Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una “Akili ya Kristo”?

Je, Una “Akili ya Kristo”?

Je, Una “Akili ya Kristo”?

“Mungu apaye uvumilivu na faraja na awaruhusu . . . mwe na mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu.”—WAROMA 15:5.

1. Yesu aonyeshwaje katika michoro mingi ya Jumuiya ya Wakristo, na kwa nini hiyo si picha ifaayo ya Yesu?

“HAJAWAHI kuonekana akicheka.” Hivyo ndivyo Yesu anavyosemwa katika hati moja inayodai kwa uwongo kuwa iliandikwa na ofisa mmoja wa kale wa Roma. Inasemekana kwamba hati hiyo, ambayo imejulikana kuwa imedumu ikiwa katika hali hiyo tangu karne ya 11, imeshawishi wachoraji wengi. * Katika michoro kadhaa, Yesu aonekana kama mtu mwenye huzuni ambaye hatabasamu hata kidogo. Lakini hiyo si picha ifaayo ya Yesu, ambaye anaonyeshwa katika Gospeli akiwa mtu mchangamfu, mwenye fadhili na hisia za ndani.

2. Tunaweza kusitawishaje “mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu,” na huo utatuandaa kufanya nini?

2 Kwa wazi, ili tumjue Yesu halisi, ni lazima tujaze akili zetu na mioyo yetu ufahamu sahihi juu ya utu wa kweli wa Yesu alipokuwa hapa duniani. Basi ebu tuchunguze masimulizi fulani ya Gospeli yanayotusaidia kufahamu kindani “akili ya Kristo”—yaani hisia zake, maoni yake, mawazo yake, na kusababu kwake. (1 Wakorintho 2:16) Tufanyapo hivyo, ebu tufikirie jinsi tuwezavyo kusitawisha “mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu.” (Waroma 15:5) Kwa kufanya hivyo, tunaweza kujiandaa vizuri maishani na katika shughuli zetu na wengine kufuata kiolezo alichotuwekea.—Yohana 13:15.

Rahisi Kufikiwa

3, 4. (a) Simulizi lililoandikwa kwenye Marko 10:13-16 lilisimuliwa katika mazingira gani? (b) Yesu alifanya nini wanafunzi wake walipojaribu kuwakataza watoto wachanga wasimwendee?

3 Yesu aliwavutia watu. Mara nyingi watu wenye umri na malezi tofauti-tofauti walikuwa huru kumfikia. Ebu fikiria tukio moja lililoandikwa kwenye Marko 10:13-16. Lilitukia mwishoni mwa huduma yake alipokuwa akielekea Yerusalemu kwa mara ya mwisho kukabili kifo chenye maumivu makali.—Marko 10:32-34.

4 Ebu wazia mazingira hayo. Watu wanaanza kuwaleta watoto wao, hata vitoto vichanga, wabarikiwe na Yesu. * Hata hivyo, wanafunzi wanajaribu kuwakataza watoto wasimwendee Yesu. Labda wanafunzi wanafikiri kwamba kwa hakika Yesu hataki kusumbuliwa na watoto katika majuma haya muhimu. Kumbe wamekosea. Yesu atambuapo wanachofanya wanafunzi, hafurahi. Yesu anawaita watoto hao, akisema: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwakomesha.” (Marko 10:14) Kisha anafanya jambo linaloonyesha utu wake ambao kwa kweli ni wenye upendo na huruma. Simulizi hilo linasema: “Akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki.” (Marko 10:16) Kwa wazi watoto hao wamestarehe Yesu awachukuapo mikononi mwake kwa upendo.

5. Simulizi la Marko 10:13-16 latuambia nini juu ya utu wa Yesu?

5 Simulizi hilo fupi latuarifu mengi juu ya utu wa Yesu. Ona kwamba ilikuwa rahisi kumfikia. Ijapokuwa alikuwa na cheo cha juu sana mbinguni, yeye hakuwa mwenye vitisho wala hakushusha hadhi ya wanadamu wasiokamilika. (Yohana 17:5) Je, si jambo muhimu kwamba hata watoto walistarehe wakiwa naye? Hakika hawangeweza kuvutiwa na mtu asiye mchangamfu, asiye na furaha na ambaye hatabasamu wala kucheka kamwe! Watu wenye umri tofauti-tofauti walimfikia Yesu kwa sababu walitambua kwamba yeye ni mchangamfu, mwenye kujali, na walikuwa na hakika kwamba hangewafukuza kamwe.

6. Wazee wanaweza kufanyaje ili wafikiwe kwa urahisi?

6 Tukifikiria simulizi hilo, twaweza kujiuliza, ‘Je, nina akili ya Kristo? Je, ninafikiwa kwa urahisi?’ Katika nyakati hizi za hatari, kondoo za Mungu wanahitaji wachungaji ambao wanafikiwa kwa urahisi, watu ambao ni kama “mahali pa kujificha na upepo.” (Isaya 32:1, 2; 2 Timotheo 3:1) Wazee, mkipendezwa kikweli na kwa moyo na ndugu zenu na kuwa tayari kujitoa kwa niaba yao, wao watatambua kwamba mnawajali. Wataona mnawajali kupitia sura zenu, sauti zenu, na hali zenu zenye fadhili. Uchangamfu wa kweli kama huo na kujali zaweza kutokeza hali zenye utumainifu ambazo wengine, hata watoto, wanaona ikiwa rahisi kuwafikia. Mwanamke mmoja Mkristo ataja kilichomfanya ajieleze kwa mzee fulani: “Alinizungumzia kwa upole na kwa huruma. Kama hangalifanya hivyo, labda nisingalisema jambo lolote. Alinifanya nihisi salama.”

Kuwajali Wengine

7. (a) Yesu alionyeshaje kwamba aliwajali wengine? (b) Huenda ni kwa nini Yesu alimponya kipofu mmoja hatua kwa hatua?

7 Yesu alikuwa mwenye kujali. Alifahamu hisia za wengine. Kuona tu watu wenye taabu kulimgusa moyo sana hivi kwamba alisukumwa kuwaondolea taabu yao. (Mathayo 14:14) Pia alitambua mipaka na mahitaji ya wengine. (Yohana 16:12) Pindi moja, watu walimletea kipofu na kumwomba Yesu amponye. Yesu alimponya macho, lakini akafanya hivyo hatua kwa hatua. Kwanza mtu huyo aliweza kuona tu maumbo—‘yaonekanayo kama miti inayotembea huku na huku.’ Kisha, Yesu akamponya macho kabisa. Kwa nini alimponya mtu huyo hatua kwa hatua? Huenda alifanya hivyo ili kumwezesha mtu huyo ambaye alikuwa amezoea sana giza aweze kustahimili mshtuko wa kuona kwa ghafula ulimwengu mwangavu wenye kutatanisha.—Marko 8:22-26.

8, 9. (a) Ni nini kilichotendeka punde tu baada ya Yesu na wanafunzi wake kuingia katika eneo la Dekapolisi? (b) Fafanua jinsi Yesu alivyomponya mtu aliyekuwa kiziwi.

8 Pia fikiria jambo lililotukia baada ya Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 32 W.K. Yesu na wanafunzi wake walikuwa wameingia katika eneo la Dekapolisi, mashariki mwa Bahari ya Galilaya. Punde si punde umati mkubwa wa watu wakawapata huko, wakamletea Yesu watu wengi waliokuwa wagonjwa na walemavu, akawaponya wote. (Mathayo 15:29, 30) Jambo la kutokeza ni kwamba Yesu alimchukua mtu mmoja kwenye umati ili amwonyeshe kwamba anajali kwelikweli. Mwandikaji wa Gospeli, Marko, ambaye ndiye mwandikaji pekee aliyeandika tukio hili, aripoti yaliyotukia.—Marko 7:31-35.

9 Mtu huyo alikuwa kiziwi na alikuwa na tatizo kubwa la kuongea. Huenda Yesu alitambua wasiwasi au aibu ya mtu huyo. Kisha Yesu akafanya jambo lisilo la kawaida. Alimwondoa mtu huyo kwenye umati, akampeleka faraghani. Kisha Yesu akatumia ishara fulani kumwambia mtu huyo jambo alilokusudia kufanya. “Akaweka vidole vyake ndani ya masikio ya yule mtu na, baada ya kutema mate, akamgusa ulimi wake.” (Marko 7:33) Kisha, Yesu akatazama mbingu na kutweta kwa njia ya sala. Matendo hayo dhahiri yangemwonyesha mtu huyo, ‘Kile ninachotaka kukufanyia chatokana na nguvu ya Mungu.’ Hatimaye Yesu akasema: “Funguka.” (Marko 7:34) Basi, mtu huyo akaweza kusikia tena, akaweza kuzungumza kama kawaida.

10, 11. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunajali hisia za wengine katika kutaniko? katika familia?

10 Yesu aliwajali wengine kama nini! Alifahamu hisia zao, na hisia-mwenzi hiyo ikamfanya atende kwa njia yenye kujali hisia zao. Tukiwa Wakristo, ni vizuri tusitawishe na kuonyesha akili ya Kristo kuhusu jambo hili. Biblia inatuhimiza hivi: “Nyinyi nyote mwe wenye akili zenye kufanana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na shauku ya kidugu, wenye huruma kwa njia ya wororo, wanyenyekevu katika akili.” (1 Petro 3:8) Kwa hakika, hilo lamaanisha tuseme na kutenda katika njia ambazo zinajali hisia za wengine.

11 Kutanikoni, tunaweza kujali hisia za wengine kwa kuwapa adhama, kuwatendea kama vile sisi tungependa kutendewa. (Mathayo 7:12) Hilo lamaanisha kwamba tuwe waangalifu kuhusu yale tusemayo na jinsi tuyasemavyo. (Wakolosai 4:6) Kumbuka kwamba ‘maneno yanenwayo bila kufikiri yanaweza kuchoma kama upanga.’ (Mithali 12:18) Namna gani katika familia? Mume na mke ambao wanapendana kikweli hujali hisia za kila mmoja. (Waefeso 5:33) Wao huepuka maneno makali, uchambuzi wa daima, na kejeli yenye kuumiza—na yote haya yanaweza kuumiza hisia na iwe vigumu kusuluhishwa. Watoto pia wana hisia, na wazazi wenye upendo huzifikiria pia. Rekebisho likihitajiwa, wazazi kama hao hulitoa kwa njia inayozingatia hadhi ya watoto wao na kutowafanya waaibike isivyofaa. * (Wakolosai 3:21) Basi, tukiwajali wengine, twadhihirisha kwamba tuna akili ya Kristo.

Kuwa Tayari Kuwaitibari Wengine

12. Yesu alikuwa na maoni gani halisi na yenye usawaziko juu ya wanafunzi wake?

12 Yesu aliwaona wanafunzi wake kwa njia halisi na yenye usawaziko. Alijua vizuri kwamba hawakuwa wakamilifu. Kwani hata angeweza kusoma mioyo ya wanadamu. (Yohana 2:24, 25) Hata hivyo, yeye hakuona tu kutokamilika kwao bali aliona sifa zao nzuri. Pia aliona mambo ambayo watu hao waliokuwa wamevutwa na Yehova wangeweza kutimiza. (Yohana 6:44) Maoni mazuri ya Yesu juu ya wanafunzi wake yalikuwa dhahiri kwa jinsi alivyowashughulikia na kuwatendea. Jambo moja alilofanya ni kuwa tayari kuwaitibari.

13. Yesu alionyeshaje kwamba aliwaitibari wanafunzi wake?

13 Yesu alionyeshaje itibari hiyo? Alipoondoka duniani, aliwapa wanafunzi wake watiwa-mafuta daraka zito. Aliwapa daraka la kutunza masilahi ya duniani pote ya Ufalme wake. (Mathayo 25:14, 15; Luka 12:42-44) Wakati wa huduma yake, alionyesha hata katika mambo madogo-madogo na kwa njia isiyo ya moja kwa moja kwamba aliwaitibari. Alipoongeza kiasi cha chakula kimuujiza ili kuulisha umati, aliwapa wanafunzi wake daraka la kugawa chakula.—Mathayo 14:15-21; 15:32-37.

14. Ungesimuliaje kwa ufupi simulizi lililoandikwa kwenye Marko 4:35-41?

14 Fikiria pia simulizi lililoandikwa kwenye Marko 4:35-41. Pindi hii Yesu na wanafunzi wake walipanda mashua na kusafiri kuelekea mashariki wakivuka Bahari ya Galilaya. Muda mfupi baada ya kuondoka, Yesu alijilaza kwenye tezi akalala fofofo. Lakini, punde tu “kukatokea dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi.” Dhoruba kama hizo zilikuwa za kawaida katika Bahari ya Galilaya. Kwa kuwa bahari hiyo iko chini sana (meta 200 hivi chini ya usawa wa bahari), hewa ya hapo ni joto sana kuliko hewa ya eneo lililo karibu, na hali hiyo hutokeza msukusuko wa hewa. Isitoshe, pepo zenye nguvu huteremka kwa kasi kwenye Bonde la Yordani kutoka Mlima Hermoni, ulioko upande wa kaskazini. Bahari shwari yaweza kugeuka kwa ghafula kuwa dhoruba kali. Ebu fikiria: Bila shaka Yesu alijua kwamba kuna dhoruba nyingi kwa kuwa alilelewa Galilaya. Lakini, yeye alilala kwa utulivu, akiitibari ustadi wa wanafunzi wake, ambao baadhi yao walikuwa wavuvi.—Mathayo 4:18, 19.

15. Tunaweza kuigaje utayari wa Yesu wa kuitibari wanafunzi wake?

15 Je, tunaweza kuiga utayari wa Yesu wa kuitibari wanafunzi wake? Ni vigumu kwa watu fulani kuwapa wengine madaraka. Ni kana kwamba sikuzote wao tu ndio lazima wafanye mambo hayo. Huenda wakafikiri hivi, ‘Nikitaka jambo lifanywe vizuri, ni lazima nilifanye mwenyewe!’ Lakini kama ni lazima tufanye kila kitu sisi wenyewe, kuna hatari ya kuchoka na labda kutumia isivyo lazima wakati ambao tungetumia na familia zetu. Isitoshe, tusipowapa wengine kazi na madaraka yafaayo, huenda tukawa tunawanyima uzoefu na mazoezi wanayohitaji. Ni vizuri kujifunza kuwaitibari wengine tukiwapa mambo fulani wafanye. Ni vizuri tujiulize hivi kwa unyofu, ‘Je, nina akili ya Kristo kuhusu jambo hili? Je, nawapa wengine kazi fulani-fulani, nikiitibari kwamba watafanya kadiri wawezavyo?’

Alionyesha Kwamba Anawaamini Wanafunzi Wake

16, 17. Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, Yesu aliwapa mitume wake uhakikishio gani, hata ingawa alijua kwamba wangemwacha?

16 Yesu alikuwa na maoni mazuri juu ya wanafunzi wake katika njia nyingine muhimu. Aliwaonyesha kwamba ana uhakika nao. Jambo hilo lilikuwa dhahiri kabisa katika maneno yenye uhakikisho aliyowaambia mitume wake usiku wa mwisho wa maisha yake duniani. Ona jambo lililotukia.

17 Yesu alikuwa na mambo mengi jioni hiyo. Aliwafunza wanafunzi wake somo la unyenyekevu kwa kuwaosha miguu. Baadaye, akaanzisha mlo wa jioni ambao ungekuwa ukumbusho wa kifo chake. Kisha, mitume wakaanza kubishana tena vikali juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu. Akiwa na subira kama kawaida yake, Yesu hakuwakemea bali alisababu nao. Aliwaambia mambo yatakayotokea: “Nyinyi nyote mtakwazika kuhusiana nami usiku huu, kwa maana imeandikwa, ‘Hakika nitampiga mchungaji, nao kondoo wa kundi watatawanywa huku na huku.’” (Mathayo 26:31; Zekaria 13:7) Alijua kwamba waandamani wake wa karibu zaidi wangemwacha pindi hiyo yenye uhitaji. Lakini hata hakuwashutumu. Badala yake, aliwaambia hivi: “Lakini baada ya mimi kuwa nimefufuliwa hakika nitawatangulia kuingia katika Galilaya.” (Mathayo 26:32) Ndiyo, aliwahakikishia kwamba ingawa wangemwacha, yeye hangewaacha. Wakati ambapo masaibu hayo makali yangepita, angekutana nao tena.

18. Huko Galilaya, Yesu aliwakabidhi wanafunzi wake utume gani mzito, na mitume walitimizaje utume huo?

18 Yesu alitimiza maneno yake. Baadaye, katika Galilaya, Yesu aliyefufuliwa aliwatokea mitume 11 waaminifu, ambao inaonekana walikusanyika pamoja na wengine wengi. (Mathayo 28:16, 17; 1 Wakorintho 15:6) Huko, Yesu aliwapa utume mzito: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kitabu cha Matendo chatupa uthibitisho wa wazi kwamba mitume walitii utume huo. Kwa uaminifu waliongoza kazi ya kuhubiri habari njema katika karne ya kwanza.—Matendo 2:41, 42; 4:33; 5:27-32.

19. Matendo ya Yesu baada ya kufufuliwa yatufundisha nini kuhusu akili ya Kristo?

19 Simulizi hilo lenye kufunua mambo linatufundisha nini kuhusu akili ya Kristo? Yesu alijua sifa mbaya za mitume wake, lakini “aliwapenda hadi mwisho.” (Yohana 13:1) Japo kasoro zao, aliwaonyesha kwamba aliwaamini. Ona kwamba Yesu hakukosea kuwaonyesha kwamba ana uhakika nao. Inaelekea kwamba uhakika na imani aliyokuwa ameonyesha kwao iliwaimarisha waazimie moyoni kutekeleza kazi ambayo alikuwa amewaamuru wafanye.

20, 21. Tunaweza kuonyeshaje maoni mazuri juu ya waamini wenzetu?

20 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna akili ya Kristo kuhusu jambo hili? Usiwe na maoni mabaya juu ya waamini wenzako. Ukifikiria tu mabaya, inaelekea maneno yako na matendo yako yatayafunua. (Luka 6:45) Hata hivyo, Biblia yatuambia kwamba upendo “hutumaini mambo yote.” (1 Wakorintho 13:7) Upendo hufikiria mema, wala si mabaya. Hujenga badala ya kubomoa. Watu huitikia kwa urahisi zaidi wakionyeshwa upendo na kutiwa moyo kuliko wanapotishwa. Tunaweza kuwajenga wengine na kuwatia moyo kwa kuonyesha kwamba tuna uhakika nao. (1 Wathesalonike 5:11) Ikiwa, kama Kristo, tuna maoni mazuri juu ya ndugu zetu, tutawatendea katika njia ambazo zinawajenga na kufanya watokeze sifa zao bora.

21 Kusitawisha akili ya Kristo na kuidhihirisha kunatia ndani mengi zaidi kuliko kuiga tu mambo ambayo Yesu alifanya. Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, ikiwa kwa kweli tunataka kutenda kama Yesu, ni lazima kwanza tujifunze kuona mambo kama alivyoyaona. Gospeli hutusaidia kuona upande mwingine wa utu wake, mawazo yake na hisia zake juu ya kazi aliyopewa afanye, kama makala ifuatayo itakavyozungumzia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Katika hati hiyo, mtu huyo mdanganyifu anataja ile isemekanayo kuwa eti sura ya Yesu, kutia ndani rangi ya nywele zake, ndevu, na macho. Mtafsiri mmoja wa Biblia Edgar J. Goodspeed aeleza kwamba udanganyifu huo “ulitayarishwa ili kuunga mkono ufafanuzi unaopatikana katika vitabu vya wachoraji kuhusu sura ya Yesu.”

^ fu. 4 Inaonekana kwamba watoto hao wana umri tofauti-tofauti. Neno lililotafsiriwa hapa “watoto wachanga” pia limetumiwa kumtaja binti Yairo mwenye umri wa miaka 12. (Marko 5:39, 42; 10:13) Hata hivyo, katika simulizi linalofanana na hilo, Luka atumia neno ambalo laweza kumaanisha pia vitoto vichanga.—Luka 1:41; 2:12; 18:15.

^ fu. 11 Ona makala “Je, Wewe Wastahi Adhama Yao?” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1998.

Je, Unakumbuka?

• Yesu alifanya nini wanafunzi wake walipojaribu kuwakataza watoto wasimwendee?

• Ni katika njia zipi Yesu alionyesha anawajali wengine?

• Tunaweza kuigaje utayari wa Yesu wa kuitibari wanafunzi wake?

• Tunaweza kuigaje uhakika ambao Yesu aliwaonyesha mitume wake?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Watoto walistarehe wakiwa na Yesu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Yesu aliwatendea wengine kwa huruma

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wazee ambao wanafikiwa kwa urahisi ni baraka