Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Ee Mungu, Utume Nuru Yako’

‘Ee Mungu, Utume Nuru Yako’

‘Ee Mungu, Utume Nuru Yako’

“Utume nuru yako na kweli yako, ziniongoze.” —ZABURI 43:3, Zaire Swahili Bible.

1. Yehova hufunuaje makusudi yake?

YEHOVA anajali sana jinsi anavyowajulisha watumishi wake makusudi yake. Badala ya kufunua kweli yote mara moja katika mmweko mkali sana wa nuru wenye kupofusha, yeye hutupa sisi nuru hatua kwa hatua. Safari yetu kwenye njia ya uhai yaweza kulinganishwa na njia ndefu anayofuata mtembeaji. Yeye aanza mwendo alfajiri na haoni kitu. Jua lianzapo kuchomoza polepole, mtembeaji huyo aanza kutambua vitu vichache anavyoona. Lakini vitu vingine bado havionekani waziwazi. Lakini jua lizidivyo kupanda ndivyo awezavyo kuona mbali zaidi na zaidi. Ndivyo ilivyo na nuru ya kiroho ambayo Mungu huandaa. Yeye hutuwezesha kufahamu mambo machache kwa wakati fulani. Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliandaa nuru ya kiroho kwa njia iyo hiyo. Ebu tuone jinsi Yehova alivyowapa watu wake nuru nyakati za kale na katika wakati wetu.

2. Yehova aliandaaje nuru katika nyakati za kabla ya Ukristo?

2 Yaelekea watungaji wa Zaburi ya 43 ni wana wa Kora. Wakiwa Walawi, walikuwa na pendeleo la kuwafundisha watu Sheria ya Mungu. (Malaki 2:7) Bila shaka, Yehova alikuwa Mfunzi wao Mkuu, nao walimtegemea akiwa Chanzo cha hekima yote. (Isaya 30:20) Mtunga-zaburi alisali: “Ee Mungu, . . . utume nuru yako na kweli yako, ziniongoze.” (Zaburi 43:1, 3, ZSB) Maadamu Waisraeli walikuwa waaminifu kwake, Yehova aliwafundisha njia zake. Karne kadhaa baadaye, Yehova aliwapendelea kwa kuwapa nuru na kweli za ajabu sana. Mungu alifanya hivyo alipomtuma Mwana wake duniani.

3. Wayahudi walijaribiwaje na mafundisho ya Yesu?

3 Akiwa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu alikuwa “nuru ya ulimwengu.” (Yohana 8:12) Aliwafundisha watu “mambo mengi kwa vielezi”—mambo mapya. (Marko 4:2) Alimwambia Pontio Pilato: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Hilo lilikuwa jambo jipya kwa Waroma na kwa hakika kwa wale Wayahudi wazalendo, kwa sababu wao walifikiri kwamba Mesiya angeishinda Milki ya Roma na kulirudishia Israeli utukufu wake wa zamani. Yesu aliangaza nuru kutoka kwa Yehova, lakini maneno yake hayakuwapendeza watawala Wayahudi, ambao “walipenda utukufu wa wanadamu zaidi ya hata utukufu wa Mungu.” (Yohana 12:42, 43) Watu wengi waliamua kushikilia mapokeo yao ya wanadamu badala ya kukubali nuru na kweli za kiroho kutoka kwa Mungu.—Zaburi 43:3; Mathayo 13:15.

4. Tunajuaje kwamba wanafunzi wa Yesu wangeendelea kupata uelewevu zaidi?

4 Hata hivyo, wanaume na wanawake wachache wenye mioyo minyofu walifurahi kukubali kweli ambayo Yesu alifundisha. Walifanya maendeleo hatua kwa hatua kuelewa makusudi ya Mungu. Hata hivyo, maisha ya Mwalimu wao duniani yalipokaribia mwisho, bado walikuwa na mengi ya kujifunza. Yesu aliwaambia: “Bado, nina mambo mengi ya kuwaambia nyinyi, lakini hamwezi kuyahimili wakati wa sasa.” (Yohana 16:12) Ndiyo, wanafunzi wangeendelea kupata ujuzi juu ya kweli ya Mungu.

Nuru Yazidi Kung’aa

5. Ni swali lipi lililozuka katika karne ya kwanza, na ni nani waliokuwa na daraka la kulitatua?

5 Baada ya kifo cha Yesu na kufufuliwa kwake, nuru itokayo kwa Mungu iliangaza zaidi ya wakati mwingine wowote. Katika ono alilopewa Petro, Yehova alifunua kwamba tokea wakati huo na kuendelea watu wasio Wayahudi ambao hawakutahiriwa wangekuwa wafuasi wa Kristo. (Matendo 10:9-17) Huo ukawa ufunuo wa ajabu kwelikweli! Lakini baadaye swali likazuka: Je, Yehova alitaka watu hao wasio Wayahudi watahiriwe baada ya kuwa Wakristo? Swali hilo halikujibiwa katika ono hilo na basi mjadala mkali ukazuka miongoni mwa Wakristo. Ilikuwa lazima suala hilo litatuliwe ili kuhifadhi muungano wao wenye thamani. Basi “mitume na wanaume wazee wakakusanyika pamoja [Yerusalemu] waone juu ya jambo hili.”—Matendo 15:1, 2, 6.

6. Mitume na wanaume wazee walifuata utaratibu gani walipofikiria suala la tohara?

6 Wale waliohudhuria mkutano huo wangejuaje matakwa ya Mungu kwa waamini wasio Wayahudi? Yehova hakutuma malaika aongoze mazungumzo hayo, wala hakuwapa wale waliohudhuria mkutano huo ono fulani. Lakini, mitume na wanaume wazee hawakuachwa kabisa bila mwongozo. Walifikiria ushuhuda wa Wakristo fulani Wayahudi waliokuwa wameona jinsi Mungu alivyoanza kushughulika na watu wa mataifa, akiwamwagia roho takatifu watu wasio Wayahudi ambao hawakutahiriwa. Pia walitafuta mwongozo wa Maandiko. Basi, mwanafunzi Yakobo akatoa pendekezo lililotegemea andiko fulani lililowapa nuru. Walipofikiria uthibitisho huo, mapenzi ya Mungu yakawa wazi. Si lazima watu wa mataifa watahiriwe ili wakubaliwe na Yehova. Mitume na wanaume wazee wakaandika uamuzi huo mara moja ili uwaongoze Wakristo wenzao.—Matendo 15:12-29; 16:4.

7. Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa wenye maendeleo katika njia ipi?

7 Tofauti na viongozi wa kidini wa Wayahudi ambao walishikilia sana mapokeo ya babu zao, Wayahudi wengi Wakristo walifurahi walipopokea uelewevu huo mpya wa kusudi la Mungu kwa watu wa mataifa, hata ingawa kuukubali kulimaanisha wabadili maoni yao kuhusu watu wasio Wayahudi kwa ujumla. Yehova alibariki unyenyekevu wao, na “makutaniko yakaendelea kufanywa imara katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”—Matendo 15:31; 16:5.

8. (a) Tunajuaje kwamba nuru zaidi ingeweza kutarajiwa baada ya karne ya kwanza kumalizika? (b) Tutafikiria maswali gani yanayotuhusu?

8 Nuru ya kiroho iliendelea kuangaza katika karne yote ya kwanza. Lakini Yehova hakufunua makusudi yake yote kwa Wakristo wa mapema. Mtume Paulo aliwaambia hivi waamini wenzake wa karne ya kwanza: “Wakati wa sasa twaona katika njia isiyo ya waziwazi kupitia kioo cha madini.” (1 Wakorintho 13:12) Kioo kama hicho hakikuangaza vizuri. Basi, mwanzoni ufahamu wa nuru ya kiroho haungekuwa wazi sana. Baada ya mitume kufa, nuru ilififia kwa muda, lakini katika nyakati za karibuni ujuzi wa Maandiko umekuwa mwingi sana. (Danieli 12:4) Yehova huwapaje nuru watu wake leo? Na twapasa kutendaje anapotusaidia kuelewa Maandiko zaidi?

Nuru Yazidi Kung’aa

9. Ni njia ipi ya kipekee na yenye matokeo ya kujifunza Biblia iliyotumiwa na Wanafunzi wa Biblia wa mapema?

9 Katika nyakati hizi nuru halisi ya kwanza iliyo hafifu ilianza kutokea mwishoni-mwishoni mwa karne ya 19 wakati kikundi kimoja cha wanaume na wanawake Wakristo walipoanza kujifunza Maandiko kwa bidii. Walitumia njia yenye matokeo ya kujifunza Biblia. Mtu mmoja angeuliza swali; kisha kikundi hicho kingechunguza Maandiko yote yanayohusiana na swali hilo. Mstari mmoja wa Biblia ulipoonekana kutofautiana na mwingine, Wakristo hao wenye mioyo myeupe walijaribu kuipatanisha mistari hiyo. Tofauti na viongozi wa kidini wa wakati huo, Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo) waliazimia kuongozwa na Maandiko Matakatifu wala si mapokeo au mafundisho ya wanadamu. Baada ya kuufikiria uthibitisho wote upatikanao wa Maandiko, waliandika uamuzi wao. Kwa njia hiyo walielewa mafundisho mengi ya msingi yanayopatikana katika Biblia.

10. Charles Taze Russell aliandika vichapo gani vinavyosaidia kujifunza Biblia?

10 Charles Taze Russell alikuwa mwenye kutokeza sana miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia. Aliandika mfululizo wa vichapo sita vinavyosaidia kusoma Biblia viitwavyo Studies in the Scriptures. Ndugu Russell alikusudia kuandika buku la saba, ambalo lingefafanua vitabu vya Biblia vya Ezekieli na Ufunuo. “Nitakapopata tu ufahamu,” akasema, “nitaandika Buku la Saba.” Lakini akaongezea kusema: “Bwana akimpa mtu mwingine ufahamu, yeye aweza kuliandika.”

11. Kuna uhusiano gani kati ya wakati na kuelewa kwetu makusudi ya Mungu?

11 Taarifa hiyo ya C. T. Russell yaonyesha jambo kuu linalohusu uwezo wetu wa kuelewa mafungu fulani ya Biblia—wakati. Ndugu Russell alijua kwamba hawezi kulazimisha nuru iangaze kitabu cha Ufunuo kama vile mtembeaji asivyoweza kulazimisha jua lichomoze upesi kabla ya wakati wake.

Yafunuliwa—Lakini kwa Wakati wa Mungu

12. (a) Unabii wa Biblia hufahamika vizuri zaidi wakati gani? (b) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba uwezo wetu wa kuelewa unabii wa Biblia wategemea ratiba ya Mungu? (Ona kielezi-chini.)

12 Kama vile mitume walivyoelewa unabii mwingi kuhusu Mesiya baada ya kifo cha Yesu na ufufuo wake, ndivyo Wakristo leo huelewa unabii wa Biblia kabisa baada ya utimizo wake. (Luka 24:15, 27; Matendo 1:15-21; 4:26, 27) Ufunuo ni kitabu cha unabii, basi twapasa kutarajia kukielewa vizuri zaidi wakati matukio yanayotajwa humo yanapotokea. Kwa mfano, C. T. Russell hangeweza kuelewa vizuri maana ya hayawani-mwitu mwekundu mwangavu wa mfano anayetajwa kwenye Ufunuo 17:9-11 kwa kuwa mashirika hayo yanayowakilishwa na wanyama hao, yaani, Ushirika wa Mataifa na Umoja wa Mataifa, yalitokea tu baada ya kifo chake. *

13. Nyakati nyingine ni jambo gani hutukia wakati nuru iangazapo habari fulani ya Biblia?

13 Wakristo wa mapema walipotambua kwamba watu wasio Wayahudi ambao hawakutahiriwa wangeweza kuwa waamini wenzao, badiliko hilo lilitokeza swali jipya la kama watu wa mataifa walipaswa kutahiriwa. Jambo hilo lilifanya mitume na wanaume wazee kuchunguza tena suala la tohara. Na ndivyo hali ilivyo leo. Mmweko mwangavu wa nuru kwenye habari fulani ya Biblia nyakati nyingine huwaongoza watumishi wa Mungu watiwa-mafuta, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” kuchunguza tena habari zinazohusika, kama mfano ufuatao wa karibuni unavyoonyesha.—Mathayo 24:45.

14-16. Rekebisho la maoni yetu kuhusu hekalu la kiroho lilibadilije jinsi tulivyoelewa Ezekieli sura ya 40 hadi 48?

14 Mwaka wa 1971 ufafanuzi wa unabii wa Ezekieli ulichapishwa katika kitabu “The Nations Shall Know That I Am Jehovah”—How? Sura moja ya kitabu hiki inazungumzia kwa ufupi ono la Ezekieli la hekalu. (Ezekieli, sura ya 40-48) Wakati huo, jambo lililozingatiwa ni jinsi ambavyo ono la Ezekieli la hekalu lingetimizwa katika ulimwengu mpya.—2 Petro 3:13.

15 Hata hivyo, makala mbili zilizochapishwa katika Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1972, zilibadili jinsi tulivyoelewa ono la Ezekieli. Zilizungumzia hekalu kubwa la kiroho lililofafanuliwa na mtume Paulo katika Waebrania sura ya 10. Mnara wa Mlinzi lilieleza kwamba sehemu ya Patakatifu na ua wa ndani wa hekalu hilo la kiroho zinahusiana na hali ya watiwa-mafuta wakiwa bado duniani. Ezekieli sura ya 40 hadi 48 ilipochunguzwa miaka fulani baadaye, ilitambuliwa kwamba hekalu ambalo Ezekieli aliona katika ono lazima liwe linatenda leo kama vile hekalu la kiroho linavyotenda leo. Kwa njia gani?

16 Katika ono la Ezekieli, makuhani waonekana wakitembea-tembea kwenye nyua za hekalu wakitumikia makabila yasiyo ya kikuhani. Kwa wazi, makuhani hao wawakilisha “ukuhani wa kifalme,” watumishi wa Yehova watiwa-mafuta. (1 Petro 2:9) Lakini, hawatakuwa wakitumikia katika ua wa kidunia wa hekalu katika kipindi chote cha Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. (Ufunuo 20:4) Karibu kipindi hicho chote, ama hata katika kipindi hicho chote, watiwa-mafuta watakuwa wakimtumikia Mungu katika Patakatifu Zaidi Sana pa hekalu la kiroho, “mbinguni kwenyewe.” (Waebrania 9:24) Kwa kuwa makuhani wanaonekana wakitembea-tembea kwenye nyua za hekalu la Ezekieli, ni lazima ono hilo linatimizwa leo, wakati ambapo baadhi ya watiwa-mafuta bado wako duniani. Basi, toleo la Machi 1, 1999 la gazeti hili lilionyesha rekebisho la habari hiyo. Kwa hiyo, kufikia mwisho wa karne ya 20, nuru ya kiroho iliangaza unabii wa Ezekieli.

Uwe Tayari Kurekebisha Maoni Yako

17. Umefanya marekebisho gani kwa maoni yako tangu upate kujua kweli, na marekebisho hayo yamekunufaishaje?

17 Mtu yeyote anayetamani kupata ujuzi wa kweli ni lazima awe tayari ‘kuteka kila fikira ili kuifanya iwe tiifu kwa Kristo.’ (2 Wakorintho 10:5) Nyakati nyingine si rahisi kufanya hivyo, hasa kama maoni fulani yameshikiliwa sana. Kwa mfano, kabla ya kujifunza kweli ya Mungu, huenda ulikuwa ukisherehekea sikukuu fulani za kidini pamoja na familia yenu. Ulipoanza kujifunza Biblia, ulitambua kwamba kumbe sherehe hizo zina asili ya kipagani. Kwanza, huenda ulisita kufuata mambo uliyokuwa ukijifunza. Lakini, hatimaye upendo wako kwa Mungu ukawa wenye nguvu kuliko maoni hayo ya kidini, ukaacha sherehe zisizompendeza Mungu. Je, Yehova hajabariki uamuzi wako?—Linganisha Waebrania 11:25.

18. Tutendeje wakati ufahamu wetu wa kweli ya Biblia unaposahihishwa?

18 Sikuzote sisi hunufaika tukifanya mambo kwa njia ya Mungu. (Isaya 48:17, 18) Kwa hiyo maoni yetu juu ya mafungu fulani ya Biblia yanaposahihishwa, tufurahi kwamba tunafanya maendeleo katika kweli! Kwa kweli, jambo la kwamba tunaendelea kupata nuru lathibitisha kwamba tuko kwenye njia ifaayo. Ni “njia ya wenye haki,” ambayo ni “kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” (Mithali 4:18) Ni kweli kwamba wakati huu twaona sehemu fulani za kusudi la Mungu “katika njia isiyo ya waziwazi.” Lakini wakati wa Mungu ufaao ufikapo, tutaona kweli yote jinsi ilivyo, maadamu miguu yetu imesimama imara kwenye “njia.” Kwa wakati huu, na tushangilie kweli ambazo Yehova amefanya ziwe wazi, tukingojea nuru iangaze mambo ambayo bado hayajaeleweka vizuri.

19. Kuna njia ipi moja ya kuonyesha kwamba twapenda kweli?

19 Tunaweza kudhihirishaje kihalisi kwamba twapenda nuru? Njia moja ni kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida—kila siku ikiwezekana. Je, unasoma Biblia kwa ukawaida? Magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! pia hutupatia chakula kingi kizuri cha kiroho. Pia fikiria vitabu, broshua, na vichapo vinginevyo ambavyo vimetayarishwa kwa manufaa yetu. Na vipi juu ya ripoti zenye kutia moyo za utendaji wa kuhubiri Ufalme ambazo huchapishwa katika Yearbook of Jehovah’s Witnesses?

20. Kuna uhusiano gani kati ya nuru na kweli zinazotoka kwa Yehova na kule kuhudhuria mikutano ya Kikristo?

20 Kwa kweli, Yehova amejibu kwa njia ya ajabu sala ambayo imetajwa kwenye Zaburi 43:3, (ZSB). Mwisho wa mstari huo wasema: “[Nuru yako na kweli yako] zinilete kwa mulima wako mutakatifu, na hata makao yako.” Je, unatazamia kumwabudu Yehova pamoja na wengine wengi? Mafundisho ya kiroho yanayoandaliwa katika mikutano yetu ni njia muhimu ambayo Yehova huandaa nuru leo. Twaweza kuonyeshaje uthamini zaidi kwa mikutano ya Kikristo? Twakuomba ufikirie habari hii kwa njia ya sala katika makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Baada ya kifo cha C. T. Russell, kichapo kilichotajwa kuwa buku la saba la Studies in the Scriptures kilitayarishwa ili kujaribu kufafanua kitabu cha Ezekieli na Ufunuo. Sehemu fulani ya buku hilo ilitegemea maelezo ya Russell ya vitabu hivyo vya Biblia. Hata hivyo, wakati wa kufunua maana ya unabii huo haukuwa umefika, na kwa ujumla, maelezo ya buku hilo la Studies in the Scriptures si wazi. Miaka iliyofuata, fadhili isiyostahiliwa ya Yehova na mambo yaliyotukia ulimwenguni yaliwafanya Wakristo waelewe vizuri zaidi maana ya vitabu hivyo vya unabii.

Ungejibuje?

• Kwa nini Yehova hufunua makusudi yake hatua kwa hatua?

• Mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu walisuluhishaje suala la tohara?

• Wanafunzi wa Biblia wa mapema walitumia njia gani ya kujifunza Biblia, na kwa nini hiyo ilikuwa njia ya kipekee?

• Onyesha jinsi nuru ya kiroho inavyofunuliwa katika wakati wa Mungu.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Charles Taze Russell alijua kwamba nuru ingeangaza kitabu cha Ufunuo katika wakati wa Mungu ufaao