wao hufa moyo haraka. “Watu wengi mno hukabiliana na kutofanikiwa kwa njia inayowaathiri,” asema mwandishi Morley Callaghan. “Wao hujisikitikia, hulaumu kila mtu, huwa na uchungu na . . . huacha wafanyalo.”

Haifai kufanya hivyo. “Tunasahau,” asema Pitts, “kwamba kuna sababu ya kuvumilia majaribu, kuna faida fulani ambayo hutokana na matatizo.” Faida gani hiyo? Yeye amalizia: “[Mtu] hujifunza kwamba kutofanikiwa si mwisho wa mambo, wala kutofaulu hakudumu milele. Mtu hupata ujuzi. Mtu huwa tayari.” Biblia husema tu hivi: “Katika kila kazi mna faida.”—Mithali 14:23.

Bila shaka, kujimudu tena baada ya kupata kipingamizi si jambo rahisi sikuzote. Nyakati nyingine tunapata magumu ambayo huenda yakaonekana kutushinda kabisa. Badala ya miradi yetu kukaribia zaidi, huenda ikaonekana kuwa hata mbali zaidi nasi. Huenda tukajihisi hoi, dhaifu, na huenda tukavunjika moyo, hata kushuka moyo. (Mithali 24:10) Lakini Biblia hututia moyo: “Acheni tusife moyo katika kufanya lililo bora, kwa maana katika majira yapasayo tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”Wagalatia 6:9.

Ni Nini Kiwezacho Kutusaidia Tuwe Wenye Udumifu?

Kuwa na miradi ifaayo tuwezayo kuifikia ndiyo hatua ya kwanza ili kudumu kwenye mwendo fulani tuliochagua. Bila shaka, mtume Paulo alielewa jambo hilo. Aliwaambia Wakorintho hivi: “Jinsi ninavyokimbia si bila uhakika; jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa.” Paulo alijua kwamba kama angetaka kufanikiwa katika jitihada zake, angehitaji miradi hususa, kama mkimbiaji anayezingatia tu kumaliza mbio. “Je, hamjui kwamba wakimbiaji katika mbio wote hukimbia, lakini ni mmoja tu apokeaye tuzo? Kimbieni kwa njia ambayo mwaweza kuipata tuzo,” akawahimiza. (1 Wakorintho 9:24, 26) Tunaweza kufanyaje hivyo?

“Mwenye busara huangalia sana aendavyo,” lasema andiko la Mithali 14:15. Ni hekima kuchunguza mara kwa mara miradi yetu maishani na kujiuliza tunakoelekea na kama tunahitaji kufanya marekebisho. Ni muhimu kujua kabisa tunachotaka kutimiza na kwa nini. Itakuwa vigumu kwetu kufa moyo ikiwa tunaendelea kuukumbuka mradi wetu mkubwa. “Macho yako yatazame mbele, na kope zako zitazame mbele yako sawasawa,” yahimiza mithali iliyopuliziwa, ili “njia zako zote zithibitike.”—Mithali 4:25, 26.

Baada ya kubainisha miradi yako, hatua inayofuata ni kuchanganua jinsi utakavyoifikia. Yesu aliuliza: “Ni nani kati yenu atakaye kujenga mnara asiyeketi kwanza na kupiga hesabu ya gharama?” (Luka 14:28) Kwa kupatana na kanuni hiyo, mtaalamu mmoja wa mambo ya akili alisema: “Jambo ambalo nimepata kujua kuhusu watu wenye mafanikio ni kwamba wanaelewa vizuri uhusiano kati ya matendo na matokeo yake maishani mwao. Watu wenye mafanikio wanaelewa kwamba wakitaka kitu fulani, ni lazima wafanye yote yahitajiwayo ili kukipata.” Kuelewa barabara hatua muhimu tunazohitaji kuchukua ili tutimize yale tutakayo kutimiza kutatusaidia tusikengeuke. Pia kutafanya iwe rahisi kwetu kujiandaa tena tukipata kipingamizi. Uchanganuzi kama huo ndio uliofanya Orville na Wilbur Wright wafanikiwe.

Hivyo, unapopatwa na vipingamizi, jitahidi sana uvichukue kwa maoni yafaayo na kuviona vipingamizi hivyo kuwa funzo. Changanua hali, pata kujua ni wapi ulipokosea, kisha usahihishe kosa hilo au urekebishe udhaifu huo. Inasaidia kuzungumza na wengine, kwa kuwa “kila kusudi huthibitika kwa kushauriana.” (Mithali 20:18) Bila shaka, kwa kila jitihada ufanyayo, unasitawisha ustadi na uhodari, sifa ambazo zitachangia mafanikio yako hatimaye.

Hatua ya tatu muhimu katika udumifu ni kuendelea kufanya jambo bila kuacha. Mtume Paulo atuhimiza hivi: “Kwa kadiri ambayo tumefanya maendeleo, acheni tuendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida hiyohiyo.” (Wafilipi 3:16) Kama mwelimishaji mmoja alivyosema, “kuwa na kiasi na kuendelea kufanya jambo lilelile kwa muda bila kuacha, huleta matokeo mazuri.” Jambo hilo limeonyeshwa vizuri katika ile hekaya maarufu ya Aesop juu ya kobe na sungura. Kobe alishinda mbio ingawa alikimbia polepole sana kuliko sungura. Kwa nini? Kwa sababu kobe alidumisha mwendo fulani thabiti na wenye utaratibu. Hakuacha mbio lakini alichagua mwendo ambao angeweza kuumudu, kisha akaudumisha hadi alipomaliza mbio. Kwa kuwa mtu mwenye utaratibu na uthabiti huzidi kufanya maendeleo, yeye hachoki na hivyo haielekei ataacha au kuondolewa kwenye shindano. Naam, “kimbieni kwa njia” ambayo mtaweza kuufikia mradi wenu.

Kuchagua Miradi Ifaayo

Bila shaka, ili udumifu upate kuwa na thamani yoyote ile, twahitaji kuwa na miradi ifaayo. Watu wengi hujitahidi kufanya mambo yasiyowaletea furaha. Lakini Biblia yasema: “Yeye achunguaye ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo . . . atakuwa mwenye furaha katika kutenda hiyo.” (Yakobo 1:25) Naam, kujifunza ili kuielewa sheria ya Mungu kama inavyoonyeshwa katika Biblia ni mradi ufaao sana. Kwa nini? Hasa, kwa sababu sheria ya Mungu hutegemea viwango vyake vikamilifu na vyenye uadilifu. Akiwa Muumba, yeye anajua kinachowafaa zaidi viumbe wake. Hivyo, tukidumu katika kujifunza maagizo ya Mungu na kuyatumia maishani mwetu, udumifu huo bila shaka utatuletea furaha. “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote . . . Katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako,” laahidi andiko la Mithali 3:5, 6.

Pia, kutwaa ujuzi juu ya Mungu na Yesu “[hu]maanisha uhai udumuo milele,” asema Yesu. (Yohana 17:3) Unabii wa Biblia waonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu. (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:3-13) Karibuni, Ufalme wa Mungu, serikali yake ya uadilifu, utatawala wakazi wa dunia. (Danieli 2:44; Mathayo 6:10) Serikali hiyo italeta kipindi kisicho na kifani cha amani, ufanisi, na hali njema kwa wanadamu wote watiifu. (Zaburi 37:10, 11; Ufunuo 21:4) “Mungu si mwenye ubaguzi,” lasema andiko la Matendo 10:34. Naam, kila mtu anaalikwa kufurahia manufaa hizo!

Biblia ni kitabu cha kale kilichojaa hekima na maana. Kuielewa kwahitaji muda na jitihada. Lakini kwa msaada wa Mungu—na ikiwa tunadumu kutafuta ujuzi wa Biblia—tunaweza kuielewa. (Mithali 2:4, 5; Yakobo 1:5) Ni kweli kwamba inaweza kuwa vigumu kutumia yale tunayojifunza. Huenda tukahitaji kufanya marekebisho katika kufikiri kwetu au mazoea yetu. Rafiki au watu wa familia wenye nia njema hata wanaweza kutupinga tusijifunze Biblia. Hivyo ni muhimu kuwa wenye udumifu. Mtume Paulo anatukumbusha kwamba Mungu atawapa uhai udumuo milele wale ‘wanaovumilia katika kazi iliyo njema.’ (Waroma 2:7) Mashahidi wa Yehova wangefurahi kukusaidia kufikia mradi huo.

Uwe na hakika kwamba utafanikiwa ukidumu katika kujifunza juu ya Mungu na mapenzi yake na kuendelea kutumia yale unayojifunza.—Zaburi 1:1-3.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Utafanikiwa ukidumu katika kujifunza juu ya Mungu na mapenzi yake

[Picha katika ukurasa wa 4]

Culver Pictures