Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, mtume Paulo alikuwa akionyesha kwamba Wakristo hawapaswi kukasirika aliposema hivi kwenye Waroma 12:19: “Msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi hasira ya kisasi”?

La, hasha. Hapa mtume Paulo alikuwa akirejezea hasira ya kisasi ya Mungu. Bila shaka, hiyo haimaanishi kwamba haidhuru Wakristo wakikasirika au la. Kwa wazi Biblia hutushauri dhidi ya kuwa na hasira ya kisasi. Ona vielelezo kadhaa vya ushauri wa Mungu.

“Ukomeshe hasira, uache ghadhabu, usikasirike, mwisho wake ni kutenda mabaya.” (Zaburi 37:8) “Kila mtu aendeleaye kuwa na hasira ya kisasi na ndugu yake atapaswa kutoa hesabu kwa mahakama ya kuamulia haki.” (Mathayo 5:22) “Kazi za mwili ni dhahiri, nazo ni uasherati, ukosefu wa usafi, mwenendo mlegevu, ibada ya sanamu, zoea la uwasiliani-roho, uadui, zogo, wivu, hasira za ghafula.” (Wagalatia 5:19, 20) “Acheni uchungu wote wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) “Kila mtu lazima awe mwepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema, wa polepole juu ya hasira ya kisasi.” (Yakobo 1:19) Isitoshe, kitabu cha Mithali chatushauri tena na tena dhidi ya kuwa na hasira ya kisasi au kuwa na mwelekeo wa kukasirika juu ya maudhiko madogo-madogo na makosa ya kibinadamu.—Mithali 12:16; 14:17, 29; 15:1; 16:32; 17:14; 19:11, 19; 22:24; 25:28; 29:22.

Muktadha wa Waroma 12:19 wapatana na ushauri huo. Paulo alipendekeza kwamba tuwe na upendo usio na unafiki, kwamba tuwabariki wale wenye kutunyanyasa, kwamba tujaribu kuwaona wengine ifaavyo, kwamba tusirudishe ovu kwa ovu, na kwamba tujitahidi kuwa wenye amani na watu wote. Kisha akatusihi hivi: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi hasira ya kisasi; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa, asema Yehova.’”—Waroma 12:9, 14, 16-19.

Naam, tusiruhusu hasira ituchochee kulipiza kisasi. Ujuzi wetu kuhusu hali na ufahamu wetu kuhusu haki si mkamilifu. Mara nyingi tutakosea tukiiruhusu hasira ituchochee kulipiza kisasi. Hiyo ingetimiza makusudi ya Mpinzani wa Mungu, Ibilisi. Paulo aliandika hivi penginepo: “Iweni na hasira ya kisasi, na bado msifanye dhambi; msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msiruhusu mahali kwa ajili ya Ibilisi.”—Waefeso 4:26, 27.

Njia iliyo nzuri na ya hekima ni kumwacha Mungu aamue atalipiza kisasi wakati gani na dhidi ya nani. Anaweza kufanya hivyo akiwa anajua mambo yote ya hakika, na adhabu yoyote atoayo itadhihirisha haki yake kamilifu. Twaweza kuona kwamba hiyo ndiyo hoja ya Paulo kwenye Waroma 12:19 tutazamapo andiko alilorejezea la Kumbukumbu la Torati 32:35, 41, ambalo latia ndani maneno haya: “Kisasi ni changu mimi, na kulipa.” (Linganisha Waebrania 10:30.) Hivyo, ingawa maneno “cha Mungu” hayapatikani katika maandishi ya Kigiriki, watafsiri kadhaa wa siku hizi wameyaongeza kwenye Waroma 12:19. Jambo hilo linafanya kuwepo fasiri kama “acheni Mungu alipize kisasi” (The Contemporary English Version); “ipeni nafasi hasira ya kisasi ya Mungu” (American Standard Version); “acheni Mungu atoe adhabu akipenda” (The New Testament in Modern English); “acheni nafasi kwa ajili ya adhabu ya Mungu.”—The New English Bible.

Hata tukidhulumiwa au kunyanyaswa na maadui wa ile kweli, tunaweza kuitibari ufafanuzi ambao Musa alisikia kumhusu Yehova Mungu: “BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.”Kutoka 34:6, 7, italiki ni zetu.