Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waovu Wataendelea Hata Lini?

Waovu Wataendelea Hata Lini?

Waovu Wataendelea Hata Lini?

“Mbona . . . [Yehova unanyamaza] kimya, hapo mtu mwovu ammezapo mtu aliye mwenye haki kuliko yeye?”—HABAKUKI 1:13.

1. Ni wakati gani dunia itakapojazwa kabisa maarifa ya utukufu wa Yehova?

JE, MUNGU atapata kuwaharibu waovu? Ikiwa ndivyo, tutasubiri hata lini? Watu ulimwenguni kote huuliza maswali hayo. Twaweza kuyapata wapi majibu? Twaweza kuyapata katika maneno ya kiunabii yaliyopuliziwa na Mungu yanayohusu wakati wake uliowekwa rasmi. Yanatuhakikishia kwamba hivi karibuni Yehova atatekeleza hukumu dhidi ya waovu wote. Ndipo tu dunia ‘itakapojazwa kabisa maarifa ya utukufu wa BWANA, kama maji yaifunikavyo bahari.’ Hiyo ndiyo ahadi ya kiunabii ipatikanayo katika Neno Takatifu la Mungu kwenye Habakuki 2:14.

2. Kitabu cha Habakuki kina hukumu gani tatu za Mungu za kufisha?

2 Kitabu cha Habakuki, kilichoandikwa wapata mwaka wa 628 K.W.K., kina hukumu tatu za kufisha za Yehova Mungu. Tayari hukumu mbili kati ya hizo zimetekelezwa. Ya kwanza ilikuwa hukumu ya Yehova dhidi ya taifa potovu la Yuda la kale. Na ya pili je? Ilikuwa hukumu ya Mungu dhidi ya Babiloni lenye kuonea. Basi, kwa hakika tuna kila sababu ya kuwa na uhakika kwamba hukumu ya tatu kati ya hukumu hizo za Mungu itatekelezwa. Kwa hakika, twaweza kutarajia itimizwe karibuni sana. Mungu atawaharibu wanadamu wote waovu kwa faida ya wale walio wanyofu katika siku hizi za mwisho. Wa mwisho kati yao atakufa kwenye “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote” inayokaribia haraka.—Ufunuo 16:14, 16.

3. Ni nini ambacho kwa hakika kitawapata waovu katika wakati wetu?

3 Vita ya siku kubwa ya Mungu yazidi kukaribia. Na hukumu ya Mungu dhidi ya waovu katika wakati wetu kwa hakika itatekelezwa kama vile hukumu za Yehova dhidi ya Yuda na Babiloni zilivyotimizwa. Hata hivyo, mbona tusiwazie sasa hivi kwamba tuko Yuda wakati wa Habakuki? Ni nini kinachoendelea katika nchi hiyo?

Nchi Yavurugika

4. Habakuki asikia habari ipi yenye kushtua?

4 Ebu wazia kwamba Habakuki, nabii wa Yehova, ameketi kwenye paa tambarare ya nyumba yake, akipunga hewa baridi ya jioni. Kuna ala ya muziki kando yake. (Habakuki 1:1; 3:19, maandishi ya mwisho katika NW) Lakini Habakuki asikia habari yenye kushtua. Mfalme Yehoyakimu wa Yuda amemwua Uria na ametupa maiti yake katika makaburi ya watu wasio na cheo. (Yeremia 26:23) Ni kweli kwamba Uria hakudumisha tumaini lake kwa Yehova bali alishikwa na hofu na kutorokea Misri. Lakini, Habakuki anajua kwamba ujeuri wa Yehoyakimu haukuchochewa na tamaa yoyote ya kutetea heshima ya Yehova. Jambo hilo ni dhahiri kwa sababu mfalme amepuuza kabisa sheria ya Mungu na amechukia nabii Yeremia pamoja na wengine wanaomtumikia Yehova.

5. Hali ya kiroho ikoje katika Yuda, na Habakuki aitikiaje?

5 Habakuki aona moshi wa uvumba ukifukiza kutoka kwenye paa za nyumba zilizo karibu. Watu hao hawachomi uvumba wakiwa waabudu wa Yehova. Wanafanya matendo ya dini isiyo ya kweli yanayoungwa mkono na Mfalme mwovu wa Yuda, Yehoyakimu. Ni aibu iliyoje! Habakuki atokwa machozi, naye aomba hivi: “Ee BWANA, nilie hata lini, wewe usitake kusikia? Nakulilia kwa sababu ya udhalimu, ila hutaki kuokoa. Mbona wanionyesha uovu, na kunitazamisha ukaidi? Maana uharibifu na udhalimu u mbele yangu; kuna ugomvi, na mashindano yatokea. Kwa sababu hiyo sheria imelegea, wala hukumu haipatikani; kwa maana watu wabaya huwazunguka wenye haki; kwa sababu hiyo hukumu ikipatikana imepotoka.”—Habakuki 1:2-4.

6. Sheria na haki zikoje katika Yuda?

6 Naam, uharibifu na udhalimu vimeenea sana. Kila mahali atazamapo Habakuki, aona ukaidi, ugomvi na mashindano. “Sheria imelegea,” haitekelezwi. Nayo haki? “Haipatikani” kamwe! Haishindi kamwe. Badala yake, “watu wabaya huwazunguka wenye haki,” wakizuia hatua za kisheria zinazokusudiwa kuwalinda wasio na hatia. Kwa kweli, “hukumu ikipatikana imepotoka.” Imepotoshwa. Ni hali mbaya kama nini!

7. Habakuki ameazimia kufanya nini?

7 Habakuki atua na kufikiria hali hiyo. Je, atakata tamaa? La hasha! Baada ya kujikumbusha kunyanyaswa kwote kwa watumishi waaminifu wa Mungu, mwanamume huyo mwaminifu-mshikamanifu aazimia tena kuendelea kuwa imara, thabiti akiwa nabii wa Yehova. Habakuki ataendelea kutangaza ujumbe wa Mungu—hata ikiwa kufanya hivyo kutamaanisha kifo.

Yehova Atenda “Tendo” Lisiloaminika

8, 9. Yehova anatenda “tendo” gani lisiloaminika?

8 Katika ono, Habakuki aona watu wa dini isiyo ya kweli, wanaomdharau Mungu. Sikiliza awaambiacho Yehova: “Angalieni, enyi mlio kati ya mataifa, katazameni.” Yaelekea Habakuki hajui ni kwa nini Mungu awaambia watu hao wabaya hivyo. Kisha amsikia Yehova akiwaambia: “Kastaajabuni sana; kwa maana mimi natenda tendo siku zenu, ambalo hamtaliamini hata mkiambiwa.” (Habakuki 1:5) Kwa hakika, Yehova mwenyewe ndiye anayetenda tendo hilo wasiloweza kuamini. Lakini ni tendo gani hilo?

9 Habakuki asikiliza kwa makini maneno ya Mungu yanayofuata, yaliyorekodiwa kwenye Habakuki 1:6-11. Huu ni ujumbe wa Yehova—wala hakuna mungu asiye wa kweli wala sanamu isiyo na uhai iwezayo kuuzuia usitimizwe: “Kwa maana, angalieni, nawaondokesha Wakaldayo, taifa lile kali, lenye haraka kupita kiasi; wapitao katikati ya dunia, ili wayamiliki makao yasiyo yao. Hao ni watu wa kutisha sana, wa kuogofya sana; hukumu yao na ukuu wao hutoka katika nafsi zao wenyewe. Farasi zao ni wepesi kuliko chui, ni wakali kuliko mbwa-mwitu wa jioni; na wapanda farasi wao hujitapa naam, wapanda farasi wao watoka mbali sana; huruka kama tai afanyaye haraka ale. Waja wote ili kufanya udhalimu; nyuso zao zimeelekezwa kwa bidii yao kama upepo wa mashariki, nao hukusanya mateka kama mchanga. Naam, huwadhihaki wafalme, na wakuu ni kitu cha kudharauliwa kwake; huidharau kila ngome; kwa maana hufanya chungu ya mavumbi, na kuitwaa. Kisha atapita kwa kasi, kama upepo, atapita na kuwa ana hatia; yeye ambaye nguvu zake ni mungu wake.”

10. Yehova awaondokesha akina nani?

10 Ni onyo la kiunabii lililoje kutoka kwa Aliye Juu Zaidi! Yehova awaondokesha Wakaldayo, taifa kali la Babiloni. Lipitapo “katikati ya dunia,” litayashinda makao mengi sana. Ni jambo lenye kuogofya kama nini! Jeshi la Wakaldayo ni lenye ‘kutisha sana na lenye kuogofya sana.’ Hilo hujitungia sheria zisizobadilika. ‘Hukumu yao hutoka katika nafsi zao wenyewe.’

11. Ungefafanuaje kuja kwa majeshi ya Babiloni dhidi ya Yuda?

11 Farasi za Babiloni ni wepesi kuliko chui wenye kasi. Jeshi lake la wapanda-farasi ni kali kuliko mbwa-mwitu wenye njaa wawindao usiku. Likiwa na hamu kubwa ya kwenda, ‘huitapa ardhi’ kwa kukosa subira. Tokea Babiloni lililo mbali waelekea Yuda. Hivi karibuni Wakaldayo watayavamia mawindo yao, wakiruka kama tai afanyaye haraka akale mlo mtamu. Je, huo ni uvamizi tu, uporaji ufanywao na askari wachache tu? La! “Waja wote ili kufanya udhalimu,” kama vile jeshi kubwa mno likusanyikavyo ili kuharibu. Nyuso zao zikiwa zimeelekezwa kwa bidii, wapanda-farasi waelekea Yuda na Yerusalemu, wakisonga kasi kama upepo wa mashariki. Majeshi ya Babiloni yateka wafungwa wengi hivi kwamba ni kana kwamba ‘wanakusanya mateka kama mchanga.’

12. Wababiloni wana mtazamo gani, na adui huyo mwenye nguvu sana ‘anakuwa na hatia’ ya nini?

12 Jeshi la Wakaldayo lawacheka wafalme na kuwadhihaki maofisa wakuu, ambao wote hawana nguvu za kukomesha mashambulizi yake makali. “Huidharau kila ngome,” kwa kuwa ngome yoyote ile huanguka Wababiloni ‘wafanyapo chungu ya mavumbi’ na kuishambulia toka hapo. Wakati uliowekwa rasmi wa Yehova ufikapo, adui huyo mwenye kutisha ‘atapita kwa kasi kama upepo.’ Katika kushambulia Yuda na Yerusalemu, ‘atakuwa na hatia’ ya kuwadhuru watu wa Mungu. Baada ya ushindi wa kasi, kamanda Mkaldayo atajivuna hivi: ‘Nguvu zetu ni mungu wetu.’ Lakini amekosea kama nini!

Msingi Mzuri wa Tumaini

13. Kwa nini Habakuki amejawa na tumaini na uhakika?

13 Moyo wa Habakuki wazidi kuwa na tumaini apatapo kuelewa vizuri zaidi kusudi la Yehova. Akiwa na uhakika kamili, asema kwa kumheshimu sana Yehova. Kama inavyotaarifiwa katika Habakuki 1:12, nabii huyo asema hivi: “Ee BWANA, Mungu wangu, mtakatifu wangu, wewe si wa milele? [“usiyekufa,” Biblia Habari Njema].” Kwa kweli Yehova ni Mungu wa “tangu milele hata milele.”—Zaburi 90:1, 2.

14. Waasi wa Yuda wamefuatia mwendo gani?

14 Akirejezea ono alilopewa na Mungu na kushangilia ufahamu wenye kina ulioandaliwa, nabii huyo aongeza kusema hivi: “Ee BWANA, umemwandikia hukumu, nawe, Ee Jabali, umemweka imara ili aadhibishwe.” Mungu amewahukumu vikali waasi wa Yuda, nao watakaripiwa, watatiwa adabu vikali na Yehova. Walipaswa kumtegemea akiwa Jabali lao, ngome yao, kimbilio lao, na Chanzo chao pekee cha wokovu halisi. (Zaburi 62:7; 94:22; 95:1) Hata hivyo, viongozi wa Yuda walioasi hawamkaribii Mungu, nao waendelea kuwaonea waabudu wake wasiodhuru.

15. Ni katika maana gani Yehova ‘ana macho safi hata asiweze kuangalia uovu’?

15 Hali hiyo yamsononesha sana nabii wa Yehova. Kwa hiyo, yeye asema hivi: “Wewe uliye na macho safi hata usiweze kuangalia uovu, wewe usiyeweza kutazama ukaidi.” (Habakuki 1:13) Naam, Yehova ‘ana macho safi hata asiweze kuangalia uovu,’ yaani, kuuvumilia ukosaji.

16. Unaweza kufafanuaje kwa ufupi mambo yaliyorekodiwa kwenye Habakuki 1:13-17?

16 Kwa hiyo, Habakuki ana maswali kadhaa yenye kuchochea fikira. Yeye auliza hivi: “Mbona unawaangalia watendao kwa hila; na kunyamaza kimya, hapo mtu mwovu ammezapo mtu aliye mwenye haki kuliko yeye; na kufanya wanadamu kuwa kama samaki wa baharini, kama vitu vitambaavyo, ambavyo havina mtawala? Yeye huwatoa wote kwa ndoana yake, huwakamata katika wavu wake, na kuwakusanya katika juya lake; ndiyo sababu afurahi na kupendezwa. Kwa sababu hiyo huutolea wavu wake sadaka, na kulifukizia uvumba juya lake; kwa sababu kwa vitu vile fungu lake limenona, na chakula chake kimekuwa tele. Je! atawatoa walio katika wavu wake, asiache kuwaua watu wa mataifa daima?”—Habakuki 1:13-17.

17. (a) Kwa kushambulia Yuda na Yerusalemu, Wababiloni wanatimizaje kusudi la Mungu? (b) Yehova atamfunulia Habakuki nini?

17 Katika kushambulia Yuda na jiji lake kuu, Yerusalemu, Wababiloni watatenda kulingana na tamaa zao wenyewe. Hawatajua kwamba wanatumiwa na Mungu kutekeleza hukumu yake ya haki dhidi ya watu wasio waaminifu. Ni rahisi kuona ni kwa nini ingekuwa vigumu kwa Habakuki kuelewa kwamba Mungu angewatumia Wababiloni waovu ili kutekeleza hukumu Yake. Wakaldayo hao wakatili si waabudu wa Yehova. Wao huwaona wanadamu kama ‘samaki na vitu vitambaavyo’ tu vinavyostahili kukamatwa na kutiishwa. Lakini mambo hayo hayatamshangaza Habakuki kwa muda mrefu. Hivi karibuni Yehova atamfunulia nabii wake kwamba Wababiloni hawatakosa kuadhibiwa kwa sababu ya utekaji-nyara wao wenye pupa na hatia yao ya kumwaga damu ovyoovyo.—Habakuki 2:8.

Tayari kwa Maneno Zaidi ya Yehova

18. Twaweza kujifunza nini kutokana na mtazamo wa Habakuki, kama uonyeshwavyo katika Habakuki 2:1?

18 Hata hivyo, sasa hivi Habakuki asubiri kusikia maneno ambayo Yehova afuatia kumwambia. Nabii huyo asema hivi kwa ujasiri: “Mimi nitasimama katika zamu yangu, nitajiweka juu ya mnara, nitaangalia ili nione atakaloniambia, na jinsi nitakavyojibu katika habari ya kulalamika kwangu.” (Habakuki 2:1) Habakuki angali anapendezwa sana na mambo ambayo Mungu bado atasema kwa kumtumia akiwa nabii. Imani katika Yehova akiwa Mungu ambaye havumilii uovu humfanya atake kujua ni kwa nini uovu umeenea sana, lakini yuko tayari kuruhusu maoni yake yarekebishwe. Hivyo basi, namna gani sisi? Tunapojiuliza ni kwa nini maovu fulani yanavumiliwa, uhakika wetu katika uadilifu wa Yehova Mungu wapaswa kutusaidia kudumisha usawaziko wetu na kuendelea kumngojea.—Zaburi 42:5, 11.

19. Kama tu Mungu alivyomwambia Habakuki, ni nini kilichowapata Wayahudi waliopotoka?

19 Kama tu alivyomwambia Habakuki, Mungu alitekeleza hukumu dhidi ya taifa potovu la Wayahudi kwa kuwaruhusu Wababiloni washambulie Yuda. Katika mwaka wa 607 K.W.K., waliharibu Yerusalemu na hekalu lake, wakaua wazee kwa wachanga, na kutwaa mateka wengi. (2 Mambo ya Nyakati 36:17-20) Baada ya uhamisho wa muda mrefu huko Babiloni, mabaki wa Wayahudi waaminifu walirudi nyumbani kwao na hatimaye wakajenga upya hekalu. Hata hivyo, baadaye Wayahudi walikosa tena uaminifu kwa Yehova—hasa walipomkataa Yesu akiwa Mesiya.

20. Paulo alitumiaje Habakuki 1:5 kuhusu kukataliwa kwa Yesu?

20 Kulingana na Matendo 13:38-41, mtume Paulo aliwaonyesha Wayahudi katika Antiokia matokeo ya kumkataa Yesu na hivyo kupuuza dhabihu yake ya fidia. Akinukuu Habakuki 1:5 kutoka katika tafsiri ya Septuagint ya Kigiriki, Paulo alionya hivi: “Hakikisheni kwamba lile lisemwalo katika Manabii haliji juu yenu, ‘Ioneni, nyinyi wenye kudharau, mwistaajabie, na mtoweke, kwa sababu mimi ninafanya kazi katika siku zenu, kazi ambayo nyinyi hamtaiamini kwa vyovyote hata ikiwa yeyote awasimulia kirefu.’” Kulingana na nukuu la Paulo, utimizo wa pili wa Habakuki 1:5 ulitukia wakati majeshi ya Roma yalipoharibu Yerusalemu na hekalu lake mwaka wa 70 W.K.

21. Wayahudi wa wakati wa Habakuki waliionaje “kazi” ya Mungu ya kufanya Wababiloni waharibu Yerusalemu?

21 Kwa Wayahudi walioishi wakati wa Habakuki, “kazi” ya Mungu ya kufanya Wababiloni waharibu Yerusalemu haikuwazika kwa sababu jiji hilo lilikuwa kituo cha ibada ya Yehova na mahali ambapo mfalme mtiwa-mafuta alitawazwa. (Zaburi 132:11-18) Kwa hiyo, Yerusalemu halikuwa limewahi kuharibiwa awali. Hekalu lake halikuwa limewahi kuchomwa. Nyumba ya kifalme ya Daudi haikuwa imewahi kupinduliwa. Haikuaminika kwamba Yehova angeruhusu mambo hayo yatukie. Lakini kupitia Habakuki, Mungu alitoa onyo la kutosha kwamba matukio hayo yenye kushtua yangetukia. Na historia yathibitisha kwamba yalitukia kama ilivyotabiriwa.

“Kazi” ya Mungu Isiyoaminika Wakati Wetu

22. “Kazi” isiyoaminika ya Yehova itahusisha nini wakati wetu?

22 Je, Yehova atatekeleza “kazi” isiyoaminika wakati wetu? Uwe na hakika kwamba atafanya hivyo, hata ingawa watu wenye kushuku huenda walione kuwa jambo lisiloaminika. Wakati huu, kazi isiyoaminika ya Yehova itakuwa kuharibu Jumuiya ya Wakristo. Kama vile Yuda la kale, hiyo yadai kumwabudu Mungu lakini imefisidika sana. Yehova atahakikisha kwamba mfumo wote wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo utafutiliwa mbali hivi karibuni, pamoja na “Babiloni Mkuu” yote, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli.—Ufunuo 18:1-24.

23. Roho ya Mungu ilimchochea Habakuki afuatishe kufanya nini?

23 Yehova alitaka Habakuki afanye kazi nyingi zaidi kabla ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Bado Mungu alikuwa na nini cha kumwambia nabii wake? Habakuki angesikia mambo ambayo yangemchochea atwae chombo chake cha muziki na kumwimbia Yehova sala za maombolezo. Hata hivyo, kwanza roho ya Mungu ingemshurutisha nabii huyo atangaze ole zenye kutokeza. Kwa hakika, tungethamini kupata ufahamu wenye kina juu ya maana ya maneno hayo ya kiunabii kwa ajili ya wakati wa Mungu uliowekwa rasmi. Kwa hiyo, ebu tuusikilize zaidi unabii wa Habakuki.

Je, Wakumbuka?

• Ni hali zipi zilizokuwapo Yuda wakati wa Habakuki?

• Yehova alitenda “tendo” gani lisiloaminika wakati wa Habakuki?

• Habakuki alikuwa na msingi gani wa tumaini?

• Mungu atatekeleza “kazi” gani isiyoaminika wakati wetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Habakuki alijiuliza ni kwa nini Mungu ameruhusu uovu uenee. Je, hata wewe hujiuliza?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Habakuki alitabiri msiba uliopata nchi ya Yuda mikononi mwa Wababiloni

[Picha katika ukurasa wa 10]

Magofu ya Yerusalemu, lililoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K.