Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Watu wa Namna Zote Nchini Uholanzi

Kuwasaidia Watu wa Namna Zote Nchini Uholanzi

Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti

Kuwasaidia Watu wa Namna Zote Nchini Uholanzi

ABRAHAMU alikuwa mtu mwenye imani isiyo ya kawaida. “Alipoitwa,” mtume Paulo akasema, Abrahamu alitii sauti ya Mungu “akatoka, ijapokuwa asijue ni wapi alikokuwa akienda.” Baada ya kuhamisha familia yake nzima, Abrahamu “alikaa kama mgeni asiye mzalia katika nchi ya ahadi” kwa miaka mia moja aliyoendelea kuishi.—Waebrania 11:8, 9.

Hata leo, wengi wa Mashahidi wa Yehova wamekubali mwito wa kuhamia nchi nyingine ili watumikie katika sehemu zenye uhitaji zaidi. Wengine wamejifunza lugha tofauti ili waweze kuwatolea ushahidi wageni ambao wamehamia nchi zao. Kama mifano ifuatayo inavyoonyesha, mtazamo huo mzuri ‘umefungua mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji’ nchini Uholanzi, ambako watu milioni moja kati ya wakazi milioni 15 wametoka nchi za kigeni.—1 Wakorintho 16:9.

□ Bahram, ambaye zamani alikuwa mkufunzi wa mbinu za kupigana za Kung Fu, alitoka nchi moja ya Mashariki ya Kati. Alipata Biblia na vichapo fulani vya Watch Tower. Kwa mwezi mmoja tu, Bahram akatambua kwamba amepata kweli. Yeye na mke wake wakaanza kujifunza, lakini kukawa na tatizo—mwalimu wao wa Biblia hakufahamu lugha yao. Walikuwa wakiwasiliana kwa ishara za mwili, wakizungumza kwa “mikono na miguu,” wao wakumbuka. Baadaye, Bahram na mkewe walifaulu kupata kutaniko lililotumia lugha yao, nao wakafanya maendeleo haraka. Sasa Bahram ni Shahidi aliyebatizwa.

□ Mume na mke walio mapainia walimfikia mtu mmoja wa Indonesia ambaye alikuwa amesimama mbele ya duka kuu moja. Alishangaa sana mapainia hao walipozungumza naye kwa lugha yake mwenyewe. Mipango ikafanywa atembelewe nyumbani kwake. Kumbe alikuwa ameishi Urusi kwa zaidi ya miaka 20 na katika muda huo, akawa daktari wa mambo ya uzazi ya wanawake. Alidai kwamba yeye haamini Mungu, lakini alikiri kwamba kila wakati alipomzalisha mwanamke, alikuwa akistaajabu sana, “Mwili wa binadamu ni mkamilifu kama nini! Huu ni muujiza ulioje!” Alikubali kujifunza Biblia, upesi akaamini kwamba kuna Muumba anayejali wanadamu. (1 Petro 5:6, 7) Sasa yeye ni ndugu aliyebatizwa naye anatumikia katika kutaniko la Kiindonesia kule Amsterdam.

□ Katika Rotterdam, ambayo ni mojawapo ya bandari kubwa zaidi ulimwenguni, kikundi cha mapainia wamekuwa stadi katika kuhubiria watu wa lugha mbalimbali wanaoshuka pwani kila siku. Kutokana na utendaji wenye bidii wa kikundi hicho cha wahubiri, mabaharia kadhaa, kutia ndani nahodha mmoja, ofisa mmoja wa mabaharia, na mtu mmoja ambaye zamani alikuwa mlinzi wa kibinafsi, wote wamekubali kweli. Sasa wao pia wanaeneza habari njema za Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote.—Mathayo 24:14.

Kama ilivyo katika sehemu nyinginezo za ulimwengu, Mashahidi wa Yehova nchini Uholanzi wameazimia kutimiza fungu lao la kutangaza habari njema idumuyo milele kwa kila taifa, kabila, lugha, na watu.—Ufunuo 14:6.