Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Yesu Kristo Awezavyo Kutusaidia

Jinsi Yesu Kristo Awezavyo Kutusaidia

Jinsi Yesu Kristo Awezavyo Kutusaidia

ALIPOKUWA duniani, Yesu Kristo alifanya mambo ya ajabu kuwasaidia watu. Jambo hilo lilikuwa kweli kiasi kwamba, baada ya kusimulia matukio mengi ya maisha ya Yesu, shahidi mmoja aliyejionea alisema: “Kwa kweli, kuna mambo mengine mengi pia aliyofanya Yesu, ambayo, kama ingetukia wakati wowote yaandikwe kirefu kabisa, mimi nadhani ulimwengu wenyewe haungeweza kuwa na nafasi ya kuziweka hati-kunjo ambazo zingeandikwa.” (Yohana 21:25) Kwa kuwa Yesu alifanya mambo mengi hivyo duniani, huenda tukauliza: ‘Anaweza kuwaje msaidiaji wetu mbinguni? Je, tunaweza kunufaika sasa na huruma nyororo ya Yesu?’

Jibu la maswali hayo linachangamsha na kutia moyo sana. Biblia hutuambia kwamba Kristo aliingia “mbinguni kwenyewe, ili sasa aonekane mbele ya uso wa Mungu kwa ajili yetu.” (Waebrania 9:24) Alitufanyia nini? Mtume Paulo aeleza: “[Kristo] aliingia, si kwa damu ya mbuzi na ya mafahali wachanga, sivyo, bali kwa damu yake mwenyewe, mara moja kwa wakati wote ndani ya mahali patakatifu [‘mbinguni kwenyewe’] na kupata ukombozi udumuo milele kwa ajili yetu.”—Waebrania 9:12; 1 Yohana 2:2.

Hizo ni habari njema kama nini! Kwenda kwa Yesu mbinguni hakukuikomesha kazi ya ajabu ambayo aliwafanyia watu, bali kulimwezesha kuwafanyia wanadamu mambo mengi hata zaidi. Hiyo ni kwa sababu Mungu, katika fadhili zake kuu zisizostahiliwa, alimweka Yesu rasmi atumikie akiwa “mtumishi wa watu wote”—kuhani wa cheo cha juu—“kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Ukuu katika mbingu.”—Waebrania 8:1, 2

“Mtumishi wa Watu Wote”

Basi, huko mbinguni Yesu angekuwa mtumishi wa watu wote. Angefanya kazi kama ile iliyofanywa na kuhani wa cheo cha juu wa Israeli kwa niaba ya waabudu wa Mungu wa nyakati za kale. Hiyo ilikuwa kazi gani? Paulo aeleza: “Kila kuhani wa cheo cha juu huwekwa rasmi ili kuzitoa zawadi na dhabihu pia; kwa sababu hiyo ilikuwa lazima kwa huyu [Yesu Kristo aliyekuwa ameenda mbinguni] pia kuwa na kitu fulani cha kutoa.”—Waebrania 8:3.

Yesu alitoa kitu bora kushinda kile kilichotolewa na kuhani wa cheo cha juu wa kale. “Ikiwa damu ya mbuzi na ya mafahali” ingeweza kuwafanya Waisraeli wawe safi kiroho kwa kadiri fulani, ‘je, si damu ya Kristo ingesafisha zaidi sana dhamiri zetu kutoka kazi zilizokufa ili tupate kutoa utumishi mtakatifu kwa Mungu aliye hai?’—Waebrania 9:13, 14.

Yesu pia ni mtumishi wa watu wote mwenye kutokeza kwa sababu amepewa hali ya kutokufa. Katika Israeli la kale “ilibidi wengi kuwa makuhani kwa mfuatano kwa sababu ya kuzuiwa na kifo wasiendelee kuwa hivyo.” Lakini namna gani Yesu? Paulo aandika: “Yeye . . . ana ukuhani wake bila kuwa na wafuataji wowote. Kwa sababu hiyo aweza pia kuokoa kikamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu yeye yuko hai sikuzote ili kuwaombea.” (Waebrania 7:23-25; Waroma 6:9) Naam, kwenye mkono wa kuume wa Mungu mbinguni, tuna mtumishi wa watu wote ambaye ‘yuko hai sikuzote ili kutuombea.’ Ebu wazia jambo hilo lamaanisha nini kwetu leo!

Yesu alipokuwa duniani, watu walimmiminikia wakitaka awasaidie, nyakati nyingine wakisafiri mbali ili wapokee msaada wake. (Mathayo 4:24, 25) Huko mbinguni, Yesu anaweza kufikiwa kwa urahisi na watu wa mataifa yote. Kutoka mahali pake panapofaa mbinguni, anaweza kufikiwa sikuzote akiwa mtumishi wa watu wote.

Yesu Ni Kuhani wa Cheo cha Juu wa Aina Gani?

Ufafanuzi wa Yesu Kristo ambao umeandikwa katika masimulizi ya Gospeli watuonyesha waziwazi kwamba yeye alikuwa mwenye kusaidia na mwenye huruma nyororo. Alikuwa mwenye kujidhabihu kama nini! Mara kadhaa, faragha yake ilivurugwa wakati yeye na wanafunzi wake walipokuwa wakijaribu kupata pumziko walilohitaji sana. Badala ya kuhisi kwamba amenyimwa wakati wenye thamani, amani, na utulivu, Yesu ‘alisukumwa na sikitiko’ kwa ajili ya watu ambao walitaka awasaidie. Hata wakati Yesu alipokuwa amechoka, mwenye njaa, na kiu, ‘aliwapokea kwa fadhili’ na alikuwa tayari kukosa chakula iwapo angeweza kuwasaidia watenda-dhambi wenye mioyo myeupe.—Marko 6:31-34; Luka 9:11-17; Yohana 4:4-6, 31-34.

Kwa kusukumwa na sikitiko, Yesu alichukua hatua hususa za kutosheleza mahitaji ya watu ya kimwili, kihisia-moyo, na kiroho. (Mathayo 9:35-38; Marko 6:35-44) Isitoshe, aliwafunza jinsi ya kupata kitulizo na faraja ya kudumu. (Yohana 4:7-30, 39-42) Kwa mfano, ni wenye kuvutia kama nini mwaliko wake: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi. Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—Mathayo 11:28, 29.

Upendo wa Yesu kwa watu ulikuwa mkubwa sana hivi kwamba hatimaye alitoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi. (Waroma 5:6-8) Kuhusiana na hilo mtume Paulo alisababu hivi: “[Yehova Mungu] ambaye hakumwachilia hata Mwana wake mwenyewe bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, kwa nini pia yeye pamoja naye hatatupa sisi kwa fadhili vitu vingine vyote? . . . Kristo Yesu ndiye aliyekufa, ndiyo, afadhali zaidi kusema ni yeye aliyefufuliwa kutoka kwa wafu, aliye katika mkono wa kuume wa Mungu, ambaye pia hutuombea.”—Waroma 8:32-34.

Kuhani wa Cheo cha Juu Awezaye Kuwa na Hisia

Akiwa mwanadamu, Yesu alipatwa na njaa, kiu, uchovu, maumivu makali, uchungu, na kifo. Mkazo na misongo aliyovumilia ilimtayarisha kwa njia ya pekee kutumikia akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu kwa ajili ya wanadamu wenye kuteseka. Paulo aliandika: “[Yesu] aliwajibika kuwa kama ‘ndugu’ zake katika mambo yote, ili apate kuwa kuhani wa cheo cha juu mwenye rehema na mwaminifu katika mambo yanayohusiana na Mungu, kusudi atoe dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi za watu. Kwa maana yeye mwenyewe ameteseka alipokuwa akitiwa kwenye jaribu, aweza kuja kusaidia wale wanaotiwa kwenye jaribu.”—Waebrania 2:17, 18; 13:8.

Yesu alionyesha kwamba anastahili na yuko tayari kuwasaidia watu kumkaribia Mungu zaidi. Hata hivyo, je, hilo lamaanisha kwamba lazima amsihi Mungu mkatili, asiye na rehema na asiye tayari kusamehe? La hasha, kwa kuwa Biblia hutuhakikishia kwamba ‘Bwana yu mwema, amekuwa tayari kusamehe.’ Biblia pia husema: “Ikiwa twaungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na mwadilifu hata kutusamehe dhambi zetu na kutusafisha ukosefu wote wa uadilifu.” (Zaburi 86:5; 1 Yohana 1:9) Ni kweli kwamba maneno mororo ya Yesu na matendo yake yadhihirisha huruma, rehema, na upendo wa Baba yake mwenyewe.—Yohana 5:19; 8:28; 14:9, 10.

Yesu anawaleteaje kitulizo watenda-dhambi wenye kutubu? Kwa kuwasaidia wapate shangwe na uradhi katika jitihada zao za moyo mweupe za kumpendeza Mungu. Alipowaandikia Wakristo wenzake watiwa-mafuta, Paulo alisema hivi kwa ufupi kuhusu hali hiyo: “Kwa hiyo, kwa kuwa tuna kuhani wa cheo cha juu aliye mkubwa ambaye amepita katika mbingu, Yesu Mwana wa Mungu, acheni tushikilie ungamo letu juu yake. Kwa maana tuna kuhani wa cheo cha juu, si mmoja asiyeweza kushiriki hisia za udhaifu wetu mbalimbali, bali mmoja ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini asiye na dhambi. Kwa hiyo, acheni tukaribie kwa uhuru wa usemi kwenye kiti cha ufalme cha fadhili isiyostahiliwa, ili tuweze kupokea rehema na kupata fadhili isiyostahiliwa kwa msaada katika wakati ufaao.”—Waebrania 4:14-16.

“Msaada Katika Wakati Ufaao”

Hata hivyo, twaweza kufanya nini, tukikabiliwa na matatizo ambayo twahisi ni makubwa sana tusiweze kuyatatua—ugonjwa mbaya, msononeko wa kujihisi wenye hatia, kuvunjika moyo sana, na kushuka moyo? Tunaweza kutumia uandalizi uleule ambao Yesu mwenyewe alitegemea kwa ukawaida—pendeleo lenye thamani la sala. Kwa mfano, usiku kabla ya kutoa uhai wake kwa ajili yetu, “a[li]endelea kusali kwa bidii zaidi; na jasho lake likawa kama matone ya damu yakianguka kwenye ardhi.” (Luka 22:44) Naam, Yesu anajua maana ya kusali kwa Mungu kwa bidii nyingi. “Alitoa dua na pia maombi ya bidii kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa kutoka katika kifo, pamoja na vilio vyenye kupaazwa kwa nguvu na machozi, naye akasikiwa kwa kupendelewa kwa sababu ya hofu yake ya kimungu.”—Waebrania 5:7.

Yesu anajua kadiri wanadamu wanavyothamini ‘kusikiwa kwa kupendelewa’ na kuimarishwa. (Luka 22:43) Isitoshe, yeye aliahidi: “Mkimwomba Baba kitu chochote atawapa katika jina langu. . . . Ombeni nanyi mtapokea, ili shangwe yenu ipate kujazwa.” (Yohana 16:23, 24) Hivyo, tunaweza kuomba Mungu tukiwa na uhakika kwamba atamruhusu Mwana wake atumie mamlaka yake na thamani ya dhabihu yake ya fidia kwa ajili yetu.—Mathayo 28:18.

Tunaweza kuwa na hakika kwamba akiwa mbinguni, Yesu atatoa msaada ufaao kwa wakati ufaao. Kwa mfano, iwapo tumefanya dhambi ambayo twajutia kwa moyo mweupe, tunaweza kupata faraja katika uhakika wa kwamba “tuna msaidiaji kwa Baba, Yesu Kristo, aliye mwadilifu.” (1 Yohana 2:1, 2) Msaidiaji wetu na Mfariji wetu katika mbingu atatuombea ili sala tunazotoa katika jina lake na kwa kupatana na Maandiko zijibiwe.— Yohana 14:13, 14; 1 Yohana 5:14, 15.

Kuonyesha Uthamini kwa Msaada wa Kristo

Mengi yanahusika kuliko tu kumwomba Mungu kupitia Mwana wake. Kwa thamani ya dhabihu yake ya fidia, “Kristo kwa kununua” akawa kama ‘mmiliki aliyeinunua’ jamii ya wanadamu. (Wagalatia 3:13; 4:5; 2 Petro 2:1) Tunaweza kuonyesha shukrani zetu kwa yote ambayo Kristo anatufanyia kwa kukubali atumiliki na kwa kuitikia kwa shangwe mwaliko wake: “Ikiwa yeyote ataka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kunifuata kwa kuendelea.” (Luka 9:23) ‘Kujikana mwenyewe’ si kusema tu kwamba unamilikiwa na mtu mwingine. Kwani, Kristo “alikufa kwa ajili ya wote ili wale waishio wapate kuishi si kwa ajili yao wenyewe tena, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao.” (2 Wakorintho 5:14, 15) Hivyo, kuthamini fidia kutakuwa na matokeo makubwa juu ya maoni yetu, miradi yetu, na jinsi tunavyoishi. Hali yetu ya kuwa wadeni milele kwa “Kristo Yesu, aliyejitoa mwenyewe kwa ajili yetu,” yapasa kutuchochea kujifunza mengi zaidi kumhusu na kuhusu Baba yake mpendwa, Yehova Mungu. Yatupasa pia tutake kukua katika imani, na kuishi kwa viwango vyenye kunufaisha vya Mungu, na kuwa “wenye bidii kwa kazi zilizo bora.”—Tito 2:13, 14; Yohana 17:3.

Kupitia kutaniko la Kikristo sisi hupata chakula cha kiroho, kitia-moyo, na mwongozo kwa wakati ufaao. (Mathayo 24:45-47; Waebrania 10:21-25) Kwa mfano, iwapo kuna wowote walio wagonjwa kiroho, wanaweza ‘kuwaita kwao wanaume wazee [wazee waliowekwa rasmi] wa kutaniko.’ Yakobo aongeza uhakikisho huu: “Na sala ya imani itamfanya huyo asiyejisikia vizuri apone, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”—Yakobo 5:13-15.

Kwa kielelezo: Mtu mmoja aliyekuwa amefungwa gerezani huko Afrika Kusini alimwandikia mzee mmoja wa kutaniko akieleza kwamba anathamini “Mashahidi wa Yehova wote wanaotekeleza kazi nzuri iliyoanzishwa na Yesu Kristo ya kuwasaidia watu kujitahidi kufikia Ufalme wa Mungu.” Kisha akaandika: “Nilifurahi sana kupokea barua yako. Hangaiko lako la kutaka nikombolewe kiroho limenigusa moyo sana. Hilo likiwa sababu nyingine inayonifanya nitii mwito wa Yehova Mungu wa kutubu. Kwa miaka 27 nimekuwa nikijikwaa na kupotea katika giza la dhambi, udanganyifu, mahusiano yasiyo halali, mazoea yasiyo ya adili, na dini zenye kutilika shaka. Baada ya kufahamiana na Mashahidi wa Yehova, nahisi kwamba hatimaye nimepata njia—njia ya kweli! Ninachopaswa kufanya ni kuifuata tu.”

Msaada Zaidi Katika Wakati Ujao Karibuni

Hali za ulimwengu zinazoendelea kuharibika zaonyesha wazi kwamba tunaishi wakati muhimu katika historia ambao ungetangulia kufyatuka kwa “dhiki kubwa.” Wakati huu, umati mkubwa kutoka kwa mataifa yote, makabila, watu, na lugha ‘wanafua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.’ (Ufunuo 7:9, 13, 14; 2 Timotheo 3:1-5) Kwa kudhihirisha imani katika Yesu katika dhabihu ya fidia ya Yesu, wanasamehewa dhambi zao na wanasaidiwa kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu na kuwa rafiki zake kwa kweli.—Yakobo 2:23.

Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, “atawachunga [waokokaji wa dhiki kubwa] na kuwaongoza kwenye mabubujiko ya maji ya uhai. Na Mungu atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao.” (Ufunuo 7:17) Kisha, Kristo ataendelea na kazi yake akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu hadi aikamilishe. Atawasaidia rafiki zote wa Mungu wanufaike kikamili na “mabubujiko ya maji ya uhai”—kiroho, kimwili, kiakili, na kihisia-moyo. Yale ambayo Yesu alianzisha mwaka wa 33 W. K. na yale ambayo ameendelea kufanya akiwa mbinguni tangu wakati huo, yatatimizwa kwa ukamilifu.

Kwa hiyo, usiache kamwe kuonyesha uthamini mkubwa kwa yale yote ambayo Mungu na Kristo wametufanyia na wanatufanyia. Mtume Paulo alisihi hivi: “Sikuzote shangilieni katika Bwana. . . . Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:4, 6, 7.

Kuna njia muhimu ya kuonyesha kwamba unathamini Yesu Kristo, Msaidiaji wetu wa mbinguni. Baada ya jua kushuka siku ya Jumatano, Aprili 19, 2000, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote watakusanyika ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo. (Luka 22:19) Hiyo itakuwa fursa ya kuzidisha uthamini wako kwa dhabihu ya fidia ya Kristo. Unaalikwa kwa uchangamfu uhudhurie na kusikia jinsi mpango wa ajabu wa wokovu wa Mungu kupitia Kristo uwezavyo kukunufaisha milele. Tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova wa kwenu ili upate kujua wakati na mahali barabara pa mkutano huo wa pekee.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu anajua maana ya kusali kwa Mungu kwa bidii nyingi

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kristo atatusaidia kukabiliana na matatizo makubwa tusiyoweza kuyatatua sisi wenyewe

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kristo hutusaidia kupitia wazee wenye upendo