Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kiasi Sifa Inayokuza Amani

Kiasi Sifa Inayokuza Amani

Kiasi Sifa Inayokuza Amani

Ulimwengu ungekuwa mzuri kama nini ikiwa kila mtu angekuwa mwenye kiasi. Watu hawangekuwa wenye kudai mno, watu wa familia hawangekuwa wagomvi sana, mashirika hayangekuwa yenye ushindani sana, na mataifa hayangekuwa yenye vita sana. Je, ungependa kuishi katika ulimwengu kama huo?

WATUMISHI wa kweli wa Yehova Mungu wanajitayarishia ulimwengu wake mpya ulioahidiwa, ambamo kiasi kitatambuliwa kote kuwa nguvu na sifa nzuri wala si udhaifu. (2 Petro 3:13) Hata sasa wao wanakuza sifa ya kiasi. Kwa nini? Hasa kwa sababu hilo ni takwa la Yehova. Nabii wake Mika aliandika: “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!”—Mika 6:8.

Neno kiasi lina maana mbalimbali, kama vile kutokuwa mwenye kiburi, au majivuno, na kutokuwa na mwelekeo wa kujisifia uwezo wako, matimizo yako, na mali zako. Kulingana na kitabu kimoja cha marejeo, kiasi pia kinamaanisha ‘kubaki katika mipaka yako.’ Mtu mwenye kiasi havuki mipaka ya mwenendo mzuri. Pia anatambua kwamba kuna mipaka ya mambo apaswayo kufanya na mambo awezayo kufanya. Anajua kwamba kuna mambo ambayo yeye hastahili. Kwa kweli sisi huvutiwa na watu wenye kiasi. “Hakuna kitu bora kama kiasi cha kweli,” ndivyo alivyoandika mshairi mmoja Mwingereza Joseph Addison.

Kiasi si sifa ambayo sisi wanadamu wasiokamilika huzaliwa nayo. Ni lazima tujitahidi kukuza sifa hiyo. Ili kututia moyo, Neno la Mungu lataja matukio kadhaa yaonyeshayo aina mbalimbali za kiasi.

Wafalme Wawili Wenye Kiasi

Mmojawapo wa watumishi wa Yehova waliokuwa waaminifu-washikamanifu zaidi ni Daudi, ambaye alitiwa mafuta akiwa kijana awe mfalme wa Israeli wa wakati ujao. Baadaye, Mfalme Sauli aliyekuwa akitawala alimsababishia Daudi mkazo mkubwa sana kwa kujaribu kumwua na kwa kumlazimisha aishi maisha ya utoro.—1 Samweli 16:1, 11-13; 19:9, 10; 26:2, 3.

Hata chini ya hali kama hizo, Daudi alitambua kwamba kuna mipaka kuhusu mambo apaswayo kufanya anapolinda uhai wake. Pindi moja akiwa nyikani, Daudi alimkataza Abishai asimdhuru Mfalme Sauli aliyekuwa amelala usingizi, akisema: “Hasha! nisiunyoshe mkono wangu juu ya masihi wa BWANA.” (1 Samweli 26:8-11) Daudi alijua kwamba halikuwa daraka lake kumwondoa Sauli kwenye ufalme. Kwa hiyo Daudi alionyesha kiasi pindi hiyo kwa kutovuka mipaka ya mwenendo mzuri. Vilevile, watumishi wa Mungu wa wakati huu wanajua kwamba ‘kwa maoni ya Yehova,’ kuna mambo ambayo hawawezi kufanya kamwe, hata kama uhai umo hatarini.—Matendo 15:28, 29; 21:25.

Solomoni mwana wa Mfalme Daudi pia alionyesha kiasi alipokuwa kijana, ingawa kwa njia tofauti kidogo. Solomoni alipotawazwa kuwa mfalme, aliona kama hawezi kutekeleza madaraka mazito ya mfalme. Alisali: “Ee BWANA, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia.” Kwa wazi Solomoni alijua hana uwezo wala ujuzi. Wakati huo alikuwa mwenye kiasi, hakuwa na kiburi, wala majivuno. Solomoni alimwomba Yehova ampe ufahamu, akapewa.—1 Wafalme 3:4-12.

Mesiya na Mtangulizi Wake

Zaidi ya miaka 1,000 baada ya wakati wa Solomoni, Yohana Mbatizaji alifanya kazi ya kumtayarishia Mesiya njia. Akiwa mtangulizi wa Mtiwa-Mafuta, Yohana alitimiza unabii wa Biblia. Yeye angeweza kujisifia pendeleo lake. Pia Yohana angeweza kujaribu kujitakia heshima kwa sababu alikuwa na ukoo na Mesiya. Lakini Yohana aliwaeleza wengine kwamba hakustahili hata kufunga kubazi la Yesu. Na Yesu alipojitokeza akabatizwe kwenye Mto Yordani, Yohana alisema: “Mimi ndimi ninayehitaji kubatizwa nawe, na je, wewe unakuja kwangu?” Jambo hilo laonyesha kwamba Yohana hakuwa mtu wa majisifu. Alikuwa mwenye kiasi.—Mathayo 3:14; Malaki 4:5, 6; Luka 1:13-17; Yohana 1:26, 27.

Baada ya Yesu kubatizwa, alianza huduma ya wakati wote, akihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Hata ingawa Yesu alikuwa mkamilifu, alisema: “Mimi siwezi kufanya kitu chochote kwa uanzisho wangu mwenyewe . . . Natafuta sana, si mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi yake aliyenituma mimi.” Na zaidi, Yesu hakutafuta heshima kutoka kwa wanadamu, bali alimtukuza Yehova kwa mambo yote aliyoyafanya. (Yohana 5:30, 41-44) Wonyesho mzuri kama nini wa kiasi!

Basi, kwa wazi watumishi waaminifu-washikamanifu wa Yehova—kama Daudi, Solomoni, Yohana Mbatizaji, na hata Yesu Kristo aliyekuwa mkamilifu—walikuwa na kiasi. Hawakujisifu, wala hawakuwa wenye majivuno, wala wenye kiburi, na hawakuvuka mipaka yao. Mifano yao ni sababu za kutosha kuwafanya watumishi wa wakati huu wa Yehova kukuza na kuonyesha kiasi maishani. Na bado kuna sababu nyinginezo zinazofanya tukuze kiasi.

Katika wakati huu wenye msukosuko katika historia ya wanadamu, kiasi ni sifa inayothaminiwa sana na Wakristo wa kweli. Kiasi humwezesha mtu awe na amani pamoja na Yehova Mungu, wanadamu wenzake, na ndani yake mwenyewe.

Amani Pamoja na Yehova Mungu

Tunaweza kuwa na amani pamoja na Yehova tukibaki tu kwenye mipaka anayowekea ibada ya kweli. Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walivuka mipaka waliyowekewa na Mungu, wakawa wanadamu wa kwanza kukosa kiasi. Walipoteza uhusiano wao mzuri na Yehova, wakapoteza makao yao, wakati wao ujao, na uhai wao. (Mwanzo 3:1-5, 16-19) Walipata hasara iliyoje!

Na tujifunze kutokana na kosa la Adamu na Hawa, kwa kuwa ibada ya kweli hutuwekea mipaka ya jinsi tunavyopaswa kutenda. Kwa mfano, Biblia yasema kwamba “wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume walalao pamoja na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawatarithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Yehova huweka kwa hekima mipaka hiyo kwa manufaa yetu, nasi huonyesha hekima kwa kutovuka mipaka hiyo. (Isaya 48:17, 18) Andiko la Mithali 11:2, NW, latuambia: “Hekima i pamoja na wenye kiasi.”

Namna gani kama dini fulani inatuambia kwamba twaweza kuvuka mipaka hiyo na bado tuwe na amani pamoja na Mungu? Basi dini hiyo inajaribu kutupotosha. Kwa upande mwingine, kiasi hutusaidia kukuza uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu.

Amani Pamoja na Wanadamu Wenzako

Kiasi pia hutokeza uhusiano wenye amani pamoja na wengine. Kwa mfano, wazazi wanapoweka mfano mzuri wa kuridhika na mambo ya lazima na kwa kutanguliza mambo ya kiroho, yaelekea watoto wao pia watakuwa na maoni kama yao. Ndipo itakapokuwa rahisi kwa watoto kuridhika, hata nyakati nyingine wasipopata vitu wanavyotaka. Jambo hilo litawasaidia kuishi kwa kiasi, na maisha ya familia yatakuwa yenye amani zaidi.

Waangalizi wanahitaji kutahadhari sana wawe wenye kiasi na kutotumia vibaya mamlaka yao. Kwa mfano, Wakristo wanashauriwa: “Msiyapite mambo ambayo yameandikwa.” (1 Wakorintho 4:6) Ni lazima wazee wa makutaniko watambue kwamba hawapaswi kamwe kujaribu kuwalazimisha wengine wakubali mapendezi yao wenyewe. Badala yake, wao hutumia Neno la Mungu kuwa msingi wa kutia watu moyo wafuate mwendo ufaao kuhusu mwenendo, mavazi, mapambo, au tafrija. (2 Timotheo 3:14-17) Washiriki wa kutaniko wanapoona kwamba wazee hawavuki mipaka ya Maandiko, hilo hufanya waheshimiwe na kuchangia roho changamfu yenye upendo na amani kutanikoni.

Amani Ndani Yako Mwenyewe

Watu wenye kiasi huthawabishwa kwa kuwa na amani ya ndani. Mtu mwenye kiasi hana tamaa kubwa ya makuu. Hiyo haimaanishi kwamba hana miradi ya kibinafsi. Kwa mfano, huenda akatamani mapendeleo zaidi ya utumishi, lakini yeye humngojea Mungu, naye humsifu Yehova kwa mapendeleo yoyote ya Kikristo apokeayo. Hayo hayaonwi kuwa matimizo yake mwenyewe. Jambo hilo huwavuta wenye kiasi karibu na Yehova, “Mungu wa amani.”—Wafilipi 4:9.

Labda nyakati nyingine twahisi tumepuuzwa na watu wengine. Je, haingekuwa afadhali kupuuzwa kwa sababu sisi tuna kiasi kuliko kutaka tutambuliwe kwa kujipendekeza bila kiasi? Watu wenye kiasi hawana tamaa kubwa ya makuu. Kwa hiyo, wana amani ndani yao wenyewe, jambo ambalo linafaa hali-njema yao ya kihisia-moyo na ya kimwili.

Kukuza na Kudumisha Kiasi

Adamu na Hawa walishindwa kwa kukosa kiasi—wakapitishia watoto wao hali hiyo. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuepuka kufanya kosa lilelile walilofanya wazazi wetu wa kwanza? Tunaweza kukuzaje sifa hii nzuri ya kiasi?

Kwanza, kufahamu vizuri hali yetu kwa kulinganishwa na Yehova, Muumba wa ulimwengu, kutatusaidia. Tunaweza kutimiza nini ambacho kinaweza kulingana na yale ambayo Mungu ametimiza? Yehova alimwuliza mtumishi wake mwaminifu Yobu: “Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi? Haya! sema, kama ukiwa na ufahamu.” (Ayubu 38:4) Yobu alishindwa kujibu. Je, si kweli kwamba hata sisi hatuna ujuzi, uwezo, na uzoefu zisizo na mipaka? Je, hatunufaiki kujua mipaka yetu?

Isitoshe, Biblia yatuambia: “Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya BWANA, dunia na wote wakaao ndani yake.” Hivyo vyatia ndani ‘kila hayawani, na makundi juu ya milima elfu.’ Yehova aweza kusema: “Fedha ni mali yangu, na dhahabu ni mali yangu.” (Zaburi 24:1; 50:10; Hagai 2:8) Ni mali zipi tuwezazo kuonyesha zinazolingana na mali za Yehova? Kwani, hata mtu aliye tajiri zaidi duniani hana sababu ya kujisifia mali yake! Kwa hiyo, ni hekima kufuata shauri hili lililopuliziwa ambalo mtume Paulo aliwapa Wakristo katika Roma: “Kupitia fadhili isiyostahiliwa niliyopewa naambia kila mtu huko miongoni mwenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.”—Waroma 12:3.

Tukiwa watumishi wa Mungu wanaotamani kukuza sifa ya kiasi, twapaswa kusali tupate matunda ya roho—upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujidhibiti. (Luka 11:13; Wagalatia 5:22, 23) Kwa nini? Kwa sababu kila mojawapo ya sifa hizi itatusaidia kuwa wenye kiasi. Kwa mfano, kuwapenda wanadamu wenzetu kutatusaidia kushinda mwelekeo wa kujisifu au kuwa wenye kiburi. Na kujidhibiti kutatusaidia kufikiria kwanza kabla ya kutenda kwa kukosa kiasi.

Tutahadhari! Twahitaji daima kulinda dhidi ya mitego ya kukosa kiasi. Wawili kati ya wafalme waliotajwa mapema hawakuwa wenye kiasi nyakati zote. Mfalme Daudi alitenda kwa kimbelembele kwa kuhesabu watu katika Israeli, kinyume cha mapenzi ya Yehova. Mfalme Solomoni akakosa kiasi hata kufikia hatua ya kujiingiza katika ibada isiyo ya kweli.—2 Samweli 24:1-10; 1 Wafalme 11:1-13.

Maadamu mfumo huu usiomcha Mungu waendelea, tunahitaji kuwa macho siku zote ili kuwa wenye kiasi. Na yafaa kujitahidi. Katika ulimwengu mpya wa Mungu, jamii ya wanadamu itakuwa wale tu ambao wana kiasi. Wataona kiasi kuwa nguvu wala si udhaifu. Itakuwa ajabu kama nini kwa watu mmoja-mmoja na familia kubarikiwa na amani itokanayo na kiasi!

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kwa sababu alikuwa mwenye kiasi, Yesu alimsifu Yehova kwa yote aliyofanya