Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumtafuta Yehova kwa Moyo Ulio Tayari

Kumtafuta Yehova kwa Moyo Ulio Tayari

Kumtafuta Yehova kwa Moyo Ulio Tayari

EZRA kuhani Mwisraeli alikuwa mtafiti, msomi, mnakili na mwalimu wa Sheria mwenye kutokeza. Yeye pia ni mfano mzuri wa utumishi wa nafsi yote kwa Wakristo leo. Jinsi gani? Kwa kuwa alidumisha ujitoaji wake kwa Mungu hata alipoishi Babiloni, jiji lililojaa miungu ya isiyo ya kweli na ibada ya mashetani.

Ujitoaji wa Ezra kwa Mungu haukutokea tu bila jitihada. Alijitahidi. Kwa kweli, yeye atuambia kwamba alikuwa “ameuelekeza [“ameutayarisha,” “NW”] moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda.”—Ezra 7:10, italiki ni zetu.

Kama Ezra, leo watu wa Yehova wanataka kufanya yote ambayo Yehova awataka wafanye huku wakiishi katika ulimwengu wenye kuchukia ibada ya kweli. Hivyo, na tuchunguze njia ambazo sisi pia tunaweza kutayarisha moyo wetu, yaani, utu wa ndani—kutia ndani mawazo yetu, mitazamo, tamaa, na vichocheo—ili “kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda.”

Kuutayarisha Moyo Wetu

“Kutayarisha” humaanisha “kuandaa kitu mapema kwa kusudi fulani: kukiweka katika hali fulani kwa ajili ya matumizi, au mpango hususa.” Kwa hakika, ikiwa umepata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na umejiweka wakfu kwa Yehova, basi moyo wako umekuwa katika hali ya utayari na unaweza kulinganishwa na “udongo ulio bora” ambao Yesu alizungumzia katika mfano wake wa mpanzi.—Mathayo 13:18-23.

Hata hivyo, moyo wetu wahitaji kuangaliwa na kusafishwa daima. Kwa nini? Kwa sababu mbili. Kwanza, kwa sababu maelekeo yenye kudhuru, kama vile magugu bustanini, yaweza kusitawi kwa urahisi, hasa wakati wa “siku [hizi] za mwisho” ambapo “hewa” ya mfumo wa Shetani imejaa sana mambo yanayofanya tuwaze kimwili. (2 Timotheo 3:1-5; Waefeso 2:2) Sababu ya pili yahusu udongo wenyewe. Usipotunzwa, udongo unaweza kukauka, kuwa mgumu, na kukosa mazao. Au watu wengi mno wanaweza kutembea katika bustani bila kujali na kuukanyaga udongo, wakiufanya uwe mgumu sana. Udongo wa moyo wetu wa mfano uko hivyo. Unaweza kukosa kuzaa usipotunzwa au ukikanyagwa na watu wasiopendezwa na hali njema yetu ya kiroho.

Basi ni muhimu kama nini kwetu sote kutumia shauri hili la Biblia: “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.”—Mithali 4:23.

Mambo Yanayoboresha “Udongo” wa Moyo Wetu

Ebu tuone mambo kadhaa, au sifa ambazo huboresha “udongo” wa moyo wetu ili kutokeza ukuaji mzuri. Bila shaka kuna mambo mengi yanayouboresha moyo wetu, lakini hapa tutazungumzia mambo sita: kutambua uhitaji wetu wa kiroho, unyenyekevu, unyofu, hofu ya kimungu, imani, na upendo.

“Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho,” Yesu akasema. (Mathayo 5:3) Kama njaa ya kimwili ambayo hutukumbusha uhitaji wa kula, kutambua uhitaji wetu wa kiroho hutufanya tuone njaa ya chakula cha kiroho. Wanadamu wana tamaa ya kiasili ya chakula hicho kwa sababu huwapa maana na kusudi la uhai. Misongo kutokana na mfumo wa mambo wa Shetani au kuzembea tu kujifunza zinaweza kufanya tusitambue uhitaji huo. Hata hivyo, Yesu alisema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.”—Mathayo 4:4.

Kihalisi, chakula cha kawaida, kilicho kamili, na kinachofaa huboresha afya ya mwili, na hufanya mwili uwe na hamu ya chakula kinachofuata wakati wa kula ufikapo. Hali iko hivyo kiroho. Huenda usijifikirie kuwa mtu mwenye bidii ya kusoma, lakini ukifanya zoea la kusoma Neno la Mungu kila siku na kujifunza kwa ukawaida vichapo vinavyotegemea Biblia, utaona hamu yako ikiongezeka. Kwa kweli, utatazamia kwa hamu vipindi vya kujifunza Biblia. Hivyo, usikate tamaa haraka; jitahidi kusitawisha hamu ifaayo ya chakula cha kiroho.

Unyenyekevu Hufanya Moyo Uwe Mwororo

Unyenyekevu ni sifa muhimu ili kuwa na moyo ulio tayari kwa sababu huo hutufanya tuwe wenye kufundishika na hutusaidia kukubali kwa urahisi mashauri na masahihisho ya upendo. Fikiria mfano mzuri wa Mfalme Yosia. Wakati wa utawala wake, hati yenye Sheria ya Mungu aliyopewa Musa ilipatikana. Yosia aliposikia maneno ya Sheria na kujua jinsi baba zake wa zamani walivyokengeuka mbali na ibada ya kweli, alirarua mavazi yake, akalia mbele za Yehova. Kwa nini Neno la Mungu liligusa sana moyo wa mfalme? Simulizi hilo lasema kwamba moyo wake ulikuwa “mwororo,” kiasi kwamba alijinyenyekeza aliposikia maneno ya Yehova. Yehova aliona moyo wa Yosia ambao ulikuwa mnyenyekevu na tayari kusikiliza, hivyo akambariki.—2 Wafalme 22:11, 18-20.

Unyenyekevu uliwawezesha wanafunzi wa Yesu “wasio na elimu na wa kawaida tu” waelewe na kutumia kweli za kiroho ambazo “wenye hekima na walio na akili” “katika njia ya kimwili” tu ndio waliokosa kuzielewa. (Matendo 4:13; Luka 10:21; 1 Wakorintho 1:26) Watu katika kikundi hiki cha pili hawakuwa tayari kukubali Neno la Yehova kwa kuwa kiburi kilifanya mioyo yao kuwa migumu. Je, ni ajabu kwamba Yehova huchukia kiburi?—Mithali 8:13; Danieli 5:20.

Unyofu na Hofu ya Kimungu

Nabii Yeremia aliandika kwamba “moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua?” (Yeremia 17:9) Udanganyifu huu hujidhihirisha kwa njia mbalimbali, kama vile kutoa udhuru tunapokosea. Hujidhihirisha pia tunapojitetea kuhusiana na kasoro mbaya za utu wetu. Hata hivyo, unyofu utatusaidia kushinda moyo mdanganyifu kwa kutusaidia kukabili ukweli juu yetu wenyewe ili kuweza kufanya maendeleo. Mtunga-zaburi alidhihirisha unyofu huo aliposali hivi: “Ee BWANA, unijaribu na kunipima; unisafishe mtima wangu na moyo wangu.” Ni wazi kwamba mtunga-zaburi alikuwa ameutayarisha moyo wake kukubali kusafishwa na kujaribiwa na Yehova, hata ingawa huenda jambo hilo lilimaanisha kukubali kwamba alikuwa na tabia zisizofaa ili aweze kuzishinda.—Zaburi 17:3; 26:2.

Hofu ya kimungu, inayotia ndani “kuchukia uovu,” ni msaada wenye nguvu katika kazi hii ya kusafisha. (Mithali 8:13) Ingawa mtu anayemhofu Yehova kwelikweli anathamini fadhili-upendo na upendo wa Yehova, yeye hutambua daima kwamba Yehova ana uwezo wa kuadhibu, hata kuwaua, wale wasiomtii. Yehova alionyesha kwamba wale wanaomhofu wangemtii pia aliposema hivi kuhusu Israeli: “Laiti wangekuwa na moyo kama huu ndani yao sikuzote, wa kunicha, na kushika amri zangu zote sikuzote, wapate kufanikiwa wao na watoto wao milele!”—Kumbukumbu la Torati 5:29.

Ni wazi kwamba lengo la hofu ya kimungu si kututiisha kwa kutuogofya, bali ni kutusukuma tutii Baba yetu mwenye upendo ambaye tunajua kwamba anataka tunufaike. Kwa kweli, hofu hiyo ya kimungu hufurahisha na hata hutokeza shangwe, ambayo Yesu Kristo mwenyewe aliidhihirisha kwa wingi.—Isaya 11:3; Luka 12:5.

Moyo Ulio Tayari Una Imani Nyingi

Moyo wenye imani yenye nguvu unajua kwamba chochote ambacho Yehova hutaka au kuagiza kupitia Neno lake ni chema sikuzote na hutunufaisha. (Isaya 48:17, 18) Mtu mwenye moyo kama huo hupata furaha na uradhi mwingi kwa kutumia himizo kwenye Mithali 3:5, 6, lisemalo: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” Lakini moyo usio na imani hautakuwa tayari kumtumaini Yehova, hasa ikiwa kufanya hivyo kwamaanisha kujidhabihu, kama vile kurahisisha maisha ili mtu azingatie masilahi ya Ufalme. (Mathayo 6:33) Ni kwa sababu nzuri kwamba Yehova huuona moyo usio na imani kuwa “mwovu.”—Waebrania 3:12.

Imani yetu kwa Yehova hudhihirishwa katika mambo mengi, kutia ndani mambo tunayofanya faraghani katika nyumba zetu wenyewe. Kwa mfano, fikiria kanuni kwenye Wagalatia 6:7: “Msiongozwe vibaya: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.” Imani yetu katika kanuni hiyo itadhihirishwa katika mambo kama sinema tunazotazama, vitabu tunavyosoma, kadiri ya usomaji wetu wa Biblia, na katika sala zetu. Naam, imani yenye nguvu ambayo hutusukuma kupanda “katika roho” ni sifa muhimu inayotusaidia kuwa na moyo ulio tayari kukubali Neno la Yehova na kulitii.—Wagalatia 6:8.

Upendo—Sifa Iliyo Kuu Zaidi

Zaidi ya sifa nyingine zote, upendo kwa kweli hufanya udongo wa moyo wetu ulitii Neno la Yehova. Hivyo, alipoulinganisha na imani na tumaini, mtume Paulo alifafanua upendo kuwa sifa “kubwa zaidi sana kati ya [hizo].” (1 Wakorintho 13:13) Moyo uliojaa upendo kwa Mungu hupata uradhi na shangwe kubwa kutokana na kumtii; kwa kweli hauudhiwi na yale Mungu hututaka tufanye. Mtume Yohana alisema: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Kuhusiana na jambo hilohilo, Yesu alisema: “Ikiwa yeyote anipenda mimi, atashika neno langu, na Baba yangu atampenda.” (Yohana 14:23) Ona kwamba upendo kama huo unaonyeshwa na pande zote. Naam, Yehova anawapenda sana wale wanaovutwa kwake kwa upendo.

Yehova anajua kwamba sisi si wakamilifu nasi hufanya dhambi dhidi yake mara kwa mara. Hata hivyo, yeye hajitengi mbali nasi. Kile ambacho Yehova hutafuta katika watumishi wake ni “moyo mkamilifu,” ambao hutuchochea kumtumikia kwa utayari tukiwa na “nia ya kumkubali.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Bila shaka, Yehova anajua kwamba tunahitaji wakati na jitihada ili kusitawisha sifa nzuri katika moyo wetu na hivyo kutokeza matunda ya roho. (Wagalatia 5:22, 23) Hivyo, yeye hutuonyesha subira, “kwa maana yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:14) Akionyesha mtazamo huohuo, Yesu hakuwachambua vikali wanafunzi wake kwa makosa yao bali aliwasaidia na kuwatia moyo kwa subira. Je, upendo, rehema, na subira ya Yehova na Yesu hazikuchochei kuwapenda hata zaidi?—Luka 7:47; 2 Petro 3:9.

Ikiwa nyakati nyingine inakuwa vigumu sana kwako kung’oa mazoea yaliyo kama magugu yenye mizizi mirefu, au kuvunjavunja mazoea yaliyo kama vibonge vya udongo mgumu, usivunjike moyo wala usikate tamaa. Badala yake, endelea kujitahidi kufanya maendeleo huku ‘ukidumu katika sala,’ na pia kumwomba Yehova mara nyingi ili upate roho yake. (Waroma 12:12) Kwa msaada wake wa utayari, utafaulu kumwiga Ezra katika kuwa na moyo ulio tayari kabisa “kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda.”

[Picha katika ukurasa wa 31]

Ezra alidumisha ujitoaji wake kwa Mungu hata akiwa Babiloni

[Picha katika ukurasa wa 29 zemeandaliwa na]

Garo Nalbandian