Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Hatakawia

Yehova Hatakawia

Yehova Hatakawia

“[Njozi hii] ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia [‘haitachelewa,’ ‘Zaire Swahili Bible’].”—HABAKUKI 2:3.

1. Watu wa Yehova wameonyesha azimio gani, nalo limewachochea kufanya nini?

“MIMI nitasimama katika zamu yangu [‘mahali pangu pa ulinzi,’ NW].” Ndivyo Habakuki, nabii wa Mungu, alivyoazimia kufanya. (Habakuki 2:1) Watu wa Yehova wa karne ya 20 wameonyesha azimio hilohilo. Kwa hiyo, wameitikia kwa bidii mwito uliotolewa katika mkusanyiko wa pekee Septemba 1922: “Hii ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme atawala! Nyinyi ni mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo, tangazeni, tangazeni, tangazeni, Mfalme na ufalme wake.”

2. Waliporudishwa kwenye utendaji mwingi baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Wakristo watiwa-mafuta wangeweza kutangaza nini?

2 Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Yehova alirudisha mabaki watiwa-mafuta waaminifu katika hali ya utendaji mwingi. Kama Habakuki, basi kila mmoja wao angeweza kutangaza: “Nitajiweka juu ya mnara, nitaangalia [‘nitalinda,’ NW] ili nione atakaloniambia.” Maneno ya Kiebrania yanayotafsiriwa “-linda” na ‘mlinzi’ yamerudiwa-rudiwa katika unabii mwingi.

‘Haitachelewa’

3. Kwa nini ni lazima tufulize kulinda?

3 Mashahidi wa Yehova watoapo onyo la Mungu leo, ni lazima wawe macho sikuzote kutii maneno ya mwisho ya unabii mkuu wa Yesu: “Fulizeni kulinda, kwa maana nyinyi hamjui ni wakati gani bwana-mkubwa wa nyumba anakuja, kama ni wakati wa jioni-jioni au katikati ya usiku au awikapo jogoo au mapema asubuhi; ili awasilipo kwa ghafula, asiwakute nyinyi mkiwa mmelala usingizi. Lakini lile niwaambialo nyinyi nawaambia wote, Fulizeni kulinda.” (Marko 13:35-37) Kama Habakuki, na kwa kupatana na maneno ya Yesu, lazima tufulize kulinda!

4. Hali yetu inafananaje na ile ya Habakuki wapata mwaka wa 628 K.W.K.?

4 Yaelekea Habakuki alimaliza kuandika kitabu chake wapata mwaka wa 628 K.W.K., hata kabla ya Babiloni kuwa serikali kubwa ya ulimwengu. Hukumu ya Yehova dhidi ya Yerusalemu lililoasi ilikuwa imetangazwa kwa miaka mingi. Hata hivyo, haikujulikana waziwazi hukumu hiyo ingetekelezwa lini. Ni nani angeweza kuamini kwamba ilikuwa imesalia miaka 21 tu na kwamba Yehova angetumia Babiloni kutekeleza hukumu hiyo? Hali kadhalika leo, hatujui ‘siku na saa’ ya mwisho wa mfumo huu, lakini Yesu ametuonya kimbele: “Jithibitisheni wenyewe kuwa tayari, kwa sababu kwenye saa msiyoifikiri kuwa hiyo, Mwana wa binadamu anakuja.”—Mathayo 24:36, 44.

5. Ni jambo gani ambalo hasa linatia moyo kuhusu maneno ya Mungu yaliyorekodiwa kwenye Habakuki 2:2, 3?

5 Akiwa na sababu nzuri, Yehova alimpa Habakuki utume huu wenye kuchochea: “Iandike njozi ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili aisomaye apate kuisoma kama maji. Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia [‘haitachelewa,’ ZSB].” (Habakuki 2:2, 3) Leo, uovu na ujeuri umeenea kotekote duniani, jambo linaloonyesha kwamba twasimama katika ukingo wenyewe wa “siku ya BWANA iliyo kuu na itishayo.” (Yoeli 2:31) Maneno yenye kutoa uhakikisho ya Yehova mwenyewe yanatia moyo kama nini: ‘Haitachelewa’!

6. Tunaweza kuokokaje siku ijayo ya kutekelezwa kwa hukumu?

6 Basi, twaweza kuokokaje siku hiyo inayokuja ya kutekelezwa kwa hukumu? Yehova ajibu kwa kuonyesha tofauti kati ya wenye haki na wasio haki: “Tazama, roho yake hujivuna, haina unyofu ndani yake; lakini mwenye haki ataishi kwa imani yake.” (Habakuki 2:4) Watu na watawala wenye kiburi na pupa wameitia mawaa historia ya kisasa kwa damu ya mamilioni ya watu wasio na hatia, hasa katika vita viwili vya ulimwengu na katika uchinjaji wa kikabila. Tofauti nao, watumishi wa Mungu watiwa-mafuta ambao ni wapenda-amani wamevumilia kwa uaminifu. Wao ni “taifa lenye haki, lishikalo kweli.” Taifa hilo, pamoja na waandamani wake, “kondoo wengine,” hutii onyo hili la upole: “Mtumainini BWANA siku zote maana BWANA YEHOVA ni mwamba wa milele.”—Isaya 26:2-4; Yohana 10:16.

7. Kupatana na jinsi Paulo alivyotumia Habakuki 2:4, ni lazima tufanye nini?

7 Akiwaandikia Waebrania, mtume Paulo alinukuu Habakuki 2:4 alipowaambia watu wa Yehova hivi: “Mna uhitaji wa uvumilivu, ili kwamba, baada ya nyinyi kuwa mmefanya mapenzi ya Mungu, mpate kupokea utimizo wa ahadi. Kwa maana bado ‘muda kidogo sana,’ na ‘yeye anayekuja atawasili na hatakawia.’ ‘Lakini mwadilifu wangu ataishi kwa sababu ya imani,’ na, ‘ikiwa yeye ajikunyata, nafsi yangu haina upendezi katika yeye.’” (Waebrania 10:36-38) Siku zetu si wakati wa kulegeza mikono au kunaswa na njia za ulimwengu wa Shetani za kufuatia vitu vya kimwili na kichaa cha anasa. Tufanye nini hadi ule “muda kidogo sana” uishe? Kama Paulo, sisi tulio watu wa taifa takatifu la Yehova lazima ‘tujinyooshe mbele kwenye mambo ya mbele, tukifuatilia sana kuuelekea mradi’ wa uhai udumuo milele. (Wafilipi 3:13, 14) Kama Yesu, lazima ‘tuvumilie kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yetu.’—Waebrania 12:2.

8. Ni nani yule “mtu” anayetajwa kwenye Habakuki 2:5, na kwa nini hatafanikiwa?

8 Habakuki 2:5 humfafanua “mtu” ambaye, tofauti na watumishi wa Yehova, hushindwa kuufikia mradi wake, hata ingawa yeye “huongeza tamaa yake kama kuzimu [‘sheoli,’ NW].” Mtu huyo ‘asiyeweza kushibishwa’ ni nani? Akiwa na ulafi kama Babiloni la wakati wa Habakuki, “mtu” huyo ambaye ni serikali za kisiasa—ziwe za Kifashisti, Kinazi, Kikomunisti, au hata zile ziitwazo eti za Kidemokrasia—hupiga vita ili kupanua maeneo yake. Pia yeye hujaza nafsi zisizo na hatia Sheoli, au kaburini. Lakini “mtu” huyo haini wa ulimwengu wa Shetani, ambaye kujiona kwake kuwa wa maana kumemlewesha, hafanikiwi hata kidogo katika kujaribu ‘kukusanya mataifa yote na kujiwekea kabila zote chungu chungu.’ Yehova Mungu tu ndiye awezaye kuwaunganisha wanadamu wote, naye atafanya hivyo kupitia Ufalme wa Kimesiya.—Mathayo 6:9, 10.

Wa Kwanza Kati ya Ole Tano Wenye Kutazamisha

9, 10. (a) Yehova aanza kutangaza nini kupitia Habakuki? (b) Kuhusu mapato yasiyo ya haki, hali ikoje leo?

9 Kupitia nabii wake Habakuki, Yehova aanza kutangaza mfululizo wa ole tano, hukumu ambazo lazima zitimizwe ili kutayarisha dunia ikaliwe na waabudu waaminifu wa Mungu. Watu hao wenye mioyo mizuri ‘hupiga mfano juu yake wakisema’ kwamba Yehova hutokeza. Twasoma hivi kwenye Habakuki 2:6: “Ole wake yeye aongezaye kisicho mali yake! hata lini? na ole wake yeye ajitwikaye mzigo wa rehani!”

10 Mapato yasiyo ya haki ndiyo yanayokaziwa hapa. Katika ulimwengu unaotuzunguka, matajiri huzidi kutajirika, nao maskini huzidi kuwa maskini. Wanaouza dawa za kulevya na walaghai hujikusanyia mali nyingi, huku watu wa kawaida wakifa njaa. Yasemekana kwamba robo moja ya wakazi wa ulimwengu wanaishi katika umaskini. Hali za maisha zafadhaisha katika nchi nyingi. Wanaotamani haki duniani hulia hivi: Maovu haya yataendelea kuongezeka “hata lini”! Hata hivyo, mwisho u karibu! Hakika, njozi hiyo ‘haitachelewa.’

11. Habakuki asema nini kuhusu kumwaga damu ya wanadamu, na kwa nini twaweza kusema kwamba kuna hatia kubwa ya damu duniani leo?

11 Nabii huyo amwambia mwovu hivi: “Kwa sababu umeteka nyara mataifa mengi, mabaki yote ya kabila watakuteka wewe; kwa sababu ya damu ya watu, na kwa sababu ya udhalimu iliotendwa nchi hii, na mji huu, na watu wote wanaokaa ndani yake.” (Habakuki 2:8) Leo duniani kuna hatia ya damu iliyoje! Yesu alitaarifu waziwazi hivi: “Wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Hata hivyo, katika karne hii ya 20 pekee, mataifa na vikundi vya kikabila vyenye hatia ya damu vimehusika katika uchinjaji wa zaidi ya wanadamu milioni mia moja. Ole wao wanaoshiriki katika uchinjaji huo!

Ole wa Pili

12. Ni nini ole wa pili uliorekodiwa kwenye Habakuki, na twawezaje kuwa na hakika kwamba utajiri usio wa haki hautasaidia?

12 Ole wa pili, ambao umerekodiwa kwenye Habakuki 2:9-11 humpata “aipatiaye nyumba yake mapato mabaya, ili apate kukiweka kioto chake juu, apate kujiepusha na mkono wa uovu!” Mapato yasiyo ya haki hayataleta faida yoyote, kama vile mtunga-zaburi aonyeshavyo waziwazi: “Usiogope mtu atakapopata utajiri, na fahari ya nyumba yake itakapozidi. Maana atakapokufa hatachukua cho chote; utukufu wake hautashuka ukimfuata.” (Zaburi 49:16, 17) Basi, shauri lenye hekima la mtume Paulo lafaa: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo uliopo wasiwe wenye kunia ya juu, na waweke tumaini lao, si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu, ambaye hututolea sisi vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu.”—1 Timotheo 6:17.

13. Kwa nini twapaswa kuendelea kutoa onyo la Mungu?

13 Ni jambo la maana kama nini kwamba ujumbe wa hukumu wa Mungu utangazwe leo! Mafarisayo walipopinga umati usimsifu Yesu kuwa “Yule anayekuja akiwa ndiye Mfalme katika jina la Yehova,” alijibu hivi: “Mimi nawaambia nyinyi, kama hawa wangekaa kimya, mawe yangepaaza kilio.” (Luka 19:38-40) Hali kadhalika, watu wa Mungu leo wasipoufichua uovu ulio ulimwenguni, “jiwe litapiga kelele katika ukuta.” (Habakuki 2:11) Basi na tuendelee kutoa onyo la Mungu kwa moyo mkuu!

Ole wa Tatu na Suala la Hatia ya Damu

14. Dini za ulimwengu zimesababisha umwagikaji upi wa damu?

14 Ole wa tatu uliotangazwa kupitia Habakuki wahusu suala la hatia ya damu. Andiko la Habakuki 2:12 lasema: “Ole wake yeye ajengaye mji kwa damu, awekaye imara mji mkubwa kwa uovu!” Katika mfumo huu wa mambo, mara nyingi ukosefu wa haki na umwagaji wa damu hutukia pamoja. Ni dhahiri kwamba dini za ulimwengu zimehusika katika umwagaji wa damu wenye kuchukiza sana katika historia. Twahitaji tu kutaja zile Krusedi, zilizowahusisha waitwao eti Wakristo dhidi ya Waislamu; lile Baraza la Kuhukumu Wazushi la Katoliki huko Hispania na Amerika ya Latini; ile Vita ya Miaka Thelathini ya Ulaya, kati ya Waprotestanti na Wakatoliki; na vita zilizomwaga damu kuliko nyingine zote, zile vita mbili za ulimwengu za karne yetu, ambazo zote mbili zilianzia katika milki ya Jumuiya ya Wakristo.

15. (a) Mataifa yanaendelea kufanya nini wakiungwa mkono na kanisa au kwa kupata kibali chake? (b) Je, Umoja wa Mataifa unaweza kumaliza ongezeko la silaha ulimwenguni?

15 Mojawapo ya mambo maovu zaidi katika vita ya ulimwengu ya pili ni yale maangamizi makubwa ya Nazi, yaliyoangamiza mamilioni ya Wayahudi na watu wengine wasio na hatia huko Ulaya. Viongozi wa Kanisa Katoliki nchini Ufaransa wamekiri hivi majuzi tu kwamba kanisa hilo lilishindwa kupinga kupelekwa kwa mamia ya maelfu ya watu kwenye kambi za kifo za Nazi. Hata hivyo, mataifa yaendelea kujitayarisha kumwaga damu, kanisa likiwaunga mkono au kuwapa kibali. Kuhusu Kanisa Othodoksi la Urusi, hivi majuzi gazeti Time (chapa ya kimataifa) lilitaarifu hivi: “Kanisa lililoanzishwa upya pia lina uvutano mkubwa katika eneo ambalo halikuwazika wakati mmoja: zana za kivita za Urusi. . . . Kubarikiwa kwa ndege za kivita na kambi za kijeshi kumekuwa kama jambo la kawaida. Mwezi wa Novemba, katika Nyumba ya Watawa ya Danilovsky huko Moscow, makao ya Askofu Mkuu wa Urusi, kanisa hata lilifikia hatua ya kutakasa silaha za nyuklia.” Je, Umoja wa Mataifa waweza kuzuia kuongezeka kwa zana za vita za kishetani ulimwenguni? Ni vigumu! Kwa mujibu wa gazeti The Guardian la London, Uingereza, mshindi wa Tuzo la Amani la Nobel alieleza: “Jambo lenye kusikitisha sana ni kwamba wale washiriki watano wa kudumu wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ndio wauzaji watano wakuu wa silaha ulimwenguni.”

16. Yehova atafanya nini kuhusu mataifa ambayo huchochea vita?

16 Je, Yehova atatekeleza hukumu dhidi ya mataifa ambayo huchochea vita? Habakuki 2:13 lataarifu: “Angalieni; je! jambo hili halikutoka kwa BWANA wa majeshi, kwamba watu wajishughulikie moto, na mataifa wajisumbue kwa ajili ya ubatili?” “BWANA wa majeshi”! Naam, Yehova ana majeshi ya kimalaika huko mbinguni, atakayotumia kukomesha watu na mataifa yapendayo vita!

17. Ujuzi wa Yehova utaijaza dunia kwa kadiri gani baada ya kutekelezwa kwa hukumu yake dhidi ya vikundi vya mataifa vyenye jeuri?

17 Ni nini kitakachofuata kutekelezwa kwa hukumu ya Yehova dhidi ya vikundi hivyo vya mataifa vyenye jeuri? Habakuki 2:14 hujibu: “Dunia itajazwa maarifa ya utukufu wa BWANA, kama maji yaifunikavyo bahari.” Ni tazamio tukufu kama nini! Kwenye Har–Magedoni, enzi kuu ya Yehova itatetewa milele. (Ufunuo 16:16) Anatuhakikishia kwamba ‘atapatukuza mahali pa miguu yake,’ dunia hii tunamoishi. (Isaya 60:13) Wanadamu wote wataelimishwa katika njia ya Mungu ya uhai, ili ujuzi wao juu ya makusudi matukufu ya Yehova uwe kama maji yaifunikavyo bahari.

Ole wa Nne na wa Tano

18. Ni upi ole wa nne unaotangazwa kupitia Habakuki, nao wadhihirishwaje katika hali ya maadili ya ulimwengu leo?

18 Ole wa nne wafafanuliwa kwenye Habakuki 2:15 kwa maneno haya: “Ole wake yeye ampaye jirani yake kiko, wewe utiaye sumu yako, na kumlevya pia, ili kuutazama uchi wao!” Hilo ladokeza hali ya ufisadi na upotovu wa ulimwengu wa leo. Ukosefu wake wa adili, unaoungwa mkono na dini zenye uendekevu, umekuwa mbaya hata zaidi. Magonjwa yenye kuenea, kama vile UKIMWI na magonjwa mengine ya kingono, yameongezeka sana duniani kote. Badala ya kudhihirisha ‘utukufu wa BWANA,’ kizazi cha leo cha mimi-kwanza kimetumbukia katika upotovu zaidi na kuelekea kwenye kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu. Ulimwengu huu mhalifu, ambao “umejaa aibu badala ya utukufu,” wakaribia kunywa kutoka katika bakuli la hasira kali ya Yehova, linalowakilisha mapenzi yake kuuelekea. ‘Aibu kuu itakuwa juu ya utukufu wake.’—Habakuki 2:16.

19. Utangulizi wa ole wa tano uliotangazwa na Habakuki wahusiana na jambo gani, na kwa nini maneno hayo yana umuhimu katika ulimwengu wa leo?

19 Kabla ya ole wa tano, maonyo makali yatolewa dhidi ya kuabudu sanamu za kuchongwa. Yehova amtumia nabii huyo atangaze maneno haya yenye nguvu: “Ole wake yeye auambiaye mti, Amka; aliambiaye jiwe lisiloweza kusema, Ondoka! Je! kitu hicho kitafundisha? Tazama, kimefunikwa kwa dhahabu na fedha, wala hamna pumzi ndani yake kabisa.” (Habakuki 2:19) Hadi leo, Jumuiya ya Wakristo na wale waitwao eti jumuiya ya wapagani husujudia misalaba, sanamu za Bikira Maria, sanamu, na mifano mingine yao ya binadamu na wanyama. Yehova ajapo kutekeleza hukumu, hakuna chochote cha vitu hivyo kiwezacho kuamka na kuokoa watu wanaokiabudu. Mitandazo yao ya dhahabu na fedha yafifia na kutokuwa na maana yoyote ilinganishwapo na utukufu wa Mungu wa milele, Yehova, na utukufu wa uumbaji wake ulio hai. Na tulihimidi milele jina lake lisilo na kifani!

20. Tumependelewa kutumikia kwa shangwe katika mpango upi wa hekalu?

20 Naam, Mungu wetu, Yehova, astahili sifa zote. Tukimstahi sana, acheni tutii onyo hilo kali dhidi ya ibada ya sanamu. Lakini sikilizeni! Yehova angali anaongea: “Lakini BWANA yumo ndani ya hekalu lake takatifu; dunia yote na inyamaze kimya mbele zake.” (Habakuki 2:20) Bila shaka nabii huyo alikuwa akirejezea hekalu la Yerusalemu. Hata hivyo, sisi leo tuna pendeleo la kuabudu katika mpango wa hekalu la kiroho lililo tukufu zaidi, ambamo Bwana wetu Yesu Kristo amewekwa kuwa Kuhani wa Cheo cha Juu. Hapa, katika nyua za kidunia za hekalu hilo, sisi hukutana, hutumikia, na kusali, tukimtolea Yehova heshima istahiliyo jina lake tukufu. Na tuna shangwe iliyoje kumwabudu Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo!

Je, Wakumbuka?

• Unayaonaje maneno ya Yehova: ‘Haitachelewa’?

• Ole mbalimbali uliotangazwa kupitia Habakuki una umuhimu gani leo?

• Kwa nini twapaswa kuendelea kutoa onyo la Yehova?

• Tuna pendeleo la kutumikia katika ua wa hekalu gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kama Habakuki, watumishi wa wakati huu wa Mungu wanajua kwamba Yehova hatakawia

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unathamini pendeleo la kumwabudu Yehova katika ua wa hekalu lake la kiroho?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 16]

U.S. Army photo